67. Kuishi kwa Kudhihirisha Mfano Kidogo wa Mwanadamu Hakika Ni Vizuri

Na Tashi, Kanada

Mwenyezi Mungu anasema, “Kabla ya hitimisho ya mpango Wake wa usimamizi wa miaka 6,000—kabla ya Yeye kuweka wazi mwisho wa kila aina ya binadamu—kazi ya Mungu ulimwenguni utakuwa kwa ajili ya wokovu, yote haya ni ili kuwafanya wale wanaompenda Yeye kukamilika kabisa, na kuwarejesha katika utawala Wake. Bila kujali jinsi ambavyo Mungu huwaokoa watu, yote hufanywa kwa kuwafanya wajitenge na asili yao ya zamani ya kishetani; yaani, Yeye huwaokoa kwa kuwafanya watafute uzima. Wasipotafuta uzima basi hawatakuwa na njia yoyote ya kukubali wokovu wa Mungu. … Kitambo, mbinu Zake za wokovu zilikuwa kuonyesha upendo na huruma mkuu, kiasi cha kwamba Alijitolea Yake yote kwa Shetani ili naye aweze kuwapata wanadamu wote. Leo haifanani kamwe na kitambo: Wokovu uliopewa leo unatokea wakati wa siku za mwisho, wakati wa uainishaji wa kila mmoja kulingana na aina yake; mbinu za wokovu wako si upendo wala huruma, lakini kuadibu na hukumu ili mwanadamu aweze kuokolewa kabisa. Hivyo basi, kila kitu unachopokea ni kuadibu, hukumu, na kupiga bila huruma, lakini jua kwamba katika kupiga huku kusiko na huruma hakuna hata adhabu ndogo zaidi, jua kwamba licha ya namna ambavyo maneno haya yanavyoweza kuwa makali, kile kinachokupata ni maneno machache yanayoonekana kutokuwa na huruma kabisa kwako, na jua kwamba, licha ya namna ambavyo hasira Yangu itakavyokuwa, kile kitakachokujia bado ni maneno ya mafunzo, na sinuii kukudhuru, au kukuua. Je, haya yote ni ukweli, sivyo? Jua kwamba leo, iwe hukumu ya haki au usafishaji na adhabu visivyo na huruma, yote haya ni kwa minajili ya wokovu. Haijalishi kama leo kila anaainishwa kulingana na aina yake, ama makundi ya wanadamu yanafichuliwa, matamko yote ya Mungu na kazi ni kwa ajili ya kuwaokoa wale wanaompenda Mungu kwa dhati. Kuhukumu kwa haki ni kwa ajili ya kumtakasa mwanadamu, utakasaji usio na huruma ni kwa ajili ya kumsafisha mwanadamu, maneno makali au kuadibu yote ni kwa ajili ya kutakasa, na kwa minajili ya wokovu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mnapaswa Kuweka Pembeni Baraka za Hadhi na Kuelewa Mapenzi ya Mungu ya Kumletea Mwanadamu Wokovu).

Kanisa lilikuwa likijiandaa kupiga picha za sinema mwaka jana, kwa hivyo ndugu walipendekeza nichukue wajibu wa mwelekezi. Nilifurahi niliposikia hivyo na nikahisi kwamba kwa kuwa walinipendekeza, hakika waliona ubora wa tabia yangu na kipaji changu. Kama sivyo walinichagua kwa sababu ipi nyingine? Nilikuza majikwezo, nikidhani kuwa nilikuwa bora kuliko wengine. Nilisoma kwa bidii, nikijifunza jinsi ya kutengeneza filamu, na nikaja kufahamu ustadi huo polepole. Nakumbuka mara ya kwanza nilipoanza wajibu huo, nilihisi uwoga kidogo, lakini nikamwomba Mungu wakati huo wote na nikatulia polepole, na niliweza kwenda kuanza kufanya wajibu wangu. Na kisha, ndugu waliendelea kukubali maoni yangu. Hasa tukio la kwanza nililoelekeza, wote walipenda picha nilizopiga na kiongozi akasema kwamba nilistahili kuwa mwelekezi. Moyo wangu ulikuwa na fahari tele, nilihisi kuwa nilikuwa hodari sana katika wajibu huu na nilikuwa mtu mwenye talanta muhimu katika nyumba ya Mungu. Nilianza kuhisi kana kwamba nilikuwa na taji kichwani pangu, na nilitembea huku na kule nikiwa nimejiamini. Nilihisi kuwa kupata sifa nyingi sana baada tu ya kuanza wajibu huu ilikuwa kwa sababu kwa kweli nilikuwa na uwezo, na kwa kufanya mazoezi zaidi, hakika ningekuwa stadi, bila shaka. Nilipokuwa nikifanya kazi na ndugu kutoka wakati huo na kuendelea, sikuwa mtu asiye na majivuno kama nilivyokuwa awali, lakini niliongea kwa kujiamini, na madaha. Nilitaka pia kuwa na kauli ya mwisho katika kila kitu na sikumjali mtu mwingine yeyote. Pindi watu walipotilia shaka wazo langu au kutoa maoni mengine, sikuyakubali, sikuwa na uvumilivu, na niliwadharau. Nilihisi kwamba niliwapiku katika kila jambo, kwamba walipaswa kufanya tu kile nilichosema badala ya kuleta fujo. Na machoni pangu, walikuwa tu wakiibua mambo yasiyokuwa muhimu ambayo hata hayakupaswa kujadiliwa. Kwa hivyo niliuliza kila mara “Je, hili ni suala la kanuni?” ili kuwanyamazisha. Wakati mmoja, Dada Zhang, mhusika mkuu, aliniambia niangalie mavazi maalum ya kuigiza ambayo alikuwa ameyachagua. Niliwaza, “Unawezaje kuchagua mavazi mabaya hivi?” Nilimwambia achague yote upya. Nilibatilisha chaguo lake la mavazi mara nyingi. Nilikuwa na majivuno kwa sababu ya kuwa mwelekezi, kwa hivyo maoni yangu yalikuwa sahihi na wanapaswa kunisikiliza. Ndugu waliishia kuhisi kuzuiwa nami na hawakutaka kutoa mapendekezo tena. Kwa kweli nilihisi vibaya nilipoona haya, lakini nikawaza, nazingatia tu kazi yetu, na siwezi kuwa mwenye makosa. Kwa hiyo, sikujali. Wakati huo, kiongozi wangu alinipa ushirika na kunifunua, akisema kwamba nilikuwa na kiburi sana na kwamba nilipenda kuwadhibiti watu, na akanionya nisiwakazie wengine macho, lakini nitafakari juu yangu na kutenda ukweli ili kutatua matatizo yangu. Lakini sikuwa na ufahamu wowote kuhusu asili yangu mwenyewe wakati huo. Nilihisi kwamba niliwajibika sana katika kazi yangu. Niliendelea tu kuishi katika hali hiyo ya uasi na ukaidi, na sikuwa tena na uwezo wa kufanya kazi vizuri na kina ndugu. Kadiri wakati ulivyoendelea matatizo yaliendelea kutokea katika kazi yetu ambayo yalizuia maendeleo yetu.

Siku moja, nilisikia kwamba kulikuwa na mwelekezi ambaye alikuwa amefukuzwa kazini kwa sababu ya kuzuia kazi kutokana na yeye kuwa na kiburi, pasipo kuweza kukubali ukweli, na kuwazuia kina ndugu. Hiyo iliniacha nikihisi uwoga kidogo. Nilijua kwamba nilikuwa na tabia kama ya mwelekezi huyo. Nilifikiri Mungu alikuwa akinipa onyo, kwa hivyo niliamua kutoendelea kuonyesha ubwana kwa namna hiyo. Badala yake, nilifaa kujidhibiti, kuzungumza kwa huruma zaidi, na kujitahidi kuwasiliana na kujadili kazi na wengine. Lakini bado sikuwa na ufahamu wowote kuhusu asili yangu mwenyewe, kwa hivyo sikutafuta ukweli ili kuitatua.

Baada ya muda mfupi, kwa kuwa maendeleo katika timu yetu yalikuwa ya polepole sana, kiongozi alipanga Dada Liu afanye kazi nami. Mwanzoni, sikuweza kukubali hilo hata kidogo. Nilidhani kiongozi huyo hakika alitilia shaka uwezo wangu, lakini kwa kuwa tayari ilikuwa imepangwa, nilikubali shingo upande. Katika majadiliano ya kazi kuanzia wakati huo na kuendelea, niligundua kuwa kiongozi yule alitafuta ushauri wa Dada Liu kila wakati. Nilikua na wasiwasi sana na nikahisi kwamba kiongozi yule hakuniheshimu. Nilianza kumchukia. Lakini hata zaidi, nilimpinga Dada Liu. Sikuweza kumkubali. Kwa hivyo kila tulipojadili kazi yetu niliketi pale nikikunja uso kimyakimya tu. Wakati mmoja, alipata matatizo kadhaa katika kazi ya timu na akatoa mapendekezo kadhaa ambayo ndugu zetu wote waliyapenda sana, lakini sikuyataka. Nilikataa kusikiliza mapendekezo yake yoyote. Kila mtu alipotaka maoni yangu, nilificha hasira yangu na kusema: “Vyovyote vile.” Kisha kiongozi akanishughulikia, akisema kuwa sikuwa nikiunga mkono kazi ya nyumba ya Mungu. Kwa kweli nilihisi vibaya na nilijua kuwa bila kujali lolote, singeendelea kuonyesha nilivyokata tamaa katika kazi ya nyumba ya Mungu. Lakini kwa kweli sikuweza kujizuia. Niliwaza, “Ikiwa ninyi humsikiliza tu Dada Liu wakati wote, kuna nini cha kujadili?” Niliendelea kufikiri kuwa nilikuwa sahihi katika kila kitu, kwa hivyo katika majadiliano machache ya kazi yaliyofuata nilishikilia maoni yangu na sikukubaliana na Dada Liu hata wakati maoni yake yalikuwa ya busara. Nilidhani kuwa alikuwa akiringa. Kuna wakati mmoja ambapo alipendekeza muigizaji fulani na nikaibua maswala ya kila aina kuhusiana na muigizaji huyo na nikabatilisha pendekezo lake. Sikuwa tayari kabisa kumsikiliza. Nilitaka kusimamia kazi yote. Dada Liu aliishia kuhisi kuzuiwa nami na hakutoa mapendekezo tena. Wakati huo, kwa kuwa nilikuwa nikiishi ndani ya tabia ya kiburi na ya kujidai na sikuwa nikitafuta ukweli, roho yangu ilitumbukia gizani polepole. Nilihisi huzuni kila siku na ilionekana kana kwamba Mungu alikuwa Akijificha mbali nami. Sikuwa na lolote la kumwambia Mungu katika sala na maneno ya Mungu hayakuwa yakiingia akilini nilipoyasoma. Sikuonyesha mawazo yoyote na nilikuwa goigoi katika wajibu wangu. Sikuweza kuona matatizo yoyote. Nilikuwa nikiishi katika hali ya wasiwasi na niliendelea kuhisi kana kwamba jambo fulani lilikuwa karibu kutokea.

Siku chache baadaye, kiongozi wetu alikuja kufanya mkutano nasi. Alifichua tabia yangu na akasema kwamba nilikuwa mwenye kiburi mno, kwamba nilikuwa holela na dikteta katika wajibu wangu, na nilikuwa nimevuruga kazi yetu sana. Aliniambia niende nyumbani kufanya ibada ya dhati na nitafakari kujihusu. Nilishtuka niliposikia hayo, lakini nilimwomba Mungu kwa dhati nikisema, “Ee Mungu, bila kujali nitakumbana na hali gani, naamini yote imeandaliwa na Wewe na niko tayari kutii.” Sikuweza kulala kabisa usiku huo. Nilikuwa nikifikiria jinsi nilivyokuwa kwenye timu ya filamu kwa muda mrefu sana, lakini kwamba kuanzia kesho sitahusika tena na timu hiyo. Sikuweza kulifumbia macho jambo hilo na nilifadhaika mno, sikuweza kuyazuia machozi yangu. Nilitaka kutumia nafasi hiyo kushughulikia ibada zangu na kutafakari kujihusu, ili niweze kujinyanyua kutoka pale ambapo nilikuwa nimejikwaa. Lakini kule nyumbani sikuweza kulenga maneno ya Mungu na kwa kweli nilikuwa na wakati mgumu. Nilichoweza tu kufanya ni kuja mbele za Mungu na kumwita tena na tena. Nilisema, “Mungu, nina uchungu mwingi sana. Tafadhali nisaidie na Uulinde moyo wangu ili niweze kuelewa mapenzi Yako katika hali hii, na nijifahamu.” Kwa kumwomba Mungu bila kukoma, niliweza kuhisi amani kiasi hatimaye.

Ndugu kadhaa walikuja kunijulia hali siku iliyofuata, kunipa ushirika na kunisaidia, na wakataja baadhi ya matatizo yangu. Nakumbuka kwamba dada mmoja alisema, “Umebadilika sana tangu ulipoanza kufanya kazi kama mwelekezi. Wewe hata huwaangalia wengine kwa njia tofauti na unataka kuwa na kauli ya mwisho katika kila kitu. Wewe kwa kweli unawadhibiti watu na kufanya kazi na wewe hakuwezekani kabisa.” Ndugu mmoja alisema, “Katika majadiliano ya kazi, sisi sote hupumzika wakati ambapo wewe haupo, lakini mara tu unapokuja sote huwa na wahaka, tukihofia kwamba utabatilisha mawazo na maoni yetu.” Kila neno lililotoka vinywani mwao lilikuwa kama kisu moyoni mwangu. Niliona haya kuwakabili na nikahisi vibaya sana. Katika maisha yangu yote, sikuwa nimewahi kuhisi kushindwa hivyo. Hali hiyo ilikuwa imekuwa mbaya zaidi sana kiasi kwamba ndugu hawakuthubutu kunijia, na waliogopa waliponiona. Nilifikiri, “Je, mimi bado ni mtu mzuri? Niliwezaje kutojali hisia za wengine kiasi hicho?” Sikuwa kamwe nimegundua kwamba tabia yangu ya kiburi inaweza kuwazuia na kuwadhuru wengine hivyo. Nilijua tayari kuwa nilikuwa mwenye kiburi na kiongozi alishiriki nami mara nyingi, lakini sikujali hilo. Badala yake, nilidhani kiburi changu kilitokana na kuwa na ubora wa juu zaidi wa tabia. Ni nani asiye na kiburi ikiwa ana kipawa na ubora wa juu wa tabia? Hiyo ndiyo sababu sikuwahi kutafuta ukweli ili kutatua hilo. Lakini kupitia msaada na ushirika wa ndugu nilipata amani moyoni mwangu hatimaye na niliweza kujituliza ili kutafakari juu ya tabia yangu.

Nilipokuwa nikitafakari, nilisoma vifungu viwili vya maneno ya Mungu, ambavyo ningependa kuvishiriki sasa. Mungu alisema, “Kama kwa kweli una ukweli ndani yako, njia unayotembea kiasili itakuwa njia sahihi. Bila ukweli, ni rahisi kufanya uovu na hutakuwa na budi kuufanya. Kwa mfano, kama kiburi na majivuno, vingekuwa ndani yako, ungeona kwamba haiwezekani kuepuka kumwasi Mungu; ungehisi kulazimishwa kumwasi. Hutafanya hivyo kimakusudi; utafanya hivyo chini ya utawala wa asili yako ya kiburi na majivuno. Kiburi na majivuno yako vitakufanya umdharau Mungu na kumwona kuwa asiye na maana; vitakufanya ujiinue, vitakufanya kujiweka kila wakati kwenye maonyesho, na mwishowe vitakufanya ukae katika nafasi ya Mungu na kujitolea ushuhuda mwenyewe. Mwishowe utayabadilisha mawazo yako mwenyewe, fikira zako mwenyewe na dhana zako yawe ukweli wa kuabudiwa. Tazama ni kiasi gani cha uovu kinafanywa na watu chini ya utawala wa asili yao ya kiburi na majivuno!(“Ni Kwa Kufuatilia Ukweli Tu Ndiyo Unaweza Kupata Mabadiliko Katika Tabia Yako” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). “Kiburi ndicho chanzo cha upotovu wa mwanadamu. Kadiri watu wanavyozidi kuwa na kiburi, ndivyo wanavyozidi kuwa na uelekeo wa kumpinga Mungu. Tatizo hili ni kubwa kiasi gani? Siyo tu kwamba watu wenye tabia ya kiburi humfikiria kila mtu mwingine kuwa duni kuwaliko, lakini lililo baya zaidi, wao hata huwa na mtazamo wa udhalilishaji kwa Mungu. Hata ingawa, kwa nje, watu wengine wanaweza kuonekana kana kwamba wanamwamini Mungu na kumfuata, hawamchukulii kama Mungu hata kidogo. Wao huhisi sikuzote kuwa wanamiliki ukweli na wanajipenda mno. Hiki ndicho kiini na chanzo cha tabia ya kiburi, na hutoka kwa Shetani. Kwa hivyo, tatizo la kiburi lazima litatuliwe. Kuhisi kuwa wewe ni bora kuliko wengine—hilo ni jambo dogo. Suala la muhimu ni kwamba tabia ya kiburi ya mtu humzuia mtu kumtii Mungu, sheria Yake, na mipango Yake; mtu kama huyo daima huhisi kuwa na uelekeo wa kushindana na Mungu kuwatawala wengine. Mtu wa aina hii hamchi Mungu hata kidogo, sembuse kumpenda Mungu au kumtii(Ushirika wa Mungu). Niligundua kutoka kwa maneno ya Mungu kwamba ufidhuli wangu na majivuno yangu vilikuwa vikinisababisha nimwasi na kumpinga Mungu. Tangu nilipokuwa nikifanya wajibu wangu kama mwelekezi, wakati nilikuwa na mafanikio kiasi nilidhani ni kwa sababu ya bidii yangu mwenyewe, kwamba nilikuwa bora kuliko wengine. Nilianza kuwapuuza wengine, na kutosalimu amri kwa ukaidi, nikitaka kuwa na kauli ya mwisho katika kila kitu. Niliposhindwa kupata matokeo katika wajibu wangu sikutafakari kamwe kuhusu iwapo tatizo hilo lilitokana nami, lakini nililenga tu ndugu zangu. Niliwashughulikia na kuwakaripia wengine nikijionyesha kuwa bora kuwaliko. Nilimchukia kila mtu kutokana na kiburi na majivuno. Sikuweza kuona uwezo wa mtu mwingine, na nikadhani kwamba mawazo yangu yalikuwa bora kabisa. Nilibatilisha mapendekezo ya kila mtu mara kwa mara, na nilikuwa nikiwadhibiti. Nilishindwa kujijua kwa sababu ya kiburi na majivuno yangu na hata baada ya kupogolewa na kushughulikiwa mara nyingi, sikukubali hayo au kutafakari juu yangu. Nilikosa moyo wa mtafutaji kabisa. Maendeleo ya kazi yangu yalipoenda polepole na ikawa wazi kwamba sikuweza kusimamia kazi, bado sikutaka kufanya kazi na wengine au kuwaruhusu waingilie kazi zangu. Nilihisi kwamba hilo lingeathiri mamlaka yangu na kutishia sifa na cheo changu. Nilitaka kuwa na mamlaka kabisa, na nilitaka kuwa na kauli ya mwisho. Je, si nilikuwa nikitembea kwenye njia ya kumpinga Mungu? Dada Liu alipopata mafanikio kiasi katika wajibu wake ambao ulitishia cheo changu, nilijua vizuri kuwa alikuwa sahihi na kile alichopendekeza kingefaidi kazi ya nyumba ya Mungu, lakini sikukubali hilo. Badala yake nilizua fujo, na nilipowaona ndugu zetu wakikubaliana naye, sikuweza kuvumilia, na nikaonyesha kukata tamaa kwangu katika kazi ya kanisa. Nilikuwa tayari kuona kazi ya nyumba ya Mungu ikiathirika ili kulinda sifa na hadhi yangu. Uchaji wangu kwa Mungu ulikuwa wapi? Dhamiri yangu na mantiki vilikuwa wapi? Niliona kwamba nilikuwa nikiishi kulingana na tabia yangu ya kishetani yenye kiburi na majivuno, nikilazimishia kina ndugu mawazo na maoni yangu kana kwamba yalikuwa ukweli, nikiwalazimisha watu wanisikilize katika kila kitu. Si huko kulikuwa kutaka kuwa sawa na Mungu, na kutaka kuwadhibiti wengine? “Mwanadamu hapaswi kujitukuza wala kujipa sifa. Anapaswa kumwabudu na kumsifu Mungu(“Amri Kumi za Utawala Ambazo Lazima Wateule wa Mungu katika Enzi ya Ufalme Wazitii” katika Neno Laonekana katika Mwili). Mwishowe niligundua kuwa nilikuwa katika hali ya hatari. Ilionekana kana kwamba nilikuwa nikifanya wajibu wangu kila siku, kwamba nilikuwa na shauku ya kujitumia, lakini nilikuwa nikifichua tabia ya kishetani katika kila njia. Matendo yangu yote yalikuwa kinyume cha ukweli, nilikuwa nikivuruga kazi ya kanisa. Nilikuwa nikitenda maovu, nikimpinga Mungu, na nikikosea tabia Yake! Nilijiuliza nilikuwa nimefikia hatua hiyo vipi. Ni kwa sababu nilikuwa na asili ya kiburi mno na isiyobadilika. Sikukubali ukweli kamwe, kwa hivyo niliishia kujiletea ghadhabu ya Mungu. Niliona kwamba nilikuwa nimepotoshwa sana na Shetani, kwamba nilikosa uhalisi wa ukweli kabisa. Kuweza kujitwisha wajibu muhimu kama huo kulikuwa Mungu kuniinua, na kuwa na ufanisi fulani katika wajibu wangu kulifanikishwa kabisa na kazi ya Roho Mtakatifu, sio kwa sababu nilikuwa na uwezo wowote hata kidogo. Niliona kwamba nilipotegemea asili yangu ya kiburi katika wajibu wangu, Roho Mtakatifu aliacha kufanya kazi na sikuweza kujua lolote au kutatua lolote. Lakini hata hivyo, bado nilihisi kana kwamba nilikuwa sawa. Nilikuwa mwenye kiburi kukithiri, asiyejitambua hata kidogo. Ni hapo tu ndipo nilianza kuikirihi na kuichukia asili yangu ya kiburi.

Baadaye nilisoma maneno haya kutoka kwa Mungu: “Nyinyi nyote mnaishi mahala pa dhambi na ufisadi; nyinyi nyote ni watu wapotovu na wenye dhambi. Leo hii hamwezi tu kumwona Mungu, ila la muhimu zaidi, mmepokea kuadibu na hukumu, mmepokea wokovu wa kina, yaani, mmepokea upendo mkubwa zaidi wa Mungu. Yote Ayafanyayo ni mapenzi ya dhati kwako; Hana nia mbaya. Anawahukumu kwa sababu ya dhambi zenu, ili kwamba mweze kujichunguza wenyewe na kupokea wokovu mkubwa. Haya yote hufanywa kwa kusudi la kumkamilisha mwanadamu. Tangu mwanzo hadi mwisho, Mungu amekuwa Akifanya kila Awezalo kumwokoa mwanadamu, na hakika hayuko tayari kuwaangamiza kabisa wanadamu Aliowaumba kwa mikono Yake Mwenyewe. Sasa Amekuja miongoni mwenu kufanya kazi; je, huu si wokovu zaidi? Je, Angalikuchukia, Angaliendelea kufanya kazi ya kiwango hicho cha juu ili kukuongoza wewe Mwenyewe? Ni kwa nini Ateseke hivyo? Mungu hawachukii wala hana nia mbaya juu yenu. Mnapaswa kufahamu kuwa mapenzi ya Mungu ndiyo mapenzi ya kweli zaidi. Anawaokoa kupitia hukumu kwa sababu tu ya uasi wa mwanadamu; la sivyo, hawangepata wokovu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ukweli wa Ndani wa Kazi ya Ushindi (4)). Nilisoma maneno ya Mungu tena na tena. Nilikuwa na hisia kubwa ya ukunjufu na niliguswa sana. Niliona kwamba, kwa kunifichua kwa njia hiyo, Mungu hakuwa akinihukumu au kuniondoa, na hakuwa Akifanya mambo yawe magumu kwangu kimakusudi. Alikuwa kwa kweli akifanya hivyo kwa ajili ya wokovu wangu. Nina asili ya kiburi mno na isiyobadilika na Mungu alijua kile nilichohitaji. Kwa kupoteza wajibu wangu na kupogolewa na kushughulikiwa na ndugu, nilikuja kujua tabia yangu ya kiburi na niliweza kutafakari juu ya njia ambayo nilikuwa nimeitembea, na kutubu kwa Mungu kwa kweli ili nisimwasi na kumpinga tena. Ingawa nilipata maumivu na uhasi wakati huo, bila hukumu na kuadibiwa kwa aina hiyo, moyo wangu usiojali usingeamshwa. Singetafakari juu ya tabia yangu au kuja kujua tabia ya Mungu yenye haki. Singetubu kwa Mungu kwa kweli, lakini ningeendelea tu kushindana na Yeye na kumpinga, mwishowe nikikosea tabia Yake na kuadhibiwa. Mwishowe nilipata uzoefu kwamba hukumu na ufunuo wa maneno ya Mungu vilikuwa ulinzi Wake kwangu, na upendo wa kweli zaidi. Nilimshukuru sana Mungu nilipogundua hayo na nikahisi kwamba napaswa kufuatilia ukweli kwa dhati katika siku zijazo ili niweze kuacha tabia yangu potovu na kuishi kwa kudhihirisha mfano wa kibinadamu hivi karibuni.

Baada ya hayo niliendelea kuomba na kutafuta. Nilijiuliza ni vipi ningeacha kuishi kulingana na tabia yangu ya kiburi na kuacha kumpinga Mungu. Nilipokuwa nikitafuta, nilisoma maneno haya kutoka kwa Mungu: “Asili ya kiburi hukufanya uwe mbishi. Watu wanapokuwa na tabia hii ya ubishi, je, si wana uelekeo wa kuwa wakaidi? Basi je, unawezaje kutatua ukaidi wako? Unapokuwa na wazo, unaliibua na kusema unachofikiri na kuamini kuhusu jambo hili, kisha, unawasiliana na kila mtu kulihusu. Kwanza, unaweza kueleza zaidi kuhusu maoni yako na kutafuta ukweli; hii ndiyo hatua ya kwanza kutia katika vitendo ili kushinda tabia hii ya ukaidi. Hatua ya pili hufanyika watu wengine wanapotoa maoni tofauti—unaweza kufanya nini ili kujizuia kuwa mkaidi? Lazima kwanza uwe na mtazamo wa unyenyekevu, upuuze kile unachoamini kuwa ni sahihi, na umwache kila mtu awe na ushirika. Hata kama unaamini kwamba njia yako ni sahihi, hupaswi kuendelea kuisisitiza. Kwanza kabisa, hayo ni maendeleo ya aina fulani; inaonyesha mtazamo wa kutafuta ukweli, wa kujinyima, na wa kuyaridhisha mapenzi ya Mungu. Unapokuwa na mtazamo huu, wakati huo huo ambapo hushikilii maoni yako, unaomba. Kwa kuwa hujui kutofautisha mema na mabaya, unamruhusu Mungu afichue na kukuambia jambo bora na linalofaa kufanywa ni lipi. Kila mtu anapojiunga katika ushirika, Roho Mtakatifu anawaletea nyote nuru(Ushirika wa Mungu). Nilipata njia ya utendaji kutoka kwa maneno ya Mungu. Iwapo sitaki kuishi katika kiburi au kuwa dikteta katika wajibu wangu, ninapaswa kuwa na moyo wa kutafuta ukweli na kumcha Mungu. Napaswa kushirikiana na ndugu na wakati ambapo kuna tofauti za maoni napaswa kuweza kujinyima na kuacha ubinafsi wangu, nimwombe Mungu na kutafuta ukweli. Nikiwa na dhamira hiyo tu ndiyo ninaweza kutiwa nuru na Roho Mtakatifu kwa urahisi, na siwezi kamwe kufika kiwango cha kumwasi na kumpinga Mungu na kuharibu kazi ya nyumba ya Mungu kwa kushikilia mawazo yangu mwenyewe. Kugundua haya yote kulikuwa kama taa kuangazwa moyoni mwangu. Niliomba ombi hili: “Mungu, kuanzia sasa na kendelea, natamani kufanya kazi kwa upatanifu na ndugu ili tuweze kutafuta ukweli pamoja na tutekeleze wajibu wetu kwa mujibu wa kanuni.”

Muda mfupi baada ya hapo niliombwa niandike mistari michache ya kaligrafia kwa ajili ya wajibu wangu. Niliposikia haya, niliwaza, “Mistari michache ya kaligrafia si kitu. Nimesomea kaligrafia, kwa hivyo ninajiamini sana katika hili.” Niliandika nakala kadhaa, na baada ya kuziangalia Dada Liu alisema, “Nadhani hayo si mabaya.” Nilihisi kumchukia tena wakati huo na nikawaza, “Unasema hivyo kwa kusita sana. Je, kaligrafia yangu ilikuwa mbaya sana? Nilisomea hili, nalielewa vyema. Je, sijui mengi kulihusu kukuliko? Bila shaka huelewi vizuri mambo haya, na unazua fujo kimakusudi.” Lakini mawazo hayo yalipokuwa yakinijia akili mwangu, niligundua ghafla kuwa nilikuwa nimekosea. Je, si huko kulikuwa kufichua tabia ya kiburi tena? Nilikuja mbele za Mungu kumwomba bila kupoteza wakati: “Ee Mungu, nataka niwe na mtazamo wa kutafuta na wa utiifu, kujitelekeza, na kujitolea kwa dhati kwa ajili ya wajibu wangu.” Niliandika nakala nyingine nikiwa na dhamira hiyo, na Dada Liu alipoliona alitoa mapendekezo zaidi, akiuliza iwapo ningeweza kulifanya livutie zaidi. Ndugu kadhaa walisema lilionekana kuwa zuri kabisa. Kulingana na jinsi nilivyokuwa hapo awali, ikiwa nilidhani kuwa nilikuwa sahihi na watu wengine wakubaliane nami pia, hakukuwa na lolote zaidi la kusema, na ningeshikilia msimamo wangu kwa ukaidi zaidi. Lakini sikufikiria hivyo wakati huo. Niliwaza, “Ndugu wanatoa maoni tofauti kwa kuwa wanafikiri juu ya wajibu wetu. Hakuna mtu anayefanya hivyo ili kufanya mambo yawe magumu kwa mtu yeyote. Na maoni yangu si lazima kwamba yako sahihi. Mwishowe, lazima tufanye uamuzi utakaoleta matokeo bora kabisa katika wajibu wetu.” Kwa kuzingatia hili, nilichukua hatua na kusema: “Mnaonaje nikiandika nakala nyingine nanyi muamue ni ipi bora. Mnaweza kutumia lolote mtakalopenda zaidi.” Nilipoandika nikiwa na dhamira hiyo nilihisi mtulivu na mwenye amani sana, kujivunjia heshima hata hakukunijia akilini. Baada ya kumaliza, nilitafuta maoni zaidi kutoka kwao na kina ndugu wakanipa mapendekezo zaidi. Yote yalikuwa ya maana sana. Kile nilichohisi wakati huo ni kwamba kwa kweli nilikuwa na makosa mengi na kwamba ndugu walikuwa na hoja nyingi muhimu ambazo sikuwa nazo. Maoni na mapendekezo yao mengi yalifidia udhaifu wangu. Kwa hivyo kupitia usaidizi wa kila mtu, kwa kufidia udhaifu wa kila mmoja, tulifanikiwa zaidi katika wajibu wetu mwishowe. Baada ya kufanya kazi na ndugu kwa njia hii kwa muda nilianza kuhisi mwenye utulivu sana, na mwenye uhusiano wa karibu sana na kila mtu. Aidha, sikuwa fidhuli au mwenye majivuno kama hapo awali, na sikuwa mbishi wengine waliponikaribia. Niligundua pia kwamba haikuwa vigumu sana kukubali mapendekezo ya kina ndugu, na niliweza kukubali kile walichoniambia kuhusu upungufu wangu kwa njia sahihi. Mambo mengine yalitokea ambayo sikuyapenda, na nilifichua majivuno kiasi, lakini kwa kukumbushwa na kina ndugu niliweza kuja mbele za Mungu papo hapo. Nilikuwa tayari kujitelekeza, kutafuta ukweli, na kutekeleza wajibu wangu kulingana na kanuni. Baada ya kupitia haya yote, niliyopitia moyoni mwangu kwa kweli ilikuwa hisia ya furaha ya kweli. Niliona kwamba hatimaye niliweza kutia baadhi ya maneno ya Mungu katika vitendo, jambo ambalo lilikuwa gumu sana kwangu hapo awali. Kujitelekeza na kukubali mapendekezo ya wengine lilikuwa jambo gumu sana, lakini sasa ninaweza kutenda maneno kiasi ya Mungu. Naweza hatimaye kuishi kwa kudhihirisha mfano kidogo wa mwanadamu. Mimi si fidhuli kama nilivyokuwa hapo awali, simchukizi sana Mungu, na siwazuii wengine kama vile nilivyofanya hapo awali. Kila ninapofikiria hayo yote, nahisi kumshukuru sana Mungu. Isingekuwa Mungu kunishughulika na kunipogoa mimi, bila hukumu na ufunuo wa maneno Yake, sijui ningeweza kuwa na kiburi au mpotovu jinsi gani hivi sasa. Ufahamu na mabadiliko kidogo sana ambayo nimepata leo ni kwa ajili tu ya hukumu na kuadibu kwa maneno ya Mungu.

Iliyotangulia: 65. Mfano wa Binadamu Unafikiwa kwa Kutatua Kiburi

Inayofuata: 68. Ulinzi wa Mungu

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

69. Kurudi kwenye Njia Sahihi

Chen Guang, MarekaniMwenyezi Mungu anasema, “Kumtumikia Mungu si kazi rahisi. Wale ambao tabia yao potovu haibadiliki hawawezi kamwe...

3. Jaribu la Foili

Na Xingdao, Korea ya Kusini“Ee Mungu! Kama nina hadhi au la, sasa ninajielewa mwenyewe. Hadhi yangu ikiwa juu ni kwa sababu ya kuinuliwa na...

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp