Baada ya Kuvumilia Shida, Upendo Wangu kwa Mungu Ni Thabiti Hata Zaidi

26/01/2021

Na Zhou Rui, Jimbo la Jiangxi

Jina langu ni Zhou Rui na mimi ni Mkristo wa Kanisa la Mwenyezi Mungu. Kuanzia wakati ambapo nilianza kufahamu mambo, niliwaona wazazi wangu wakifanya kazi kwa bidii mashambani kuanzia asubuhi hadi usiku ili kupata riziki. Licha ya jitihada zao nyingi, ilikuwa vigumu kupata pesa zozote kila mwaka, kwa hivyo familia yetu iliishi daima katika umaskini mkubwa. Kila mara nilipowaona wale watu wenye nguvu na ushawishi walioishi kwa raha bila kuhitaji kufanya kazi ngumu, niliwaonea husuda, na kwa hivyo nilifanya azimio thabiti: Nitakapokuwa mtu mzima, hakika nitafanikiwa kazini au kupata nafasi serikalini ili nirekebishe umaskini na hali ya kuwa nyuma kwa familia yangu ili wazazi wangu, pia, waweze kuishi maisha ya matajiri. Hata hivyo, nilijitahidi sana kupata hali hii ya njozi kwa miaka mingi, lakini kamwe sikuweza kupata kile nilichotaka; niliendelea kuishi maisha duni. Mara nyingi nilitanasufi kwa wasiwasi kuhusu kutokuwa na matunda ya kuonyesha nilivyokuwa na shughuli, na polepole nilipoteza imani yangu maishani. Nilipoanza tu kuvunjika moyo na kukata tamaa ya maisha, wokovu wa Mwenyezi Mungu wa siku za mwisho ulinijia. Kutoka katika maneno Yake nilifahamu ukweli fulani na nikakuja kujua sababu ya mateso ya wanadamu ulimwenguni. Pia nilifahamu jinsi watu walivyohitaji kuishi ili waishi maisha ambayo yalikuwa ya maana zaidi na ya kufaa zaidi. Kuanzia wakati huo, ingawa nilikuwa nimechanganyikiwa na asiyejiweza, nilipata mwelekeo wangu maishani. Nilipoacha mfadhaiko na majonzi, nilihisi uchangamfu na nguvu mpya ya maisha, na nikaona tumaini la maisha. Baadaye, ili wale ambao walikuwa bado wakiishi katika mateso na wasiojiweza pia waweze kupata wokovu huu wa nadra sana, nilianza kwenda sehemu moja hadi nyingine, nikihubiri kwa bidii wokovu wa Mungu wa siku za mwisho. Hata hivyo, kile ambacho sikutarajia ni kwamba katika mchakato wa kueneza injili, nitakamatwa mara mbili na serikali ya China na kupitia mateso ya kikatili, na ya kinyama…. Katika shimo hili la giza la maovu makubwa, Mwenyezi Mungu hakuniacha kamwe; maneno Yake yalinipa imani na nguvu, yakiniongoza tena na tena hadi kwa ushindi dhidi ya nguvu za giza za Shetani na kuimarisha mapenzi yangu Kwake.

Ilikuwa siku moja mnamo Juni mwaka wa 2003; mimi na ndugu zangu wawili tulikuwa tumekwenda katika kijiji kimoja kueneza injili, tuliporipotiwa na mtu mwovu. Polisi watano au sita waliokuwa katika magari matatu ya polisi walitushambulia na kutuweka pingu mikononi bila kuuliza swali lolote. Wakitusukuma na kutupiga mateke, walitulazimisha kuingia katika magari hayo na kutupeleka kwenye Ofisi ya Usalama wa Umma. Katika gari sikuhisi woga hata kidogo. Daima nilikuwa nikiona kuwa nia ya kueneza injili ilikuwa kuwaletea watu wokovu, kwa hivyo hatukuwa tukifanya chochote kibaya; mara tu tulipofika kwa PSB, ningeeleza hali hiyo, na polisi wangetuachilia. Hata hivyo, ningejuaje kuwa polisi wa serikali ya China walikuwa wakatili zaidi na wakali zaidi kuliko majambazi wowote au madikteta waovu. Baada ya kufika katika ofisi za PSB, polisi hawakutupa hata nafasi ya kueleza kabla ya kututenganisha na kutuhoji mmoja mmoja. Mara nilipoingia kwenye chumba cha mahojiano polisi mmoja alinifokea mara moja, “Sera ya Chama cha Kikomunisti ni ‘Huruma kwa wale wanaokiri, na ukali kwa wale wanaopinga.’ Je, unajua hivyo?” Baadaye, aliuliza kuhusu habari yangu ya kibinafsi. Alipoona kwamba majibu yangu hayakumridhisha, polisi mwingine alisogea karibu nami na kuguna, “Mh! Hushirikiani. Itatulazimu tukuadhibu ili tuone ikiwa hilo litakufanya useme ukweli.” Kisha akapunga mkono wake na kusema, “Leteni matofali kadhaa ili tuweze kumuadhibu!” Mara aliposema hayo polisi wawili walikuja mara moja, wakachukua mmoja wa mikono yangu, na kuuvuta kwa nguvu kutoka juu ya bega langu hadi chini kupitia mgongo wangu huku wakiuvuta juu kwa ghafla mkono wangu mwingine, na kisha wakaitia pingu pamoja kwa nguvu. Mara moja nilisikia maumivu yasiyoweza kuvumilika, kana kwamba mikono yangu ilikuwa karibu kuvunjika. Mtu dhaifu kama mimi angewezaje kuvumilia mateso kama hayo? Muda mfupi baadaye nilianguka chini. Walipoona hivyo, polisi waovu ghafla walivuta pingu kuelekea juu na kuminya matofali mawili kati ya mikono yangu na mgongo wangu. Maumivu makali ya ghafla, yaliniingia moja kwa moja moyoni mwangu, kana kwamba maelfu ya siafu walikuwa wakitafuna kupitia mifupa yangu. Kwa uchungu mkubwa, nilitumia nguvu zangu zote zilizobaki kumwomba Mungu: “Mwenyezi Mungu, niokoe. Mwenyezi Mungu, niokoe….” Ingawa wakati huo nilikuwa nimekubali wokovu wa Mungu wa siku za mwisho kwa muda wa takribani miezi mitatu tu, sikuwa nimejiandaa na maneno Yake mengi, na nilielewa ukweli chache adimu tu, hata hivyo, nilipokuwa nikiomba bila kukoma, Mungu alinipa imani na nguvu na akapanda msimamo thabiti ndani yangu: sina budi kuwa shahidi kwa Mungu; inanipasa nisijisalimishe kwa Shetani hata kidogo! Kwa sababu hiyo, nilikereza meno yangu na kukataa kata kata kusema neno lingine. Wakihangaikahangaika na kukasirika, polisi hao wabaya walijaribu hila nyingine mbaya ili kujaribu kunidhibiti: Waliweka matofali mawili kwenye sakafu na kunilazimisha kupiga magoti juu yao; wakati huohuo, waliinua pingu zangu kwa nguvu. Mikono yangu mara moja ilikuwa na maumivu mengi yasiyoweza kuvumilika na ilihisi kama ilikuwa imevunjwa. Nilijikaza kupiga magoti hapo kwa muda wa dakika chache kabla ya kuanguka chini tena bila kusonga, ndipo polisi walininyanyua kwa nguvu kwa pingu zangu, na kunilazimisha kuendelea kupiga magoti. Kwa njia hii walinitesa tena na tena. Ilikuwa upeo wa majira ya joto, kwa hivyo nilikuwa na uchungu na nilihisi joto; matone ya jasho yalitiririka kutoka usoni mwangu bila kukoma. Nilikuwa na wakati mgumu sana kusalia thabiti kwamba ilikuwa vigumu kwangu kupumua, na karibu nizirai. Hata hivyo, genge hili la polisi waovu lilifurahi tu kwa ajili ya taabu yangu. “Unahisi vyema?” Mmoja wao alisema. “Ikiwa utaendelea kukataa kuzungumza, tuna njia nyingi zaidi za kukabiliana nawe!” Walipoona kwamba sikuwa najibu, walighadhabika kwa kukata tamaa na kusema, “Kwa hivyo hujachotosheka? Tena!”… Baada ya muda wa saa mbili au tatu ya mateso haya, nilikuwa naumwa kutoka utosini hadi kidoleni na sikuwa na nguvu iliyosalia. Nilianguka sakafuni na singeweza kusonga, na hata nilipoteza udhibiti wote wa kibofu changu na uchengelele wangu. Kwa ajili ya kukabiliana na mateso makali ya hawa polisi waovu, nilijichukia kwa dhati kwa ajili ya kuwa kipofu na mjinga hapo awali; kwa ujinga, nilikuwa nimedhani kwamba PSB ingekuwa mahali pa haki na kwamba polisi wangetetea haki na kuniachilia. Sikuwahi kutarajia kwamba wangekuwa wenye nia mbaya na wakatili kiasi cha kujaribu kupata ukiri kupitia mateso bila ushahidi wowote, na kunitesa hadi karibu nife. Kwa kweli wao ni waovu kabisa! Nililala sakafuni kana kwamba nimevurugikiwa na singeweza kusonga hata kama ningetaka. Sikujua jinsi walivyopanga kunitesa zaidi, wala sikujua ningeweza kuwa thabiti kwa muda gani zaidi. Katika mateso na kutojiweza kwangu, nilichoweza tu kufanya ni kumwomba Mungu aendelee kunipa nguvu ili niendelee kuvumilia. Mungu alisikia maombi yangu, na Akanihurumia, Akinikumbusha mojawapo ya maneno Yake: “Sasa ni muda muhimu. Kuwa na uhakika usivunjike moyo au kukataa tamaa. Ni lazima uangalie mbele katika kila kitu na usirudi nyuma…. Mradi pumzi moja bado inasalia nawe, vumilia hadi mwisho kabisa; hii tu ndiyo inastahili sifa(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 20). Maneno ya Mungu yalinipa imani na nguvu kubwa. Yalikuwa ya kweli kabisa. Kwa kuwa nilikuwa nikitembea katika njia ya nuru na haki, nilipaswa kuwa na imani ya kuendelea kusihi; hata ikiwa ni pumzi yangu ya mwisho kabla ya kufa, bado nilihitajika kuvumilia hadi mwisho! Maneno ya Mungu yalivuma kwa nguvu ya uzima, yaliniwezesha kuwa na imani na ujasiri wa kupigana na pepo hawa wabaya hadi mwisho, na polepole nilipata tena nguvu yangu ya mwili vile vile. Baada ya hapo, polisi hao waovu waliendelea kunihoji, na waliendelea kunikanyaga kwenye nyayo zangu mpaka zikapondeka na kulemezwa. Hata hivyo, sikuhisi maumivu zaidi. Nilijua kuwa hii ilikuwa kwa sababu ya matendo mazuri ya Mungu; kwa kunihurumia na kunionyesha kutaka kunisaidia kwa ajili ya udhaifu wangu, Alikuwa amepunguza mateso yangu. Baadaye, polisi hao wenye chuki walituzuilia kwa shtaka la “kuvuruga usalama wa umma.” Usiku huo, walimtia kila mmoja wetu pingu kwenye bloku moja ya saruji yenye uzito wa ratili mia tatu au mia nne, ambapo tulibaki tukiwa tumefungwa hadi jioni iliyofuata, wakati ambapo walitusafirisha hadi kwenye kizuizi ya eneo letu.

Kuingia ndani ya kizuizi kulikuwa kama kutupwa katika aina fulani ya kuzimu. Askari jela walinilazimisha kuunganisha balbu zenye rangi. Mwanzoni, nililazimishwa kuunganisha balbu elfu sita kwa siku, lakini baada ya hapo, idadi hiyo iliongezeka kila siku hadi hatimaye ilifikia elfu kumi na mbili. Kwa ajili ya kazi hii nyingi kupindukia ya kila siku, nilifanya kazi kwa bidii mno, lakini bado sikuweza kumaliza kazi. Sikuwa na lingine la kufanya ila kuendelea kuziunganisha pamoja usiku kucha. Wakati mwingine sikuweza kustahimili, na nilitaka kulala, lakini mara tu nilipoonekana na wao, ningepigwa kikatili. Maafisa wa marekebisho waliweza hata kuchochea waonevu wa gerezani kwa kusema kwa sauti kubwa, “Ikiwa wafungwa hawa hawawezi kumaliza kazi au kuifanya kwa usahihi, mnapaswa kuwapiga sindano kadhaa za ‘penesilini’.” Walichomaanisha kwa kuwapiga sindano ya “penesilini” ni kubamiza goti la mtu kwenye msamba wa mfungwa, kumpiga kikumbo kwa nguvu katikati ya mgongo alipokuwa akiinama kwa ajili ya maumivu, na kisha kutumia kisigino kukanyaga mguu wa mfungwa. Njia hii ya kikatili ingeweza wakati mwingine kumfanya mtu azirai papo hapo na hata kubaki kilema maisha yake yote. Katika gereza hili la kishetani, nilifanya kazi ngumu za sulubu kila siku na bado ilibidi nivumilie kichapo cha kikatili. Zaidi ya hayo, milo mitatu tuliyolishwa kila siku haikufaa kuliwa hata na mbwa au nguruwe: Vyakula tulivyokula vilitayarishwa kwa majani ya figili yasiyotiwa viungo na kabichi ya kinamasi (ambayo mara nyingi ilikuwa imechanganyika na majani yaliyooza, mizizi, na tope), pamoja na takribani gramu mia moja hamsini za wali na kikombe cha maji ambayo yalikuwa yametumika kusafishia mpunga. Siku nzima, niliona njaa sana hadi tumbo langu lilikuwa likinguruma kila wakati. Katika mazingira ya aina hii, nilikuwa na Mwenyezi Mungu pekee wa kutegemea; kila mara nilipopigwa, ningeomba kwa haraka, nikimsihi Mungu anipe imani na nguvu ili niweze kushinda majaribu ya Shetani. Baada ya zaidi ya siku ishirini za kupigwa na kuteswa, mwili wangu ulikuwa umedhoofika zaidi ya kutambuliwa: Sikuwa na nguvu katika mikono na miguu yangu, singeweza kusimama wima, na sikuwa na nguvu hata ya kunyoosha mikono yangu. Hata hivyo, walinzi hao wenye kichaa hawakujali tu shida yangu, lakini pia walibadhiri mamia kadhaa ya yuani ambazo familia yangu ilinitumia. Kadiri muda ulivyopita, hali yangu ya mwili ilizidi kuzorota; nilidhoofika sana hata singeweza kujizuia kujilalamikia mwenyewe, “Kwa nini, katika nchi hii, mtu anayemwamini Mungu analazimika kuteswa hivi? Je, si sababu yangu ya kueneza injili ni kuwaleta watu mbele za Mungu ili wapokee wokovu wa Mungu? Na hata sijafanya makosa yoyote….” Kadiri nilivyozidi kuwaza kuhusu haya, ndivyo ikawa vigumu zaidi kuvumilia na ndivyo nilivyohisi kudhulumiwa zaidi. Nilichoweza tu kukifanya ni kumwomba Mungu bila kukoma na kumsihi Anihurumie na aniokoe. Wakati wa taabu yangu na kutojiweza, Mungu aliniongoza nikumbuke wimbo wa maneno Yake: “… 2 Pengine utayakumbuka maneno haya: ‘Kwa kuwa huzuni yetu nyepesi, ambayo ni ya muda mdogo pekee, inatufanyia utukufu mkubwa na wa daima ambao unazidi kuwa mkuu kabisa.’ Maneno haya ndiyo yatakayotimizwa na Mungu katika enzi za mwisho. Yatatimia kwa wale walioteswa na joka kuu jekundu katika sehemu linakoishi. Joka kuu jekundu humtesa Mungu na ni adui wa Mungu, kwa hiyo katika nchi hii, wanaomwamini Mungu wanateswa na kudhihakiwa. Ndiyo sababu maneno haya yatakuja kuwa kweli kwenu nyie kundi la watu. 3 Ni vigumu kabisa kwa Mungu kutekeleza kazi yake katika nchi yenye joka kuu jekundu, lakini ni kupitia ugumu huu ndipo Mungu Hupiga hatua katika kazi Yake ili kudhihirisha hekima Yake na matendo Yake ya ajabu. Mungu Huchukua fursa hii kuwakamilisha watu hawa wa kikundi hiki. Kwa ajili ya mateso ya watu, tabia yao na hulka ya kishetani ya watu katika nchi hii najisi, Mungu Anafanya kazi Yake ya kutakasa na ushindi, ili, kutokana na hili, apokee utukufu na kuwapata wale wote wanaoshuhudia matendo Yake. Huu ndio umuhimu wa kujitoa kwa Mungu kwa ajili ya kikundi hiki cha watu(“Ninyi Ndio Wale Watakaopokea Urithi wa Mungu” katika Mfuateni Mwanakondoo na Kuimba Nyimbo Mpya). Maneno ya Mungu yalinipa faraja kubwa na kunitia moyo, na yaliniwezesha kufahamu mapenzi Yake. Kwa sababu tunamwamini Mungu katika nchi inayomkana Mungu, tumekusudiwa kuvumilia ukandamizaji na mateso ya pepo Shetani; hata hivyo, kuteswa kwetu kumeruhusiwa na Mungu, kwa hivyo mateso kama haya yana thamani na maana. Ni kwa njia hasa ya mateso na taabu kama hii ndiyo Mungu huingiza wazo wa ukweli ndani yetu, na kwa hivyo kutupa sifa za kuwa na ahadi Yake. “Taabu” hii ni baraka ya Mungu, na kuweza kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu kupitia mateso haya ni ushuhuda wa ushindi wa Mungu dhidi ya Shetani, na pia ni ushahidi wa kuaminisha kwamba nimepatwa na Mungu. “Leo,” niliwaza, “kwa sababu ninamfuata Mungu, ninapitia mateso kama haya mikononi mwa pepo za Chama cha Kikomunisti cha China, na huyu ni Mungu anayenionyesha neema maalum, kwa hivyo kwa haki ninapaswa kujisalimisha kwa mipango ya Mungu na kukabiliana nayo kwa furaha na kuikubali kwa utulivu thabiti.” Nilikumbuka maneno mengine ya Mungu, yaliyosemwa katika Enzi ya Neema: “Wamebarikiwa wale wanaoteswa kwa sababu ya haki; kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao(Mathayo 5:10). Katika wakati huo, nilikuwa hata na imani na nguvu zaidi: Bila kujali Shetani na pepo zake walinitesa jinsi gani, nilikuwa nimeazimia kutojisalimisha kwao, na niliapa kwamba nitakuwa shahidi na kumridhisha Mungu! Nikiwa nimejaliwa na mamlaka na nguvu, maneno ya Mungu yalikuwa yameondoa ukiwa na kutojiweza ambako nilihisi ndani, na kupunguza mateso yenye kudhuru ya mwili ambayo niliteswa. Yaliniruhusu kuona nuru gizani, na roho yangu ikawa thabiti zaidi na isiyokubali kushindwa.

Baadaye, licha ya kutokuwa na ushahidi wowote, serikali ya China iliamuru nipewe kifungo cha mwaka mmoja cha marekebisho kupitia kazi. Polisi waliponisafirisha kwenda kwenye kambi ya kazi, walinzi wa gereza huko waliona kuwa nilikuwa mwebamba mno na sikuonekana kama binadamu tena. Wakiogopa kwamba nitakufa, hawakuthubutu kunikubali, kwa hivyo polisi hawakuwa na lingine la kufanya ila kunirudisha kizuizini. Kufikia wakati huo nilikuwa nimeteswa na polisi hao waovu hadi kiwango ambacho singeweza kula, tena sio tu kwamba hawakunipa matibabu, lakini pia walisema kuwa nilikuwa nikijisingizia. Walipoona kuwa siwezi kumeza chakula chochote, walimleta mtu wa kukifungua kinywa changu na kukimiminia chakula kwa nguvu. Waliponiona nikiwa na tatizo la kumeza, walinipiga. Nililazimishwa kula na kupigwa kama mwanaserere wa matambara mara tatu kwa jumla. Baada ya kuona kwamba hawangeweza kunimiminia chakula kingine zaidi, hawakuwa na lingine la kufanya ila kunipeleka hospitalini. Uchunguzi ulifichua kuwa mishipa yangu ilikuwa imekuwa migumu; damu yangu ilikuwa imegeuka kuwa lahamu nyeusi, na haikuweza kuzunguka vizuri. Daktari alisema, “Ikiwa mtu huyu atazuiliwa kwa muda mrefu zaidi, hakika atakufa.” Hata hivyo, polisi wenye chuki, waovu bado hawangeniachilia. Baadaye, maisha yangu yakiwa hatarini, wafungwa wengine walisema kuwa sikuwa na matumaini na nilikuwa mtu aliyezidiwa kabisa. Kufikia wakati huo nilikuwa katika uchungu mwingi; nilihisi kwamba kuwa mchanga sana na kuwa nilikuwa nimekubali kazi ya Mungu ya siku za mwisho hivi majuzi tu, bado kulikuwa na mengi sana ya mimi kufurahia, na bado sikuwa nimeiona siku ya utukufu wa Mungu. Kwa kweli sikuwa tayari kukubali kuteswa hadi kufa na serikali ya China. Nilidharau kabisa kikundi hiki cha polisi wasio na huruma, na waovu, na hata nilikuwa na chuki zaidi kwa utawala huu potovu, wa kuasi mbingu, wa kuumiza, na wa Shetani ambao ulikuwa serikali ya China. Ni kitu ambacho kilininyima uhuru wangu wa kumfuata Mungu wa kweli, na ndicho kilichosababisha nichungulie kaburi na hakikuniruhusu nimwabudu Mungu wa kweli. Chama cha Kikomunisti kinampinga Mungu kwa wayowayo, kinawatesa Wakristo kikatili, na kinataka kumwangamiza kila mtu anayeamini katika Mungu na kugeuza China kuwa eneo lisilomtambua Mungu. Pepo huyu Shetani mwovu kweli ni adui anayempinga Mungu bila uwezekano wa kupatana, na zaidi ya hayo, ni adui ambaye kamwe siwezi kumsamehe. Niliapa kwamba hata kama ningekuwa wa kuteswa hadi kufa siku hiyo, kwa kweli singeafikiana au kukubali kushindwa na Shetani hata kidogo! Katika huzuni na hasira yangu, nilikumbuka jambo ambalo Mungu alikuwa amelisema: “Maelfu ya miaka ya chuki ikiwa imejaa kifuani, milenia ya dhambi imeandikwa katika moyo—inawezekanaje hii isichochee chuki? Kumlipiza Mungu, kuuondoa kabisa uadui wake, usimwache kutangatanga tena, na usimruhusu kufanya fujo zaidi kama anavyotaka! Sasa ndio wakati: Mwanadamu ana muda mrefu tangu akusanye nguvu zake zote, amejitolea nguvu zake zote, amelipa kila gharama, kwa hili, kuchana uso uliojificha wa pepo hili na kuwafanya watu, ambao wamepofushwa na kuvumilia kila aina ya mateso na taabu, kuinuka kutoka katika maumivu na kurudi kwa ibilisi huyu wa zamani(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi na Kuingia (8)). Baada ya kutafakari maneno ya Mungu, niliona waziwazi sura ya uovu, ya kikatili ya serikali ya China, na nilitambua kuwa katika wakati huo huo, nilikuwa nikikabili vita vya kiroho kati ya uzima na mauti, kati ya mema na mabaya. Lengo la serikali ya China la kunitesa hivi lilikuwa kunilazimisha nimwache Mungu na nimsaliti, lakini Mungu alikuwa amenikumbusha na kunitia moyo nisimame kidete, nijiondoe kutoka katika mshiko ambao mauti yalikuwa nao kwangu, na kuwa na ushuhuda wa ushindi kwa Mungu. Sikuweza kujiondosha na kuingia katika uhasi; ilinibidi nishirikiane kwa bidii na Mungu na kujisalimisha kwa mipango na utaratibu Wake. Kama Petro, ilinibidi nijisalimishe kwa mauti na, katika wakati wangu wa mwisho wa kuishi, niwe na ushuhuda thabiti, mkubwa kwa Mungu na kuufariji moyo Wake. Maisha yangu yalikuwa mikononi mwa Mungu na, ingawa Shetani anaweza kudhuru na kuua mwili wangu, hangeweza kuangamiza roho yangu, sembuse kufanya kitu chochote kuzuia azimio langu la kumwamini Mungu na kufuatilia ukweli. Ikiwa nilinusurika siku hiyo au la, tamanio langu la pekee lilikuwa kuyakabidhi maisha yangu kwa Mungu na kukubali mipango Yake; hata kama ningejeruhiwa hadi kufa, singejisalimisha kwa Shetani hata kidogo! Nilipokuwa tayari kuyatoa maisha yangu na nikaamua kuwa shahidi kwa Mungu, Mungu alinifungulia njia kwa kuwachochea wafungwa wengine wanilishe. Hayo yalipofanyika, nilijawa na msisimko; moyoni nilijua Mungu yuko nami na alikuwa nami kila wakati. Wakati wote huo, Alikuwa akinilinda na kunihifadhi, Akielewa udhaifu wangu na kupanga kwa uangalifu kila kitu kwa ajili yangu. Katika pango hilo la giza la pepo, hata ingawa mwili wangu ulikuwa umeharibiwa, ndani ya moyo wangu sikuhisi tena uchungu mwingi au dhiki. Baada ya hayo, askari waovu waliniweka kizuizini kwa siku zingine kumi na tano, lakini walipoona kuwa maisha yangu yalikuwa hatarini na kwamba ningeweza kufa wakati wowote, mwishowe hawakuwa na lingine la kufanya ila kuniachilia huru. Hapo awali nilikuwa na uzito zaidi ya kilo hamsini, lakini wakati wa takribani miezi miwili ambayo nilikuwa nimefungwa, nilikuwa nimeteswa hadi nikawa mwebamba sana, nikiwa na uzito wa kilo ishirini na tano au thelathini tu, na maisha yangu yalikuwa katika hali mahututi. Hata hivyo, kikundi hiki cha madubwana bado kilitaka kunitoza faini ya yuani elfu kumi. Mwishowe, walipoona kwamba familia yangu haikuwa na njia yoyote ya kupata kiasi kikubwa hivyo cha pesa, walidai yuani mia sita ya kutosheleza gharama yangu ya chakula, na ni baada tu ya kulipwa ndipo waliponiachilia.

Kupitia mateso haya ya kinyama na ya kikatili mikononi mwa serikali ya China kuliniacha nikijisikia kana kwamba nilikuwa nimetoroka milango ya kuzimu. Kwamba nilikuwa nimeweza kutoroka nikiwa hai ilikuwa kwa ajili ya utunzaji na ulinzi wa Mungu kabisa; ni Mungu aliyekuwa akinionyesha wokovu Wake mkuu. Nilipofikiria upendo wa Mungu, niliguswa sana, na nikapata hata kuthamini zaidi thamani ya maneno ya Mungu. Kwa sababu hii, nilisoma kwa shauku maneno Yake kila siku baada ya hapo, na nilimwomba Mungu mara kwa mara. Hatua kwa hatua, nilipata ufahamu zaidi na zaidi juu ya kazi ambayo Mungu alikuwa akifanya kuwaokoa wanadamu katika siku za mwisho. Baada ya muda, chini ya utunzaji wa Mungu, mwili wangu ulipona polepole, na tena nilianza kueneza injili na kuwa na ushuhuda kwa kazi ya Mungu ya siku za mwisho. Hata hivyo, ilimradi serikali ya shetani ibaki mamlakani, haitakoma kujaribu kuvuruga na kuharibu kazi ya Mungu. Baadaye, nilifuatiliwa kwa wayowayo na kukamatwa na polisi wa serikali ya China.

Siku moja mnamo Novemba ya mwaka wa 2004, upepo wa msimu wa baridi ulikuwa ukivuma baridi kali, na hewa ilikuwa ikizunguka upesi ikiwa na chembe nene za theluji. Nilipokuwa nikieneza injili, mimi na ndugu zangu kadhaa tulifuatwa kisirisiri na polisi wa CCP. Saa mbili kamili jioni, tulikuwa katikati ya mkutano, wakati ghafla tulisikia mshindo wa bisho la haraka na ukelele kwenye mlango: “Fungua! Fungua mlango! Tunatoka kwenye Ofisi ya Usalama wa Umma! Ikiwa hutafungua mlango huu hivi sasa, tutaupiga teke na kuingia! …” Bila wakati wa kufikiria, tulificha hima vipechuro, vitabu, na vitu vingine. Muda mfupi baadaye, polisi watano au sita waliingia kwa ghafla kupitia mlango, wakiingia kwa fujo kama kikundi cha majambazi au waporaji. Mmoja wao alisema kwa sauti, “Mtu yeyote asisonge! Wekeni mikono yenu juu ya vichwa vyenu na mchutame chini kando ya ukuta!” Mara moja, polisi kadhaa waliingia kwa upesi katika kila chumba na kuchakura sehemu nzima. Walichukua ngawira vipechuro vinne vyenye kubebeka na vitabu kadhaa kuhusu imani katika Mungu. Mara tu baadaye, walitulazimisha kuingia katika magari ya polisi na kutusafirisha hadi kwenye kituo cha polisi cha eneo letu. Njiani kuelekea huko, tukio baada ya tukio la mateso mabaya niliyopokea kutoka kwa polisi waovu mwaka uliopita lilikupuka kupitia kumbukumbu yangu, na bila kuepukika nilihisi kwa hakika kuwa mwenye wasiwasi, kwa sababu ya kutokujua ni nini kingine ambacho polisi hawa wa kishetani wangefanya ili kunitesa wakati huu. Nikiogopa kwamba singeweza kuvumilia ukatili wao na kwamba ningeweza kuishia kufanya jambo la kumsaliti Mungu, nilimwomba kimoyomoyo kwa bidii. Ghafla nilikumbuka baadhi ya maneno Mungu ambayo tulikuwa tumesoma wakati wa mkutano siku chache zilizopita: “Nimejawa tumaini kwa ajili ya ndugu Zangu, na Naamini kwamba hamjavunjika moyo wala kukata tamaa, na haijalishi kile ambacho Mungu anafanya, ninyi ni kama chungu chenye moto—huwa hamna uvuguvugu kamwe na mnaweza kushikilia mpaka mwisho, mpaka kazi ya Mungu ifichuliwe kwa ukamilifu …(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Njia … (8)). “Na naomba sote tukule kiapo hiki mbele za Mungu: Kufanya kazi pamoja kwa bidii! Kuwa waaminifu hadi mwisho kabisa! Kutowahi kutengana, na kuwa pamoja daima! Natumai kwamba ndugu wote watoe ahadi hii mbele za Mungu, ili mioyo yetu isibadilike kamwe, na azma yetu isiyumbayumbe kamwe!(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Njia … (5)). Maneno ya Mungu yalinigusa sana. Niliwaza kuhusu jinsi Mungu alivyoshuka kutoka mbinguni kuja duniani na kupitia majaribu na majonzi mengi katika kazi Yake ili kuleta wokovu kwa wanadamu. Ni tumaini Lake kwamba watu watabaki waaminifu thabiti Kwake hadi mwisho, bila kujali hali yao ni ngumu kiasi gani. Kama mtu aliyeteuliwa na Mungu, na aliyefurahia utoaji wa maneno Yake, ilinibidi nijidhabihu Kwake kikamilifu. Niliwaza, “Bila kujali ninaweza kuteseka au kuteswa kiasi gani, moyo wangu huna budi kusalia kujawa na imani; nisibadilishe hisia zangu kwa Mungu, na mapenzi yangu hayafai kuwa na shaka. Sina budi kutoa ushuhuda mkubwa kwa ajili ya Mungu, na nisijisalimishe au kushindwa na Shetani. Zaidi ya hayo, ni sharti nisimsaliti Mungu ili tu kwamba niweze kuendeleza maisha yasiyokuwa na maana, ya aibu. Mungu ndiye ninayemtegemea na, zaidi ya hayo, ndiye nguzo yangu thabiti. Iliradi nishirikiane na Mungu kwa dhati, hakika Ataniongoza kupata ushindi dhidi ya Shetani.” Kwa hivyo, niliazimia kimoyomoyo kwa Mungu, “Ee Mungu! Hata kama ni lazima nijitolee mhanga, nitakuwa shahidi Kwako. Bila kujali nitavumilia mateso ya aina gani, nitashikilia njia ya kweli. Ninakataa kabisa kukubali kushindwa na Shetani!” Kwa ajili ya kutiwa moyo na maneno ya Mungu, imani yangu iliongezeka mara mia, na nilipata imani na azimio la kudhabihu kila kitu ili kuwa shahidi kwa Mungu.

Mara tu tulipofika kwenye kituo cha polisi, polisi walienda kwa haraka kuota moto kando ya stovu. Kila mmoja wao alinikodolea macho, na wakiwa na nyuso zilizokunjwa na macho ya hasira, waliniuliza kwa sauti kali: “Anza kuzungumza! Jina lako ni nani? Umeenezea watu wangapi injili? Je, umekuwa ukiwasiliana na nani? Kiongozi wa kanisa lako ni nani?” Alipoona kwamba nilikuwa nimeazimia kukaa kimya, mmoja wa polisi waovu alifichua hulka yake ya kinyama kwa kunirukia na kunikamata shingoni kwa nguvu. Kisha alibamiza kichwa changu ukutani, tena na tena, mpaka nikahisi kizunguzunguzu na masikio yangu yalikuwa yakiwangwa. Kisha, aliinua ngumi yake na kuupiga mfululizo uso wangu na kichwa changu kikatili huku akisema kwa sauti kubwa, “Wewe ndiye kiongozi, siyo? Zungumza! Usipozungumza, nitakuning’iniza kutoka juu ya jengo na kukuacha ugande hadi ufe!” Polisi hao waovu walinipiga vikali kwa muda wa nusu saa au zaidi, hadi nilikuwa naona vimulimuli na pua langu lilikuwa likitokwa na damu. Walipoona kwamba hawangeweza kupata majibu waliyotaka, walinipeleka kwa Ofisi za PSB. Njiani, niliwaza kuhusu kichapo cha kikatili nilichokuwa nimepokea tu kutoka kwa polisi waovu, na wimbi la woga lilipitia ndani yangu bila hiari. Nilijiwazia, “Kwa kuwa walikuwa wametumia nguvu nyingi kwangu mara tu baada ya kufika kwenye kituo cha polisi, basi je, polisi wa PSB watatumia mateso gani ya kikatili ili unitesa? Hali inayokuja inaonekana itakuwa mbaya kwangu. Kuna uwezekano kuwa sitaweza kuibuka nikiwa hai wakati huu….” Nilipokuwa nikifikiria jambo hili, moyo wangu ulijawa na hisia isiyoelezeka ya kukata tamaa na kuhuzunika. Katika hali yangu ya uchungu na kutojiweza, ghafla nilikumbuka jinsi Mungu alivyoniruhusu kuponea chupuchupu kimiujiza mwaka uliopita polisi waovu waliponitesa nusura nife. Nilichangamka mara moja, na kuwaza, “Kama nitaishi au kufa ni uamuzi wa Mungu, siyo? Bila idhini ya Mungu, Shetani hawezi kufanikiwa kuniua bila kujali atakalolijaribu. Nimeona matendo ya ajabu ya Mungu zamani, kwa hivyo ningewezaje kusahau? Ninawezaje kukosa imani kiasi hiki?” Wakati huo, niliona kwamba kimo change hakikuwa kimekomaa bado—nilipokabiliwa na jaribio la kifo kilicho karibu, bado sikuweza kusimama katika upande wa Mungu. Sikuweza kujizuia kukumbuka mojawapo ya maneno ya Mungu: “Lakini kuishi katika mawazo yako ni kuchukuliwa na Shetani na huu ni mwisho wa njia. Ni rahisi sana sasa: Nitegemee Mimi kwa moyo wako na roho yako mara moja itakuwa imara, utakuwa na njia ya kutenda na Mimi nitakuongoza katika kila hatua. Neno Langu litafichuliwa kwako wakati wote na katika maeneo yote. Bila kujali ni wapi au wakati upi, au mazingira yako ni mabaya namna gani, Mimi nitakuonyesha kwa uwazi na moyo Wangu kufichuliwa kwako ukinitegemea Mimi kwa moyo wako; kwa njia hii utaikimbilia barabara iliyo mbele bila kupoteza njia(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 13). Maneno ya Mungu yalikuwa nuru inayoongoza njia, yakiniletea uwazi zaidi wa mawazo. Niligundua kuwa Mungu alitaka kutumia hali hii ngumu kunitakasa, ili wakati wa hatari ningeachana na fikira na mawazo yangu na mashaka yangu kuhusu mwili wangu, na kwenda mbele huku nikimtegemea Mungu tu na kutegemea maneno ya Mungu peke yake. Huu ulikuwa wakati muhimu sana ambao Mungu alikuwa akiniongoza ili nione kazi Yake, na nilijua kuwa sitashtuka hata kidogo. Ilinibidi niweke maisha yangu na kifo changu mikononi mwa Mungu kikamilifu na kumtegemea Mungu ninapokuwa nikikabiliana dhidi ya Shetani hadi mwisho!

Tulipofika katika kituo cha PSB, polisi walitutenganisha tena na kutuhoji mmoja mmoja. Walipokuwa wakijaribu kunilazimisha niwaeleze juu ya mambo yanayohusu imani yangu katika Mungu, mmoja wa polisi wabaya aliona kwamba nilikuwa nikisisitiza kukaa kimya, jambo lililomfanya aghadhabike kwa ghafla: “Unafikiri kuwa unaweza kuepuka kuadhibiwa baada ya kujifanya bubu. Sina subira na hilo!” Alipokuwa akisema hivyo, alinishika kwa nguvu kwenye kola na mikono yote mawili na kunitupa chini kwa nguvu kama mfuko wa mchanga. Kisha wale polisi wengine waovu wakasonga mbele na kuanza kunipiga mateke na kunikanyaga kote mwilini mwangu, hadi nilikuwa nikibingirika kwa ajili ya maumivu. Baada ya hayo, waliweka miguu yao kichwani mwangu na kunigandamiza kuelekea chini, wakifikicha kwenda mbele na nyuma…. Bado sikuwa nimepona kabisa kutokana na mateso ya kikatili ambayo nilivumilia mwaka uliopita, kwa hivyo baada ya kupigwa vibaya sana, ghafla nilihisi kizunguzungu na kichefuchefu. Nikiwa katika maumivu makali kabisa kutoka utosini hadi kidoleni, nilikunjamana kwa umbo la mpira. Kisha, polisi waovu walinivua viatu vyangu na soksi kwa fujo, kisha wakanilazimisha kusimama pekupeku sakafuni. Ilikuwa baridi sana meno yangu yalitatarika bila kutaka, na nyaya zangu zote zikakufa ganzi kabisa. Nilihisi kuwa singeweza kuvumilia tena, na kwamba ningeanguka chini wakati wowote. Nilipokumbana na mateso haya ya kikatili na yenye nia mbaya ya polisi, sikujizuia kuhisi hasira kali na uchungu. Niliwadharau watumishi hawa wovu wa ibilisi, na nikachukia serikali mbaya, yenye kupinga maendeleo ya China. Inapinga Mbingu na ni adui ya Mungu, na ili kunilazimisha nimsaliti Mungu na kumkataa, ilikuwa ikiniumiza na kunitesa, ikinuia kuniua bila hadhari. Nikikabiliwa na ukali na ukatili wa Shetani, nilifikiria zaidi juu ya upendo wa Mungu. Nilifikiri sana kuhusu ukweli kwamba ili kuleta wokovu kwa wanadamu, na kwa ajili ya maisha yetu ya siku zijazo, Alikuwa amevumilia fedheha kubwa alipokuwa akitembea katika mwili kati yetu ili kufanya kazi Yake. Alikuwa ametoa maisha Yake kwa ajili yetu, na sasa alikuwa akionyesha maneno Yake kwa ustahimilivu na kwa bidii maneno Yake ili kutuongoza kwenye njia ya kufuatilia ukweli ili kupata wokovu.… Nilipohesabu gharama yote ya bidii ya kazi ambayo Mungu alikuwa amelipa kwa ajili ya wokovu wa wanadamu, nilihisi kwamba hakuna mtu aliyenipenda zaidi kuliko Mungu; Mungu alithamini maisha yangu kuliko mtu mwingine yeyote. Shetani angeweza tu kuniumiza, au kuniumiza na kuniua. Wakati huo huo, nilihisi upendo zaidi na heshima kubwa zaidi kwa Mungu ikinawiri moyoni mwangu na sikuweza kujizuia kumwomba kimya kimya: “Mungu, asante kwa kuniongoza na kuniokoa namna hii. Bila kujali jinsi Shetani anavyonitesa leo, kwa hakika nitafanya bidii kushirikiana na Wewe. Ninaapa, sitakubali kushindwa au kujisalimisha kwa Shetani!” Nikiwa nimetiwa moyo na upendo wa Mungu, ingawa mwili wangu ulikuwa dhaifu na haukuwa na nguvu kutokana na kuteswa, moyo wangu ulikuwa thabiti na wenye nguvu, na sikuwahi kukubali kushindwa na polisi hao wabaya. Waliendelea kunitesa hadi saa saba kamili usiku uliofuata wakati, walipoona kwamba hawangepata majibu yoyote kutoka kwangu, hawakuwa na lingine la kufanya ila kunipeleka kizuizini.

Baada ya kufika kizuizini, polisi waovu waliwachochea tena waonevu wa gereza wafikirie njia yoyote wanayoweza kuniadhibu. Kufikia wakati huo nilikuwa nimeteswa sana hadi mwili wangu ulikuwa umejawa na majeraha na vilio vya damu; nilikuwa mlegevu kabisa, na mara tu nilipoingia katika seli yangu ya gereza nilianguka moja kwa moja hadi kwenye sakafu baridi sana mara moja. Waliponiona nikiwa hivi, bila kusema neno lingine, waonevu wa nyumba ya gereza walinichukua na kunipiga mfululizo kichwani mwangu kwa ngumi. Walinipiga mpaka nikapatwa na kizunguzungu, na tena nilianguka chini kwa kishindo. Baada ya hapo, wafungwa wote walikuja kunitania, na kunilazimisha nigandamize mkono mmoja dhidi ya sakafu na mwingine juu ya sikio langu, na kisha nizunguke kwa mviringo sakafuni kama dira. Baada ya kuniona nikianguka sakafuni kwa ajili ya kizunguzungu kabla kukamilisha mizunguko mingine kadhaa, walinipiga mateke na kunichapa tena. Mmoja wa wafungwa hata aligonga tumbo langu vikali, na kusababisha nizimie papo hapo. Baada ya hapo, wafungwa walipewa maagizo na maafisa wa marekebisho ya kunitesa na kunidhalilisha katika njia tofauti kila siku, na kunishurutisha nifanye kazi zote ndogo ndogo zisizopendeza za kila siku kama vile kuosha vyombo vyote, kusafisha vyoo, na kadhalika. Nililazimishwa hata kuoga kwa maji baridi wakati wa siku zenye theluji. Zaidi ya hayo, kila nilipooga, wote walinilazimisha nijiwekeee povu kwa sabuni kutoka utosini hadi kidoleni na kisha kuacha maji baridi sana yatiririke polepole mwilini mwangu mwote. Baada ya kuoga kwa takribani nusu saa, nilihisi baridi sana hadi nilikuwa na rangi ya zambarau kote na kutetemeka. Nikikabiliwa na mateso haya ya kinyama na ukatili, nilimwomba Mungu kila wakati, nikiwa na hofu kwamba ikiwa ningemwacha Mungu, ningechukuliwa mateka kikamilifu na Shetani. Kupitia maombi, maneno ya Mungu yalivuma mfululizo ndani yangu na kuniongoza: “Wale wanaoitwa washindi na Mungu ni wale ambao bado wanaweza kusimama kama mashahidi, wakidumisha imani yao, na ibada yao kwa Mungu wanapokuwa chini ya ushawishi wa Shetani na kuzingirwa na Shetani, hiyo ni, wanapokuwa katika nguvu za giza. Kama bado unaweza kudumisha moyo wa utakaso na upendo wako wa kweli kwa Mungu kwa vyovyote vile, unasimama shahidi mbele ya Mungu, na hii ndio Mungu Anaita kuwa mshindi(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Unapaswa Kudumisha Ibada Yako kwa Mungu). Maneno ya Mungu yalikuwa nuru, yakiniangaza na kutuliza mawazo yangu. Nilijua kuwa nilipokuwa nikizingirwa na Shetani ndio wakati halisi ambao nilihitaji kuwa na uaminifu na upendo kwa Mungu. Hata ingawa hali hii ya taabu ilikuwa imeleta mateso na maumivu katika mwili wangu, chanzo chake kilichofichika kilikuwa ni upendo mkubwa na baraka za Mungu. Ni Mungu ndiye aliyekuwa amenipa nafasi ya kuwa shahidi Kwake mbele ya Shetani na kumdhalilisha kabisa na kumshinda Shetani. Kwa hivyo, nilipokuwa nikipitia mateso haya, nilijionya tena na tena kwamba sina budi kuwa mvumilivu hadi mwisho, kuwa shahidi kwa Mungu kwa kutegemea mwongozo Wake katika pango hili la giza la pepo, na kujitahidi kuwa mshindi. Nikiongozwa na maneno ya Mungu, moyo wangu ulizidi kuwa thabiti na imara. Licha ya udhaifu na uchungu uliuotesa mwili wangu, nilikuwa na imani kwamba ningeweza kuvumilia yote ili kuanzisha vita vya kufa na kupona dhidi ya Shetani na kuwa shahidi kwa Mungu na pumzi yangu ya mwisho kabla ya kufa.

Baada ya kuzuiliwa kwa zaidi ya siku ishirini, ghafla nilipata homa kali. Viungo vyangu vyote vinne vikaanza kuuma na kulegea, nilikuwa nimedhoofishwa kabisa, na akili yangu ikachanganyikiwa. Pamoja na hali yangu iliyokuwa ikizorota na kupigwa bila huruma na mateso kutoka kwa wafungwa wengine, nilihisi kuwa singeweza kuvumilia tena. Moyoni mwangu, nilihisi hasa dhaifu na mwenye huzuni, na nilijiwazia, “Je, mateso na ukatili huu wa kila siku utakoma lini? Inaonekana kuwa nitahukumiwa wakati huu, kwa hivyo hakuna tumaini kubwa kwamba nitatoka hapa nikiwa hai….” Mara tu nilipofikiria hivyo, ghafla moyo wangu ukahisi kana kwamba ulikuwa umeanguka kwenye lindi lisilo na mwisho, na nilizama katika hali ya kukata tamaa kabisa na maumivu kiasi kwamba sikuweza kupata njia ya kujinasua. Katika wakati wangu wa kukata tamaa kabisa, nilikumbuka wimbo wa maneno ya Mungu: “Mimi sitamani wewe uweze kuongea maneno mengi matamu, au utoe hadithi nyingi za kufurahisha; badala yake Ninauliza kuwa uweze kuwa na ushuhuda mzuri Kwangu, na kwamba unaweza kuingia kikamilifu na kwa kina katika hali halisi. … Msifikiri juu ya matarajio yenu tena, na mtende vile ambavyo mmeamua mbele Yangu kutii mipango ya Mungu katika kila kitu. Wale wote wanaosimama miongoni mwa kaya Yangu wanapaswa kufanya mengi kiasi wanachoweza; unafaa utoe hali yako bora zaidi kwa sehemu ya mwisho ya kazi Yangu duniani. Je, unayo nia ya kuviweka vitu vya aina hii katika matendo?(“Kweli Unaweza Kutii Utaratibu wa Mungu” katika Mfuateni Mwanakondoo na Kuimba Nyimbo Mpya). Mstari kwa mstari, maneno ya Mungu yalinigusa moyoni mwangu, na kunifanya nione aibu sana. Nilifikiria kuhusu idadi ya nyakati ambazo nilikuwa nimelia machozi machungu, na nikaazimia zaidi kujitolea kwa Mungu katika kila jambo na kujisalimisha kwa mipangilio na utaratibu Wake. Nilifikiria pia jinsi, maneno ya Mungu yalipokuwa yameniongoza wakati ambapo nilikuwa nikivumilia mateso na uchungu, nilikuwa nimeahidi maisha yangu mbele ya Mungu kwamba nitakuwa shahidi Kwake, lakini kwamba mara tu Mungu aliponihitaji nilipe gharama halisi ili kumridhisha, nilikuwa badala yake nimeshikilia maisha kwa kwa njia ya kudhalilisha mno na kuogopa kifo, nikijali tu kuhusu kile kitakachotokea kwa mwili wangu. Nilikuwa nimepuuza kabisa mapenzi ya Mungu, na nilifikiria tu kuhusu kutoroka shida yangu na kufika mahali pa usalama haraka iwezekanavyo. Niliona jinsi nilivyokuwa kweli duni na asiyefaa kitu; sikuwa na imani ya kutosha katika Mungu, na nilikuwa nimejawa na udanganyifu mno. Sikuweza kumpa Mungu ibada yoyote ya kweli, na sikuwa na utii wowote wa dhati mwilini mwangu. Katika wakati huo nilifahamu kuwa katika kazi ya Mungu ya siku za mwisho, Alichotaka ni upendo na uaminifu wa kweli wa wanadamu; haya ni matakwa ya mwisho ya Mungu, na jukumu la mwisho ambalo amemkabidhi wanadamu. “Kama mtu anayeamini katika Mungu,” niliwaza, “ninapaswa kujiweka mikononi Mwake kabisa. Kwa sababu nimepewa maisha yangu na Mungu, ana uamuzi wa kuamua iwapo nitaishi au kufa. Kwa kuzingatia kwamba nimemchagua Mungu, napaswa kujidhabihu Kwake na kujisalimisha kwa utaratibu Wake; bila kujali ni mateso au udhalilishaji gani ambao ninapitia, ninapaswa kujitolea kwa Mungu kwa matendo yangu. Sipaswi kuwa na chaguo au madai yangu mwenyewe; huu ni wajibu wangu, na pia kufikiria nikakopaswa kuwa nako. Ukweli kwamba bado nilikuwa na uwezo wa kuvuta pumzi na nilikuwa hai yote yalitokana na ulinzi na utunzaji wa Mungu; huu ndio ulikuwa utoaji Wake wa maisha!—vinginevyo, si ningekuwa nimeumizwa na ibilisi hadi kufa hapo zamani? Wakati wa kwanza nilipopitia mateso na shida kubwa kama hizi, Mungu alikuwa ameniongoza kuzishinda. Je, nilikuwa na sababu gani ya kupoteza imani katika Mungu? Je, ninawezaje kuwa hasi na dhaifu, nikirudi nyuma na kutamani kukimbia?” Wazo hili lilipokuwa likinitokea, nilikiri hatia yangu kwa Mungu kimoyomoyo: “Mwenyezi Mungu! Mimi ni mbinafsi na mwenye tamaa sana; nimekuwa nikitaka tu kufurahia upendo Wako na baraka Zako, lakini sijataka kujitolea kwa dhati Kwako. Ninapofikiria juu ya kuvumilia mateso ya kufungwa gerezani kwa muda mrefu, ninataka tu kutoroka gereza na kuiepuka. Kwa kweli nimeumiza hisia Zako vibaya. Ee Mungu! Sitaki kuendelea kuzama zaidi; ninataka tu kujisalimisha kwa mipango na utaratibu Wako na kukubali mwongozo Wako. Hata nikifa gerezani, bado ninataka kuwa shahidi Kwako. Ingawa ninaweza kuteswa hadi kufa, nitabaki mwaminifu Kwako hadi mwisho!” Baada ya kuomba, niliguswa maradufu. Hata ingawa bado nilikuwa na uchungu kama awali, moyoni mwangu nilihisi imani na azimio la kutokata tamaa ilimradi sikuwa nimetimiza ahadi yangu ya kumridhisha Mungu. Mara tu nilipokuwa nimeazimia na kujiamini kuwa nitakuwa shahidi kwa Mungu mpaka kifo, jambo la kimiujiza lilitokea. Mapema asubuhi moja, nilitoka kitandani, na nikagundua kuwa sikuwa na hisia katika miguu yangu yoyote. Sikuweza kusimama hata kidogo, sembuse kutembea. Mwanzoni polisi waovu hawakuniamini; wakichukulia kuwa nilikuwa nikijisingizia, walijaribu kunilazimisha nisimame. Hata hivyo, bila kujali nilijitahidi kiasi gani, sikuweza kusimama. Walirudi siku iliyofuata kunikagua tena. Walipogundua kuwa miguu yangu yote ilikuwa baridi mno na bila mzunguko wowote wa damu, walisadikishwa kuwa kweli nilikuwa nimepooza. Baada ya hapo, waliiarifu familia yangu kuwa wanaweza kunipeleka nyumbani. Siku ambayo nilikwenda nyumbani, hisia zilirejeshwa kimiujiza kwa miguu yangu, na sikuwa na tatizo la kutembea hata kidogo! Ninajua moyoni mwangu kwamba hii ilikuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu aliyekuwa akionyesha huruma kwa ajili ya udhaifu wangu. Yeye Mwenyewe alikuwa amenifungulia njia mpya, Akiniruhusu kutoroka kutoka katika pango la Shetani bila kikwazo baada ya kuzuiliwa kinyume na sheria kwa muda wa mwezi mmoja na serikali ya China.

Baada ya kuwekwa kizuizini mara mbili na kupitia mateso ya kinyama ya kikatili ya serikali ya China, hata ingawa niliteseka kiasi kimwili na hata nilikaribia kufa, matukio haya mawili yasiyo ya kawaida kwa kweli yaliunda msingi thabiti kwenye njia yangu ya kuwa na imani katika Mungu. Katika hali ya mateso yangu na dhiki, Mwenyezi Mungu alikuwa ameninyunyuzia ukweli na utoaji wa maisha kwa utendaji, sio kuniruhusu tu kuing’amua serikali ya China, chuki yake kwa ukweli, uadui wake kwa Mungu, na sura yake ya shetani, na kufahamiana na uhalifu wake wa kuchukiza wa kumpinga Mungu kwa hasira na kuwatesa waumini Wake, lakini pia alinipa utambuzi wa nguvu na mamlaka ya maneno ya Mungu. Kwamba niliweza kutoroka mifumbato ya uovu ya Chama cha Kikomunisti cha China nikiwa na maisha yangu, mara mbili, ilikuwa ni matokeo ya utunzaji na huruma ya Mungu. Zaidi ya hayo, ilikuwa mfano na uthibitisho wa nguvu ya ajabu ya maisha ya Mungu. Niligundua kwa kina kwamba wakati wowote na mahali popote, Mwenyezi Mungu alikuwa daima msaada wangu na wokovu wangu wa pekee! Katika maisha haya, bila kujali ni hatari gani au shida gani ninazoweza kukabiliwa nazo, niliazimia kubaki nimejitolea nafsi kumfuata Mwenyezi Mungu, kueneza neno Lake na kuwa shahidi kwa jina la Mungu, na kulipiza upendo wa Mungu kwa kujitolea kwangu kwa dhati!

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Upendo wa Mungu Hauna Mipaka

Na Zhou Qing, Mkoa wa ShandongNimepitia taabu ya maisha haya kikamilifu. Sikuwa nimeolewa kwa miaka mingi kabla ya mume wangu kufariki, na...

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp