Maono ya Kazi ya Mungu (2)
Enzi ya Neema ilihubiri injili ya toba, na alimradi mwanadamu aliamini, basi angeokolewa. Leo, badala ya wokovu kuna majadiliano tu ya ushindi na ukamilifu. Haisemwi katu kwamba mtu mmoja akiamini, familia yake yote itabarikiwa, au kwamba wokovu ni ya mara moja na kwa wote. Leo, hakuna mtu anayezungumza maneno haya, na vitu kama hivyo vimepitwa na wakati. Wakati huo kazi ya Yesu ilikuwa ni ukombozi wa wanadamu wote. Dhambi za wote ambao walimwamini zilisamehewa; ilimradi wewe ulimwamini, Angeweza kukukomboa wewe; kama wewe ulimwamini Yeye, wewe hukuwa tena mwenye dhambi, wewe ulikuwa umeondolewa dhambi zako. Hii ndiyo ilikuwa maana ya kuokolewa, na kuhesabiwa haki kwa imani. Hata hivyo, kati ya wale walioamini, kulibaki na kitu ambacho kilikuwa na uasi na pingamizi kwa Mungu, na ambacho bado kilibidi kiondolewe polepole. Wokovu haukuwa na maana kuwa mwanadamu alikuwa amepatwa na Yesu kabisa, lakini ni kuwa mwanadamu hakuwa tena mwenye dhambi, na kuwa alikuwa amesamehewa dhambi zake; mradi tu uliamini, wewe kamwe hungekuwa mwenye dhambi. Wakati huo, Yesu alifanya kazi kubwa ambayo haikueleweka kwa wanafunzi Wake, na kusema mengi kwamba watu hawakuelewa. Hii ni kwa sababu, wakati huo, Hakutoa maelezo. Kwa hivyo, miaka kadhaa baada ya Yeye kuondoka, Mathayo aliunda nasaba Yake, na wengine pia walifanya kazi kubwa ambayo ilikuwa ya mapenzi ya mwanadamu. Yesu hakuja kumkamilisha na kumpata mwanadamu, lakini kufanya awamu moja ya kazi: kuleta injili ya ufalme wa mbinguni na kukamilisha kazi ya kusulubiwa—na punde tu Yesu Aliposulubishwa, kazi Yake ilifika mwisho kamili. Lakini kwa awamu iliyoko sasa—kazi ya ushindi—maneno mengi zaidi lazima yasemwe, kazi nyingi zaidi lazima ifanywe, na lazima kuwe na hatua nyingi. Hivyo pia ni lazima siri za kazi ya Yesu na Yehova zitafichuliwa, ili wanadamu wote waweze kuwa na ufahamu na uwazi wa imani yao, kwa kuwa hii ni kazi ya siku za mwisho, na siku za mwisho ni mwisho wa kazi ya Mungu, wakati wa kuhitimisha kazi hii. Hii awamu ya kazi itakufafanulia sheria ya Yehova na ukombozi wa Yesu, na ni hasa ili uweze kuelewa kazi nzima ya mpango wa usimamizi wa Mungu wa miaka elfu sita, na kuelewa umuhimu na kiini cha mpango huu wa usimamizi wa miaka elfu sita, na kuelewa kusudi la kazi zote Alizozifanya Yesu na maneno Aliyoyasema, na hata upofu wako wa imani kwenye na katika kuabudu Biblia. Yote haya yatakuwezesha kuelewa kabisa. Wewe utakuja kufahamu kazi aliyoifanya Yesu na kazi ya Mungu leo; utaelewa na kushuhudia ukweli wote, uzima, na njia. Katika hatua ya kazi iliyofanywa na Yesu, kwa nini Yesu aliondoka bila kufanya kazi ya mwisho? Kwa sababu hatua ya kazi ya Yesu haikuwa kazi ya hitimisho. Wakati Yeye Alisulubishwa msalabani, maneno Yake pia yalifika mwisho; baada ya kusulubiwa kwake, kazi Yake kwa hivyo ilimalizika. Awamu ya sasa ni tofauti. Ni baada tu ya maneno hayo kusemwa hadi mwisho na kazi nzima ya Mungu iwe imehitimika ndipo kazi yake itakapokuwa imemalizika. Wakati wa hatua ya kazi ya Yesu, kulikuwa na maneno mengi ambayo hayakusemwa, au ambayo hayakuelezwa kikamilifu. Hata hivyo, Yesu hakujali Alichosema au kile ambacho hakusema, kwa kuwa huduma yake haikuwa huduma ya maneno; na hivyo baada ya Yeye kusulubishwa msalabani Aliondoka. Awamu hiyo ilikuwa hasa kwa ajili ya kusulubiwa, na ni tofauti na awamu ya sasa. Hatua hii ya kazi kimsingi ni kwa ajili ya kukamilisha, kusafisha, na kuhitimisha kazi yote. Kama maneno hayasemwi hadi tamati yake kabisa, hakutakuwa na mbinu ya kuhitimisha kazi hii, kwa kuwa awamu hii ya kazi yote inafikishwa mwisho na kukamilika kwa kutumia maneno. Wakati huo, Yesu Alifanya kazi kubwa isiyoeleweka kwa mwanadamu. Akaondoka kimyakimya, na leo bado kunao wengi wasioelewa maneno Yake, ambao ufahamu wao ni potofu lakini bado unaaminika nao kwamba ni sahihi, ambao hawajui kuwa wao si sahihi. Mwishoni, awamu hii ya sasa itafikisha kazi ya Mungu mwisho ulio kamilifu, na kutoa hitimisho Lake. Wote watakuja kufahamu na kujua mpango wa usimamizi wa Mungu. Dhana zilizo ndani ya mwanadamu, nia yake, ufahamu wake potofu, dhana zake kuhusu kazi ya Yehova na Yesu, maoni yake kuhusu Mataifa, na kupotoka kwake na makosa mengine yatarekebishwa. Na mwanadamu ataelewa njia zote sahihi za maisha, na kazi yote inayofanywa na Mungu, na ukweli wote. Wakati hayo yatafanyika, awamu hii ya kazi itafikia kikomo. Kazi ya Yehova ilikuwa uumbaji wa ulimwengu, ilikuwa mwanzo; awamu hii ya kazi ni mwisho wa kazi, na ni hitimisho. Hapo mwanzo, kazi ya Mungu ilifanyika miongoni mwa wateule wa Israeli, na ilikuwa mapambazuko ya kipindi kipya katika pahali patakatifu zaidi ya popote. Awamu ya mwisho ya kazi inafanywa katika nchi ambayo ni chafu zaidi ya zote, kuhukumu ulimwengu na kuleta enzi kwenye kikomo. Katika awamu ya kwanza kazi ya Mungu ilifanyika katika maeneo yenye kung’aa kuliko maeneo yote, na awamu ya mwisho inafanyika katika maeneo yaliyo katika giza kuliko maeneo yote, na giza hili litaondolewa, na mwanga kufunguliwa, na watu wote kushindwa. Wakati watu wa maeneo haya yaliyo chafu kuliko yote na yaliyo na giza watakuwa wameshindwa na idadi yote ya watu wametambua kuwa Mungu yupo, na ya kuwa ni Mungu wa kweli, na kila mtu Amemwamini kabisa, basi ukweli huu utatumika kutekeleza kazi ya ushindi katika ulimwengu mzima. Awamu hii ya kazi ni ya ishara: Punde tu kazi ya kipindi hiki itakapomalizika, kazi ya miaka 6,000 ya usimamizi itafikia mwisho kabisa. Mara baada ya wale walioko katika maeneo yaliyo na giza kuliko yote watakapokuwa wameshindwa, bila shaka itakuwa hivyo pia kila mahali pengine. Kwa hivyo, kazi ya ushindi tu katika China inabeba ishara ya maana. China inajumuisha nguvu zote za giza, na watu wa China wanawakilisha wale wote ambao ni wa mwili, wa Shetani, na wa nyama na damu. Ni watu wa China ndio wamepotoshwa sana na joka kubwa jekundu, ambao wana upinzani wenye nguvu dhidi ya Mungu, ambao wana ubinadamu ulio mbovu zaidi na ulio mchafu, na kwa hivyo hao ni umbo asili la wanadamu wote wenye matendo maovu. Hii si kusema kwamba nchi nyingine hazina shida kabisa; dhana za mwanadamu ni sawa zote, na ingawa watu wa nchi hizi wanaweza kuwa na uhodari mzuri, ikiwa hawamjui Mungu, basi ni lazima iwe kwamba wanampinga. Kwa nini Wayahudi pia walimpinga na kumwasi Mungu? Kwa nini Mafarisayo pia walimpinga? Kwa nini Yuda alimsaliti Yesu? Wakati huo, wengi wa wanafunzi hawakumjua Yesu. Kwa nini, baada ya Yesu kusulubiwa na kufufuliwa tena, watu bado hawakumwamini? Je, uasi wa mwanadamu sio sawa wote? Ni tu kwamba watu wa China wamefanyika mfano, na watakaposhindwa watakuwa mfano na kielelezo, na watatumika kama kumbukumbu kwa wengine. Kwa nini mimi daima Nimesema yakuwa nyinyi ni kiungo cha mpango wangu wa usimamizi? Ni katika watu wa China ambapo upotovu, uchafu, udhalimu, upinzani, na uasi unadhihirishwa kikamilifu zaidi na kufichuliwa kwa hali zao mbalimbali. Kwa upande mmoja, wao ni wa kimo cha umaskini, na kwa upande mwingine, maisha yao na mawazo yao ni ya nyuma kimaendeleo, na tabia zao, mazingira ya kijamii, familia ya kuzaliwa—yote ni ya umaskini na ya nyuma kimaendeleo kuliko yote. Hadhi yao, pia, ni ya chini. Kazi katika eneo hili ni ya ishara, na baada ya kazi hii ya majaribio hufanywa kwa ukamilifu wake, na kazi yake inayofuata itakwenda vizuri zaidi. Kama awamu hii ya kazi inaweza kukamilika, basi kazi inayofuata itakamilika bila shaka. Mara baada ya awamu ya kazi hii kutimizwa, na mafanikio makubwa kufikiwa kikamilifu, kazi ya ushindi katika ulimwengu mzima itakua imefikia kikomo kamili. Kwa kweli, mara baada ya kazi miongoni mwenu imekuwa ya mafanikio, hii itakuwa sawa na mafanikio katika ulimwengu mzima. Huu ndio umuhimu wa sababu Yangu kuwafanya mfano wa kuigwa na kielelezo. Uasi, upinzani, uchafu, udhalimu—yote haya hupatikana kwa watu hawa, na ndani yao pamewakilishwa uasi wote wa wanadamu. Wao ni wa kushangaza kweli. Hivyo, wanafanywa kuwa mfano wa ushindi, na punde tu watakaposhindwa watakuwa kama ilivyo kawaida kielelezo na mfano wa kuigwa na wengine. Hakuna kilichokuwa cha ishara zaidi ya awamu ya kwanza iliyofanyika katika Israeli: Waisraeli walikuwa watakatifu zaidi na wenye upotovu wa chini zaidi kuliko watu wote, na hivyo pambazuko la kipindi kipya katika nchi hii kilibeba umuhimu mkubwa. Inaweza kusemwa kwamba mababu wa wanadamu walitoka Israeli, na kwamba Israeli ilikuwa mahali pa kuzaliwa kwa kazi ya Mungu. Hapo mwanzo, watu hawa walikuwa watakatifu sana, na wote walimwabudu Yehova, na kazi ya Mungu ndani yao iliweza kuzaa mazao makubwa. Biblia nzima inarekodi kazi ya enzi mbili: Moja ilikuwa kazi ya Enzi ya Sheria, na moja ilikuwa kazi ya Enzi ya Neema. Agano la Kale hurekodi maneno ya Yehova kwa Waisraeli na kazi Yake katika Israeli; Agano Jipya linarekodi kazi ya Yesu huko Uyahudi. Lakini kwa nini Biblia haina majina yoyote ya Kichina? Kwa sababu sehemu mbili za kwanza za kazi ya Mungu zilifanyika katika Israeli, kwa sababu watu wa Israeli walikuwa wateule—ambayo ni kusema kwamba wao walikuwa wa kwanza kukubali kazi ya Yehova. Walikuwa wenye upotovu wa chini zaidi ya wanadamu wote, na hapo mwanzo, walikuwa na nia ya kumtazamia Mungu na kumheshimu Yeye. Walitii maneno ya Yehova, na daima walihudumu hekaluni, na walivaa kanzu za ukuhani au taji. Walikuwa watu wa kwanza kabisa kumwabudu Mungu, na chombo cha kwanza kabisa cha kazi yake. Watu hawa walikuwa kielelezo na mfano wa kuiga kwa wanadamu wote. Walikuwa kielelezo na mfano wa kuiga wa utakatifu na haki. Watu kama Ayubu, Ibrahim, Lutu, au Petro na Timotheo—wote walikuwa Waisraeli, na vielelezo na mifano mitakatifu zaidi ya watu wote. Israeli ilikuwa nchi ya kwanza ya kumwabudu Mungu miongoni mwa wanadamu wote, na watu wengi wenye haki walitoka hapa kuliko mahali pengine popote. Mungu Alifanya kazi kati yao ili aweze kusimamia vizuri mwanadamu katika nchi zote na katika siku zijazo. Mafanikio yao na haki ya ibada yao ya Yehova yaliandikwa kwenye kumbukumbu, ili waweze kuhudumu kama vielelezo na mifano kwa watu waliokuwa nje ya Israeli wakati wa Enzi ya Neema; na matendo yao yamezingatia miaka elfu kadhaa ya kazi, mpaka hivi leo.
Baada ya msingi wa ulimwengu, hatua ya kwanza ya kazi ya Mungu ilitekelezwa katika Israeli, na hivyo Israeli ilikuwa mahali pa kuzaliwa kwa kazi ya Mungu duniani, na msingi wa kazi ya Mungu duniani. Upeo wa kazi ya Yesu ulienea Yudea yote. Wakati wa kazi Yake, wachache sana wa wale waliokuwa nje ya Yudea walijua juu yake, kwani Hakufanya kazi yoyote nje ya Yudea. Leo, kazi ya Mungu imeletwa nchini China, na inatekelezwa kabisa ndani ya eneo hili. Katika awamu hii, hakuna kazi inayozinduliwa nje ya China; kuenea kwake zaidi ya China ni kazi ambayo itakuja baadaye. Hatua hii ya kazi inafuatilia kutoka kwa hatua ya kazi ya Yesu. Yesu alifanya kazi ya ukombozi, na hatua hii ni kazi inayofuata; ukombozi umekamilika, na katika hatua hii hakuna haja ya kuzaliwa na Roho Mtakatifu, kwa sababu hatua hii ya kazi ni tofauti na hatua ya mwisho, na, zaidi ya hayo, kwa sababu China ni tofauti na Israeli. Hatua ya kazi iliyofanywa na Yesu ilikuwa kazi ya ukombozi. Mwanadamu alimwona Yesu, na muda mfupi baadaye, kazi Yake ilianza kuenea kwa Mataifa. Leo, kuna wengi ambao wanaamini katika Mungu huko Amerika, Uingereza na Urusi, hivyo kwa nini kuna wachache nchini China? Kwa sababu China ni taifa lililotengwa zaidi. Kwa hivyo, China ilikuwa ya mwisho kukubali njia ya Mungu, na hata sasa imekuwa chini ya miaka mia tangu kuikubali—baadaye zaidi ya Amerika na Uingereza. Hatua ya mwisho ya kazi ya Mungu inafanywa katika nchi ya China ili kutamatisha kazi Yake, na ili kazi Yake yote iweze kukamilika. Watu wa Israeli wote walimwita Yehova, Bwana wao. Wakati huo, walimwona kama kichwa cha familia zao, na Israeli yote ikawa familia kubwa ambapo kila mtu alimwabudu Bwana wao Yehova. Roho wa Yehova mara nyingi Aliwatokea, naye akanena na kutamka sauti Yake, na kutumia nguzo ya wingu na sauti kuongoza maisha yao. Wakati huo, Roho alitoa mwongozo Wake katika Israeli moja kwa moja, Akizungumza na kutoa sauti Yake kwa watu, na waliona mawingu na kusikia sauti za ngurumo, na kwa njia hii Aliyaongoza maisha yao kwa maelfu kadhaa ya miaka. Kwa hiyo, watu wa Israeli pekee wamekuwa wakimwabudu Yehova daima. Wanaamini kwamba Yehova ni Mungu wao, na si Mungu wa Mataifa. Hii haishangazi: Yehova, hata hivyo, alikuwa amefanya kazi kati yao kwa karibu miaka 4,000. Katika nchi ya China, baada ya maelfu ya miaka ya kulala kwa uchovu, sasa tu ndipo wapotovu wamejua kwamba mbingu na ardhi na vitu vyote hazikuundwa kwa kawaida, bali zilifanywa na Muumba. Kwa sababu injili hii imetoka ng’ambo, wale wenye mawazo ya kimwinyi, wenye msimamo mkali wanaamini kwamba wale wote wanaoikubali injili hii wanafanya uhalifu wa kutisha, wao ni laana wanaomsaliti Buddha—babu wao. Zaidi ya hayo, wengi wa wenye mawazo haya ya kikabaila wanauliza, Watu wa China wanawezaje kuamini katika Mungu wa wageni? Je, hawawasaliti baba zao? Je, hawatendi mabaya? Leo, watu wamesahau kitambo kwamba Yehova ndiye Mungu wao. Wamemsukuma Muumba nyuma ya akili zao kitambo, na badala yake wanaamini katika nadharia ya mageuko, ambayo ina maana kwamba mtu amebadilika kutoka kuwa nyani, na kwamba ulimwengu wa asili ulikuja kama jambo la lazima. Chakula chote kizuri kinachofurahiwa na mwanadamu hutolewa kwa asili, kuna utaratibu wa maisha na kifo cha mwanadamu, na hakuna Mungu anayetawala juu ya yote. Isitoshe, kuna watu wengi wasioamini kwamba kuna Mungu wanaosema kwamba kumwamini Mungu ni ushirikina na si jambo la kisayansi. Lakini je, sayansi inaweza kuchukua nafasi ya kazi ya Mungu? Je, sayansi inaweza kutawala juu ya wanadamu? Kuhubiri injili katika nchi ambayo inatawaliwa na kutomwamini Mungu si kazi rahisi, na inahusisha vikwazo vingi. Leo, je, si kuna wengi ambao wanampinga Mungu kwa njia hii?
Yesu alipokuja kufanya kazi Yake, watu wengi walilinganisha kazi Yake dhidi ya kazi ya Yehova, walipopata kwamba hazilingani, walimsulubisha Yesu msalabani. Kwa nini hawakupata mambo yanayofanana katika kazi Zao? Ilikuwa, kwa sehemu, kwa sababu Yesu alifanya kazi mpya, na pia kwa sababu kabla ya Yesu kuanza kazi Yake, hakuna mtu aliyeandika ukoo Wake. Kama mtu angefanya hivyo, basi kusingekuwa na haja ya kuwa na wasiwasi, na nani bado angempigilia misumari Yesu msalabani? Ikiwa Mathayo angeandika ukoo wa Yesu miongo kadhaa kabla, basi Yesu asingepitia mateso hayo makuu. Je, si hivyo? Mara tu watu walipojifunza kuhusu ukoo wa Yesu—kwamba alikuwa mwana wa Ibrahimu, na mzao wa Daudi—basi wangekoma kumtesa Yeye. Je, si jambo la kusikitisha kwamba ukoo Wake ulikawia mno kuandikwa? Na ni jambo la kusikitisha kwamba Biblia inarekodi tu hatua mbili za kazi ya Mungu: hatua moja ambayo ilikuwa kazi ya Enzi ya Sheria, na moja ambayo ilikuwa kazi ya Enzi ya Neema; hatua moja ambayo ilikuwa kazi ya Yehova, na moja ambayo ilikuwa kazi ya Yesu. Ingekuwa bora zaidi kama nabii mkuu angetabiri kazi ya leo. Kungekuwa na sehemu ya ziada ya Biblia yenye mada “Kazi ya Siku za Mwisho”—je, si hiyo ingekuwa bora sana? Kwa nini mwanadamu akabiliwe na magumu mengi hivi leo? Mmekuwa na wakati mgumu sana! Ikiwa mtu yeyote anastahili kuchukiwa, ni Isaya na Danieli kwa ajili ya kutotabiri kazi ya siku za mwisho, na kama mtu yeyote anastahili kulaumiwa, ni mitume wa Agano Jipya ambao hawakuandika orodha ya uzazi wa kupata mwili kwa Mungu kwa mara ya pili mapema. Aibu iliyoje! Mnalazimika kutafuta ushahidi kila mahali, na hata baada ya kupata vipande kiasi vya maneno madogo bado hamwezi kujua kama kweli ni ushahidi. Aibu iliyoje! Kwa nini Mungu ni msiri sana katika kazi Yake? Leo, watu wengi bado hawajapata ushahidi thabiti, lakini pia hawawezi kukataa. Basi wanapaswa kufanya nini? Hawawezi kumfuata Mungu kwa uthabiti, wala pia hawawezi kuendelea mbele katika shaka hiyo. Na hivyo, “wasomi mahiri na wenye vipawa” wengi hukubali mtazamo wa “jaribu na kuona” wanapomfuata Mungu. Hii ni shida kubwa sana! Je, si mambo yangekuwa rahisi sana kama Mathayo, Mariko, Luka na Yohana wangeweza kutabiri yajayo? Ingekuwa bora kama Yohana angekuwa ameona ukweli wa ndani wa uzima katika ufalme—ni jambo la kusikitisha sana kwamba yeye aliona tu maono na hakuona kazi halisi, yakinifu duniani. Aibu iliyoje! Ni nini kibaya na Mungu? Kwa nini, baada ya kazi yake kwenda vizuri sana katika Israeli, sasa Amefika China, na kwa nini alipaswa kuwa mwili, na kufanya kazi na kuishi kati ya watu? Mungu hamfikirii mwanadamu kabisa! Sio tu kwamba Hakuwaambia watu mapema, lakini pia ghafla Alileta kuadibu na hukumu Yake. Kwa kweli haileti maana! Mara ya kwanza Mungu kuwa mwili, Aliteseka dhiki nyingi kutokana na kutomwambia mwanadamu ukweli wote wa ndani mapema. Hakika Yeye Hawezi kuwa Anasahau hilo? Na kwa nini bado Hamwambii mwanadamu wakati huu? Leo, ni bahati mbaya sana kwamba kuna vitabu sitini na sita tu katika Biblia. Inahitajika tu kuwa na mtu mmoja zaidi anayetabiri kazi ya siku za mwisho! Je, hufikirii? Hata Yehova, Isaya na Daudi hawakutaja kazi ya leo. Waliondolewa zaidi kutoka wakati wa sasa, na utengano wa muda wa zaidi ya miaka 4,000. Wala Yesu hakutabiri kikamilifu kazi ya leo, Akizungumzia kidogo tu, na bado mwanadamu hupata ushahidi mchache. Ukilinganisha kazi ya leo na ya awali, zote mbili zinawezaje kulingana? Hatua ya kazi ya Yehova ilielekezwa kwa Israeli, hivyo ukilinganisha kazi ya leo nayo kutakuwa na hitilafu kubwa hata zaidi; hizo mbili haziwezi kulinganishwa kabisa. Wala wewe si wa Israeli, au Myahudi; uhodari wako na kila kitu kinachokuhusu kina upungufu—unawezaje kujilinganisha nao? Je, hii inawezekana? Jua kwamba leo ni Enzi ya Ufalme, na ni tofauti na Enzi ya Sheria na Enzi ya Neema. Kwa hali yoyote, usijaribu kutumia fomyula; Mungu hawezi kupatikana katika fomyula yoyote kama hiyo.
Yesu aliishije katika kipindi cha miaka 29 baada ya kuzaliwa Kwake? Biblia haina kumbukumbu yoyote ya utoto na ujana Wake; unajua yalivyokuwa? Inawezekana kuwa hakuwa na utoto au ujana, na kwamba alipozaliwa alikuwa tayari mwenye umri wa miaka 30? Unajua kidogo sana, hivyo usiwe mzembe unapotoa maoni yako. Haikupi faida! Biblia inarekodi tu kwamba kabla ya siku ya kuzaliwa kwa Yesu ya miaka 30, alibatizwa na kuongozwa na Roho Mtakatifu hadi jangwani ili kupitia majaribu ya shetani. Na Injili Nne zinarekodi kazi Yake ya miaka mitatu na nusu. Hakuna rekodi ya utoto na ujana Wake, lakini hii haithibitishi kuwa Hakuwa na utoto na ujana; ni kwamba tu, mwanzoni, Hakufanya kazi yoyote, na Alikuwa mtu wa kawaida. Kwa hivyo, unaweza kusema kwamba Yesu aliishi kwa miaka 33 bila ujana au utoto? Inawezekana kwamba Alifika umri wa miaka 33 na nusu ghafla? Kila ambacho mwanadamu huyu anafikiria kumhusu Yeye ni cha miujiza na kisichowezekana. Hakuna shaka kwamba Mungu mwenye mwili ana ubinadamu wa kawaida na wa desturi, lakini Anapotekeleza kazi Yake ni moja kwa moja na ubinadamu Wake usio kamili na uungu Wake kamili. Ni kwa sababu ya hili watu wana mashaka juu ya kazi ya leo, na hata juu ya kazi ya Yesu. Ingawa kazi ya Mungu inatofautiana katika nyakati mbili Alizopata mwili, dutu Yake haitofautiani. Bila shaka, ukisoma kumbukumbu za Injili Nne, tofauti ni kuu. Unawezaje kurudi kwenye maisha ya Yesu wakati wa utoto na ujana Wake? Unawezaje kuelewa ubinadamu wa kawaida wa Yesu? Labda una ufahamu thabiti wa ubinadamu wa Mungu leo, lakini hufahamu ubinadamu wa Yesu, hata zaidi hauuelewi. Isingeandikwa na Mathayo, usingekuwa na fununu ya ubinadamu wa Yesu. Labda, Nitakapokuambia kuhusu hadithi za Yesu wakati wa maisha Yake, na kukuambia ukweli wa ndani wa utoto na ujana wa Yesu, utatikisa kichwa chako: Hapana! Haiwezekani kuwa Alikuwa hivyo. Hawezi kuwa na udhaifu wowote, sembuse kuwa na ubinadamu wowote! Hata utapaza sauti na kupiga yowe. Ni kwa sababu humjui Yesu kwamba una dhana juu Yangu. Unamwamini Yesu kuwa mwenye uungu pia, kuwa bila kitu cha mwili kumhusu. Lakini ukweli bado ni ukweli. Hakuna mtu anayetaka kuzungumza kinyume na ukweli wa ukweli, kwa maana Ninapozungumza ni kuhusiana na ukweli; sio bahatisho, wala si unabii. Jua kwamba Mungu anaweza kuinuka kwa kiwango kikubwa, na, zaidi ya hayo, Anaweza kujificha katika vina virefu. Yeye ni Asiyefikirika na akili yako, Yeye ni Mungu wa viumbe vyote, na sio Mungu binafsi ambaye Amedhaniwa na mtu mmoja hasa.