Maono ya Kazi ya Mungu (1)

Yohana alimfanyia Yesu kazi kwa miaka saba, na tayari alikuwa ameandaa njia Yesu alipofika. Kabla ya haya, injili ya ufalme wa mbinguni iliyohubiriwa na Yohana ilisikika kotekote katika nchi, hivyo ilienea kutoka upande mmoja hadi upande mwingine wa Uyahudi, na kila mtu alimwita nabii. Wakati huo, Mfalme Herode alitamani kumuua Yohana, lakini hakuthubutu, kwani watu walimheshimu sana Yohana, na Herode aliogopa kwamba kama angemuua Yohana wangemuasi. Kazi iliyofanywa na Yohana ilikita mizizi miongoni mwa watu wa kawaida, na aliwafanya Wayahudi kuwa waumini. Kwa miaka saba alimwandalia Yesu njia, mpaka wakati ambapo Yesu alianza kutekeleza huduma Yake. Kwa sababu hii, Yohana alikuwa mkuu zaidi kwa manabii wote. Ilikuwa tu baada ya Yohana kufungwa gerezano ndipo Yesu alianza kazi Yake rasmi. Kabla ya Yohana, hakukuwahi kuwa na nabii aliyemwandalia Mungu njia, kwa sababu kabla ya Yesu, Mungu hakuwa amewahi kupata mwili. Hivyo, kwa manabii wote mpaka Yohana, yeye pekee ndiye angemwandalia Mungu mwenye mwili njia, na kwa jinsi hii Yohana akawa nabii mkuu zaidi wa Agano la Kale na Jipya. Yohana alianza kueneza injili ya ufalme wa mbinguni miaka saba kabla ya ubatizo wa Yesu. Kwa watu, kazi aliyoifanya ilionekana kuwa juu zaidi ya kazi ya baadaye ya Yesu, ilhali yeye alikuwa, hata hivyo, nabii tu. Hakufanya kazi au kuzungumza ndani ya hekalu, lakini katika miji na vijiji nje yake. Hii alifanya, bila shaka, miongoni mwa taifa la Wayahudi, hasa wale waliokuwa maskini. Ni mara chache ambapo Yohana alitangamana na watu kutoka ngazi za juu za jamii, na alieneza injili miongoni mwa watu wa kawaida wa Yudea tu ili kuandaa watu wema kwa Bwana Yesu, na kuandaa maeneo yafaayo Kwake kufanya kazi. Kwa sababu ya kuwa na nabii kama Yohana wa kuandaa njia, Bwana Yesu Alikuwa na uwezo wa kuanzisha njia Yake ya msalaba mara moja punde tu Alipowasili. Wakati Mungu Alipogeuka kuwa mwili ili kufanya kazi yake, hakuwa na jukumu la kufanya kazi ya kuwachagua watu, na hakuwa na haja ya kuwatafuta watu binafsi au mahali ambapo Angefanyia kazi. Hakufanya kazi kama hii Alipokuja; mtu afaaye alikuwa tayari Amemwandalia kabla Yeye hajawasili. Yohana alikuwa tayari amemaliza kazi yake kabla Yesu kuanza kazi Yake, kwani wakati ambapo Mungu mwenye mwili aliwasili kufanya kazi Yake, Alianza kufanya kazi moja kwa moja kwa wale ambao walikuwa wakimngoja kwa muda mrefu. Yesu hakuwa amekuja kufanya kazi ya mwanadamu ya urekebishaji. Alikuwa amekuja tu kutekeleza huduma ambayo ilikuwa Yake kutekeleza, na mengine yote hayakuwa na uhusiano Naye. Yohana alipokuja, hakufanya lolote ila kutoa hekaluni na miongoni mwa Wayahudi kundi la wale waliokubali injili ya ufalme wa mbinguni, ili waweze kuwa vyombo vya kazi ya Bwana Yesu. Yohana alifanya kazi kwa miaka saba, ambapo ni kusema kwamba alieneza injili kwa miaka saba. Wakati wa kazi yake, Yohana hakufanya miujiza mingi, kwa sababu kazi yake ilikua kuandaa njia, ilikuwa kazi ya maandalizi. Kazi zote zingine, kazi ambazo Yesu Alikuwa afanye, hazikuwa na uhusiano naye; alimwomba mwanadamu tu aungame dhambi zake na atubu, na aliwabatiza watu, ili waweze kuokolewa. Ingawa alifanya kazi mpya, na kufungua njia ambayo kamwe mwanadamu alikuwa bado hajaitembea, bado alimwandalia Yesu njia. Alikuwa nabii tu ambaye alifanya kazi ya maandalizi, na hakuwa na uwezo wa kufanya kazi ya Yesu. Ingawa Yesu hakuwa wa kwanza kuhubiri kuhusu ufalme wa mbinguni, na japokuwa aliendelea na njia ambayo Yohana alianzisha, bado hakukuwa na mwingine ambaye angeweza kufanya kazi yake, na ilikuwa juu zaidi ya kazi ya Yohana. Yesu hangeandaa njia yake mwenyewe; kazi yake ilitekelezwa moja kwa moja kwa niaba ya Mungu. Na hivyo, bila kujali ni miaka mingapi Yohana alifanya kazi, bado alikuwa nabii, na bado yule aliyeandaa njia. Miaka mitatu ya kazi iliyofanywa na Yesu ilizidi miaka saba ya kazi aliyofanya Yohana, kwa kuwa kiini cha kazi yake hakikuwa cha kiwango sawa. Yesu alipoanza kutekeleza huduma Yake, ambao pia ni wakati kazi ya Yohana ilifika mwisho, Yohana alikuwa amewatayarisha watu wa kutosha na mahali pa kutumiwa na Bwana Yesu, na walitosha kwa ajili ya Bwana Yesu kuanza miaka mitatu ya kazi. Na kwa hiyo, punde tu kazi ya Yohana ilipomalizika, Bwana Yesu alianza rasmi kazi Yake Mwenyewe, na maneno yaliyonenwa na Yohana yakarushwa kando. Hiyo ni kwa sababu kazi iliyofanywa na Yohana ilikuwa tu kwa ajili ya mabadiliko, na maneno yake hayakuwa maneno ya uzima ambayo yangemwelekeza mwanadamu kwa ukuaji mpya; mwishowe, maneno yake yalikuwa tu ya matumizi ya muda.

Kazi ambayo Yesu alifanya haikuwa ya mwujiza; kulikuwa na mchakato kwayo, na yote iliendelea mbele kufuatana na sheria za kawaida za vitu. Kufikia miezi sita ya mwisho ya maisha Yake, Yesu alijua kwa uhakika kwamba Alikuwa Amekuja kuifanya kazi hii, na Alijua kwamba Alikuwa Amekuja kupigiliwa misumari msalabani. Kabla ya Yeye kusulubiwa, Yesu alimwomba Mungu Baba siku zote, kama tu Alivyoomba mara tatu katika Bustani la Gethsemane. Baada ya kubatizwa, Yesu alitekeleza huduma Yake kwa miaka mitatu na nusu, na kazi Yake rasmi ilidumu kwa miaka miwili na nusu. Katika mwaka wa kwanza, Alishtakiwa na Shetani, na Akasumbuliwa na mwanadamu, na Akapitia majaribu ya mwanadamu. Alishinda majaribu mengi wakati huo huo Alipotekeleza kazi Yake. Katika miezi sita ya mwisho, wakati ambapo Yesu alikaribia kusulubiwa, kutoka kinywani mwa Petro yalitoka maneno haya kwamba alikuwa Mwana wa Mungu aishiye, kwamba alikuwa Kristo. Ni wakati huo tu ndipo kazi Yake ilijulikana kwa wote, na ni wakati huo tu ndipo utambulisho Wake ulifichuliwa kwa watu wote. Baada ya hilo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Angepaswa kusulubiwa kwa ajili ya mwanadamu, na kwamba siku tatu baadaye Angefufuka tena; kwamba Alikuwa Amekuja kutekeleza kazi ya ukombozi, na Yeye alikuwa Mwokozi. Ni katika miezi sita ya mwisho tu ndiyo Alifichua utambulisho Wake na kazi Aliyokusudia kufanya. Huu pia ulikuwa wakati wa Mungu, na kazi ilipaswa kutekelezwa hivyo. Wakati huo, sehemu ya kazi ya Yesu ilikuwa kwa mujibu wa Agano la Kale, pia na sheria za Musa na maneno ya Bwana wakati wa kipindi cha Enzi ya Sheria. Yote hayo Yesu Alitumia kufanya sehemu ya kazi yake. Alihubiri kwa watu na kuwafundisha kwenye masinagogi, na yeye Alitumia utabiri wa manabii katika Agano la Kale kuwakemea Mafarisayo waliokuwa na uhasama Naye, na Alitumia maneno katika Maandiko kufichua uasi wao na hivyo kuwahukumu. Kwa maana wao walidharau mambo ambayo Yesu Aliyafanya; hasa, nyingi ya kazi ya Yesu haikufuatana na sheria katika Maandiko, na zaidi ya hayo, kile Alichofundisha kilikuwa kikuu kuliko maneno yao wenyewe, na hata kikubwa kuliko kile ambacho kilikuwa kimetabiriwa na manabii katika Maandiko. Kazi ya Yesu ilikuwa kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu na kusulubiwa tu. Kwa hivyo, hakukuwa na haja Kwake kusema maneno zaidi ili kumshinda mtu yeyote. Mengi ya yale Aliyomfundisha mwanadamu yalitolewa kutoka kwa Maandiko, na hata kama kazi yake haikuzidi Maandiko, bado Aliweza kutimiza kazi ya kusulubiwa. Yake haikuwa kazi ya neno, wala kwa ajili ya kumshinda mwanadamu, lakini kwa minajili ya kumkomboa mwanadamu. Yeye Alihusika kama dhabihu ya dhambi tu kwa mwanadamu, na hakuhusika kama chanzo cha Neno kwa mwanadamu. Hakufanya kazi ya watu wa Mataifa mengine, ambayo ilikuwa kazi ya kumshinda mwanadamu, bali Alifanya kazi ya kusulubiwa, kazi ambayo ilifanywa miongoni mwa wale ambao waliamini kulikuwa na Mungu. Japokuwa kazi yake ilifanywa juu ya msingi wa Maandiko, na Alitumia yale yaliyotabiriwa na manabii wa kale kuwahukumu Mafarisayo, hii ilikuwa ya kutosha kukamilisha kazi ya kusulubiwa. Kama kazi ya leo ingekuwa bado inafanyika juu ya misingi ya utabiri wa manabii wa kale katika Maandiko, basi haingewezekana nyinyi kushindwa, kwa kuwa Agano la Kale halina kumbukumbu ya uasi na dhambi zenu nyinyi watu wa China, hakuna historia ya dhambi zenu. Kwa hivyo, kama kazi hii bado ingedumu katika Biblia, hamngeweza kutoa matunda. Biblia inaandika lakini kwa uchache historia ya wana wa Israeli, ambayo haina uwezo wa kusadikisha iwapo nyinyi ni waovu ama wema, ama ya kukuhukumu. Hebu Fikiria kama Ningekuwa wa kuwahukumu nyinyi kadri ya historia ya wana wa Israeli—bado mngenifuata Mimi kama mnavyonifuata hivi leo? Je, mnajua jinsi ambavyo nyinyi m wagumu? Kama hakuna maneno ambayo yalisemwa wakati wa awamu hii, basi itakuwa vigumu kukamilisha kazi ya ushindi. Kwa sababu Mimi sijakuja kugongomewa msumari msalabani, sharti Mimi niseme maneno ambayo ni tofauti na yatokayo kwa Biblia, ilimradi muweze kushindwa. Kazi iliyofanywa na Yesu ilikuwa tu hatua moja juu zaidi ya Agano la Kale; ilitumiwa kuianza enzi, na kuiongoza enzi hiyo. Kwa nini Alisema, “Sikuja kuharibu sheria, bali kuitimiza”? Lakini katika kazi Yake kulikuwa na mengi ambayo yalitofautiana na sheria zilizotumika na amri zilizofuatwa na Waisraeli wa Agano la Kale, kwani Hakuja kuitii sheria, bali kuitimiza. Mchakato wa kuitimiza ulikuwa pamoja na mambo mengi halisi: Kazi Yake ilikuwa ya vitendo zaidi na halisi, na, aidha, ilikuwa hai, na hakukuwa tu kufuata masharti bila kufikiri. Je, Waisraeli hawakuitii Sabato? Yesu alipokuja Hakuitii Sabato, kwani Alisema kwamba Mwana wa Adamu alikuwa Bwana wa Sabato, na wakati ambapo Bwana wa Sabato alikuja, Angefanya Alivyopenda. Alikuwa Amekuja kutimiza sheria za Agano la Kale na kuzibadilisha sheria. Yote ambayo hufanywa leo ni kwa msingi wa siku hizi, lakini bado yako juu ya msingi wa kazi ya Bwana katika Enzi ya Sheria, na hayavuki mipaka ya eneo hili. Kuulinda ndimi zenu, na kutozini, kwa mfano—Je, hizi si sheria za Agano la Kale? Leo, kile kinachotakikana kwenu sio chenye upeo wa amri kumi tu, lakini ni kuwa na amri na sheria ambazo zina ukuu kuliko hizo zilizokuja hapo awali, ila hii haina maana kuwa kile kilichokuja hapo awali kimeondolewa, kwa kuwa kila awamu ya kazi ya Mungu hufanywa juu ya msingi wa awamu ambayo ilikuja hapo awali. Na kuhusu kile ambacho Yehova aliwasilisha kwa Israeli, kama vile kuwahitaji watu kutoa sadaka, kuwaheshimu wazazi wao, kutoabudu sanamu, kutowadhulumu au kutukana wengine, kutozini, kutovuta sigara au kutokunywa pombe, na kutokula nyamafu au kunywa damu, je, huo si muundo msingi wa utendaji wenu hata leo? Kazi iliyotekelezwa hadi leo iko juu ya msingi wa mambo ya zamani. Ingawa sheria za zamani hazitajwi tena, nawe umewekewa madai mapya, sheria hizi mbali na kufutwa, badala yake, zimeinuliwa katika hadhi ya juu zaidi. Kusema kwamba zimefutwa kuna maana kwamba enzi ya awali imepitwa na wakati, wakati kuna amri zingine ambazo lazima uzitii milele yote. Amri za zamani tayari zimetiwa katika vitendo, tayari zimekuwa nafsi ya mwanadamu, na hakuna haja ya kurudia kusema amri za kutovuta sigara, kutokunywa pombe, na kadhalika. Juu ya msingi huu, amri mpya zimeagizwa kufuatana na mahitaji yenu leo, kufuatana na kimo chenu, na kufuatana na kazi ya leo. Kutangaza amri kwa ajili ya enzi mpya hakumaanishi kufuta amri za enzi ya kale, bali kuziinua juu zaidi ya msingi huu, kuyafanya matendo ya mwanadamu kuwa kamili zaidi, na kufuatana na uhalisi zaidi. Kama, leo, mngetakiwa tu kufuata amri na kutii sheria za Agano la Kale, kwa namna sawa na wana wa Israeli, na kama, hata, nyinyi mlitakiwa mkariri sheria ambazo ziliwekwa na Bwana, hakungekuwa na uwezekano kwamba mngeweza kubadilika. Kama mngekuwa tu mnatakiwa kutii zile amri chache zilizo na mipaka ama kukariri sheria zisizohesabika, asili zenu za zamani zingebaki zimekita mizizi, na hakungekuwa na mbinu ya kuzing’oa. Hivyo mngeendelea kuzidi kupotoshwa, na hakuna hata mmoja wenu angeweza kuwa mtiifu. Ambayo ni kusema kwamba amri chache rahisi au sheria zisizohesabika hazina uwezo wa kuwasaidia kujua matendo ya Yehova. Nyinyi si sawa na wana wa Israeli: kwa kufuata sheria na kukariri amri waliweza kushuhudia matendo ya Yehova, na kumpa Yeye pekee ibada yao, lakini hamwezi kufanikisha hili, na amri chache za Agano la Kale haziwezi tu kuwafanya nyinyi kupeana mioyo yenu, au kuwalinda, lakini badala yake itawafanya muwe wazembe, na kuwateremsha mpaka Kuzimu. Kwa sababu kazi Yangu ni kazi ya ushindi, na inalenga uasi wenu na asili yenu ya zamani. Maneno yenye huruma ya Yehova na Yesu yanapungukiwa mno na maneno makali ya hukumu leo. Bila maneno makali kama haya, ingekuwa vigumu kuwashinda ninyi “wataalam,” ambao mmekua wasiotii kwa miaka elfu nyingi. Sheria za Agano la Kale zilipoteza nguvu zake kwenu kwa muda mrefu uliopita, na hukumu ya leo ni ya kuogofya mno kuliko sheria za zamani. Ya kuwafaa nyinyi zaidi ni hukumu, na wala si vikwazo duni vya sheria, kwa kuwa ninyi si wanadamu wa mwanzo kabisa, lakini wanadamu ambao wamekuwa fisadi kwa miaka elfu nyingi. Kile ambacho mwanadamu lazima atimize sasa ni kulingana na hali halisi ya mwanadamu leo, kulingana na tabia bora na kimo halisi cha mwanadamu wa siku hizi, na hakihitaji kwamba wewe ufuate mafundisho ya dini. Hii ni kwa minajili ya mabadiliko yaweze kupatikana katika asili zako za zamani, na ili uweze kutupa kando dhana zako. Je, unadhani sheria hizi ni mafundisho ya dini? Hizo ni, inaweza kusemwa, masharti ya kawaida kwa mwanadamu. Hayo si mafundisho ya dini unayotakiwa kufuata. Chukua mfano wa, kukataza kuvuta sigara—je, hayo ni mafundisho ya dini? Hayo si mafundisho ya dini! Yanahitajika na ubinadamu wa kawaida; si mafundisho ya dini, bali ni sheria kwa wanadamu wote. Leo, idadi kubwa au zaidi ya amri ambazo zimetangazwa si sheria; ni kinachohitajika ili kutimiza ubinadamu wa kawaida. Watu hawakuwa na au kujua vitu kama hivyo zamani, na kwa hiyo wanatakiwa kuvitimiza leo, ambavyo havihesabiki kama mafundisho ya dini. Sheria si sawa na mafundisho ya dini. Mafundisho ya dini Ninayozungumzia yanahusu sherehe, urasmi au desturi za mwanadamu za kuacha maadili na zenye kosa; ni masharti na kanuni ambazo hazimsaidii mwanadamu, hazina manufaa kwake, na ni kusudi la kitendo lisilo na umuhimu. Hiki ni kifano cha mafundisho ya dini, na mafundisho ya dini kama hayo lazima yaachwe, kwani hayampi mwanadamu manufaa yoyote. Ni yale yaliyo ya manufaa kwa mwanadamu ndiyo yanatakiwa kutiwa katika vitendo.

Iliyotangulia: Kazi na Kuingia (10)

Inayofuata: Maono ya Kazi ya Mungu (2)

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp