J. Juu ya Kufuatilia Kumpenda Mungu

436. Kiini cha Mungu sio tu kwa mwanadamu kuamini; vilevile ni, kwa mwanadamu kupenda. Lakini wengi wa wale wanaomwamini Mungu hawana uwezo wa kugundua hii “siri.” Watu hawathubutu kumpenda Mungu, wala hawajaribu kumpenda Yeye. Hawajawahi kugundua kuwa kuna mengi sana ya kupendeza kuhusu Mungu, hawajawahi kugundua kwamba Mungu ni Mungu anayempenda mwanadamu, na kwamba ni Mungu ambaye mwanadamu anapaswa kumpenda. Upendo wa Mungu umeonyeshwa katika kazi Yake: ni baada tu ya kupitia kazi Yake ndipo wanaweza wakagundua upendo Wake, ni katika matukio wanayopitia ya hakika tu ambapo wanaweza kufahamu upendo wa Mungu, na bila kuupitia katika maisha halisi, hakuna anayeweza kugundua kupendeza kwa Mungu. Kuna mengi ya kupendeza kumhusu Mungu, lakini bila ya kujihusisha na Yeye kwa hakika watu wengi hawana uwezo wa kuyagundua. Hivi ni kusema, kama Mungu asingefanyika mwili, watu wasingekuwa na uwezo wa kujihusisha na Yeye, na kama wasingekuwa na uwezo wa kujihusisha na Yeye, pia wasingeweza kupitia Kazi Yake—na kwa hivyo upendo wao kwa Mungu ungetiwa doa la uongo mwingi na mawazo. Upendo wa Mungu ulio mbinguni si halisi kama upendo wa Mungu ulio ulimwenguni, kwa kuwa ufahamu wa watu kuhusu Mungu aliye mbinguni umejengwa katika mawazo yao, bali si kwa yale ambayo wameyaona kwa macho yao, na yale ambayo wameyapitia wao wenyewe. Mungu anapokuja ulimwenguni, watu wanaweza kuyaona matendo Yake halisi na upendo wake, na wanaweza kuona kila kitu katika matendo na tabia Zake za kawaida, ambayo ni mara elfu halisi kuliko ufahamu wa Mungu aliye mbinguni. Bila kujali ni vipi ambavyo watu wanampenda Mungu aliye mbinguni, hakuna kitu halisi kuhusu huu upendo, na umejaa mawazo ya kibinadamu. Haijalishi udogo wa upendo wao kwa Mungu aliye duniani, huu upendo ni halisi; hata kama ni kidogo, ungali ni halisi. Mungu huwafanya watu kumjua kupitia kazi halisi, na kupitia ufahamu huu Anapata upendo wao. Ni kama Petro: kama hangeishi na Yesu, haingewezekana yeye kumwabudu Yesu. Aidha, huu uaminifu ulijengwa kwenye uhusiano wake na Yesu. Ili kumfanya mwanadamu ampende, Mungu amekuja miongoni mwa wanadamu na kuishi na wanadamu, na yote Anayomfanya mwanadamu kuona na kupitia ni uhalisi wa Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wanaompenda Mungu Wataishi Milele Katika Mwangaza Wake

437. “Upendo,” kama unavyoitwa, unaashiria hisia safi isiyo na dosari, ambapo unatumia moyo wako kupenda, kuhisi, na kuwa na mawazo. Katika upendo hakuna masharti, hakuna vizuizi na hakuna kutenga. Katika upendo hakuna shaka, hakuna uongo na hakuna ujanja. Katika upendo hakuna mabadilishano na hakuna kitu kisicho safi. Ukipenda, basi hutadanganya, hutalalamika, hutaasi kulazimisha au kutafuta kupata kitu au kupata kiwango fulani. Ukipenda, basi utajinyima bila kusononeka na kuvumilia hali ngumu, na utaambatana na Mimi. Utaacha kila kitu chako kwa sababu Yangu, utaacha familia yako, siku zako za baadaye, ujana wako, na ndoa yako. La sivyo, basi upendo wako haungekuwa upendo hata kidogo, bali ungekuwa uongo na usaliti! Upendo wako ni upendo wa aina gani? Je, ni upendo wa kweli? Je, ni wa uongo? Umejinyima kiasi gani? Umejitolea kiasi gani? Je, Nimepata upendo kiasi gani kutoka kwako? Je, unajua? Mioyo yenu imejaa maovu, usaliti na uongo na hivyo kuna kiwango kipi cha uchafu katika upendo wenu? Mnafikiri kuwa mmeacha vya kutosha kwa ajili Yangu; mnafikiri kuwa upendo wenu Kwangu tayari umetosha. Ila ni kwa nini basi maneno yenu na matendo yenu huambatana na uasi na uongo daima? Mnanifuata, ilhali hamkubali neno Langu. Je, hili linachukuliwa kama upendo? Mnanifuata, kisha mnanitenga na kunitupa kando. Je, huu unachukuliwa kama upendo? Mnanifuata, na bado mko na shaka na Mimi. Je, huu unachukuliwa kama upendo? Mnanifuata, ilhali hamkubali kuwepo Kwangu. Je, huu ni upendo? Mnanifuata, ilhali hamnitendei vile Ninavyopaswa kutendewa na mnafanya mambo yawe magumu Kwangu katika kila hatua. Je, hili linachukuliwa kama upendo? Mnanifuata, na bado mnanichukulia kama mjinga na kunidanganya Mimi katika kila jambo. Je, hili linachukuliwa kama upendo? Mnanihudumia, na bado hamnichi. Je, hili linachukuliwa kama upendo? Mnanipinga katika kila hali na kila jambo. Je, yote haya yanachukuliwa kama upendo? Mmejinyima mengi, huu ni ukweli, lakini bado hamjawahi kutenda Ninayowaagiza mfanye. Je, huu unaweza kuchukuliwa kama upendo? Uchunguzi wa makini unaashiria kuwa hamna upendo Kwangu ndani yenu. Baada ya miaka mingi sana ya kazi na maneno yote mengi Niliyosambaza, ni kiasi kipi mlichopokea kwa hakika? Je, hili halistahili kuangaliwa tena kwa makini?

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wengi Wanaitwa, Lakini Wachache Wanachaguliwa

438. Hakuna funzo lililo kubwa kuliko lile la kumpenda Mungu, na inaweza kusemwa kuwa funzo ambalo watu hujifunza katika maisha yao yote ya imani ni jinsi ya kumpenda Mungu. Hii ni kusema, kama unamwamini Mungu ni lazima umpende Mungu. Ikiwa unamwamini tu Mungu lakini humpendi, hujapata ufahamu wa Mungu, na hujawahi kumpenda Mungu kwa upendo wa kweli utokao moyoni mwako, basi imani yako kwa Mungu ni bure; kama katika imani yako kwa Mungu humpendi Mungu, basi unaishi bure, na maisha yako yote ndiyo ya duni zaidi kwa maisha yote. Ikiwa katika maisha yako yote hujawahi kumpenda au kumtosheleza Mungu, basi kuna haja gani ya kuishi? Kuna haja gani ya imani yako kwa Mungu? Huku si kuharibu nguvu? Hii ni kusema, kama watu wanataka kuamini na kumpenda Mungu, ni sharti wagharamike. Badala ya kujaribu kuenenda kwa namna fulani kwa nje tu, wanapaswa watafute utambuzi wa kweli kutoka ndani ya mioyo yao. Ikiwa unapenda sana kuimba na kucheza lakini huwezi kuonyesha ukweli katika vitendo, unaweza kusemekana kwamba unampenda Mungu? Kumpenda Mungu kunahitaji utafutaji wa mapenzi ya Mungu katika mambo yote, na kwamba ujisaili wewe mwenyewe kwa kina jambo lolote likikutokea, kujaribu kujua mapenzi ya Mungu na kujaribu kuona mapenzi ya Mungu ni yapi katika suala hili, Anataka ufanikishe nini, na ni jinsi gani utayajali mapenzi Yake? Kwa mfano: jambo fulani linafanyika linalokutaka uvumilie hali ngumu, wakati huo unapaswa ufahamu ni nini mapenzi ya Mungu, na ni jinsi gani unapaswa kuyajali mapenzi ya Mungu. Usijiridhishe mwenyewe: Jiweke kando kwanza. Hakuna kitu kilicho duni kuliko mwili. Ni lazima udhamirie kumridhisha Mungu, na ni lazima utekeleze wajibu wako. Katika mawazo kama hayo, Mungu atakupa nuru ya kipekee katika jambo hili, na moyo wako pia utapata faraja.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kumpenda Mungu tu Ndiko Kumwamini Mungu Kweli

439. Leo, nyote mnajua ya kwamba imani ya mwanadamu katika Mungu si kwa ajili ya wokovu wa roho na hali njema ya mwili tu, wala si kuimarisha maisha yake kwa njia ya upendo kwa Mungu, na kadhalika. Kama ilivyo sasa, kama unampenda Mungu kwa ajili ya ustawi wa mwili au furaha ya muda, basi hata kama, mwishowe, upendo wako kwa Mungu unafikia kilele chake na usiombe chochote, upendo huu unaoutafuta bado ni upendo mchafu na haumpendezi Mungu. Wale wanaotumia upendo kwa Mungu kusitawisha maisha yao yasiyopendeza na kujaza utupu katika mioyo yao ni wale ambao wanataka kuishi katika raha, si wale ambao kweli wanatafuta kumpenda Mungu. Upendo wa aina hii ni kinyume na matakwa ya mtu, harakati ya ridhaa ya hisia, na Mungu hahitaji upendo wa aina hii. Upendo wako, basi, ni upendo wa aina gani? Ni kwa ajili gani unampenda Mungu? Je, ni kiasi gani cha upendo wa kweli, ulicho nacho kwa Mungu sasa? Upendo wa watu wengi kati yenu ni kama uliotajwa hapo awali. Upendo wa aina hii unaweza tu kudumisha hali kama ilivyo; hauwezi kufikia uthabiti wa milele, wala kukita mizizi ndani ya mwanadamu. Aina hii ya upendo ni ule wa ua ambalo halizai matunda baada ya kuchanuka na hatimaye kunyauka. Kwa maneno mengine, baada ya wewe kumpenda Mungu mara moja kwa jinsi hii na hakuna mtu wa kukuongoza kwa njia ya mbele, basi utaanguka. Kama unaweza tu kumpenda Mungu katika wakati wa kumpenda Mungu na kutofanya mabadiliko katika tabia ya maisha yako baadaye, basi utaendelea kufunikwa na ushawishi wa giza, bila uwezo wa kutoroka, na bila uwezo wa kujinasua kwa kufungwa na kupumbazwa na Shetani. Hakuna mtu kama huyu anayeweza kukubaliwa na Mungu; mwishowe, roho zao, nafsi na mwili bado ni mali ya Shetani. Hili ni bila ya shaka. Wale wote ambao hawawezi kukubaliwa kikamilifu na Mungu watarudi mahali pao pa awali, yaani, kwa Shetani, na watakwenda chini kwa ziwa liwakalo moto wa jahanamu kukubali hatua ya pili ya adhabu kutoka kwa Mungu. Wale wanaokubaliwa na Mungu ni wale ambao wanamkataa shetani na kutoroka kutoka kwa miliki ya Shetani. Watu kama wale watahesabiwa rasmi miongoni mwa watu wa ufalme. Hivi ndivyo watu wa ufalme huja kuwa. Je, uko tayari kuwa mtu wa aina hii? Je, uko tayari kukubaliwa na Mungu? Je, uko tayari kutoroka kutoka kwa miliki ya Shetani na kurudi kwa Mungu? Je, sasa wewe ni mali ya Shetani au umehesabiwa miongoni mwa watu wa ufalme?

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Maoni Wanayopaswa Kushikilia Waumini

440. Mwanadamu amekuwa akiishi katika funiko la ushawishi wa giza, huku akiwa amezuiliwa bila ya kuachiliwa na ushawishi wa Shetani. Nayo tabia ya mwanadamu, baada ya kutengenezwa na Shetani, inaendelea kuongezeka kuwa potovu. Mtu anaweza kusema kwamba binadamu huishi daima na tabia yake potovu ya kishetani, asiweze kumpenda Mungu kikweli. Kwa sababu ya hili, kama mwanadamu anataka kumpenda Mungu, lazima anyang’anywe kujidai kwake, kujigamba, kiburi, majivuno, na sifa nyingine kama hizo zinazomilikiwa na tabia ya Shetani. La sivyo, upendo wake si safi, ni upendo wa kishetani, na ule ambao hauwezi kabisa kupokea idhini ya Mungu. Bila kukamilishwa, kushughulikiwa, kuvunjwa, kupogolewa, kufundishwa nidhamu, kuadibiwa, au kusafishwa na Roho Mtakatifu moja kwa moja, hakuna yeyote anayeweza kumpenda Mungu kwa kweli.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mwanadamu Mpotovu Hawezi Kumwakilisha Mungu

441. Watu wanapowasiliana na Mungu na mioyo yao, mioyo yao inapoweza kumgeukia Yeye kikamilifu, hii ni hatua ya kwanza ya upendo wa wanadamu kwa Mungu. Ikiwa unataka kumpenda Mungu, lazima kwanza uweze kugeuza moyo wako Kwake. Kugeuza moyo wako kwa Mungu ni nini? Ni wakati ambapo kila kitu unachofuatilia ndani ya moyo wako ni kwa ajili ya kumpenda na kumpata Mungu, na hii inaonyesha kwamba umeugeuza moyo wako kikamilifu kwa Mungu. Mbali na Mungu na maneno Yake, hakuna takriban kitu chochote kingine ndani ya moyo wako (familia, mali, mume, mke, watoto au vitu vingine). Hata kama vipo, haviwezi kuumiliki moyo wako, na hufikirii juu ya matazamio yako ya baadaye lakini unafuatilia tu kumpenda Mungu. Wakati huo utakuwa umegeuza moyo wako kwa Mungu kabisa. Ikiwa bado unajitengenezea mipango ndani ya moyo wako na kila mara unafuatilia manufaa yako binafsi, na kila mara unafikiri: “Ni lini ninaweza kumwomba Mungu ombi ndogo? Familia yangu itakuwa tajiri lini? Ninawezaje kupata mavazi kadhaa mazuri? …” Ikiwa unaishi katika hali hiyo inaonyesha kwamba moyo wako haujamgeukia Mungu kwa ukamilifu. Ikiwa una maneno ya Mungu tu moyoni mwako na unaweza kumwomba Mungu na kuwa karibu naye nyakati zote, kana kwamba Yeye yu karibu sana nawe, kana kwamba Mungu yu ndani yako nawe u ndani Yake, ikiwa uko katika hali ya aina hiyo, inamaanisha kwamba moyo wako umekuwa katika uwepo wa Mungu. Ukimwomba Mungu na kula na kunywa maneno Yake kila siku, unafikiria kila mara kuhusu kazi ya kanisa, ukifikiria juu ya mapenzi ya Mungu, ukitumia moyo wako kumpenda Yeye kwa uhalisi na kuridhisha moyo Wake, basi moyo wako utakuwa wa Mungu. Ikiwa moyo wako unamilikiwa na vitu vingine vingi, basi bado unamilikiwa na Shetani na haujamrudia Mungu kweli. Wakati moyo wa mtu umemrudia Mungu kweli, atakuwa na upendo halisi, wa hiari Kwake na ataweza kufikiria kazi ya Mungu. Ingawa bado atakuwa na hali za kipumbavu na zisizo na akili, ataweza kuwa na fikira kwa ajili ya maslahi ya nyumba ya Mungu, ya kazi Yake, na ya mabadiliko katika tabia yake. Moyo wake utakuwa sahihi kabisa. Watu wengine kila mara hupeperusha bendera ya kanisa haijalishi wanachofanya; kweli ni kwamba hii ni kwa manufaa yao. Mtu wa aina hiyo hana aina nzuri ya nia. Yeye ni mhalifu na mdanganyifu na mambo mengi sana anayofanya ni ya kutafuta manufaa yake mwenyewe. Mtu wa aina hiyo hafuatilii kumpenda Mungu; moyo wake bado ni wa Shetani na hauwezi kumgeukia Mungu. Mungu hana njia ya kumpata mtu wa aina hiyo.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Upendo Halisi kwa Mungu ni wa Hiari

442. Kila hatua ya kazi anayoifanya Mungu kwa watu kwa nje inaonekana kama maingiliano kati ya watu, kana kwamba yalizaliwa kwa mipango ya wanadamu au kutokana na usumbufu wa wanadamu. Lakini nyuma ya kila hatua ya kazi, na kila kitu kinachotokea, ni dau linalofanywa na Shetani mbele ya Mungu, na linawahitaji watu kusimama imara katika ushuhuda wao kwa Mungu. Kwa mfano, tazama wakati Ayubu alijaribiwa: kisirisiri, Shetani alikuwa akiweka dau na Mungu, na kilichomtendekea Ayubu kilikuwa ni matendo ya wanadamu na usumbufu wa wanadamu. Nyuma ya kila hatua ya kazi ambayo Mungu anafanya juu yenu kuna dau la Shetani na Mungu—nyuma yake kuna vita. Kwa mfano, ikiwa unawabagua ndugu na dada zako, utakuwa na maneno ambayo unataka kusema—maneno unayohisi huenda yasimpendeze Mungu—lakini usipoyasema, utahisi kutoridhika ndani, na kwa wakati huu vita vitazuka ndani yako: “Niseme au nisiseme?” Hivi ndivyo vita. Kwa hivyo, katika kila jambo unalopitia kuna vita, na wakati kuna vita ndani yako, kutokana na ushirikiano wako na kuteseka kwako, Mungu anafanya kazi ndani yako. Hatimaye unaweza kuliweka kando jambo lenyewe na hasira yako inazimika. Hayo ndiyo matokeo ya ushirikiano wako na Mungu. Kila kitu wafanyacho watu kinawahitaji kulipa gharama fulani katika juhudi zao. Bila taabu ya kweli, hawawezi kumridhisha Mungu, hata hawakaribii kumridhisha Mungu, na wanarusha tu maneno matupu! Je, haya maneno matupu yaweza kumridhisha Mungu? Wakati Mungu na Shetani wanapigana katika milki ya kiroho, utamridhishaje Mungu, na utasimamaje imara katika ushuhuda wako Kwake? Unapaswa kujua kuwa kila kitu unachokipitia ni majaribu makubwa na ndipo Mungu hukuhitaji kuwa na ushuhuda. Kwa nje yataonekana kama mambo madogo; lakini haya mambo yakitendeka huonyesha kama unampenda Mungu au la. Ikiwa unampenda, utaweza kusimama imara katika ushuhuda wako Kwake, na ikiwa hujaweka upendo Wake katika vitendo, hili linaonyesha kuwa wewe si Mtu ambaye anapenda kuuweka ukweli katika vitendo, kwamba huna ukweli, huna uzima, kuwa wewe ni makapi! Mambo huwatokea watu wakati Mungu anawataka wasimame imara katika ushuhuda wao Kwake. Hakuna kubwa lililokutendekea kwa sasa, na huna ushuhuda mkubwa, lakini kila chembe ya maisha yako ya kila siku inahusiana na ushuhuda kwa Mungu. Ikiwa utawavutia ndugu na dada zako, wanafamilia, na kila aliye karibu nawe; ikiwa siku moja wasioamini watakuja na wavutiwe na yote unenayo na utendayo, na kuona kuwa yote afanyayo Mungu ni ya ajabu, basi utakuwa umekuwa na ushuhuda. Ijapokuwa huna ufahamu na wewe si mwerevu sasa, kupitia kwa kufanywa mkamilifu na Mungu, unaweza kumridhisha na kuzingatia mapenzi Yake, ukiwaoshyesha wengine kazi kubwa Aliyofanya miongoni mwa watu wenye ubora duni wa tabia. Watu wanapokuja kumjua Mungu na kuwa washindi mbele ya Shetani, waaminifu kwa Mungu kwa kiwango kikubwa, basi hakuna aliye na uthabiti kuliko hili kundi la watu, na huu ndio ushuhuda mkubwa zaidi. Ijapokuwa huwezi kufanya kazi kubwa, unaweza kumridhisha Mungu. Wengine hawawezi kuweka kando dhana zao, lakini unaweza; wengine hawawezi kutoa ushuhuda kwa Mungu wakati wa uzoefu wao halisi, lakini unaweza kutumia kimo na matendo yako halisi kulipa upendo wa Mungu na kutoa ushuhuda thabiti Kwake. Hili ndilo huhesabika kama mapenzi ya kweli kwa Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kumpenda Mungu tu Ndiko Kumwamini Mungu Kweli

443. Kadiri unavyoweka ukweli katika vitendo, ndivyo unavyokuwa na ukweli; kadiri unavyoweka ukweli katika vitendo, ndivyo unavyokuwa na upendo wa Mungu; na kadiri unavyoweka ukweli katika vitendo, ndivyo unavyobarikiwa na Mungu. Kama utatenda kwa njia hii kila mara, upendo wa Mungu kwako utakuwezesha kuona polepole, jinsi tu ambavyo Petro alivyokuja kumjua Mungu: Petro alisema kuwa si kuwa Mungu ana busara ya kuumba mbingu na dunia na vitu vyote vilivyomo pekee, lakini, aidha, kuwa Ana busara ya kufanya kazi halisi ndani ya watu. Petro alisema kuwa Mungu hastahili tu upendo wa watu kwa sababu ya uumbaji Wake wa mbingu na dunia na vitu vyote vilivyomo, lakini, vilevile, kwa sababu ya uwezo Wake wa kuumba mwanadamu, kumwokoa, kumfanya mwanadamu awe mkamilifu, na kutoa upendo wake kwa mwanadamu. Petro alimwambia Yesu: “Je, Hustahili upendo wa watu zaidi ya kuumba mbingu na dunia na vitu vyote vilivyomo? Kuna mengi ndani Yako ambayo yanapendeka, unatenda na kuendelea katika maisha halisi, Roho Wako ananigusa ndani, unanifundisha nidhamu, unanikemea—haya mambo yanastahili zaidi upendo wa watu.” Kama unataka kuona na kupitia upendo wa Mungu, basi lazima uchunguze na utafute katika maisha halisi, na lazima uwe tayari kuweka kando mwili wako mwenyewe. Lazima ufanye azimio hili: kuwa mtu mwenye azimio, ambaye anaweza kumridhisha Mungu katika mambo yote, bila ya kuzembea, au kutamani kuufurahisha mwili, kutoishi kwa ajili ya mwili lakini kuishi kwa ajili ya Mungu. Kunaweza kuwa na nyakati ambazo hukumridhisha Mungu. Hii ni kwa sababu huelewi mapenzi ya Mungu; wakati ujao, hata kama itahitaji juhudi zaidi, lazima umridhishe Mungu, na lazima usiuridhishe mwili. Unapopitia kwa njia hii, utakuja kumjua Mungu. Utaona kuwa Mungu angeweza kuumba mbingu na dunia na vitu vyote vilivyomo, na Amekuwa mwili ili watu wamwone kwa uhakika, na kujihusisha na Yeye, kuwa ana uwezo wa kuishi miongoni mwa wanadamu, kuwa Roho Wake aweza kufanya watu kuwa wakamilifu katika maisha halisi, kuwawezesha kuona upendo na uzoefu wa nidhamu Yake, kurudi Kwake, na baraka Zake. Kama huwa unapitia kwa njia hii, katika maisha halisi hutatenganishwa na Mungu, na kama siku moja uhusiano wako na Mungu utaacha kuwa wa kawaida, utaweza kupatwa na aibu, na kuweza kuhisi huzuni. Unapokuwa na uhusiano wa kawaida na Mungu, hutatamani kamwe kutaka kumuacha, na siku moja Mungu akisema Atakuacha, utaogopa, na kusema kuwa ni heri ufe kuliko kuachwa na Mungu. Punde tu unapokuwa na hisia hizi, utahisi kuwa hakuna uwezo wa kumwacha Mungu, na kwa njia hii utakuwa na msingi, na utafurahia upendo wa Mungu wa kweli.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wanaompenda Mungu Wataishi Milele Katika Mwangaza Wake

444. Unampenda Mungu kiasi gani hasa leo? Na unajua kiasi gani hasa kuhusu yote ambayo Mungu amefanya ndani yako? Haya ni mambo unayopaswa kujifunza. Mungu anapowasili duniani, yote ambayo Amefanya ndani ya mwanadamu na kumkubalia mwanadamu kuona ni ili mwanadamu atampenda na kumjua Yeye kweli. Kwamba mwanadamu anaweza kuteseka kwa ajili ya Mungu na ameweza kufikia umbali huu ni, kuhusiana na jambo moja, kwa sababu ya upendo wa Mungu, na kuhusiana na jambo lingine, ni kwa sababu ya wokovu wa Mungu; zaidi ya hayo, ni kwa sababu ya kazi ya hukumu na kuadibu ambayo Mungu ametekeleza ndani ya mwanadamu. Kama hamna hukumu, kuadibu, na majaribio ya Mungu, na kama Mungu hajawafanya mteseke, basi, kusema ukweli, ninyi hammpendi Mungu kweli. Kadri kazi ya Mungu ilivyo kuu zaidi ndani ya mwanadamu, na kadri mateso ya mwanadamu yalivyo makuu zaidi, ndivyo inavyoweza kuonyesha zaidi hasa vile kazi ya Mungu ilivyo ya maana, na ndivyo moyo wa mwanadamu unavyoweza kumpenda Mungu kweli zaidi. Unajifunzaje jinsi ya kumpenda Mungu? Bila mateso makali na usafishaji, bila majaribio ya kuumiza—na kama, zaidi ya hayo, yote ambayo Mungu alimpa mwanadamu ingekuwa neema, upendo, na rehema—je, ungeweza kufikia upendo wa kweli kwa Mungu? Kwa upande mmoja, wakati wa majaribio ya Mungu mwanadamu huja kujua kasoro zake, na huona kwamba yeye ni mdogo, wa kudharauliwa, na duni, kwamba hana chochote, na si kitu; kwa upande mwingine, wakati wa majaribio Yake Mungu humuumbia mwanadamu mazingira tofauti yanayomfanya mwanadamu aweze zaidi kupitia kupendeza kwa Mungu. Ingawa maumivu ni makubwa, na wakati mwingine yasiyoshindika—na hata hufikia kiwango cha huzuni ya kuseta—baada ya kuyapitia, mwanadamu huona vile kazi ya Mungu ndani yake ni ya kupendeza, na ni juu ya msingi huu tu ndiyo ndani ya mwanadamu huzaliwa upendo wa kweli kwa Mungu. Leo mwanadamu huona kwamba na neema, upendo na rehema ya Mungu pekee, hana uwezo wa kujijua mwenyewe kweli, sembuse kuweza kujua kiini cha mwanadamu. Ni kupitia tu usafishaji na hukumu ya Mungu, ni wakati tu wa usafishaji kama huo ndiyo mwanadamu anaweza kujua kasoro zake, na kujua kwamba hana chochote. Hivyo, upendo wa mwanadamu kwa Mungu umejengwa juu ya msingi wa usafishaji na hukumu ya Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu

445. Leo, watu wengi sana hawana ufahamu huo. Wao huamini kwamba mateso hayana thamani, wao hukanwa na ulimwengu, maisha yao ya nyumbani yamesumbuliwa, wao si wapendwa wa Mungu, na matazamio yao ni matupu. Kuteseka kwa watu wengine hufikia kiwango fulani, na fikira zao hugeukia kifo. Huu si upendo wa kweli kwa Mungu; watu kama hao ni waoga, hawana ustahamilivu, wao ni wadhaifu na wasio na nguvu! Mungu ana hamu ya mwanadamu kumpenda Yeye, lakini kadri mwanadamu anavyompenda Yeye, ndivyo kuteseka kwa mwanadamu huwa kwingi zaidi, na kadri mwanadamu anavyompenda Yeye, ndivyo majaribio ya mwanadamu huwa makubwa zaidi. Ikiwa unampenda Yeye, basi kila aina ya mateso yatakufika—na ikiwa humpendi, basi labda kila kitu kitaendelea kwa urahisi kwako, na kila kitu kinachokuzunguka kitakuwa kitulivu kwako. Unapompenda Mungu, utahisi kwamba mengi kandokando yako hayawezi kushindikana, na kwa sababu kimo chako ni kidogo sana utasafishwa; aidha, huwezi kumridhisha Mungu, na daima utahisi kwamba mapenzi ya Mungu ni ya juu sana, kwamba hayawezi kufikiwa na mwanadamu. Kwa sababu ya haya yote utasafishwa—kwa sababu kuna udhaifu mwingi ndani yako, na mengi yasiyoweza kuridhisha mapenzi ya Mungu, utasafishwa ndani. Lakini lazima muone kwa dhahiri kwamba utakaso hutimizwa tu kupitia usafishaji. Hivyo, katika siku hizi za mwisho lazima muwe na ushuhuda kwa Mungu. Haijalishi mateso yenu ni makubwa vipi, mnapaswa kuendelea hadi mwisho kabisa, na hata wakati wa pumzi yenu ya mwisho, bado lazima muwe waaminifu kwa Mungu, na kudhibitiwa na Mungu; huku pekee ndiko kumpenda Mungu kweli, na huu pekee ndio ushuhuda thabiti na mkubwa sana. Unapojaribiwa na Shetani, unapaswa kusema: “Moyo wangu ni wa Mungu, na Mungu tayari amenipata. Siwezi kukuridhisha wewe—lazima nitoe kila kitu changu ili kumridhisha Mungu.” Kadri unavyomridhisha Mungu, ndivyo Mungu hukubariki zaidi, na ndivyo nguvu za upendo wako kwa Mungu huwa kuu zaidi; kwa hiyo, vilevile, utakuwa na imani na azimio, na utahisi kwamba hakuna kilicho na thamani zaidi au cha maana kuliko kutumia maisha ukimpenda Mungu. Inaweza kusemwa kwamba mwanadamu anatakiwa tu kumpenda Mungu ili kuishi bila huzuni. Ingawa kuna nyakati ambazo mwili wako ni dhaifu na unazongwa na matatizo mengi ya kweli, katika nyakati hizi utamtegemea Mungu kweli, na ndani ya roho yako utafarijiwa, na utahisi hakika, na kwamba una kitu cha kutegemea. Kwa njia hii, utaweza kushinda hali nyingi, na kwa hiyo hutalalamika kuhusu Mungu kwa sababu ya uchungu unaopitia; utataka kuimba, kucheza, na kuomba, kukusanyika na kuwasiliana kwa karibu, kumfikiria Mungu, na utahisi kwamba watu wote, mambo, na vitu vilivyo kandokando yako ambavyo vimepangwa na Mungu vinafaa. Kama humpendi Mungu, yote ambayo unategemea yatakuwa yenye kero kwako, hakuna kitakachokuwa cha kufurahisha machoni mwako; ndani ya roho yako hutakuwa huru bali wa kudhulumiwa, moyo wako daima utalalamika kuhusu Mungu, na daima utahisi kwamba unapitia mateso mengi sana, na kwamba ni udhalimu sana. Kama hufuatilii kwa ajili ya furaha, bali ili umridhishe Mungu na kutoshtakiwa na Shetani, basi ukimbizaji kama huo utakupa nguvu nyingi za kumpenda Mungu. Mwanadamu anaweza kutekeleza yote yanayonenwa na Mungu, na yote ayafanyayo yanaweza kumridhisha Mungu—hii ndiyo maana ya kuwa na hakika. Kufuatilia ridhaa ya Mungu ni kuutumia upendo wa Mungu kuweka maneno Yake katika vitendo; bila kujali wakati—hata kama wengine hawana nguvu—ndani yako bado kuna moyo unaompenda Mungu, ambao unamtamani Mungu sana, na humkosa Mungu. Hiki ni kimo halisi.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu

446. Ni wakati wa usafishaji mkali ambapo mwanadamu anaweza kujipata chini ya ushawishi wa Shetani kwa urahisi zaidi—kwa hivyo ni jinsi gani unapaswa kumpenda Mungu wakati wa usafishaji kama huu? Unapaswa kuyaita mapenzi yako, kuuweka moyo wako mbele ya Mungu na kutenga muda wako wa mwisho Kwake. Haijalishi jinsi gani Mungu hukusafisha, unafaa kuwa na uwezo wa kutia ukweli katika vitendo kutimiza mapenzi ya Mungu, na unafaa kujitolea kumtafuta Mungu na kutafuta mawasiliano. Nyakati kama hizi, zaidi unavyokaa tu, ndivyo utakuwa mtu hasi zaidi, na ndivyo itakuwa rahisi zaidi kwako kurudi nyuma. Wakati ambapo inakulazimu kutenda kazi yako, ingawa huitendi vyema, unafanya kila unachoweza, na unaifanya kwa kutumia tu upendo wako kwa Mungu; bila kujali kile ambacho wengine husema—ikiwa wanasema umetenda vyema, au kwamba umetenda vibaya—motisha zako ni sahihi, na wewe sio wa kujidai, kwani unatenda kwa niaba ya Mungu. Wengine wanapokuelewa vibaya, unaweza kumwomba Mungu na kusema: “Ee Mungu! Siombi kwamba wengine wanivumilie au kunitendea vyema, wala kwamba wanielewe au kunikubali. Naomba tu kwamba niweze kukupenda moyoni mwangu, kwamba niwe na utulivu moyoni mwangu, na kwamba dhamiri yangu iwe safi. Siombi kwamba wengine wanisifu, au kuniheshimu, ninatafuta tu kukuridhisha kutoka moyoni mwangu, ninatenda wajibu wangu kwa kufanya kila ninachoweza, na ingawa mimi ni mpumbavu na mjinga, na wa hali duni, na kipofu, najua kwamba Unapendeza, na niko tayari kukutolea kila ninacho.” Punde tu unapoomba kwa jinsi hii, upendo wako kwa Mungu huibuka, na unahisi utulivu zaidi moyoni mwako. Hili ndilo linalomaanishwa na kutenda upendo wa Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia Usafishaji tu Ndiyo Mwanadamu Anaweza Kuwa na Upendo wa Kweli

447. Je, mwanadamu anapaswa kumpenda Mungu jinsi gani wakati wa usafishaji? Kwa kutumia azimio la kumpenda Mungu kukubali usafishaji Wake: Wakati wa usafishaji, unateseka ndani, kana kwamba kisu kinasokotwa moyoni mwako, ilhali uko tayari kumridhisha Mungu kwa kutumia moyo wako, ambao unampenda, na hauko tayari kuutunza mwili. Hii ndiyo maana ya kutenda upendo wa Mungu. Unaumia ndani, na mateso yako yamefikia kiwango fulani, lakini bado uko tayari kuja mbele ya Mungu na kuomba ukisema: “Ee Mungu! Siwezi kukuacha. Ingawa kuna giza ndani yangu, ningependa kukuridhisha; Unaujua moyo wangu, na ningependa kwamba Uwekeze zaidi upendo Wako ndani yangu.” Huu ndio utendaji wakati wa usafishaji. Ukitumia upendo wa Mungu kama msingi, usafishaji unaweza kukuleta karibu zaidi na Mungu na kukufanya mwandani zaidi wa Mungu. Kwa kuwa unamwamini Mungu, ni lazima uukabidhi moyo wako mbele ya Mungu. Ukiutoa moyo wako na kuuweka mbele ya Mungu, basi wakati wa usafishaji, haitawezekana wewe kumkana Mungu, au kumwacha Mungu. Kwa njia hii, uhusiano wako na Mungu utakuwa wa karibu hata zaidi, na wa kawaida hata zaidi, na mawasiliano yako na Mungu yatakuwa ya mara kwa mara zaidi. Ikiwa kila mara unafanya mazoezi kwa njia hii, basi utatumia muda zaidi katika nuru ya Mungu, na muda zaidi chini ya uongozi wa maneno Yake, pia kutakuwa na mabadiliko zaidi na zaidi katika tabia yako, na ufahamu wako utaongezeka siku baada ya siku. Siku itakapokuja na majaribu ya Mungu yakufike kwa ghafla, hutaweza tu kusimama kando ya Mungu, bali pia utaweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu. Wakati huo, utakuwa kama Ayubu, na Petro. Baada ya kuwa na ushuhuda kwa Mungu, utampenda kwa kweli, na utamtolea maisha yako kwa furaha; utakuwa shahidi wa Mungu, na yule ambaye ni mpendwa wa Mungu. Upendo ambao umepitia usafishaji ni wa nguvu, na sio dhaifu. Haijalishi ni lini au vipi Mungu anakufanya upatwe na majaribu Yake, unaweza kutojali ikiwa unaishi au unaangamia, kuachana na kila kitu kwa furaha kwa ajili ya Mungu, na kuvumilia chochote kwa furaha kwa ajili ya Mungu—na hivyo upendo wako utakuwa safi, na imani yako halisi. Ni hapo tu ndipo utakuwa mtu anayependwa na Mungu kwa kweli, na ambaye amefanywa kamili na Mungu kwa kweli.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia Usafishaji tu Ndiyo Mwanadamu Anaweza Kuwa na Upendo wa Kweli

448. Mungu humwadibu na kumhukumu mwanadamu kwa sababu inahitajika na kazi Yake, na, zaidi ya hayo, kwa sababu inahitajika na mwanadamu. Mwanadamu anahitaji kuadibiwa na kuhukumiwa, na ni hapo tu ndipo anaweza kufikia upendo wa Mungu. Leo, mmesadikishwa kabisa, lakini mnapokumbana na kizingiti kidogo mko taabani; kimo chenu bado ni kidogo sana, na bado mnahitaji kupata uzoefu zaidi wa kuadibu na hukumu kama hiyo ili kupata maarifa ya kina. Leo, mna heshima kidogo kwa Mungu, na mnamcha Mungu, na mnajua Yeye ni Mungu wa kweli, lakini hamna upendo mkubwa Kwake, na bado hamjafikia upendo safi; maarifa yenu ni ya juujuu, na kimo chenu bado hakitoshi. Wakati nyinyi mnapatana na mazingira, bado hamjashuhudia, sehemu ndogo ya kuingia kwenu ndiyo makini, na nyinyi hamjui jinsi ya kufanya mazoezi. Watu wengi ni watazamaji tu na si watendaji; wao humpenda Mungu tu kwa siri katika nyoyo zao, lakini hawana njia ya mazoezi, wala hawafahamu vizuri malengo yao ni nini. Wale ambao wamefanywa wakamilifu hawana tu ubinadamu wa kawaida, lakini wanao ukweli unaozidi vipimo vya dhamiri, na kwamba ni kuu zaidi kuliko viwango ya dhamiri; wao hawatumii tu dhamiri yao kulipia upendo wa Mungu, lakini, zaidi ya hayo, wanamjua Mungu, na wameona kwamba Mungu ni mzuri, na Anastahili upendo wa mtu, na kwamba kuna mambo mengi ya upendo katika Mungu ambayo mtu hana budi ila kumpenda Mungu. Upendo kwa Mungu wa wale ambao wamekuwa wakamilifu ni kwa ajili ya kutimiza matarajio yao binafsi. Upendo wao ni wa hiari, upendo usiouliza malipo yoyote, na sio wa kubadilishana na kitu. Wanampenda Mungu kwa sababu ya maarifa Kwake, na sio kwa sababu nyingine. Watu kama hawa hawajali kama Mungu anawapa neema au la, wanaridhishwa na kumridhisha Mungu. Hawabishani na Mungu wapate kitu kwa badala yake, wala kupima upendo wao kwa Mungu na dhamiri: Umenipa, kwa hivyo nitakupenda kwa badala yake; kama Wewe Hunipi, basi sina chochote cha kukupa kwa badala yake. Wale ambao wamekuwa wakamilifu daima huamini kwamba: Mungu ni Muumba, na Yeye hufanya kazi Yake juu yetu. Kwa vile nina fursa hii, hali, na uwezo wa kufanywa kamili, azimio langu linafaa kuwa kuishi kwa kudhihirisha maisha yaliyo na maana, na ninapaswa kumridhisha Yeye.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matukio Aliyopitia Petro: Ufahamu Wake wa Adabu na Hukumu

449. Wakati wa maisha yake, Petro alipitia usafishaji mara mamia na alipitia majaribu mengi yenye uchungu. Usafishaji huu ukawa msingi wa upendo wake mkuu kwa Mungu, na ukawa uzoefu muhimu zaidi wa maisha yake yote. Kwamba aliweza kuwa na upendo wa hali ya juu kwa Mungu ilikuwa, kwa namna moja, kwa sababu ya azimio lake la kumpenda Mungu; muhimu zaidi, hata hivyo, ilikuwa ni kwa sababu ya usafishaji na mateso ambayo alipitia. Mateso haya yakawa mwongozo wake katika njia ya kumpenda Mungu, na yakawa jambo lililokumbukwa zaidi kwake. Ikiwa watu hawapitii uchungu wa usafishaji wanapompenda Mungu, basi upendo wao umejaa uchafu na mapendeleo yao wenyewe; upendo kama huu umejaa mawazo ya Shetani, na hauwezi hata kabisa kuridhisha mapenzi ya Mungu. Kuwa na azimio la kumpenda Mungu sio sawa na kumpenda Mungu kwa kweli. Hata ingawa yote wanayofikiria mioyoni mwao ni kwa ajili ya kumpenda Mungu, na kumridhisha Mungu, kana kwamba fikira zao hazina mawazo yoyote ya kibinadamu, kana kwamba zote ni kwa ajili ya Mungu, fikira zao zinapoletwa mbele ya Mungu, fikira kama hizi hazisifiwi wala kubarikiwa na Mungu. Hata wakati watu wameelewa kikamilifu ukweli wote—wakati wamekuja kuujua wote—hili haliwezi kusemwa kuwa ishara ya kumpenda Mungu, haiwezi kusemwa kwamba watu hawa hakika wanampenda Mungu. Licha ya kuelewa ukweli mwingi bila kupitia usafishaji, watu hawana uwezo wa kutia ukweli huu katika vitendo; ni wakati wa usafishaji tu ndipo watu wanaweza kuelewa maana halisi ya ukweli huu, hapo tu ndipo watu wanaweza kufahamu kwa kweli maana yao ya ndani. Wakati huo, wanapojaribu tena, wanaweza kutia ukweli katika vitendo kwa njia ya kufaa, na kulingana na mapenzi ya Mungu; wakati huo, mawazo yao ya kibinadamu yanapunguzwa, upotovu wao wa kibinadamu unapunguzwa, na hisia zao za kibinadamu zinapunguzwa; ni wakati huo tu ndipo utendaji wao ni onyesho la ukweli la upendo wa Mungu. Athari ya ukweli wa upendo wa Mungu haitimizwi kupitia ufahamu wa kusemwa au kuwa tayari kiakili, wala haiwezi kutimizwa kwa kueleweka tu. Inahitaji kwamba watu walipe gharama, na kwamba wapitie uchungu mwingi wakati wa usafishaji, na hapo tu ndipo upendo wao utakuwa safi, na wa kuupendeza moyo wa Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia Usafishaji tu Ndiyo Mwanadamu Anaweza Kuwa na Upendo wa Kweli

450. Karibuni mwishoni mwa maisha yake, baada ya yeye kukamilishwa, Petro alisema, “Ee Mungu! Ikiwa ningeishi miaka michache zaidi, ningetamani kufikia upendo safi na wa kina zaidi kwako.” Alipokuwa karibu kusulubiwa, katika moyo wake akaomba, “Ee Mungu! Wakati Wako umewadia, wakati ulionitayarishia umefika. Mimi lazima nisulubiwe kwa ajili Yako, lazima niwe na ushuhuda huu Kwako, na ninatumai kwamba upendo wangu utaweza kukidhi mahitaji Yako, na kwamba unaweza kuwa safi zaidi. Leo, kuwa na uwezo wa kufa kwa ajili Yako, na kusulubiwa kwa ajili Yako, ni faraja na ya kutia moyo kwangu, kwa maana hakuna kinachonifurahisha kuliko kuweza kusulubiwa kwa ajili Yako na kukidhi matakwa Yako, na kuweza kujitoa Kwako, kutoa maisha yangu Kwako. Ee Mungu! Wewe ni wa kupendeza kweli! Kama Ungeniruhusu niishi, ningenuia kukupenda zaidi. Mradi tu ninaishi, mimi nitakupenda. Natamani kukupenda kwa undani zaidi. Unanihukumu, Unaniadibu, na kunijaribu kwa sababu mimi si mwenye haki, kwa sababu nimetenda dhambi. Na tabia Yako ya haki inakuwa dhahiri zaidi kwangu. Hii ni baraka kwangu, kwa maana ninapata uwezo wa kukupenda kwa undani zaidi, na mimi niko tayari kukupenda kwa njia hii hata kama Hunipendi. Mimi niko tayari kutazama tabia Yako ya haki, kwa maana inafanya niweze kuishi maisha ya maana zaidi. Mimi ninahisi kwamba maisha yangu sasa ni ya maana zaidi, kwa maana nimesulubiwa kwa ajili Yako, na ni jambo la maana kufa kwa ajili Yako. Hata hivyo bado mimi sijaridhika, kwa maana najua kidogo sana kukuhusu, najua kwamba siwezi kutimiza matakwa Yako kikamilifu, na kuwa nimekulipa kidogo mno. Katika maisha yangu, sijaweza kurudisha nafsi yangu Kwako kikamilifu; Niko mbali sana na hili. Nikitazama nyuma kwa wakati huu, mimi huhisi kuwa nina mzigo mkubwa wa madeni kwako, na sina muda mwingine ila huu kwa ajili ya kurekebisha makosa yangu na upendo wote ambao sijakulipa Wewe.”

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matukio Aliyopitia Petro: Ufahamu Wake wa Adabu na Hukumu

451. Mwanadamu lazima azingatie kuishi kwa kudhihirisha maisha ya maana, na hapaswi kuridhika na hali yake ya sasa. Kuishi kama mfano wa Petro, lazima awe na maarifa na uzoefu wa Petro. Mtu lazima ashikilie mambo ambayo ni ya juu na zaidi ya yaliyo makuu. Ni lazima yeye afuatilie kwa ndani zaidi, usafi zaidi wa upendo wa Mungu, na maisha ambayo yana thamani na umuhimu. Haya tu ndiyo maisha; hivi tu ndivyo mwanadamu atakuwa sawa na Petro. Lazima kuzingatia kuwa makini kwa kuingia kwako kwa upande chanya, na lazima uhakikishe kwamba haurudi nyuma kwa ajili ya urahisi wa kitambo na kupuuza mambo mengine makubwa, zaidi maalum, na zaidi kwa ukweli wa vitendo. Upendo wako lazima uwe wa vitendo, na lazima utafute njia ya kujitoa katika upotovu huu, maisha yasiyo na kujali ambayo hayana tofauti na ya mnyama. Lazima uishi maisha ya maana, maisha ya thamani, na usijipumbaze, au kufanya maisha yako kama kitu cha kuchezea. Kwa kila mtu ambaye anatumai kumpenda Mungu, hakuna ukweli usioweza kupatikana, na hakuna haki wasioweza kusimama imara nayo. Unafaa kuishije maisha Yako? Unapaswa kumpenda Mungu vipi na kutumia upendo huu ili kukidhi hamu Yake? Hakuna jambo kubwa zaidi katika maisha Yako. Zaidi ya yote, lazima uwe na matarajio hayo na uvumilivu, na hupaswi kuwa kama wanyonge wasio na nia. Lazima ujifunze jinsi ya kupitia maisha ya maana, na kuuona ukweli wa maana, na hupaswi kujichukua kipurukushani katika njia hiyo. Bila wewe kujua, maisha Yako yatakupita tu; na baada ya hapo, je utakuwa una fursa nyingine ya kumpenda Mungu? Je, mwanadamu anaweza kumpenda Mungu baada ya kufa? Lazima uwe na matarajio na dhamiri sawa na ya Petro; maisha Yako ni lazima yawe na maana, na usifanye mchezo na nafsi yako. Kama mwanadamu, na kama mtu ambaye anamfuata Mungu, ni lazima uweze kufikiria na kuyachukulia maisha yako kwa makini—ukizingatia jinsi unavyopaswa kujitoa mwenyewe kwa Mungu, jinsi unapaswa kuwa na imani yenye maana zaidi katika Mungu, na jinsi, kwa kuwa wewe unampenda Mungu, unapaswa kumpenda Yeye kwa njia ambayo ni safi zaidi, nzuri zaidi, na bora zaidi.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matukio Aliyopitia Petro: Ufahamu Wake wa Adabu na Hukumu

452. Ikiwa watu wanataka kumpenda Mungu, lazima waonje uzuri wa Mungu, na waone uzuri wa Mungu; ni hapo tu ndipo unaweza kuamshwa ndani yao moyo unaompenda Mungu, moyo ambao uko tayari kugharamika kwa uaminifu kwa ajili ya Mungu. Mungu hawafanyi watu kumpenda kupitia maneno na sura, au kwa mawazo yao, na Hawalazimishi watu kumpenda. Badala yake, Anawafanya wampende kwa hiari yao, na huwafanya kuyaona mapenzi Yake katika kazi Yake na matamshi, ambapo baadaye wanakuwa na upendo wa Mungu. Ni kwa njia hii tu ndio watu wanaweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu. Watu hawampendi Mungu kwa sababu wameombwa na wengine kufanya vile, wala si msukumo wa hisia wa muda mfupi. Wanampenda Mungu kwa sababu wameuona upendo wake, na wameona kuwa kuna mengi kumhusu ambayo yanastahili upendo wao, kwa sababu wameona wokovu wa Mungu, busara, na matendo ya ajabu—na kutokana na hayo, wanamsifu Mungu kwa kweli, na kumtamani kwa kweli, na wanaamshiwa msisimko ndani yao kwamba hawawezi kuishi bila kumpata Mungu. Sababu ya wale ambao humshuhudia Mungu wanaweza kumtolea ushuhuda wa kufana ni kwa kuwa ushuhuda wao umekitwa kwenye msingi wa ufahamu wa kweli pamoja na matamanio ya kweli kwa Mungu, si kutokana na msukumo wa hisia, lakini kulingana na ufahamu wa Mungu na tabia Zake. Kwa sababu wamepata kumjua Mungu, wanahisi kwamba lazima wamshuhudie Mungu, na kuwafanya wale wote wamtamanio Mungu wamjue Mungu, na kufahamu upendo wa Mungu, na uhalisi Wake. Sawa na upendo ya watu kwa Mungu, ushuhuda wao ni wa hiari, ni halisi, na una umuhimu halisi na thamani. Si baridi, au tupu na usiokuwa na maana. Sababu ya wale tu wanaompenda Mungu kweli kuwa na thamani na maana katika maisha yao, na kuamini katika Mungu tu, ni kwa sababu watu hawa wanaishi katika mwangaza wa Mungu, na wanaweza kuishi kwa ajili ya kazi ya Mungu na usimamizi Wake; hawaishi gizani, bali wanaishi katika mwangaza; hawaishi maisha yasiokuwa na maana, ila wanaishi maisha ambayo yamebarikiwa na Mungu. Ni wale tu wanaompenda Mungu ndio wanaoweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu, ni wao tu ndio mashahidi wa Mungu, na ni wao tu ndio waliobarikiwa na Mungu, na ni wao tu ndio wanaoweza kupokea ahadi za Mungu. Wale wanaompenda Mungu ndio wandani wa Mungu; ndio watu ambao wanapendwa na Mungu, na wanaweza kufurahia baraka pamoja na Mungu. Ni watu wa aina hii tu ndio watakaoishi milele, na ni wao tu watakaoishi milele katika utunzaji na ulinzi wa Mungu. Mungu anastahili kupendwa na watu, na Anastahili upendo wa watu wote, lakini sio watu wote wanaoweza kumpenda Mungu, na si watu wote wanaoweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu na kushikilia mamlaka pamoja na Mungu. Kwa sababu wanaweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu na kutoa juhudi zao zote kwa kazi ya Mungu, wale wanaompenda Mungu kwa kweli wanaweza kutembea mahali popote chini ya mbingu bila ya mtu yeyote kuwa na ujasiri wa kuwapinga, na wanaweza kushika mamlaka duniani na kuwatawala watu wote wa Mungu. Watu hawa wamekusanyika pamoja kutoka kote duniani. Ni watu kutoka kote duniani wanaozungumza lugha tofauti na ni wenye rangi tofauti za ngozi, lakini maana ya kuwepo kwao ni sawa, wote wana moyo unaompenda Mungu, wote wana ushuhuda sawa, na wana maazimio sawa, na matamanio sawa. Wale wanaompenda Mungu wanaweza kutembea ulimwenguni kote wakiwa huru, na wale walio na ushuhuda kwa Mungu wanaweza kusafiri katika ulimwengu mzima. Watu hawa wamependwa na Mungu, wamebarikiwa na Mungu, na wataishi milele ndani ya mwangaza Wake.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wanaompenda Mungu Wataishi Milele Katika Mwangaza Wake

Iliyotangulia: I. Kuhusu Jinsi ya Kuchagua Njia ya Mtu katika Imani

Inayofuata: K. Kuhusu Jinsi ya Kupata Kumjua Mungu

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp