64. Kiburi Huja Kabla ya Kuanguka

Na Xinjie, Uchina

Mwenyezi Mungu anasema, “Kiburi ndicho chanzo cha upotovu wa mwanadamu. Kadiri watu wanavyozidi kuwa na kiburi, ndivyo wanavyozidi kuwa na uelekeo wa kumpinga Mungu. Tatizo hili ni kubwa kiasi gani? Siyo tu kwamba watu wenye tabia ya kiburi humfikiria kila mtu mwingine kuwa duni kuwaliko, lakini lililo baya zaidi, wao hata huwa na mtazamo wa udhalilishaji kwa Mungu. Hata ingawa, kwa nje, watu wengine wanaweza kuonekana kana kwamba wanamwamini Mungu na kumfuata, hawamchukulii kama Mungu hata kidogo. Wao huhisi sikuzote kuwa wanamiliki ukweli na wanajipenda mno. Hiki ndicho kiini na chanzo cha tabia ya kiburi, na hutoka kwa Shetani. Kwa hivyo, tatizo la kiburi lazima litatuliwe. Kuhisi kuwa wewe ni bora kuliko wengine—hilo ni jambo dogo. Suala la muhimu ni kwamba tabia ya kiburi ya mtu humzuia mtu kumtii Mungu, sheria Yake, na mipango Yake; mtu kama huyo daima huhisi kuwa na uelekeo wa kushindana na Mungu kuwatawala wengine. Mtu wa aina hii hamchi Mungu hata kidogo, sembuse kumpenda Mungu au kumtii(Ushirika wa Mungu). Kusoma maneno haya ya Mungu kulinikumbusha jambo ambalo nilipitia wakati fulani uliopita. Hapo zamani, nilikuwa mwenye kiburi na mwenye kujidai sana. Nilikuwa kiongozi wa kanisa kwa miaka kadhaa, nilikuwa nimefanya kazi kiasi na nilikuwa nimeteseka kidogo, na niliweza kutatua masuala fulani ya vitendo katika wajibu wangu. Kwa hivyo nilitumia yote haya kwa manufaa yangu, na sikumjali mtu mwingine yeyote. Kisha nilishughulikiwa na kufundishwa nidhamu, na kupitia hukumu na ufunuo wa maneno ya Mungu, mwishowe nilipata ufahamu wa asili yangu ya kiburi. Nilihisi majuto na nilijichukia. Nilianza kulenga kutenda ukweli, na nilipitia mabadiliko kiasi.

Nilichukua wadhifa wa uongozi katika kanisa moja mnamo 2015. Dada Li alifanya kazi pamoja nami, na alikuwa ameanza tu kutumikia kama kiongozi. Mashemasi wa kanisa na viongozi wa makundi walikuwa wapya katika imani, kwa hivyo ushirika wao juu ya ukweli ulikuwa wa juu juu kidogo. Niliwaza, “Nimekuwa muumini kwa muda mrefu kuliko yeyote kati yenu, na nimekuwa kiongozi kwa muda. Nitalazimika kuwajibikia kazi kubwa hapa na nimfanye kila mtu aone tofauti inayoletwa na uzoefu.” Kwa hivyo, katika jambo lolote, nilikimbia mbele na wakati wowote ambapo ndugu alikuwa dhaifu au alikuwa na shida katika wajibu wake, wakati wowote ambapo kazi ya kanisa ilichelewa, katika matatizo yoyote ambayo yalikuwa mabaya sana, au vitu ambavyo mbia na wafanyakazi wenzangu hawangeweza kusuluhisha, nilijitokeza kuyashughulikia yote hayo. Kazi ya kanisa ilianza kupata kasi baada ya muda mfupi na hali za kina ndugu zilikuwa zimebadilika. Wote waliweza kufanya wajibu wao ipasavyo. Walipenda pia kunitafuta ili tufanye ushirika juu ya shida zao, na waliuliza maoni yangu. Nilipendezwa na kazi yangu sana na sikuweza kujizuia kujumuisha kazi yote ambayo nilikuwa nimefanya, nikiwaza: “Bila mimi uongozini, hakuna jinsi ambavyo kazi ya kanisa ingekuwa inaendelea vizuri sana. Isingekuwa kwa sababu ya ushirika wangu, hali za wengine zisingeboreka sana. Inaonekana kama kweli nina uhalisi wa ukweli na ninaweza kufanya kazi ya vitendo.” Dada Li baadaye alilazimika kurudi nyumbani ili ashughulikie mambo fulani, kwa hivyo ilibidi niifanye kazi ya kanisa peke yangu. Mwanzoni, nilihisi mfadhaiko kidogo na nilimweka Mungu moyoni mwangu wakati wote. Baada ya kila mkutano nilifanya tathmini ya jinsi mkutano ulivyoenda, na nilikimbia kumsaidia mtu yeyote aliyehisi dhaifu au hasi. Baada ya muda, niliona kwamba kila mtu alikuwa akikusanyika na kufanya wajibu wake anavyopaswa, na kazi zote za kanisa zilikuwa zikienda vizuri. Nilitanafusi na sikuweza kujizuia kupendezwa na juhudi zangu. Nilihisi kama kwamba nilikuwa nimejithibitisha katika miaka hii yote ya kutumikia kama kiongozi, kwamba nilikuwa nimeona mengi na kushughulikia matatizo mengi. Nilikuwa na uzoefu mbali mbali wa kazi na ningeweza kushughulikia mambo peke yangu. Nilifikiria kweli nilikuwa nguzo ya kanisa. Hasa katika kipindi hicho, wakati nilikuwa nikiamka mapema na kufanya kazi hadi usiku bila kulalamika kuhusu uchovu au ugumu, nilihisi kweli nilipaswa kuheshimiwa. Punde si punde, nilikuwa nikiishi katika hali ya kuridhika mwenyewe sana na kila niliposoma maneno ya Mungu yakiwahukumu na kuwafunua wanadamu, sikuwa nikiyatumia kwangu mwenyewe. Wakati kina ndugu walikuwa katika hali mbaya, sikufanya ushirika juu ya ukweli pamoja nao, lakini badala yake niliwadharau na mara nyingi niliwakaripia, nikisema, “Umekuwa muumini kwa muda mrefu, lakini bado hufuatilii ukweli. Unawezaje kuwa hujabadilika hata kidogo?” Wakati mwingine baada ya kufanya ushirika juu ya jambo, kina ndugu walisema bado hawakujua la kufanya. Bila kuuliza kwa nini, ningewasuta tu, nikisema, “Siyo kwamba hujui, ni kwamba hutaki kulitia katika vitendo!” Wote walihisi kuzuiliwa na mimi na hawakuthubutu kuzungumza nami kuhusu shida zao tena.

Dada Liu baadaye alichaguliwa kama kiongozi kufanya kazi pamoja nami. Nilidhani kwamba hakuwa amedumu katika imani kwa muda mrefu na hangeweza kuelewa mambo fulani hata baada ya majadiliano, kwa hivyo nilipaswa kuwa na kauli ya mwisho kwa masuala mengi ya kanisa, makubwa kwa madogo. Wakati mwingine nilifanya uamuzi na kisha kumtuma Dada Liu aende kutekeleza. Wakati mmoja, tulipata barua kutoka kwa kiongozi akituuliza tumpendekeze mtu kwa ajili ya wajibu fulani. Nilijua hili lilihusiana na kazi ya nyumba ya Mungu, kwa hivyo lilihitaji majadiliano na mbia wangu na wafanyakazi wenzangu, lakini nikawaza, “Nimekuwa nikifanya wajibu wangu kanisani kwa muda mrefu sana. Ninajua kila kitu kuwahusu kina ndugu, kwa hivyo itakuwa sawa nikifanya uamuzi huo.” Kwa hivyo, nilifanya uamuzi bila kujadili na Dada Liu kisha nikamwambia aende apange mambo. Hata ingawa tulitumikia kama viongozi pamoja, nilikuwa nikimtendea kama mdogo kwa cheo. Wakati mwingine wakati hakufanya kitu vizuri, nilimkasirikia. Alikuwa akiishi katika uhasi na alihisi kama kwamba hakuweza kuelewa chochote au kufanya wajibu wake vizuri. Alikuwa amefikia hatua hiyo kutokana na mimi kumzuilia, lakini bado sikujitafakari. Badala yake, nilihisi hata zaidi kuwa nilikuwa na uhalisi wa ukweli na nilikuwa na uwezo katika kazi yangu, kwa hivyo ilinibidi nisimamie kazi ya kanisa. Nilizidi kuwa mwenye kujiona sana na mwenye kiburi. Wafanyakazi wenzangu walipotoa maoni tofauti wakati wa majadiliano ya kazi, wakati mwingi sikutafuta kabisa, lakini niliyakataa tu kabisa. Niliwaza, “Unajua nini hata hivyo? Mimi sijui zaidi baada ya miaka mingi kama kiongozi?” Niliishia kuwa na usemi wa mwisho juu ya kila kitu katika kazi ya kanisa. Baadaye Mungu aliruhusu hali fulani ziibuke ili Anishughulikie. Niliendelea kugonga mwamba katika wajibu wangu. Nilikosa miadi na watu, na kuwateua watu ambao hawakulingana na kanuni. Kiongozi huyo alitaja makosa katika kazi yangu, na akanishughulikia na kunipogoa. Hata nikikabiliwa na haya, bado sikutafakari kujihusu. Nilidhani kwamba nilihitaji tu kuwa mwenye kuzingatia zaidi. Mfanyakazi mwenzangu alinionya, “Je, hupaswi kutafakari ni kwa nini shida hizi zimeibuka?” Nilisema kwa dharau, “Hakuna mtu aliye mkamilifu, na kila mtu hufanya makosa. Hakuna haja ya kutafakari juu ya kila kitu.” Ndugu wengine waliniuliza ikiwa nilikuwa nikiendelea vizuri, na nikasema nilikuwa sawa, lakini ndani nilikuwa nikiwaza, “Kwa nini kitu kisiwe sawa? Hata kama ningekuwa katika hali mbaya, ningeweza kuishughulikia mwenyewe. Hakuna haja ya wewe kuwa na wasiwasi. Nimekuwa kiongozi kwa muda mrefu hivyo si ninaelewa ukweli vyema kuliko wewe?” Haijalishi jinsi walivyonitahadharisha, sikusikiza. Mimi nilikuwa nikiishi kabisa ndani ya tabia yangu potovu na roho yangu ilikuwa ikizidi kuwa ovu. Nilianza kusinzia niliposoma maneno ya Mungu na nikakosa kitu cha kusema katika maombi. Shida zaidi na zaidi zilianza kutokea kanisani. Nilikuwa kipofu kabisa. Nilikosa utambuzi katika shida nyingi na sikujua jinsi ya kuzishughulikia. Muda si muda, uchunguzi wa maoni ya jumla ulifanywa kanisani, na kina ndugu wote walisema kwamba nilikuwa mwenye kiburi sana na sikukubali ukweli. Walisema nilikuwa dikteta, kwamba niliwakemea watu na kuwazuia. Niliishia kuondolewa kutoka katika wadhifa wangu. Siku hiyo, kiongozi alishiriki na mimi tathmini za kila mtu. Niliweza kuhisi Mungu akinieleza waziwazi ghadhabu Yake kwangu kupitia kina ndugu kunifunua na kunishughulikia. Nilihisi kama panya wa mitaani anayemchukiza kila mtu na hata kukataliwa kwa dharau na Mungu. Sikuelewa jinsi nilikuwa mwovu sana. Katika uchungu wangu, nilikuja mbele za Mungu katika kutafuta: “Ee Mungu, Siku zote nimejifikiria kuwa mwenye kuwajibika katika kazi yangu ya kanisa, kama aliye na uhalisi fulani wa ukweli. Sikuwahi kufikiria ningepata shida nyingi kama ninavyopata sasa. Machoni pa wengine, mimi ni mtu mwenye kiburi asiyekubali ukweli. Mungu, sijui nilikuwaje hivi. Tafadhali nipe nuru na Uniongoze nijijue na nielewe mapenzi Yako.”

Kisha nilisoma maneno haya kutoka kwa Mungu: “Ingekuwa bora kwenu kuweka juhudi zaidi kwa ukweli wa kuzijua nafsi zenu. Mbona hamjapata fadhili kwa Mungu? Kwa nini tabia zenu ni chukizo sana Kwake? Kwa nini maneno yenu yanachochea chuki Yake? Punde ambapo mmeonyesha uaminifu kidogo, nyinyi mnajisifu wenyewe, na mnadai malipo kwa ajili ya mchango mdogo; nyinyi huwadharau wengine wakati nyinyi mnaonyesha utiifu kidogo, na kumdharau Mungu baada ya kufanya kazi ndogo. … Wale ambao wanatekeleza wajibu wao na wale wasiofanya; wale ambao huongoza na wale ambao hufuata; wale wanaompokea Mungu na wale wasiompokea; wale wanaotoa na wale wasiotoa; wale wanaohubiri na wale ambao hupokea neno, na kadhalika; watu wote kama hawa hujisifu wenyewe. Je, hamuoni hili likiwa la kuchekesha? Mkijua vyema kwamba mnamwamini Mungu, hata hivyo ninyi hamwezi kulingana na Mungu. Kweli mnajua vyema kwamba hamstahili hata kidogo. Je, hamhisi kuwa hisia yenu imepunguka kiasi kwamba hamwezi tena kujizuia?(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wale Ambao Hawalingani na Kristo Hakika Ni Wapinzani wa Mungu). “Usidhani kwamba unaelewa kila kitu. Nakueleza kwamba yote uliyokwishayaona na kuyapitia hayakutoshelezi wewe kuelewa hata sehemu ndogo kabisa ya mpango Wangu wa usimamizi. Hivyo kwa nini basi unakuwa mwenye kiburi sana? Talanta ndogo hiyo uliyonayo na maarifa kidogo hayo uliyonayo hayatoshelezi kutumika na Yesu hata katika sekunde moja ya kazi Yake! Je, una uzoefu kiasi gani hasa? Yale uliyoyaona na yote uliyoyasikia katika maisha yako yote na yale uliyoyafikiria ni kidogo kuliko kazi Ninayoifanya kwa muda mfupi sana! Ni bora usichambue na kutafuta kosa. Haijalishi una kiburi kiasi gani, wewe bado ni kuimbe tu mdogo kuliko mchwa! Vyote vilivyomo katika tumbo lako ni vichache zaidi ya vile vilivyomo katika tumbo la mchwa! Usifikiri kwamba kwa kuwa tu umepata uzoefu na ukubwa kiasi, unaweza kuashiria kiburi na kuzungumza kwa maringo. Je, uzoefu wako na ukubwa wako sio matokeo ya maneno Niliyoyazungumza? Je, unaamini kwamba yalikuwa mbadala wa kufanya kwako kazi kwa bidii na kutokwa jasho?(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kupata Mwili Mara Mbili Kunakamilisha Umuhimu wa Kupata Mwili). Kile ambacho maneno ya Mungu yalifichua kilikuwa hali yangu hasa. Nilisikitika sana, na ni hapo tu ndipo nilianza kutafakari juu yangu mwenyewe. Baada ya kufanya wajibu wangu kama kiongozi kwa miaka michache, nilidhani kwamba kwa vile nilikuwa katika nafasi hiyo kwa muda, nilielewa ukweli zaidi na nilikuwa na uwezo zaidi kuliko wale wengine, ya kwamba nilikuwa nguzo ya kanisa, na kanisa halingeweza kuendelea bila mimi. Nilipofanikiwa kidogo katika wajibu wangu, nilidhani kwamba nilielewa kila kitu, kwamba nilikuwa na uhalisi wa ukweli, kwamba nilikuwa bora kuliko kila mtu. Nilidhani kwamba kuwa na imani kwa muda, kuwa na uzoefu kiasi kilikuwa kibali changu cha kuwa mwenye kiburi na kwamba nilikuwa kwenye ngazi ya juu kuliko watu wengine. Sikuyatilia maanani maoni ya kina ndugu hata kidogo, sembuse kutafuta au kuyakubali. Hata wakati ambapo walinijali na waliuliza kuhusu hali yangu, nilihisi nilikuwa na kimo kikubwa kuwaliko, kwa hivyo niliweza kuishughulikia, na sikuhitaji msaada wao. Nilipogundua makosa na ugumu wao, sikufanya ushirika juu ya ukweli kuwasaidia, lakini niliwapuuza. Hawakuweza tu kufanya vyema kabisa machoni pangu na niliwakaripia sana. Kama matokeo, kina ndugu walizuiliwa na mimi na waliishi katika uhasi. Huko kulikuwaje kufanya wajibu wangu? Ni wazi kwamba kulikuwa kufanya uovu. Nilifichua tu tabia ya kishetani ya kiburi, yenye majivuno. Mungu alipokuwa mwili katika siku za mwisho, Akionyesha ukweli na kufanya kazi ili kumwokoa mwanadamu, Alifanya kazi kubwa sana, lakini Hakujionyesha kamwe, na Hakujiwasilisha kama Mungu. Badala yake, Alikuwa mnyenyekevu na Aliyefichwa, Akifanya kazi ya wokovu kimya kimya. Niliona kwamba Mungu ni mnyenyekevu na Anayependeza sana, lakini mimi, nikiwa nimepotoshwa sana na Shetani na niliyejaa tabia za kishetani, nilifikiria makuu sana kujihusu na kuhusu uwezo wangu kwa sababu tu nilikuwa na imani kwa muda, na nilielewa mafundisho zaidi, na nilikuwa na uzoefu kiasi wa kazi. Nilijikweza na singeshuka. Nilikosa kujifahamu kabisa, sikujua chochote kujihusu, na nilikuwa mwenye kiburi kupita kiasi. Nilikuwa mtu mbaya mno. Baada ya kufunuliwa na Mungu, mwishowe niliona kimo changu cha kweli. Niliweza kusuluhisha masuala fulani katika wajibu wangu kwa sababu tu ya kazi ya Roho Mtakatifu. Bila kazi na mwongozo Wake, nilikuwa kipofu kabisa na sikuelewa chochote. Sikuweza kusuluhisha matatizo yangu mwenyewe, sembuse ya watu wengine. Hata hivyo, nilizidi kuwa mwenye kuwalazimisha wengine. Kwa kweli nilikuwa mwenye kiburi. Wakati huo nilihisi aibu kwa sababu ya tabia yangu.

Kisha nilisoma maneno haya ya Mungu: “Kama kwa kweli una ukweli ndani yako, njia unayotembea kiasili itakuwa njia sahihi. Bila ukweli, ni rahisi kufanya uovu na hutakuwa na budi kuufanya. Kwa mfano, kama kiburi na majivuno, vingekuwa ndani yako, ungeona kwamba haiwezekani kuepuka kumwasi Mungu; ungehisi kulazimishwa kumwasi. Hutafanya hivyo kimakusudi; utafanya hivyo chini ya utawala wa asili yako ya kiburi na majivuno. Kiburi na majivuno yako vitakufanya umdharau Mungu na kumwona kuwa asiye na maana; vitakufanya ujiinue, vitakufanya kujiweka kila wakati kwenye maonyesho, na mwishowe vitakufanya ukae katika nafasi ya Mungu na kujitolea ushuhuda mwenyewe. Mwishowe utayabadilisha mawazo yako mwenyewe, fikira zako mwenyewe na dhana zako yawe ukweli wa kuabudiwa. Tazama ni kiasi gani cha uovu kinafanywa na watu chini ya utawala wa asili yao ya kiburi na majivuno! Kutatua matendo yao maovu, lazima kwanza watatue matatizo ya asili yao. Bila mabadiliko katika tabia, haitawezekana kuleta suluhu ya kimsingi kwa shida hii(“Ni Kwa Kufuatilia Ukweli Tu Ndiyo Unaweza Kupata Mabadiliko Katika Tabia Yako” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Baada ya kusoma maneno ya Mungu niligundua kuwa asili yangu ya majivuno ndicho kiini cha mimi kufanya uovu na kumpinga Mungu. Nikiongozwa na asili yangu ya kiburi, nilijichukulia sifa za matokeo ya kazi ya Roho Mtakatifu nilipokuwa na mafanikio kidogo katika wajibu wangu, nikijionyesha kama anayeheshimiwa zaidi kanisani. Niliamini bila aibu kuwa mpokeaji wa wokovu wa Mungu, ilhali sikujijua hata kidogo. Katika wajibu wangu, nilikuwa nikionyesha ukuu wangu kila wakati, nikijifikiria kuwa bora na wa juu zaidi ya mtu yeyote, kila wakati nikiwatala wengine. Hata nilitumia maneno ya Mungu kuwaonya kina ndugu, na wakati wa kupanga kazi sikujadili mambo na dada huyo aliyefanya kazi na mimi. Badala yake, nilifanya kazi kidikteta na nilikuwa na kauli ya mwisho. Hata nilifanya maamuzi peke yangu juu ya mambo muhimu kwa kazi ya nyumba ya Mungu. Nilimfanya dada huyo mkubwa wa jina tu na nikajiundia ufalme wangu mwenyewe kanisani. Kwa sababu ya asili yangu ya kiburi, nilimdharau kila mtu mwingine na sikumweka Mungu moyoni mwangu. Sikufuta kanuni za ukweli nilipokabiliwa na tatizo, na hata niliyachukua maoni yangu mwenyewe kama ukweli, nikimfanya kila mtu mwingine anisikilize na kunitii. Ilinikumbusha kuhusu Mungu akimpa malaika mkuu mamlaka kiasi ya kuwasimamia malaika wengine mbinguni, lakini alipoteza busara yote katika kiburi chake, akihisi kwamba alikuwa wa kipekee na alitaka kuwa sawa na Mungu. Kama matokeo, hili liliikosea tabia ya Mungu, na Mungu akamlaani na kumtupa kutoka mbinguni. Na sasa, Mungu aliniinua kufanya kazi kama kiongozi ili niweze kumwinua na kumshuhudia katika mambo yote, ili niweze kushiriki juu ya ukweli kusuluhisha matatizo ya vitendo, niwasaidie wengine waelewe ukweli na wamtii Mungu. Lakini sikufuta ukweli au kufanya wajibu wangu kulingana na mahitaji ya Mungu. Badala yake nilishikilia madaraka, nikajiweka katikati, na nikamfanya kila mtu anisikilize na kunitii. Je, nilikuwaje tofauti na malaika mkuu? Mungu alipanga hali ili kuizuia njia yangu, na kisha Akanionya kupitia kwa kina ndugu, lakini sikukubali hilo au kujitafakari. Nilikuwa mgumu na mwasi sana! Nilikuwa nikifanya wajibu wangu na tabia yangu ya kiburi, nikiwazuilia kina ndugu, hili likisababisha waishi katika uhasi na wasiweze kutatua shida zao. Hakukuwa na maendeleo yoyote katika kazi ya kanisa. Huo wote ni uovu niliofanya kutokana na kudhibitiwa na majivuno yangu! Nina asili kaidi na ya kiburi sana. Bila Mungu kunifunua na kunishughulikia vikali kupitia kina ndugu, na kuniondoa kutoka katika wajibu wangu, singewahi kujitafakari. Kama hilo lingeendelea, ningetenda tu uovu zaidi. Ningeikosea tabia ya Mungu, kisha nilaaniwe na kuadhibiwa na Mungu, kama tu malaika mkuu. Wakati huo nilipata ufahamu wa nia njema za Mungu. Alikuwa akifanya hivi ili Anikomeshe katika njia zangu za uovu na kunipa nafasi ya kutubu. Huyu alikuwa ni Mungu aliyekuwa akinilinda na kuniokoa. Nilimshukuru Mungu kwa dhati.

Baada ya mimi kubadilishwa, Dada Liu aliweza kutekeleza wajibu wake kawaida, na kutoka kwa yale ambayo wengine walisema, hata ingawa kiongozi aliyekuwa amechaguliwa tu na mashemasi hawakuwa wameamini kwa muda mrefu, wakati wa kujadili kazi hakuna mtu aliyeshikilia maoni yake, lakini badala yake waliomba na kumtegemea Mungu, wakitafuta kanuni za ukweli pamoja. Wote walifanya kazi kwa pamoja, na kazi ya kanisa ilishika kasi tena polepole. Kwa kweli niliaibika kusikia hili. Siku zote nilifikiria kazi ya kanisa haingeendelea bila mimi, lakini nikikabiliwa na ukweli, niliona kwamba kazi yote ya nyumba ya Mungu inafanywa na kuungwa mkono na Roho Mtakatifu, na si jambo ambalo mtu yeyote mmoja anaweza kufanya. Watu wanashirikiana tu na kufanya wajibu wao wenyewe. Haijalishi tumemwamini Mungu kwa muda gani, mradi tunamtegemea Mungu kutafuta na kutenda ukweli katika wajibu wetu, tutakuwa na mwongozo na baraka za Mungu. Kufanya wajibu wangu bila kutafuta ukweli, lakini kufanya chochote nilichotaka kwa kiburi, na kuwa na udikteta kulimchukiza Mungu. Bila mwongozo wa Mungu, nilipoteza kazi ya Roho Mtakatifu na nikawa sina thamani. Sikuweza kufanya chochote. Nilikuwa mwenye kiburi bila kujua, nikifanya nilichotaka, nikiwaamuru watu huku na kule kwa kiburi, nikiwazuia na kuwadhuru kina ndugu, na niliivuruga kazi ya kanisa. Nilijihisi mwenye hatia sana, na nilijilaumu sana. Nilimwomba Mungu: “Mungu, nimekuwa kipofu sana. Sijajijua, kila wakati nikifikiria kwamba nilielewa zaidi kwa sababu nilikuwa kiongozi kwa muda mrefu, kwa hivyo nilikuwa bora kumliko kila mtu. Kiburi changu kiliniongoza katika wajibu wangu, na hili liliivuruga kazi ya nyumba Yako. Ee Mungu, sitaki kukupinga tena, na natamani kutubu kweli.”

Kisha nilisoma haya katika maneno ya Mungu: “Ni lazima ujue aina ya watu ambao Ninataka; wale walio najisi hawakubaliki kuingia katika ufalme, wale walio najisi hawakubaliki kuchafua nchi takatifu. Ingawa unaweza kuwa umefanya kazi nyingi, na umefanya kazi kwa miaka mingi, mwishowe kama bado wewe ni mwovu kupindukia—hakuvumiliki kwa sheria ya Mbinguni kwamba wewe unataka kuingia katika ufalme wangu! Tangu mwanzo wa dunia hadi leo, kamwe Sijatoa njia rahisi ya kuingilia ufalme Wangu kwa wale wenye neema Yangu. Hii ni sheria ya Mbinguni, na hakuna awezaye kuivunja. Ni lazima utafute uzima. Leo, wale watakaofanywa wakamilifu ni wa aina sawa na Petro: ni wale ambao hutafuta mabadiliko katika tabia yao wenyewe, na wako tayari kuwa na ushuhuda kwa Mungu na kutekeleza wajibu wao kama kiumbe wa Mungu. Ni watu kama hawa pekee watakaofanywa wakamilifu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mafanikio au Kushindwa Kunategemea Njia Ambayo Mwanadamu Hutembea). “Ninaamua hatima ya kila mtu si kwa kuzingatia umri, ukubwa, kiwango cha mateso, sembuse kiwango ambacho kwacho anataka huruma, bali kulingana na ikiwa anao ukweli. Hakuna chaguo lingine ila hili. Sharti mtambue kwamba wale wote ambao hawafuati mapenzi ya Mungu wataadhibiwa pia. Huu ni ukweli usiobadilika(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Tayarisha Matendo Mema ya Kutosha kwa ajili ya Hatima Yako). Maneno ya Mungu yalikuwa wazi kabisa. Mungu huwa haamui matokeo ya watu kulingana na muda ambao wameamini, wanaweza kuhubiri kiasi gani, au wamefanya kazi kiasi gani, lakini kulingana na kama wanafuatilia ukweli, ikiwa wamebadili tabia zao potovu, na ikiwa wanaweza kufanya wajibu wa kiumbe aliyeumbwa. Hivi ndivyo vitu muhimu sana. Hapo awali, sikuwahi kuijua tabia ya Mungu ya haki. Nilikuwa nimeamini kwa muda, nilikuwa na uzoefu wa miaka michache kama kiongozi, na nilikuwa nimepata ufanisi kiasi katika wajibu wangu. Nilitumia yote haya kwa faida yangu. Nilidhani kama ningeendelea kufuatilia kwa njia hiyo, ningeokolewa na Mungu, kwa hivyo sikulenga kupitia kuhukumiwa, kuadibiwa, kushughulikiwa na kupogolewa na Mungu. Hasa sikujali sana kutafutilia ukweli katika wajibu wangu ili kutatua tabia zangu potovu. Kama matokeo, tabia yangu ya maisha ilibadilika kidogo sana baada ya miaka mingi ya imani katika Mungu, na nilikuwa nikiishi kwa kufuata asili yangu ya kishetani, ya kiburi, nikifanya uovu na kumpinga Mungu. Niliona kuwa hatuwezi kujijua au kutubu kwa kweli kwa Mungu tusipofuatilia ukweli katika imani yetu. Haijalishi tumefanya kazi kiasi gani, tumehubiri kiasi gani, bila mabadiliko katika tabia yetu ya maisha, bado tutashutumiwa na kuondolewa na Mungu. Hili linaamuliwa na tabia ya haki ya Mungu na kiini Chake kitakatifu. Baada ya kuelewa mapenzi ya Mungu sikuchukulia faida kuamini kwangu kwa muda au kiasi cha kazi niliyokuwa nimefanya, lakini nilianza kuzingatia kuweka bidii katika maneno ya Mungu, nikitafakari na kujijua, na kufuatilia mabadiliko katika tabia zangu za kishetani.

Baada ya hapo, nilipewa wajibu mwingine kanisani. Wakati wa kufanya kazi na kina ndugu, nilikuwa mnyenyekevu zaidi, na walipotoa maoni tofauti, wakati mwingine nilihisi kwamba nilikuwa sahihi na nilitaka wanisikilize, lakini niligundua haraka kwamba nilikuwa nikionyesha tabia yangu ya majivuno tena, kwa hivyo nilimwomba Mungu na kujitelekeza ili nitafute ukweli pamoja na kina ndugu, na kutatua mambo kupitia majadiliano. Ndugu wote walisema kwamba sikuwa mwenye kiburi kama hapo awali, kwamba nilikuwa mkomavu zaidi. Kusikia tathmini hii kutoka kwao kulinigusa sana. Nilijua haya yalifanikishwa na hukumu na kuadibu kwa maneno ya Mungu. Hata ingawa sijatupilia mbali tabia yangu ya majivuno kabisa na mimi bado niko mbali sana na viwango ambavyo Mungu anahitaji, nimeuona upendo na wokovu wa Mungu. Nimeona kwamba kazi na maneno ya Mungu kweli yanaweza kuwabadilisha na kuwatakasa watu.

Iliyotangulia: 63. Ni Nani Anayesema Tabia Ya Kiburi Haiwezi Kubadilishwa

Inayofuata: 65. Mfano wa Binadamu Unafikiwa kwa Kutatua Kiburi

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

1. Nimebahatika Kumhudumia Mungu

Na Gensui, Korea ya KusiniMwenyezi Mungu anasema, “Ni kupitia nini ndiyo ukamilishaji wa Mungu kwa mwanadamu hutimizwa? Kupitia tabia Yake...

62. Kuinuka licha ya kushindwa

Na Fenqi, Korea ya KusiniKabla ya kumwamini Mungu, nilifundishwa na CCP, na sikufikiria chochote ila jinsi ya kufaulu kutokana na juhudi...

13. Ukombozi wa Moyo

Na Zheng Xin, MarekaniMnamo Oktoba ya 2016, mimi na mume wangu tulikubali kazi ya Mungu katika siku za mwisho wakati tulikuwa ughaibuni....

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp