Neno La Mungu Ni Nguvu Yangu Katika Maisha

26/01/2021

Na Xu Zhigang, Manispaa ya Tianjin

Hapo zamani, niliathiriwa sana na maadili ya kitamaduni ya China, na kufanya ununuzi wa mali isiyohamishika kwa ajili ya watoto na wajukuu wangu kuwa lengo langu la maisha. Ili kufanikisha hili, nilijitolea kujifunza kuhusu teknolojia ya matengenezo ya magari. Pia nilifungua gereji la matengenezo, na biashara iliendelea vizuri sana. Wakati huo maishani mwangu, niliamini kuwa nilidhibiti kudura yangu mwenyewe, kwa hivyo shemeji yangu aliponihubiria injili ya Bwana Yesu, sikukataa tu kuipokea, kwa kweli nilimdhihaki, kwa sababu nilihisi kuwa ningeweza kuishi vizuri tu bila kumwamini Bwana. Hata hivyo, nyakati nzuri hazikudumu. Biashara ilizidi kuwa mbaya zaidi kwenye gereji langu, na bila kujali nilijitahidi kiasi gani, sikuweza kubadilisha hali kuwa nzuri. Nilijichosha kwa kazi ngumu nikijaribu kubadilisha hali hiyo, na nilikuwa mchovu na mnyonge, kwa hivyo nilianza kunywa pombe siku nzima ili kupunguza wasiwasi wangu. Kwa sababu hiyo, siku moja, sikumakinika nilipokuwa nikiliendesha gari na nikaishia kuhusika katika ajali. Gari langu lilipondeka lisiweze kutambuliwa, lakini kwa bahati nzuri na kimiujiza, niliponea chupuchupu. Muda mfupi baadaye, katika majira ya kuchipuka ya mnamo mwaka wa 1999, mke wangu alinihubiria injili ya Mwenyezi Mungu ya siku za mwisho. Nilikuja kufahamu ukweli kiasi kwa kusoma maneno ya Mwenyezi Mungu, na niligundua kwamba sababu ambayo nilikuwa nikiishi katika hali kama hiyo yenye taabu, isiyo na msaada ni kwamba nilikuwa nimekubali kanuni za maisha ambazo Shetani huwafundisha watu. Nilikuwa nikitaka kutegemea juhudi yangu mwenyewe kujijengea maisha ya furaha, na matokeo yake ni kwamba nilidanganywa hadi kiwango ambacho nilijikuta katika mateso ya kuzidi kiasi, na karibu nipoteze maisha yangu. Ni Mwenyezi Mungu ndiye aliyenitoa katika hali ya kuchungulia kaburi na kunipeleka ndani ya nyumba Yake, na nilimshukuru sana kwa kunirehemu. Kuanzia wakati huo, kila siku nilisoma neno la Mungu, na pia nilihudhuria mikutano na kushirikiana na ndugu zangu, na nuru ilijaa moyoni mwangu. Nilifurahia, na kushangilia kuwa nilikuwa nimepata njia ya kweli maishani. Hata hivyo, muda si muda, nikawa mlengwa wa kukamatwa na serikali ya CCP kwa ajili ya imani yangu katika Mungu, na nililazimika kuiacha familia yangu na kwenda mafichoni. Wakati huo, hata ingawa nilipitia nyakati za udhaifu, niliamini kwamba bila kujali nilikoenda na bila kujali jinsi pepo wa Shetani wanavyoweza kuniandama, maneno ya Mungu yangeniongoza. Zaidi ya miaka kumi baadaye, kupitia mwongozo na riziki ya neno la Mungu, nilielewa ukweli fulani polepole, na maisha yangu yalikuwa ya kuridhisha sana. Katika wakati wote uliofuata, wakati ambao nilikamatwa na kuteswa, nilipata kuona zaidi kwa utendaji kwamba neno la Mungu ni nguvu yangu maishani, kwa kuwa lilikuwa neno la Mungu ambalo liliniruhusu kusimama kidete, wima, na bila woga katikati ya maumivu makali na mateso ya ukatili ya Shetani, ili hatimaye niweze kumdhalilisha Shetani kabisa. Baada ya tukio hili, nilithamini neno la Mungu hata zaidi, na singeweza kuwa mbali na neno la Mungu hata kwa muda mfupi.

Siku moja mnamo Februari mwaka wa 2013, nilikuwa nje nikieneza injili na baadhi ya ndugu, lakini tulipokuwa tukirudi, tulisimamishwa na gari ndogo. Maafisa watatu wa polisi walishuka kutoka kwenye gari hilo na kuulizia vitambulisho vyetu, na waliposikia lafudhi yangu isiyo ya eneo hilo, walinipekua kwa nguvu bila hata kutoa sababu. Walinipokonya kutoka kwa mifuko yangu kadi ya Benki ya Kilimo ya China ambayo ilikuwa na yuani zaidi ya 700, zaidi ya yuani 300 pesa taslimu, simu ya rununu, pataningo, na baadhi ya habari za injili. Mara tu mmoja wa maafisa hao alipogundua kuwa namwamini Mwenyezi Mungu, mwenendo wake ulianza kuwa mkali sana, na alinitia pingu kwa nguvu na kunisukuma ndani ya gari. Kwenye kituo cha polisi, waliniamuru nisimame kando ya ukuta, ambapo afisa mmoja aliniuliza kwa ukali, “Jina lako ni nani? Makaazi yako yapo wapi? Ni nani aliyekuhubiria kuhusu imani katika Mungu?” Alipoona kuwa sikumjibu, alighadhabika kwa ghafla, akavua koti langu, kisha akanigeuza na kuvuta sweta yangu kutoka mgongoni mwangu juu ya kichwa changu na kuupiga mgongo wangu vibaya kwa kirungu chake. Kila baada ya mipigo kadhaa, aliniuliza, “Utazungumza sasa?” Baada ya kunipiga tena na tena mara kumi na tano, nyama mgongoni mwangu ilihisi imekwaruzwa, na uti wangu ulihisi kama ulikuwa umevunjika, uliuma sana. Lakini bila kujali walinipiga kiasi gani, nilikataa kuzungumza. Mwishowe, akibabaika kwa hasira, alifoka, akisema, “Barabara, nimesalimu amri! Kukupiga kwa namna hii kunafanya kifundo cha mkono wangu kuuma, na bado huzungumzi!” Moyoni mwangu, nilijua kuwa Mungu alikuwa akinilinda. Singeweza kuhimili kichapo cha nguvu nyingi peke yangu. Nilimshukuru Mungu kimoyomoyo.

Waliona kwamba kunipiga hakukuwa na ufanisi dhidi yangu, kwa hivyo walibadilisha mbinu. Mmoja wa polisi hao waovu alileta fimbo lenye urefu wa takriban mita moja na sentimita sita katika kipenyo, na akiwa na tabasamu baya alisema, “Hebu tumfanye ‘aonje raha’ ya kupiga magoti juu ya fimbo hii kisha tuone ikiwa atazungumza!” Nilikuwa nimesikia kwamba baada ya kupiga magoti juu ya fimbo kama hii kwa muda wa dakika 30, mtu hangeweza kusimama wima au kutembea. Nilipokabiliwa na mateso ya aina hii, nilihisi kwamba kimo changu cha kiroho kilikuwa kidogo sana, na kwamba mwili wangu haungeweza kuvumilia. Niliogopa, kwa hivyo kwa nguvu zangu zote nilimwomba Mungu, “Mungu! Kimo changu ni kidogo sana, na ninaogopa kuwa siwezi kuhimili maumivu makali ya aina hii. Tafadhali ulinde moyo wangu na Unipe nguvu ya kuvumilia maumivu haya makali na sio kukusaliti.” Nilimwomba Mungu tena na tena, na Mungu alijua kuwa mwili wangu ulikuwa dhaifu. Alisikia maombi yangu, kwa sababu mwishowe, polisi hawa wabaya waliamua kutotumia aina hii ya mateso. Ukweli mbele zangu ulidhihirisha rehema na ulinzi wa Mungu kwangu, ambao uliongeza imani yangu Kwake na kupunguza woga wangu kwa kiasi kikubwa. Ingawa waliamua kutotumia njia hiyo ya mateso, bado hawakuwa tayari kunichilia. Badala yake, walifikiria njia nyingine ya mateso. Walinilazimisha nipige magoti sakafuni kiuno changu kikiwa kimenyooshwa, kisha wakamfanya afisa wa kiume aliyekuwa jitu mwenye kimo zaidi ya mita 1.8 asimame juu ya mashavu ya miguu yangu kwa nyaya zake zote mbili na kukanyaga chini kwa nguvu awezavyo. Aliposimama juu ya miguu yangu, nilihisi maumivu makali, kisha nikamwomba Mungu kwa nguvu yangu yote, “Mungu! Siwezi kuhimili mateso ya kinyama kama haya, lakini ningependa kukutosheleza, kwa hivyo ninakuomba Unipe imani, nguvu, na dhamira ya kuvumilia mateso. Ningependa kusimama kidete katika ushuhuda wangu Kwako.” Shukrani ziwe kwa Mungu, kwa ajili mara nyingine tena Alisikia maombi yangu. Afisa huyo wa polisi mnene hakuweza kudumisha mkao imara juu ya mashavu ya miguu yangu, kwa hivyo kabla ya muda mrefu aliondoka kutoka kwangu. Afisa aliyekuwa karibu naye alighadhabika ghafla na akasema, “Ewe mpumbavu asiye na maana! Kwa nini unaondoka kwake baada ya muda mfupi sana hivi?” Pepo hawa kwa kweli walikuwa waovu na wenye ukatili usio na kifani. Walifikiria kila njia inayowezekana ya kunitesa, na walikuwa na hamu ya kuniua, kana kwamba kifo changu tu ndicho kingewaridhisha. Walinilazimisha nikae katika mkao wa kupiga magoti wima na hawakaniruhusu nisonge. Baadaye, mmoja wa maafisa wa polisi aliwatazama wengine kwa mtazamo wa ishara, na kisha wengine wote wakatoka, wakiniacha peke yangu chumbani na afisa huyo wa polisi akinilinda. Alinijia na kujaribu kujipendekeza kwangu, akitabasamu kinafiki alipokuwa akisema, “Mama yangu pia anaamini katika Mungu. Niambie jinsi ulivyokuja kuamini. Ningependa kumwamini Mungu pamoja nawe, kwa hivyo nipeleke nikutane na wakubwa wako.” Niliposikia uwongo wake na kutazama tabasamu lake la kilaghai, ghafla nilihisi kuchukizwa sana. Nilipokuwa karibu kuweka wazi hila yake, ghafla nilikumbuka neno la Mungu: “Lazima uwe na ushujaa Wangu ndani yako…. Lakini kwa ajili Yangu, si lazima pia usikubali kushindwa na nguvu zozote za giza. Tegemea hekima Yangu ili kutembea kwa njia kamili; usiruhusu njama za Shetani kuchukua umiliki(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 10). Maneno ya Mungu yalinipa mwongozo wa wakati wa kufaa, yakiniwezesha kufahamu kwamba, hata zaidi ya ujasiri, ninahitaji hekima mbele ya Shetani. Wakati wote lazima tumtegemee Mungu atupe hekima ya kupambana na Shetani. Kupitia nuru na mwongozo wa neno la Mungu, nilijua cha kufanya, kwa hivyo nilisema, “Ikiwa kweli unataka kuamini, unahitaji tu kusoma neno la Mungu nyumbani. Huhitaji kutoka na kumwona mtu yeyote.” Baada tu ya kumaliza kuzungumza, polisi mwovu ambaye alinipiga aliingia na kuniambia kwa nia mbaya, “Wewe ni msumbufu sana kufanya kazi naye!” Nilijua kuwa Shetani alikuwa ameshindwa na alidhalilishwa, kwa hivyo nilimshukuru Mungu kimoyomoyo. Niliona kuwa Mungu alikuwa na mimi kila wakati, Akiniongoza, Akinitia moyo, na Akikinga kimiujiza vurugu la mkono mbaya wa ibilisi. Upendo wa Mungu kwangu ni mkubwa sana! Wakati huo, ingawa nilikuwa nimenaswa katika seli, nilihisi kwamba uhusiano wangu na Mungu ulikuwa wa karibu zaidi kuliko wakati wowote hapo awali, na nilihisi raha na kuegemezwa sana. Walinilazimisha kupiga magoti kwa zaidi ya muda wa saa mbili. Mwishowe, baada ya saa saba usiku, walipogundua kwamba mahojiano hayakuwa yakileta matokeo, hawangeweza kufanya chochote ila kuondoka wakiwa na moyo mzito.

Asubuhi ya siku ya pili, polisi walinipeleka katika ofisi ya tawi la Ofisi ya Usalama wa Umma. Baada ya kuingia katika chumba cha mahojiano, mkuu wa polisi wa jinai aliniuliza kwa hasira, “Jina lako ni nani? Makaazi yako yapo wapi? Ni nani aliyekujulisha kwa imani katika Mungu? Je, umemwamini Mungu kwa muda gani? Watu unaohusiana nao ni kina nani? Niambie kila kitu, au ninakuahidi kuwa utakiona cha mtema kuni!” Lakini bila kujali alichouliza, sikumwambia chochote. Siku nzima alinihoji kwa kutumia mbinu kali na za upole, lakini hakupata habari yoyote kutoka kwangu, na hatimaye, akiwa ameghadhabika, alisema kwa sauti kubwa, “Hutazungumza?! Basi hebu tuone jinsi utakavyopenda maisha kizuizini! Ikiwa unataka mambo yawe magumu, hakika tunaweza kufanya hivyo! Ikiwa hutatupa majibu tunayotaka, tutakuzuilia humo ndani milele!” Na kwa hivyo, nilipelekwa kizuizini na kufungwa katika seli ambayo ilihifahdi idadi kubwa zaidi ya wahalifu waliofanya makosa makubwa. Nilipoingia kwenye seli, nilipatwa na hofu kubwa kwa sababu ya mazingira ya huzuni na ya kutisha ya mahali hapo. Kuta za seli zilikuwa na urefu wa mita nne, kulikuwa na giza na unyevu, dirisha moja dogo tu ndilo liliruhusu miale michache ya jua kuingia ndani, na kulikuwa na uvundo mbaya, wenye harufu nzito iliyooza ambayo ilifanya hewa kuwa vigumu kupumua. Chumba hiki kidogo kilijaa kabisa wahalifu; kulikuwa na wauaji, watumiaji wa dawa za kulevya, na waporaji, wote wahalifu wa makosa makubwa. Kila mmoja wao alionekana mkatili na mkali, na kadhaa walikuwa warefu, wenye misuli minene na nyuso mbaya za nyuzinyuzi, na miili iliyojawa na michoro ya mazimwi, mafiniksi, nyoka, na mengineyo kama hayo. Baadhi ya wafungwa walikuwa wembamba kama reki, kama viunzi vya mifupa viliyo hai, na walinifanya nitetemeke kwa kuwatazama tu. Kulikuwa na mpangilio wa nafasi kati ya wafungwa, na waumini katika Mwenyezi Mungu walikuwa chini kabisa, bila haki yoyote kabisa ya kuzungumzia. Kitufe cha kupiga simu ya dharura kilichowekwa kwenye ukuta kilikuwa mwanzoni kimekusudiwa kutumiwa na wafungwa katika hali za dharura kumwita askari jela, lakini waumini katika Mwenyezi Mungu hawakuwa na haki ya “kufaidika na” matumizi yake hata kidogo. Bila kujali udhalimu ulikuwa wa kinyama kiasi gani, hakuna mtu angejibu kamwe.

Siku yangu ya kwanza kwenye seli, mfungwa mkuu alinidhihaki baada ya kupata habari kuhusu hali yangu, akisema, “Kwa kuwa unaamini katika Mwenyezi Mungu, mwambie Akutoe hapa. Ikiwa Mungu wako ni mzuri sana, kwa nini Alikuruhusu uishie kuwa mahali hapa?” Mfungwa mwovu aliyekuwa karibu naye alijiunga kwenye dhihaka, “Unadhani ni nani bora, mfungwa wetu mkuu hapa au Mungu wako?” Nilipowasikia wakimdharau na kumtusi Mungu nilikasirika. Nilitaka kubishana nao, lakini sikuweza kufanya hivyo. Nilikumbuka kwamba Mahubiri na Ushirika Kuhusu Kuingia Katika Maisha yanasema kwamba asili ya wapotovu ni ile ya pepo, na hii ni kweli kabisa! Pepo hawa hawakuwa na busara hata kidogo, na walistahili kulaaniwa! Nilipokosa kujibu, mfungwa mkuu alighadhabika kwa ghafla na kunizaba kofi vibaya mara mbili, baada ya hapo alinipiga makonde kwa nguvu kwenye kidevu, akiniangusha sakafuni. Niliogopa sana kukabiliana na pepo hawa, na sikuweza kujizuia kumwomba Mungu, “Ee Mungu! Unajua kuwa mimi ni mwenye hofu na dhaifu, na kwamba daima nimewaogopa wauaji na majambazi. Tafadhali Unilinde, Unipe imani na nguvu, na Uniwezeshe nisipoteze ushuhuda wangu katika hali hii.” Ibilisi hawa waliona kwamba sitazungumza, kwa hivyo walifikiria njia nyingine ya kunitesa. Mhalifu ambaye alionekana kama kiunzi cha mifupa alinijia na akanishurutisha kusonga nyuma dhidi ya ukuta. Kisha akawaambia wafungwa wengine wawili washikilie mabega yangu dhidi ya ukuta, baada ya hapo alifinya paja langu la ndani kwa nguvu alivyoweza, kwanza kushoto, kisha kulia, na kila wakati nilikuwa nikisikia maumivu makali ambayo yalikuwa ya kuumiza isivyoelezeka. (Baadaye, miguu yangu ilijaa michubuko kadhaa mikubwa, ambayo hata leo haijatoweka). Halafu, aligonga kwa ukali upande wa nje wa mapaja yangu kwa ngumi zake. Mara tu baada ya hapo, nilichuchumaa kwenye sakafu, na ikawa vigumu sana kwangu kusimama tena. Hata wakati huo, hawakukoma kuniumiza vibaya. Ilikuwa katikati ya msimu wa baridi na kulikuwa baridi kali, lakini ibilisi hawa waliniamuru nivue nguo zangu na kuchuchumaa dhidi ya ukuta chini ya mfereji. Walinimwagia maji bila kukoma na kufungua dirisha kimakusudi, wakinifanya nihisi baridi sana sikuweza kukoma kutetemeka. Mmoja wa wafungwa alipoona kwamba nilikuwa nikikereza meno yangu ili kuvumilia mateso, alichukua kipande cha bodi ya povu na kukibembeza kama feni ili kupuliza hewa baridi kwangu, mara moja akifanya nihisi kama damu yangu ilikuwa imeganda kabisa, na meno yangu hayakukoma kutatarika. Sikuweza kujizuia kumwomba Mungu kimoyomoyo “Ee Mungu! Ninajua nia Yako nzuri ndiyo chanzo cha kile kinachonipata sasa, kwa hivyo ninaomba mwongozo Wako katika kufahamu mapenzi Yako, kwa sababu peke yangu, kwa kweli siwezi kuvumila maumivu makali ya pepo hawa. Ee Mungu! Tafadhali nipe imani na nguvu kubwa zaidi, ili niwe na dhamira na azimio la kushinda matatizo haya.” Baada ya kuomba, nilikumbuka maneno ya Mungu: “‘Kwa kuwa huzuni yetu nyepesi, ambayo ni ya muda mdogo pekee, inatufanyia utukufu mkubwa na wa daima ambao unazidi kuwa mkuu kabisa.’ Zamani, mlisikia msemo huu, lakini hakuna aliyeelewa maana kamili ya maneno yale. Leo, unajua vyema umuhimu wa maneno yale. Maneno haya ndiyo yatakayotimizwa na Mungu katika enzi za mwisho. Yatatimia kwa wale walioteswa na joka kuu jekundu katika sehemu linakoishi. Joka kuu jekundu humtesa Mungu na ni adui wa Mungu, kwa hiyo katika nchi hii, wanaomwamini Mungu wanateswa na kudhihakiwa. Ndiyo sababu maneno haya yatakuja kuwa kweli kwenu nyie kundi la watu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Kazi ya Mungu Ni Rahisi Kama Vile Mwanadamu Anavyodhania?). Kwa kutafakari maneno ya Mungu, nilifahamu mapenzi ya Mungu. Ukweli kwamba sasa nilikuwa nikiteseka kwa ajili ya imani yangu katika Mungu lilikuwa jambo tukufu na ilikuwa heshima yangu. Shetani alikuwa akinitesa kwa lengo la kunifanya nimsaliti na kumkataa Mungu kwa sababu sikuweza kuhimili kuteseka kwa mwili, kwa hivyo sikuweza kujisalimisha kwa Shetani. Wakati huo, nilikumbuka ghafla jinsi polisi mwovu alikuwa amenitisha na maisha kizuizini, na nilipata utambuzi wa ghafla—wafungwa walikuwa wakinitesa na kunidhulumu bila huruma kwa sababu walikuwa wameamuriwa kufanya hivyo na polisi wabaya! Ni wakati huo tu ndipo nilipofahamu wazi kuwa hawa “Polisi wa Watu” wanafiki, kwa kweli ni waovu sana na wa kudharauliwa. Walikuwa wakitumia wafungwa hawa kufanya kazi yao isiyo ya haki. Wao ni waovu sana hadi ndani ya nafsi zao, wao ni ibilisi tu wanaoua bila hata kumwaga damu wao wenyewe! Shetani alikuwa akijaribu kila mbinu anayoweza kunifanya nijisalimishe kwao, lakini hekima ya Mungu hutumika kulingana na hila za Shetani. Mungu alikuwa Akitumia hali hii kunipa imani ya kweli ndani Yake, ili Aniruhusu nione wazi uso usiopendeza wa Shetani na asili yake mbovu, na hivyo kusababisha chuki ya kweli kwake moyoni mwangu. Mara tu nilipofahamu mapenzi ya Mungu, moyo wangu ulichangamka na nilipata nguvu. Sikuweza kujiruhusu nidanganywe na Shetani. Bila kujali nilihisi maumivu au udhaifu wa mwili kiasi gani, ilinibidi nisimame kidete katika ushuhuda wangu kwa Mungu. Nilimshukuru Mungu kwa kunipa nguvu ya kushinda mateso na maumivu makali ya ibilisi hawa, na kumshinda Shetani tena.

Kizuizini, milo yetu ya kila siku ilikuwa na kabichi ya barafu iliyochemshwa majini, mboga zilizotengenezwa kwa achali, na mkate mdogo wa ngano uliopikwa kwa mvuke, ambao haukujaza tumbo kwa njia yoyote. Usiku, mfungwa mkuu na msafara wake walilala kwenye jukwaa la kulala huku wengine tulilala sakafuni. Nilipokuwa nikilala kwenye sakafu baridi, nikitazama wafungwa kandokando yangu, niliwaza kuhusu hali yangu ya kusikitisha na mara moja nilihisi mfadhaiko wa upweke ukiikamata moyo wangu. Niliwaza kuhusu nilipokuwa na ndungu zangu, na kila siku ilikuwa ya furaha na shangwe. Lakini sasa, nilitumia kila siku na wahalifu hawa, na pia ilibidi nivumilie uonevu wao na matusi yao, na nilihisi mwenye taabu ya kutesa sana na isiyoelezeka…. Nilikwenda mbele za Mungu na kumwomba, “Ee Mungu! Sijui nitaishi kwa namna hii kwa muda gani zaidi, na sijui jinsi ya kuvumilia siku zijazo. Sasa, mwili wangu ni dhaifu, na singependa kuikabili hali hii tena. Ee Mungu! Tafadhali nipe azimio la kuvumilia mateso, na Uniongoze katika kufahamu mapenzi Yako, ili niweze kukuridhisha katika hali hii.” Baada ya kuomba, maneno ya Mungu yalinijia waziwazi kwa ghafla akilini mwangu: “Mungu amevumilia sana kulala bila kupata usingizi kwa ajili ya kazi ya binadamu. Kutoka vina vya juu hadi vya chini, Amepanda kwenda katika kuzimu ambapo mwanadamu anaishi kupitisha siku Zake na mwanadamu, hajawahi kulalamikia uchakavu walionao wanadamu, hajawahi kumlaumu kwa ukaidi wake, lakini Anavumilia mateso makuu kadri Anavyofanya kazi Yake. … Kwa ajili ya binadamu wote, ili binadamu wote waweze kupata pumziko mapema zaidi, Amestahimili fedheha na kupitia udhalimu kuja duniani, na Aliingia mwenyewe ‘jahanamu’ na ‘kuzimu,’ katika tundu la duma, kumwokoa mwanadamu. Mwanadamu amestahili vipi kumpinga Mungu? Ana sababu gani tena ya kumlaumu Mungu? Anawezaje kuwa na ujasiri wa kumwangalia Mungu tena? Mungu wa mbinguni Amekuja katika nchi hii chafu zaidi ya uovu, na Hajawahi kutangaza manung’uniko au malalamiko Yake kuhusu mwanadamu, lakini badala yake Anakubali kimyakimya maangamizi[1] na ukandamizaji wa mwanadamu. Kamwe Hajawahi kujibu matakwa ya mwanadamu yasiyokuwa na msingi, hajawahi kutaka mambo mengi yanayomuelemea mwanadamu, na hajawahi kumwekea mwanadamu matakwa yasiyokuwa na msingi; Anafanya tu kazi ambazo mwanadamu alitakiwa kufanya bila malalamiko: kufundisha, kutia mwanga, kukaripia, usafishaji wa maneno, kukumbusha, kusihi, kufariji, kuhukumu na kufunua(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi na Kuingia (9)). Nilizingatia maneno ya Mungu, na nilifikiria mateso ambayo Mungu alivumilia kwa ajili ya wanadamu mara zote mbili alipokuja kuwa mwili ulimwenguni, na macho yangu yalidondokwa na machozi bila kupenda. Bwana Yesu alipigiliwa misumari msalabani, Akitumia maisha Yake mwenyewe kuwakomboa wanadamu ambao walikuwa wamepotoshwa na Shetani. Leo, Mwenyezi Mungu amepata mwili tena na amekuja China, taifa linalompinga Mungu zaidi, ambako Anahatarisha maisha Yake ili kuzungumza maneno Yake na kutuokoa. Ni nani angejua shida na mateso ambayo Amevumilia ili kufanya hivyo? Je, ni nani angeweza kutambua jambo hilo vyema? Wakati huohuo, mimi, mmoja wa wanadamu wapotovu, nilihisi mnyonge kwa namna isiyovumilika na nilitamani sana kutoroka hali yangu baada ya kushinda siku chache pamoja na wahalifu hao. Mungu, ambaye ni mtakatifu na mwenye haki, Ameishi nasi katika ulimwengu huu mwovu, uliopotea kwa muda wa miongo kadhaa. Je, Mungu hajateseka zaidi? Zaidi ya hayo, nilikuwa nikiteseka ili kujisafisha upotovu na kupata wokovu wa kweli. Lakini Mungu hana hatia na si wa ulimwengu huu, wala wa kuzimu hii hapa duniani, bali kwa sababu tu ya upendo Wake kwa wanadamu, Alikuja ndani ya pango la joka kubwa jekundu, tayari kutoa kafara maisha Yake ili kuwaokoa wanadamu. Upendo wa Mungu ni wa ajabu sana! Ikiwa ningekuwa na upendo wowote kwa Mungu, sikupaswa kuhisi kwamba hali yangu mwenyewe ilikuwa isiyovumilika, na sikupaswa kuhisi aliyedhulumiwa sana. Mbele za upendo wa Mungu, nilihisi tu majuto na aibu. Na nilipokuwa nikitafakari upendo wa Mungu, nilihisi ongezeko la uchangamfu moyoni mwangu. Mungu ni mkubwa kweli, na upendo Wake kwa wanadamu ni mkubwa sana na wa kweli! Nisingepitia hali kama hizi binafsi, nisingefahamu upendo wa Mungu na uzuri Wake. Ingawa kupitia hali hizi kuliuumiza mwili wangu, kulikuwa kwenye manufaa sana kwa maisha yangu. Nilipowaza kuhusu jambo hili, moyo wangu ulijawa na shukrani kwa Mungu, na nilipata azimio la kusimama kidete katika ushuhuda wangu kwa Mungu licha ya maumivu makali.

Kizuizini, mfungwa mkuu alikuwa alinieleza mara kwa mara kuhusu mbinu zote askari jela walizotumia kuwatesa “wahalifu” wanaomwamini Mungu: wao huchoma pini kwenye vidole vya waumini, na kusababisha maumivu yasiyoelezeka; wao hujaza chupa kwa maji moto sana na kumlazimisha muumini kuingiza vidole vyake, na baada ya ngozi kuchomwa, humfanya muumini atoe kidole chake kisha wanasugua poda ya pilipili kwenye malengelenge…. Niliposikiliza mateso haya ya kuogofya yakielezwa, nilikasirika sana, na chuki yangu kwa serikali ya CCP, utawala huu wa Shetani, ilizidi kuongezeka tu. Inajieleza kwa kila njia chanya wakati inafanya kila tendo mbaya. Inatangaza “uhuru wa imani ya kidini,” na “watu wote wanafaidika na haki halali na manufaa ya raia,” na “wafungwa huchukuliwa kama familia,” huku wanawadhulumu na kuwatesa watu kisirisiri, bila kuonyesha kujali maisha ya wanadamu, na kutowatendea watu kama wanadamu. Kwa mtu ambaye anamwamini Mungu, kuingia katika ulimwengu wao ni sawa na kuingia kuzimu, mahali ambapo watateswa na kudhalilishwa, na mahali ambapo kamwe hawataweza kujua ikiwa wataibuka na maisha yao. Mawazo kuhusu jambo hilo yaliniogofya, kwa sababu niliogopa kuwa mateso hayo yangetumiwa kwangu. Kila nilipowasikia maafisa wa urekebishaji wakilifungua dirisha dogo kwenye mlango wa chuma, nilijawa na woga mwingi, kwa sababu niliogopa kuvutwa nje na kuteswa. Nilishinda kila siku nikiwa nimejawa na woga, na nilihisi nimenaswa kwa namna isiyochanganulika. Katika taabu yangu, niliweza tu kumwomba Mungu kimoyomoyo: “Ee Mungu! Moyo wangu ni dhaifu sasa, na ninahisi mwoga, lakini ningependa kukuridhisha, kwa hivyo nipe imani na nguvu. Ningependa kukutegemea kushinda majaribu ya Shetani!” Baada ya kuomba, nilipata mwongozo katika neno la Mungu: “Msiogope, Mwenyezi Mungu wa majeshi hakika atakuwa pamoja nawe; Yeye anawasaidia na Yeye ni ngao yenu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 26). “Watu wanapokuwa tayari kuyatoa maisha yao, kila kitu huwa hafifu, na hakuna anayeweza kuwashinda. Ni nini kingekuwa muhimu zaidi kuliko uzima? Hivyo, Shetani anakuwa hawezi kufanya chochote zaidi ndani ya watu, hakuna anachoweza kufanya na mwanadamu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ufafanuzi wa Mafumbo ya “Maneno ya Mungu kwa Ulimwengu Mzima”, Sura ya 36). Neno la Mungu lilinipa faraja ya ajabu na kunitia moyo. “Ndiyo,” niliwaza. “Mungu ninayemwamini ni Bwana wa uumbaji Aliyeumba mbingu na ardhi na vitu vyote vilivyomo, ambaye ni mkuu wa vitu vyote, na Anayedhibiti vitu vyote na watu wote. Zaidi ya hayo, je, si maisha na kifo cha kila mtu kimeshikiliwa mikononi mwa Mungu? Bila idhini ya Mungu, ibilisi Shetani hangethubutu kunifanyia chochote. Je, si ni ukweli kwamba nilishinda siku nzima nikiwa katika hali ya woga na hofu kwa ajili tu ya woga wa kifo na woga wa mateso ya mwili? Shetani alikuwa akitumia udhaifu huu kunishambulia, ili anifanye nishindwe na nimsaliti Mungu. Hii ni hila ya Shetani ya kuwaangamiza watu. Lakini ikiwa niko tayari kusalimisha maisha yangu, je, kunaweza kuwa na kitu chochote ambacho singeweza kukivumilia?” Niliwaza kuhusu matukio ya Ayubu: Shetani alipoweka dau na Mungu, Ayubu alipata mateso ya mwili, lakini bila idhini ya Mungu, bila kujali jinsi Shetani alivyomtesa Ayubu, hakuweza kumuua. Sasa, nilitaka kufuata mfano wa Ayubu na kuwa na imani ya kweli katika Mungu, kwa sababu hata kama mwili wangu ungeteswa na pepo hadi kufa, roho yangu ilikuwa mikononi mwa Mungu. Bila kujali jinsi pepo hawa wangenitesa au kunitia maumivu makali, kamwe singekubali kushindwa na udhalimu wake wa kikatili. Niliapa kwamba kamwe sitakuwa Yuda! Nashukuru kwa mwongozo wa wakati wa kufaa niliopata katika neno la Mungu kwa ajili ya kuniongoza kutoka utumwani na kikwazo cha kifo na kutoniruhusu kukamatwa na mpango wa Shetani. Kwa ajili ya ulinzi wa Mungu, sikuweza kupitia aina hizo za mateso, na katika jambo hili, niliona tena upendo na rehema ya Mungu kwangu.

Siku chache baadaye, afisa huyo mwovu wa polisi alikuja tena kunihoji, akitarajia kupata habari kutoka kwangu kuhusu viongozi wa kanisa, lakini nilipokosa kujibu, alianza kuwa mkatili sana. Alinikodolea macho huku akishika kidevu changu kwa nguvu na akigeuza kichwa changu kushoto na kulia, kisha akasema kupitia meno yaliyokerezwa, “Je, kuna kitu chochote chenye utu ndani yako hata kidogo? Endelea basi, mwamini Mungu! Nitaweka picha yako mtandaoni na kutunga hadithi kadhaa kukuhusu, na nitamfanya kila mtu anayemwamini Mwenyezi Mungu afikirie kuwa ulimsaliti Mungu na kuwasaliti ndugu zako. Hakuna atakayezungumza nawe tena. Na kisha, nitakupeleka mahali ambapo hakuna mtu anapajua, nichimbe shimo, na nikuzike ukiwa hai, na hakuna mtu atakayegundua kamwe.” Katika ghadhabu yake, ibilisi huyu alielezea njama zake za siri zenye aibu, na hii pia ilikuwa mbinu yake ya kawaida ya kuwadanganya watu—kusingizia, kukashifu kwa maandishi, kutoa mashtaka ya uwongo, na mauaji. Anaonyesha kuwa hayajali kabisa maisha ya watu, na ni vigumu kujua vitendo vya kinyama, na vya ukatili ambavyo amevifanya kwa siri! Wakati huu, nikisikia vitisho vyake vya kusema kwa sauti kubwa, nilikuwa mtulivu, na sikuhisi hofu hata kidogo, kwa sababu Mungu alikuwa tegemeo langu thabiti. Mungu alikuwa nami, kwa hivyo sikuhitaji kuogopa chochote. Kadiri Shetani anavyokuwa katili zaidi, ndivyo anavyofichua ubaya na udhaifu wake; kadiri anavyowatesa waumini, ndivyo anavyofichua asili yake ya kupinga maendeleo, mbovu ya kufanya uadui na Mungu, kufanya mambo mabaya, na kwenda kinyume na Mbingu na ulimwengu; kadiri anavyowaumiza waumini katika Mungu, ndivyo anavyohimiza azimio langu la kumwamini Mungu na kumfuata Mungu hadi mwisho: Ninataka kujitolea maisha yangu kwa Mungu na kumuacha Shetani sasa na kwa mara ya mwisho! Kama neno la Mungu lisemavyo: “Mwanadamu ana muda mrefu tangu akusanye nguvu zake zote, amejitolea nguvu zake zote, amelipa kila gharama, kwa hili, kuchana uso uliojificha wa pepo hili na kuwafanya watu, ambao wamepofushwa na kuvumilia kila aina ya mateso na taabu, kuinuka kutoka katika maumivu na kurudi kwa ibilisi huyu wa zamani(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi na Kuingia (8)). Kufikia wakati huu, nilijawa na hasira, na niliapa kiapo kimoyomoyo: bila kujali ningelazimika kukaa hapo muda gani, na bila kujali pepo hao wangenitesa jinsi gani, singewahi kumsaliti Mungu. Polisi aliona kuwa sitajibu, na mwishowe alinirudisha kwenye seli. Na kwa hivyo, kwa ajili ya mwongozo wa neno la Mungu, nilishinda majaribio yaliyotokea mara nyingi ya pepo ya kunilazimisha kukiri kwa mateso yao. Sikuwahi kufichua habari yoyote kuhusu kanisa, na baada ya kukaa kwa zaidi ya siku 50 kizuizini, polisi walilazimika kuniachilia huru bila mashtaka.

Baada ya kupitia tukio la kukamatwa, nilifahamu dhahiri asili ya kishetani ya serikali ya CCP. Inapigana na Mbingu na kujifanya adui wa Mungu. Inakataa kumwabudu Mungu, na pia hutumia njia zote zinazowezekana kuwadanganya na kuwadhibiti watu, kuwazuia watu kumwamini au kumwabudu Mungu. Hujaribu kuwafanya watu waepukane na Mungu na kumpinga Mungu, ili mwishowe waangamizwe kuzimuni pamoja nayo. Ni ya kudharauliwa, katili na yenye uovu! Lakini muhimu zaidi, tukio hili lilinipa ufahamu wa kweli kuhusu ustaajabishaji na hekima ya Mungu na mamlaka na nguvu ya neno Lake. Katika nchi kama hii, ambapo Mungu anaonekana kama adui mgumu kuvumiliwa, waumini katika Mungu ni kero mbele za serikali hii inayomkana Mungu. Hata hivyo, haiwezi hata kidogo kuwawekea mipaka wale wanaomwamini Mungu kwa kweli. Bila kujali jinsi inavyokandamiza, inavyofunga, na kuiumiza miili yetu, haiwezi kuondoa shauku yetu ya kwenda kwenye nuru na kufuatilia ukweli, na haiwezi kudhoofisha azimio letu la kumwamini na kumfuata Mungu. Nilikamatwa na kupitia mwenyewe ukatili mkali wa pepo hawa. Shetani alitamani bila mafanikio kunifanya nishindwe na utawala wake wa kidikteta kwa kunikamata na kunitesa, lakini neno la Mungu liliniongoza siku zote, na lilinipa hekima, imani, na nguvu ambayo iliniwezesha kusimama imara wakati wa mateso ya kikatili ya Shetani. Kupitia tukio langu halisi, niliona matendo ya Mungu ya kushangaza, imani yangu katika Mungu iliongezeka kiasi kikubwa, na nilipata ufahamu zaidi wa utendaji wa neno la Mungu. Nilipata kuona kwamba neno la Mungu ni ukweli, na kwamba ni nguvu na chanzo cha maisha ya watu. Nikiwa na mwongozo wa neno la Mungu, sihitaji kuogopa kitu chochote, na bila kujali nitakabili shida ngapi au vizuizi vingapi ninakoelekea, ningependa kumfuata Mungu hadi mwisho kabisa!

Tanbihi:

1. “Maangamizi” inatumiwa kuweka wazi kutotii kwa wanadamu.

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Leave a Reply

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp