Mwanadamu Aliyepotoka Anahitaji Zaidi Wokovu wa Mungu Mwenye Mwili
Mungu alifanyika mwili kwa sababu lengo la kazi Yake si roho ya Shetani, au kitu chochote kisicho cha mwili, ila mwanadamu, ambaye ni wa mwili na ambaye amepotoshwa na Shetani. Ni kwa sababu hii hasa kwamba mwili wa mwanadamu umepotoshwa ndiyo maana Mungu amemfanya mwanadamu mwenye mwili kuwa mlengwa wa kazi Yake; aidha, kwa sababu mwanadamu ni mlengwa wa upotovu, Amemfanya mwanadamu kuwa mlengwa wa pekee wa kazi Yake katika hatua zote za kazi Yake ya wokovu. Mwanadamu ni kiumbe anayekufa, ni wa mwili na damu, na Mungu tu ndiye Anayeweza kumwokoa mwanadamu. Kwa namna hii, ni lazima Mungu awe mwili ambao una tabia zinazofanana na mwanadamu ili Aweze kufanya kazi Yake, ili kwamba kazi Yake iweze kupata matokeo mazuri zaidi. Ni lazima Mungu afanyike mwili ili Aweze kufanya kazi Yake kwa ufanisi kwa sababu mwanadamu ni wa mwili, na hana uwezo wa kushinda dhambi au kujitenga na mwili. Ingawa kiini na utambulisho wa Mungu unatofautiana kwa kiasi kikubwa na kiini na utambulisho wa mwanadamu, bado kuonekana Kwake kunafanana na kuonekana kwa mwanadamu, Ana umbo la mwanadamu wa kawaida, na Anaishi maisha ya mwanadamu wa kawaida, na wale wanaomwona hawawezi kuona tofauti na mtu wa kawaida. Kuonekana huku kwa kawaida na ubinadamu wa kawaida vinatosha Kwake kwa ajili ya kufanya kazi Yake ya kiungu katika ubinadamu wa kawaida. Mwili Wake unamruhusu kufanya kazi Yake katika ubinadamu wa kawaida, na unamsaidia kufanya kazi Yake miongoni mwa wanadamu, na ubinadamu Wake wa kawaida, aidha, humsaidia kufanya kazi ya wokovu miongoni mwa wanadamu. Ingawa ubinadamu Wake wa kawaida umeleta misukosuko mingi miongoni mwa wanadamu, misukosuko hio haijaathiri matokeo ya kawaida ya kazi Yake. Kwa ufupi, kazi ya ubinadamu Wake wa kawaida ni ya manufaa makubwa kwa mwanadamu. Ingawa watu wengi hawakubali ubinadamu Wake wa kawaida, kazi Yake bado inaweza kuwa ya ufanisi, na matokeo haya yanapatikana kutokana na ubinadamu Wake wa kawaida. Kuhusu hili hakuna shaka. Kutokana na kazi Yake ya mwili, mwanadamu anapata vitu mara kumi au dazeni kadhaa zaidi kuliko dhana zilizopo miongoni mwa wanadamu kuhusu ubinadamu Wake wa kawaida, na dhana hizo hatimaye zitamezwa na kazi Yake. Na matokeo ambayo kazi Yake imefanikisha, ambayo ni kusema, maarifa ambayo mwanadamu anayo juu Yake, yanapita kwa mbali sana dhana za mwanadamu kuhusu Yeye. Hakuna namna ya kufikiri au kupima kazi Anayofanya katika mwili, maana mwili Wake si kama wa mwanadamu; ingawa sura za nje zinafanana kiini chao si sawa. Mwili Wake huibua dhana nyingi miongoni mwa wanadamu kuhusu Mungu, ilhali mwili Wake unaweza pia kumruhusu mwanadamu kupata maarifa mengi, na unaweza hata kumshinda mtu yeyote aliye na umbo sawa la nje. Kwa kuwa Yeye si mwanadamu wa kawaida tu, bali ni Mungu mwenye umbo la nje kama la mwanadamu, na hakuna anayeweza kumwelewa au kumfahamu kikamilifu. Mungu asiyeonekana na Asiyeshikika anapendwa na kukaribishwa na wote. Kama Mungu ni Roho tu Asiyeonekana kwa mwanadamu, ni rahisi sana kwa mwanadamu kumwamini Mungu. Mwanadamu anaweza kuzipa uhuru fikra zake mwenyewe, anaweza kuchagua taswira yoyote anayotaka kuwa taswira ya Mungu ili ajiridhishe mwenyewe na kujifurahisha. Kwa njia hii, watu wanaweza kufanya chochote ambacho Mungu wao wenyewe anapenda zaidi, na kile anachotaka wakifanye, bila mashaka yoyote. Zaidi ya hayo, watu hawa wanaamini kwamba hakuna ambaye ni mwaminifu na anayejitolea zaidi kwa Mungu kuliko wao, na kwamba wengine wote ni mbwa wa Mataifa, na wasiokuwa waaminifu kwa Mungu. Inaweza kusemwa kwamba hiki ndicho kinachotafutwa na wale ambao imani yao kwa Mungu ni ya kidhahania na ambayo imejikita katika mafundisho; vile wanavyotafuta vinafanana, vikiwa na tofauti ndogo tu. Ni kwamba tu taswira za Mungu katika mawazo yao ni tofauti, lakini viini vyao kimsingi vinafanana.
Mwanadamu hasumbuliwi na imani yake ya kutojali katika Mungu, na jinsi anavyomwamini Mungu vyovyote vile anavyotaka. Hii ni moja ya “haki na uhuru wa mwanadamu,” ambao hakuna mtu anayeweza kuuingilia kwa sababu mwanadamu anamwamini Mungu wake mwenyewe na wala si Mungu wa mtu yeyote yule; ni mali yake binafsi, na takribani kila mtu anamiliki aina hii ya mali binafsi. Mwanadamu anaichukulia mali hii kama hazina ya thamani, lakini kwa Mungu hakuna kitu ambacho ni duni au hakina thamani zaidi ya hiki, maana hakuna kiashiria cha wazi cha upinzani kwa Mungu kuliko mali hii binafsi ya mwanadamu. Ni kwa sababu ya kazi ya Mungu mwenye mwili ndipo Mungu amefanyika mwili ambao una umbo la kugusika, na ambao unaweza kuonekana na kuguswa na mwanadamu. Yeye si Roho asiyekuwa na umbo, bali ni mwili ambao unaweza kuhusiana na kuonekana na mwanadamu. Hata hivyo, Miungu mingi ambayo watu wanaamini kwayo ni miungu isiyo na mwili na umbo maalumu, na ambayo haifungwi na umbo maalumu. Kwa njia hii, Mungu mwenye mwili amekuwa adui wa wengi wanaomwamini Mungu, na wale ambao hawawezi kuukubali ukweli wa Mungu mwenye mwili, vilevile, wamekuwa maadui wa Mungu. Mwanadamu amejawa na dhana si kwa sababu ya namna anavyofikiri, au kwa sababu ya uasi wake, bali ni kwa sababu ya mali hii binafsi ya mwanadamu. Ni kwa sababu ya mali hii kwamba watu wengi wanakufa, na ni Mungu huyu asiye dhahiri, ambaye hawezi kuguswa, hawezi kuonwa, na ambaye hayupo ndio hasa ambaye anaangamiza maisha ya mwanadamu. Maisha ya mwanadamu yanapotea si kwa sababu ya Mungu mwenye mwili, wala si kwa sababu ya Mungu wa mbinguni, bali ni Mungu wa fikra za mwanadamu mwenyewe. Sababu pekee ambayo Mungu mwenye mwili Amekuja katika mwili ni kwa sababu ya mahitaji ya mwanadamu aliyepotoka. Ni kwa sababu ya mahitaji ya mwanadamu na si ya Mungu, na mateso Yake na sadaka ni kwa ajili ya mwanadamu na si kwa manufaa ya Mungu Mwenyewe. Hakuna faida wala hasara au tuzo kwa Mungu; Hatavuna mavuno yoyote ya baadaye, bali ni kile ambacho hapo awali Aliwiwa. Yote Anayoyafanya na kujitolea kwa ajili mwanadamu si kwa sababu Atapata thawabu kubwa, bali ni kwa ajili ya mwanadamu. Ingawa kazi ya Mungu mwenye mwili inahusisha ugumu mwingi usiofikirika, matokeo ambayo yanapatikana mwishowe yanazidi kwa mbali sana kazi inayofanywa na Roho Mtakatifu moja kwa moja. Kazi ya mwili inahusisha taabu nyingi sana, na mwili hauwezi kuwa na utambulisho mkubwa kama wa Roho, hauwezi kufanya matendo ya kimiujiza kama Roho, sembuse kuwa na mamlaka kama ya Roho. Lakini bado kiini cha kazi inayofanywa na mwili huu usio wa ajabu ni bora zaidi ikilinganishwa na kazi inayofanywa moja kwa moja na Roho, na mwili huu Wenyewe ndio jibu la mahitaji ya wanadamu wote. Kwa wale watakaookolewa, thamani ya Roho ipo chini zaidi ikilinganiswha na ile ya mwili. Kazi ya Roho inaweza kuufikia ulimwengu wote, kuvuka milima yote, mito, maziwa, na bahari, lakini kazi ya mwili kwa ufanisi zaidi inahusiana na kila mtu anayekutana na Yeye. Aidha, mwili wa Mungu katika umbo la kushikika unaweza kueleweka vizuri na kuaminiwa na mwanadamu, na unaweza kuimarisha maarifa ya mwanadamu kuhusu Mungu, na unaweza kumwachia mwanadamu hisia ya kina zaidi ya matendo halisi ya Mungu. Kazi ya Roho imefungwa sirini, ni vigumu kwa viumbe wenye mwili wa kufa kuielewa, na ni vigumu zaidi kwao kuiona, na hivyo wanaweza kutegemea tu vitu vya kufikirika. Hata hivyo, kazi ya mwili ni ya kawaida, na imejikita katika uhalisi, na ina hekima kubwa sana, na ni ukweli unaoweza kuonekana kwa macho ya mwanadamu; mwanadamu anaweza kupitia uzoefu wa hekima ya Mungu, na hana haja ya kuwa na fikira zake kubwa. Huu ndio usahihi na thamani halisi ya kazi ya Mungu mwenye mwili. Roho anaweza tu kufanya vitu ambavyo havionekani kwa mwanadamu na ni vigumu kwake kuvifikiria, kwa mfano nuru ya Roho, mguso wa Roho na uongozi wa Roho, lakini kwa mwanadamu mwenye akili, hivi havitoi maana inayoeleweka. Vinatoa tu mguso, au maana ya jumla, na havitoi maelekezo kwa maneno. Hata hivyo, kazi ya Mungu mwenye mwili, ni tofauti sana: Ina mwongozo sahihi wa maneno, ina nia ya wazi, ina malengo ya wazi yanayohitajika. Na hivyo mwanadamu hahitaji kupapasa, au kutumia fikra zake, au kufanya makisio. Huu ndio uwazi wa kazi katika mwili, na tofauti yake kubwa kutoka kwa kazi ya Roho. Kazi ya Roho inafaa tu kwa mawanda finyu, na haiwezi kuchukua kazi ya mwili. Kazi ya mwili inampa mwanadamu malengo halisi zaidi na yanayohitajika na maarifa ya kivitendo zaidi na yenye thamani kuliko kazi ya Roho. Ni kazi ambayo ina thamani kubwa kwa mwanadamu aliyepotoka ambayo inatoa maneno sahihi, malengo ya wazi ya kufuata, na ambayo inaweza kuonekana na kuguswa. Ni kazi halisi tu na mwongozo wa wakati sahihi kwa mahitaji ya mwanadamu, na kazi ya kivitendo pekee ndiyo inayoweza kumwokoa mwanadamu kutoka katika tabia yake iliyopotoka na kusawijika. Hii inaweza kufanywa na Mungu mwenye mwili tu; ni Mungu mwenye mwili peke yake ndiye Anayeweza kumwokoa mwanadamu kutoka katika hali yake ya zamani ya kupotoka. Ingawa Roho ni kiini cha asili ya Mungu, kazi kama hii inaweza tu kufanywa na mwili Wake. Kama Roho angefanya kazi peke Yake, basi haingewezekana kwa kazi Yake kuwa na ufanisi—huu ni ukweli ulio wazi kabisa. Ingawa watu wengi wamekuwa maadui wa Mungu kwa sababu ya mwili huu, Anapokamilisha kazi Yake, wale ambao wapo kinyume Naye hawataacha tu kuwa maadui Zake, bali kinyume chake watakuwa mashahidi Wake. Watakuwa mashahidi watakaokuwa wameshindwa na Yeye, mashahidi wanaolingana na Yeye, na wasiotenganishwa Naye. Atamfanya mwanadamu ajue umuhimu wa kazi Yake katika mwili kwa mwanadamu, na mwanadamu atajua umuhimu wa mwili huu katika maana ya uwepo wa mwanadamu, atajua thamani Yake halisi katika ukuaji wa maisha ya mwanadamu, na, zaidi ya hayo, atajua kwamba mwili huu utakuwa ni chemchemi hai ya uzima ambayo kwayo mwanadamu hataachana nayo. Ingawa mwili wa Mungu mwenye mwili unatofautiana sana na utambulisho na nafasi ya Mungu, na unaonekana kwa mwanadamu kuwa haulingani na hadhi Yake halisi, mwili huu, ambao hauna sura halisi ya Mungu, au utambulisho halisi wa Mungu, unaweza kufanya kazi ambayo Roho wa Mungu hawezi kuifanya moja kwa moja. Huo ndio umuhimu na thamani ya kweli ya kupata mwili kwa Mungu, na ni umuhimu na thamani hii ambayo mwanadamu hawezi kuithamini na kuikubali. Ingawa wanadamu wote wanamtazamia Roho wa Mungu na wanamdharau Mungu mwenye mwili, bila kujali vile wanavyoona au kufikiri, umuhimu na thamani halisi ya mwili inazidi kwa mbali ile ya Roho. Bila shaka, hii ni kwa mujibu wa mwanadamu aliyepotoka. Kwa kuwa kila mtu anayetafuta ukweli na kutamani kuonekana kwa Mungu, kazi ya Roho inaweza tu kutoa mguso au msukumo, na hisia ya kuona maajabu ambayo hayaelezeki na kufikirika, na hisia ambayo ni kuu, ya juu sana kuliko uwezo wa mwanadamu, na inayotamanika, lakini ambayo pia haifikiwi na haipatikani kwa wote. Mwanadamu na Roho wa Mungu wanaweza tu kutazamana kwa mbali, kana kwamba kuna umbali mkubwa kati yao, na hawawezi kufanana kamwe, kana kwamba mwanadamu na Mungu wametenganishwa na mgawanyiko usioonekana. Kwa hakika, hizi ni fikra za uongo ambazo Roho amempa mwanadamu, ambazo ndiyo sababu Roho na mwanadamu sio wa aina moja, na Roho na mwanadamu hawawezi kuishi pamoja katika ulimwengu mmoja, na kwa sababu Roho hana kitu chochote cha mwanadamu. Kwa hivyo mwanadamu hana haja ya Roho, maana Roho hawezi kufanya kazi inayohitajika sana na mwanadamu moja kwa moja. Kazi ya mwili inampatia mwanadamu malengo ya kivitendo ya kufuata, maneno halisi, na hisia kwamba Yeye ni halisi na wa kawaida, kwamba ni mnyenyekevu na wa kawaida. Ingawa mwanadamu anaweza kumwogopa, kwa watu wengi Yeye ni rahisi kuhusiana na Yeye: Mwanadamu anaweza kuuona uso Wake, na kuisikia sauti Yake, na hahitaji kumwangalia kwa kutokea mbali. Mwanadamu anahisi kuwa ni rahisi kuufikia mwili huu, sio wa mbali au usioeleweka, bali unaonekana na kushikika, maana mwili huu upo katika ulimwengu mmoja na mwanadamu.
Kwa wale wote ambao wanaishi katika mwili, kubadilisha tabia zao kunahitaji kuwe na malengo ya kufuata, na kumjua Mungu kunahitaji kushuhudia matendo halisi na sura halisi ya Mungu. Yote haya yanaweza kufikiwa tu na Mungu mwenye mwili, na yote yanaweza kukamilishwa na mwili wa kawaida na halisi. Hii ndiyo maana kufanyika mwili ni muhimu, na kwa nini kunahitajika na wanadamu wote wapotovu. Kwa kuwa watu wanahitajika kumjua Mungu, taswira za Mungu wa kufikirika na wa kimiujiza zinapaswa ziondolewe kutoka katika mioyo yao, na kwa kuwa wanatakiwa kutupilia mbali tabia zao potovu, lazima kwanza wajue tabia yao potovu. Ikiwa mwanadamu anafanya tu kazi ya kuondoa taswira za Miungu isiyo dhahiri kutoka katika mioyo ya watu, basi atashindwa kupata matokeo sahihi. Taswira za Miungu isiyo dhahiri katika mioyo ya watu haziwezi kufichuliwa, kuachwa, au kuondolewa kikamilifu kwa maneno pekee. Kwa kufanya hivyo, mwisho wake haitawezekana kuondoa vitu hivi vilivyokita mizizi kwa watu. Ni kwa kubadilisha vitu hivi visivyo dhahiri na vya kimiujiza na Mungu anayeonekana tu na mwenye taswira halisi ya Mungu, na kuwafanya watu wayajue hatua kwa hatua ndipo matokeo mazuri yanaweza kupatikana. Mwanadamu anatambua kwamba Mungu aliyekuwa anamtafuta huko nyuma ni asiye dhahiri na wa kimiujiza. Kile ambacho kinaweza kufanikisha matokeo haya sio uongozi wa moja kwa moja wa Roho, sembuse mafundisho ya mtu fulani, bali ni Mungu mwenye mwili. Dhana za mwanadamu huwekwa wazi Mungu mwenye mwili anapofanya kazi Yake rasmi, kwa sababu hali ya kawaida na uhalisi wa Mungu mwenye mwili ni kinyume cha Mungu asiye yakini na asiye wa kawaida katika fikira za mwanadamu. Dhana asili za mwanadamu zinaweza tu kufunuliwa kupitia tofauti zao na Mungu mwenye mwili. Bila ulinganisho na Mungu mwenye mwili, dhana za mwanadamu zisingefichuliwa; kwa maneno mengine, bila tofauti ya uhalisi vitu visivyo dhahiri visingefichuliwa. Hakuna anayeweza kutumia maneno ili kufanya kazi hii, na hakuna anayeweza kuizungumzia kazi hii kwa kutumia maneno. Ni Mungu Mwenyewe pekee ndiye Anayeweza kufanya kazi Yake, na hakuna mtu mwingine anayeweza kufanya kazi hii kwa niaba Yake. Haijalishi lugha ya mwanadamu ni tajiri kiasi gani, haiwezi kuzungumzia uhalisi na ukawaida wa Mungu. Mwanadamu anaweza tu kumjua Mungu kivitendo zaidi, na anaweza tu kumwona kwa uwazi zaidi, ikiwa Mungu binafsi anafanya kazi miongoni mwa wanadamu na kuonyesha kabisa sura Yake na uungu Wake. Athari hii haiwezi kutimizwa na mwanadamu yeyote yule mwenye mwili. Bila shaka, Roho wa Mungu pia hawezi kupata matokeo haya. Mungu anaweza kumwokoa mwanadamu kutoka katika ushawishi wa Shetani, lakini kazi hii haiwezi kukamilishwa moja kwa moja na Roho wa Mungu; badala yake, inaweza kufanywa tu na mwili ambao Roho wa Mungu anauvaa, na mwili wa Mungu mwenye mwili. Mwili huu ni mwanadamu na pia ni Mungu, ni mwanadamu aliye katika ubinadamu wa kawaida na pia ni Mungu ambaye ana uungu wote. Na hivyo, hata kama mwili huu sio Roho wa Mungu, na unatofautiana kwa kiasi kikubwa na Roho, bado ni Mungu mwenye mwili Mwenyewe ambaye Anamwokoa mwanadamu, ambaye ni Roho, pia ni mwili. Haijalishi Anaitwa majina gani, hatimaye bado ni Mungu Mwenyewe anayemwokoa mwanadamu. Maana Roho wa Mungu hatenganishwi na mwili, na kazi ya mwili pia ni kazi ya Roho wa Mungu; ni kwamba tu kazi hii haifanywi kwa kutumia utambulisho wa Roho, lakini inafanywa kwa kutumia utambulisho wa mwili. Kazi inayotakiwa kufanywa moja kwa moja na Roho haihitaji kupata mwili, na kazi ambayo inahitaji mwili kuifanya haiwezi kufanywa moja kwa moja na Roho, na inaweza kufanywa tu na Mungu mwenye mwili. Hiki ndicho kinachohitajika kwa kazi hii, na ndicho kinachohitajika na mwanadamu aliyepotoka. Katika hatua tatu za kazi ya Mungu, ni hatua moja tu ndiyo iliyofanywa moja kwa moja na Roho, na hatua mbili zilizobaki zimechukuliwa na Mungu mwenye mwili, na hazifanywi moja kwa moja na Roho. Kazi ya Enzi ya Sheria iliyofanywa na Roho haikuhusisha kubadilisha tabia potovu ya mwanadamu, na wala haikuwa na uhusiano wowote na maarifa ya mwanadamu kuhusu Mungu. Hata hivyo kazi ya Mungu mwenye mwili katika Enzi ya Neema na Enzi ya Ufalme, inahusisha tabia potovu ya mwanadamu na maarifa yake juu ya Mungu, na ni sehemu ya maana na muhimu ya kazi ya wokovu. Kwa hiyo, mwanadamu aliyepotoka anahitaji zaidi wokovu wa Mungu mwenye mwili, na anahitaji zaidi kazi ya moja kwa moja ya Mungu mwenye mwili. Mwanadamu anamhitaji Mungu mwenye mwili ili kumchunga, kumsaidia, kumnywesha maji, kumlisha, kumhukumu na kumwadibu, na anahitaji neema zaidi na wokovu mkubwa kutoka kwa Mungu mwenye mwili. Ni Mungu katika mwili pekee ndiye anayeweza kuwa msiri wa mwanadamu, mchungaji wa mwanadamu, msaada wa wakati huu wa mwanadamu, na haya yote ndiyo umuhimu wa kufanyika mwili kwa nyakati za leo na zilizopita.
Mwanadamu amepotoshwa na Shetani, na yeye ndiye kiumbe wa juu kabisa kuliko viumbe vyote vya Mungu, hivyo mwanadamu anahitaji wokovu wa Mungu. Mlengwa wa wokovu wa Mungu ni mwanadamu, si Shetani, na kile kitakachookolewa ni mwili wa mwanadamu, na roho ya mwanadamu, na si mashetani. Shetani ni mlengwa wa uharibifu wa Mungu, mwanadamu ni mlengwa wa wokovu wa Mungu, na mwili wa mwanadamu umepotoshwa na Shetani, kwa hivyo kitu cha kwanza kuokolewa ni mwili wa mwanadamu. Mwili wa mwanadamu umepotoshwa kwa kiasi kikubwa, na umekuwa kitu cha kumpinga Mungu, ambacho kinapinga na kukana waziwazi uwepo wa Mungu. Mwili huu uliopotoka ni vigumu sana kushughulika nao, na hakuna kitu ambacho ni kigumu sana kushughulika nacho au kukibadilisha kuliko tabia potovu ya mwili. Shetani anaingia katika mwili wa mwanadamu ili kuchochea usumbufu, na anatumia mwili wa mwanadamu kuisumbua kazi ya Mungu, na kuharibu mpango wa Mungu, na hivyo mwanadamu amekuwa Shetani, na adui wa Mungu. Ili mwanadamu aweze kuokolewa, kwanza ni lazima aweze kushindwa. Ni kwa sababu hii ndiyo maana Mungu anainuka na kuingia katika vita na Anaingia katika mwili ili afanye kazi ambayo Amekusudia kuifanya, na kupambana na Shetani. Lengo Lake ni wokovu wa mwanadamu, mwanadamu ambaye amepotoshwa, na kushindwa na kuangamizwa na Shetani, ambaye ameasi dhidi Yake. Anamshinda Shetani kupitia kazi Yake ya kumshinda mwanadamu, na wakati huo huo Anamwokoa mwanadamu aliyepotoka. Hiyo, ni kazi ambayo inafanikisha malengo mawili kwa wakati mmoja. Anafanya kazi katika mwili, na kuzungumza katika mwili, na Anafanya kazi zote katika mwili ili Aweze kujihusisha vyema na mwanadamu, na kumshinda mwanadamu vyema zaidi. Mara ya mwisho ambapo Mungu alifanyika mwili, kazi Yake ya siku za mwisho itahitimishwa katika mwili. Atawapanga watu wote kulingana na aina, Atahitimisha usimamizi Wake wote, na pia kuhitimisha kazi Yake yote katika mwili. Baada ya kazi Yake yote duniani kuisha, Atakuwa mshindi kikamilifu. Kwa kufanya kazi katika mwili, Mungu atakuwa amemshinda mwanadamu kikamilifu na atakuwa amempata mwanadamu kikamilifu. Je, hii haimaanishi kwamba usimamizi Wake wote utakuwa umefika mwisho? Mungu Atakapohitimisha kazi Yake katika mwili, kwa kuwa atakuwa Amemshinda Shetani kikamilifu, na Amekuwa mshindi, Shetani hatakuwa na fursa zaidi ya kumpotosha mwanadamu. Kazi ya Mungu mwenye mwili ya mara ya kwanza ilikuwa ni wokovu na msamaha wa dhambi za mwanadamu. Sasa ni kazi ya kuwashinda na kuwapata wanadamu kikamilifu, ili kwamba Shetani asiwe na njia yoyote tena ya kufanya kazi yake, na atakuwa amepoteza kabisa, na Mungu atakuwa ameshinda kabisa. Hii ni kazi ya mwili, na ni kazi inayofanywa na Mungu Mwenyewe. Kazi ya kwanza ya hatua tatu za kazi ya Mungu ilifanywa moja kwa moja na Roho, na wala si mwili. Hata hivyo, kazi ya mwisho ya hatua tatu za kazi ya Mungu, inafanywa na Mungu mwenye mwili, na wala haifanywi moja kwa moja na Roho. Kazi ya ukombozi ya hatua ya katikati pia imefanywa na Mungu mwenye mwili. Katika kazi yote ya usimamizi, kazi muhimu sana ni wokovu kutoka katika ushawishi wa Shetani. Kazi muhimu ni kumshinda kabisa mwanadamu aliyepotoka, na hivyo kurejesha heshima ya awali ya Mungu katika moyo wa mwanadamu, na kumruhusu kufikia maisha ya kawaida, ni sawa na kusema, maisha ya kawaida ya kiumbe wa Mungu. Kazi hii ni muhimu, na ni kiini cha kazi ya usimamizi. Katika hatua tatu za kazi ya wokovu, hatua ya kwanza ya kazi ya Enzi ya Sheria ilikuwa mbali sana na kiini cha kazi ya usimamizi; ilikuwa na mwonekano mdogo tu wa kazi ya wokovu, na haikuwa mwanzo wa kazi ya Mungu ya kumwokoa mwanadamu kutoka katika utawala wa Shetani. Hatua ya kwanza ya kazi ilifanywa moja kwa moja na Roho kwa sababu, chini ya sheria, mwanadamu alijua tu kuzishika sheria, na hakuwa na ukweli zaidi, na kwa sababu kazi katika Enzi ya Sheria haikujihusisha na kubadilisha tabia ya mwanadamu, sembuse haikuwa inajihusisha na kazi ya jinsi ya kumwokoa mwanadamu kutoka katika utawala wa Shetani. Roho wa Mungu alikamilisha hatua hii rahisi ya kazi ambayo haikujihusisha na tabia potovu ya mwanadamu. Hatua hii ya kazi ilikuwa na uhusiano mdogo na kiini cha usimamizi na haikuwa na uhusiano mkubwa na kazi rasmi ya wokovu wa mwanadamu, na kwa hivyo haikumhitaji Mungu afanyike mwili binafsi ili aweze kuifanya kazi Yake. Kazi inayofanywa na Roho haipo wazi sana na haifahamiki, na ya kutisha sana na haiwezi kufikiwa na mwanadamu; Roho hafai kikamilifu kwa ajili ya kufanya kazi ya wokovu moja kwa moja, na hafai kikamilifu kwa ajili ya kumpa mwanadamu uzima moja kwa moja. Kinachomfaa zaidi mwanadamu ni kuibadilisha kazi ya Roho na kuwa katika hali ambayo inamkaribia mwanadamu, yaani, kile kinachomfaa mwanadamu zaidi ni Mungu kuwa mtu wa kawaida ili kufanya kazi Yake. Hili linahitaji Mungu apate mwili ili kuchukua kazi ya Roho, na kwa mwanadamu, hakuna njia nyingine inayofaa zaidi kwa Mungu kufanya kazi. Kati ya hatua hizi tatu za kazi, hatua mbili zinafanywa na mwili, na hatua hizi mbili ni awamu muhimu za kazi ya usimamizi. Kupata mwili mara mbili kunakamilishana na kuafikiana. Hatua ya kwanza ya Mungu mwenye mwili iliweka msingi kwa ajili ya hatua ya pili, na tunaweza kusema kwamba kupata mwili mara mbili kwa Mungu kunaunda kitu kimoja, na zote hazipingani. Hatua hizi mbili za kazi ya Mungu zinafanywa na Mungu katika utambulisho Wake wa mwili kwa sababu zina umuhimu sana katika kazi nzima ya usimamizi. Inaweza kusemwa kuwa, bila kazi ya Mungu mwenye mwili katika hatua hizi mbili, kazi nzima ya usimamizi ingefikia kikomo kwa ghafla, na kazi ya kumwokoa mwanadamu isingekuwa kitu isipokuwa maneno matupu. Haijalishi kazi hii ni muhimu au si muhimu lakini imejikita katika mahitaji ya mwanadamu, na uhalisi wa upotovu wa mwanadamu, na uzito wa kutotii kwa Shetani na usumbufu wake katika kazi. Yule aliye sahihi ambaye ataifanya kazi hiyo itategemea na asili ya kazi inayofanywa na huyo mfanyakazi, na umuhimu wa kazi hiyo. Inapokuja kwa umuhimu wa kazi hii, kuhusiana na ni mbinu gani ya kazi itumiwe—kazi inayofanywa moja kwa moja na Roho wa Mungu, au kazi inayofanywa na Mungu mwenye mwili, au kazi inayofanywa kupitia mwanadamu—ya kwanza kuondolewa ni kazi inayofanywa kupitia mwanadamu, na kulingana na asili ya kazi, na asili ya kazi ya Roho dhidi ya ile ya mwili, hatimaye inaamuliwa kwamba kazi inayofanywa na mwili ni ya manufaa zaidi kwa mwanadamu kuliko kazi inayofanywa moja kwa moja na Roho, na inakuwa na manufaa zaidi. Hili ni wazo la Mungu wakati wa kuamua kama kazi ifanywe na Roho au ifanywe na mwili. Kuna umuhimu na msingi katika kila hatua ya kazi. Siyo fikra tu zisizo na msingi, na wala hazifanywi kiholela; kuna hekima fulani ndani yake. Huo ndio ukweli wa kazi zote za Mungu. Hasa, kuna mpango wa Mungu zaidi katika kazi kubwa kama hiyo kwa Mungu mwenye mwili mwenyewe kufanya kazi miongoni mwa wanadamu. Na kwa hivyo, hekima ya Mungu na yote Aliyo yanadhihirishwa katika kila tendo, fikira, na wazo Lake katika kufanya kazi; hivi ndivyo Mungu alivyo kwa njia maalum na kwa utaratibu. Fikira hizi na mawazo ya kutatiza ni magumu kwa mwanadamu kuyafikiria, na ni mambo magumu kwa mwanadamu kuyaamini, na, zaidi ya hayo, ni magumu kwa mwanadamu kuyafahamu. Kazi inayofanywa na mwanadamu ni kulingana na kanuni ya jumla, ambayo, kwa mwanadamu, ni ya kuridhisha sana. Hata hivyo ikilinganishwa na kazi ya Mungu, kuna tofauti kubwa sana; ingawa matendo ya Mungu ni makuu na kazi ya Mungu ni ya kiwango cha juu sana, nyuma yake kuna mipango na mipangilio midogo ya uhakika ambayo haiwezi kufikiriwa na mwanadamu. Kila hatua ya kazi Yake sio kulingana na kanuni tu, lakini pia inajumuisha vitu vingi ambavyo haviwezi kusemwa kwa lugha ya kibinadamu, na haya ni mambo ambayo hayaonekani kwa mwanadamu. Bila kujali kama ni kazi ya Roho au kazi ya Mungu mwenye mwili, kila kazi inajumuisha mpango wa kazi Yake. Hafanyi kazi bila kuwa na msingi, na hafanyi kazi isiyokuwa na maana. Roho anapofanya kazi moja kwa moja, ni kwa malengo Yake, na Anapokuwa mwanadamu (ambayo ni sawa na kusema, Anapobadilisha umbo Lake la nje) ili kufanya kazi, hata zaidi ni kwa lengo Lake. Kama sivyo, je, Angebadilisha utambulisho Wake kwa urahisi? Kama sivyo, je, Angekubali kwa urahisi kuwa mtu ambaye anachukuliwa kuwa duni na kuteswa?
Kazi Yake katika mwili ni ya umuhimu mkubwa, ambao umezungumzwa kuhusiana na kazi, na Yule ambaye hatimaye anahitimisha kazi ni Mungu mwenye mwili, na sio Roho. Baadhi ya watu wanaamini kwamba Mungu wakati fulani anaweza kuja duniani na kumtokea mwanadamu, ambapo Atawahukumu wanadamu wote, Akimjaribu mmoja baada ya mwingine bila mtu yeyote kupitwa. Wale wanaofikiri kwa namna hii hawafahamu hatua hii ya kazi ya Mungu mwenye mwili. Mungu hamhukumu mwanadamu mmoja baada ya mwingine, na hamjaribu mwanadamu mmoja baada ya mwingine; kufanya hivyo hakungekuwa kazi ya hukumu. Je, upotovu wa wanadamu wote si ni sawa? Je, kiini cha wanadamu wote hakifanani? Kinachohukumiwa ni kiini cha mwanadamu kilichopotoka, kiini cha mwanadamu kilichopotoshwa na Shetani, na dhambi zote za mwanadamu. Mungu hahukumu makosa madogo madogo ya mwanadamu na yasiyokuwa na umuhimu. Kazi ya hukumu ni ya uwakilishi, na haifanywi mahususi kwa ajili ya mtu fulani. Badala yake, ni kazi ambayo kwayo kundi la watu wanahukumiwa ili kuiwakilisha hukumu ya wanadamu wote. Kwa Yeye mwenyewe kufanya kazi Yake katika kundi la watu, Mungu mwenye mwili anatumia kazi Yake ili kuwakilisha kazi ya wanadamu wote, ambayo inaenea taratibu. Kazi ya hukumu pia iko hivyo. Mungu hahukumu aina fulani ya mtu au kundi fulani la watu, bali Anawahukumu wasio na haki wote miongoni mwa wanadamu—kwa mfano, upinzani wa mwanadamu kwa Mungu, au mwanadamu kutomcha Yeye, au kusababisha usumbufu katika kazi ya Mungu, na kadhalika. Kile kinachohukumiwa ni kiini cha mwanadamu cha kumpinga Mungu, na kazi hii ni kazi ya ushindi ya siku za mwisho. Kazi na neno la Mungu mwenye mwili lililoshuhudiwa na mwanadamu ni kazi ya hukumu mbele ya kiti kikuu cheupe cha enzi wakati wa siku za mwisho, ambacho kilibuniwa na mwanadamu katika kipindi cha siku za nyuma. Kazi ambayo sasa inafanywa na Mungu mwenye mwili ni hukumu yenyewe mbele ya kiti kikuu cheupe cha enzi. Mungu mwenye mwili wa leo ni Yule Mungu anayewahukumu wanadamu wote wakati wa siku za mwisho. Mwili huu na kazi, neno, na tabia yote ya nwili hii ni ukamilifu Wake. Ingawa mawanda ya kazi Yake ni finyu, na hayahusishi moja kwa moja ulimwengu wote, kiini cha kazi ya hukumu ni hukumu ya moja kwa moja kwa wanadamu wote; si kazi inayofanywa kwa ajili ya watu weteule wa Uchina tu, au kwa ajili ya idadi ndogo ya watu. Wakati wa kazi ya Mungu mwenye mwili, ingawa mawanda ya kazi hii hayahusishi ulimwengu mzima, inawakilisha kazi ya ulimwengu mzima na, baada ya kuhitimisha kazi ndani ya mawanda ya mwili Wake, Ataipanua kazi hii mara moja katika ulimwengu mzima, kwa namna ile ile, injili ya Yesu ilivyoenea ulimwengu mzima baada ya kufufuka Kwake na kupaa mbinguni. Bila kujali endapo ni kazi ya Roho au ni kazi ya mwili, ni kazi ambayo inafanywa ndani ya mawanda finyu, lakini ambayo inauwakilisha ulimwengu mzima. Wakati wa siku za mwisho, Mungu anaonekana ili kufanya kazi Yake kwa kutumia utambulisho Wake wa Mungu mwenye mwili, na Mungu mwenye mwili ni Mungu anayemhukumu mwanadamu mbele ya kiti kikuu cheupe cha enzi. Bila kujali endapo ni Roho au mwili, Yule ambaye anafanya kazi ya hukumu ni Mungu anayemhukumu mwanadamu katika siku za mwisho. Hili linafafanuliwa kulingana na kazi Yake, na halifafanuliwa kulingana na mwonekano Wake wa nje au sababu nyinginezo. Ingawa mwanadamu ana dhana kuhusu maneno haya, hakuna anayeweza kukana ukweli wa hukumu ya Mungu mwenye mwili na kuwashinda wanadamu wote. Bila kujali kile mwanadamu anachofikiria juu yake, ukweli ni, baada ya yote, ukweli tu. Hukuna anayeweza kusema kwamba “Kazi imefanywa na Mungu, lakini mwili si Mungu.” Huu ni upuuzi, kwasababu kazi hii haiwezi kufanywa na mtu yeyote isipokuwa Mungu mwenye mwili. Kwa kuwa kazi hii imekwishakamilika, kufuatia kazi hii, kazi ya hukumu ya Mungu kwa mwanadamu haitatokea kwa mara ya pili; Mungu katika kupata mwili Kwake kwa mara ya pili amekwishaikamilisha kazi yote ya usimamizi, na hakutakuwa na hatua ya nne ya kazi ya Mungu. Kwa sababu yule anayehukumiwa ni mwanadamu, mwanadamu ambaye ni wa mwili na ambaye amepotoshwa, na sio roho ya Shetani ambayo inahukumiwa moja kwa moja, kazi ya hukumu haifanywi katika ulimwengu wa kiroho, bali miongoni mwa wanadamu. Hakuna anayefaa zaidi na anayestahili, kuliko Mungu mwenye mwili kwa ajili ya kuhukumu upotovu wa mwili wa mwanadamu. Ikiwa hukumu ingefanywa moja kwa moja na Roho wa Mungu, basi isingekuwa inajumuisha wote. Zaidi ya hayo, kazi kama hiyo ingekuwa ngumu kwa mwanadamu kuikubali, maana Roho hawezi kukutana uso kwa uso na mwanadamu, na kwa sababu hii, matokeo hayawezi kuwa ya haraka, sembuse mwanadamu hangeweza kuona kwa uwazi kabisa tabia ya Mungu isiyokosewa. Shetani anaweza tu kushindwa kabisa ikiwa Mungu mwenye mwili anahukumu upotovu wa mwanadamu. Kuwa sawa na mwanadamu Akiwa na ubinadamu wa kawaida, Mungu mwenye mwili anaweza kumhukumu mwanadamu asiye na haki; hii ni ishara ya utakatifu Wake wa asili na hali Yake ya kutokuwa wa kawaida. Ni Mungu pekee ndiye anayestahili, na Yuko katika nafasi ya kumhukumu mwanadamu, maana Ana ukweli, na haki, na kwa hivyo Ana uwezo wa kumhukumu mwanadamu. Wale ambao hawana ukweli na haki hawafai kuwahukumu wengine. Kama kazi hii ingefanywa na Roho wa Mungu, basi isingekuwa ushindi dhidi ya Shetani. Roho kiasili huwa Ameinuliwa zaidi kuliko viumbe wenye mwili wa kufa, na Roho wa Mungu ni mtakatifu kwa asili, na Anaushinda mwili. Ikiwa Roho angefanya kazi hii moja kwa moja, Asingeweza kuhukumu uasi wote wa mwanadamu, na Asingeweza kufichua hali nzima ya mwanadamu ya kutokuwa na haki. Kwa maana kazi ya hukumu pia inafanywa kupitia dhana za mwanadamu kuhusu Mungu, na mwanadamu hajawahi kuwa na dhana yoyote juu ya Roho, na hivyo Roho hana uwezo wa kufunua hali ya mwanadamu ya kutokuwa na haki, wala Hawezi kuweka wazi kabisa hali hiyo ya kutokuwa na haki. Mungu mwenye mwili ni adui wa wale wote wasiomjua. Kupitia kuhukumu dhana na upinzani wa mwanadamu Kwake, Anafichua uasi wote wa wanadamu. Matokeo ya kazi Yake katika mwili yapo dhahiri zaidi kuliko yale ya kazi ya Roho. Na hivyo, hukumu ya wanadamu wote haifanywi moja kwa moja na Roho, bali ni kazi ya Mungu mwenye mwili. Mungu mwenye mwili anaweza kuonekana na kuguswa na mwanadamu, na Mungu mwenye mwili anaweza kumshinda kabisa mwanadamu. Katika uhusiano wake na Mungu mwenye mwili, mwanadamu huwa anapiga hatua kutoka katika upinzani na kuwa mtiifu, kutoka katika mateso na kukubaliwa, kutoka katika dhana na kuwa na maarifa, na kutoka kwa kukataliwa hadi kupendwa—haya ndiyo matokeo ya kazi ya Mungu mwenye mwili. Mwanadamu anaokolewa tu kwa kukubali hukumu Yake, mwanadamu anakuja tu kumjua hatua kwa hatua kupitia maneno ya kinywa Chake, mwanadamu anashindwa na Yeye wakati wa upinzani wake Kwake, na anapata uzima kutoka Kwake wakati wa kukubali kuadibu Kwake. Hii yote ni kazi ya Mungu mwenye mwili, na sio kazi ya Mungu katika utambulisho Wake kama Roho. Kazi inayofanywa na Mungu mwenye mwili ni kazi kubwa sana, na ni kazi ya kina sana, na sehemu muhimu ya hatua tatu za kazi ya Mungu ni hatua mbili za kazi ya kupata mwili. Upotovu wa kina wa mwanadamu ni kikwazo kikubwa sana katika kazi ya Mungu mwenye mwili. Hasa, kazi inayofanywa kwa watu wa siku za mwisho ni ngumu sana, na mazingira ni ya uadui, na ubora wa tabia ya kila aina ya mwanadamu ni duni sana. Lakini mwishoni mwa kazi hii, bado itapata matokeo mazuri, bila dosari yoyote; haya ni matokeo ya kazi ya mwili, na matokeo haya yanashawishi zaidi kuliko kazi ile ya Roho. Hatua tatu za kazi ya Mungu zitahitimishwa katika mwili, na ni lazima zikamilishwe na Mungu mwenye mwili. Kazi muhimu sana imefanywa katika mwili, na wokovu wa mwanadamu ni lazima ufanywe na Mungu mwenye mwili. Ingawa binadamu wote wanahisi kwamba Mungu katika mwili hahusiani na mwanadamu, kwa kweli mwili huu unahusiana na hatima na uwepo wa wanadamu wote.
Kila hatua ya kazi ya Mungu ni kwa ajili ya wanadamu wote, na inawalenga wanadamu wote. Ingawa ni kazi Yake katika mwili, bado inaelekezwa kwa wanadamu wote; Yeye ni Mungu wa wanadamu wote, na ni Mungu wa viumbe vyote vilivyoumbwa na ambavyo havijaumbwa. Ingawa kazi Yake katika mwili ipo ndani ya mawanda finyu, na lengo la kazi hii pia lina mipaka, kila wakati Anapofanyika mwili ili kufanya kazi Yake, Anachagua walengwa wa kazi Yake ambao ni wawakilishi wakuu; Hachagui kundi la watu walio rahisi na wasiofaa kwa ajili ya kufanya kazi, lakini badala yake Anachagua kama walengwa wa kazi Yake kundi la watu wenye uwezo wa kuwa wawakilishi wa kazi Yake katika mwili. Kundi hili la watu linachaguliwa kwa sababu mawanda ya kazi Yake katika mwili ni finyu, na limeandaliwa mahususi kwa ajili ya kupata mwili Kwake, na limechaguliwa hasa kwa ajili ya kazi Yake katika mwili. Uchaguzi wa Mungu wa walengwa wa kazi Yake si usio na msingi, bali unafanyika kulingana na kanuni: Mlengwa wa kazi anapaswa kuwa na manufaa katika kazi ya Mungu mwenye mwili, na anapaswa kuwa na uwezo wa kuwawakilisha wanadamu wote. Kwa mfano, Wayahudi waliweza kuwawakilisha wanadamu wote katika kupokea wokovu binafsi wa Yesu, na Wachina wanaweza kuwawakilisha wanadamu wote katika kuukubali ushindi binafsi wa Mungu mwenye mwili. Kuna msingi kwa Wayahudi kuwa wawakilishi wa wanadamu wote, na kuna msingi kwa uwakilishi wa Wachina kwa wanadamu wote katika kuukubali ushindi binafsi wa Mungu. Hakuna kinachoonyesha maana ya ukombozi kuliko kazi ya ukombozi iliyofanywa miongoni mwa Wayahudi, na hakuna kinachoonyesha ukamilifu na mafanikio ya kazi ya ushindi kuliko kazi ya ushindi iliyofanywa miongoni mwa Wachina. Kazi na neno la Mungu mwenye mwili vinaonekana kuelekezwa kwa kundi dogo la watu, lakini kwa kweli, kazi Yake miongoni mwa kundi hili dogo ni kazi ya ulimwengu mzima, na neno Lake linaelekezwa kwa wanadamu wote. Baada ya kazi Yake katika mwili kufika mwisho, wale wanaomfuata wataanza kueneza kazi ambayo Ameifanya miongoni mwao. Kitu kizuri zaidi kuhusu kazi Yake katika mwili ni kwamba, Anaweza kuacha maneno na mawaidha sahihi, na mapenzi Yake mahususi kwa ajili ya wanadamu kwa wale wanaomfuata, ili baadaye wafuasi Wake waweze kwa usahihi zaidi na kwa uthabiti zaidi kupitisha kazi Yake yote katika mwili, na mapenzi Yake kwa wanadamu wote, kwa wale wanaoikubali njia hii. Ni kazi ya Mungu mwenye mwili pekee miongoni mwa wanadamu ndiyo inayokamilisha ukweli wa Mungu kuwepo na kuishi pamoja na mwanadamu. Ni kazi hii pekee ndiyo inayotimiza shauku ya mwanadamu kuutazama uso wa Mungu, kushuhudia kazi ya Mungu, na kusikia neno la Mungu. Mungu mwenye mwili Anahitimisha enzi ambapo ni mgongo wa Yehova pekee ndio ulioonekana kwa wanadamu, na pia Anahitimisha enzi ya mwanadamu kuamini katika Mungu asiye dhahiri. Hasa, kazi ya Mungu mwenye mwili wa mwisho inawaleta wanadamu wote katika enzi ambayo ni halisi zaidi, ya kivitendo zaidi na nzuri zaidi. Hahitimishi tu enzi ya sheria na mafundisho ya kidini; la muhimu zaidi, Anamfunulia mwanadamu Mungu ambaye ni halisi na wa kawaida, ambaye ni Mwenye haki na mtakatifu, ambaye Anafungua kazi ya mpango wa usimamizi na kufafanua mafumbo na hatima ya wanadamu, ambaye Aliwaumba wanadamu na kuhitimisha kazi ya usimamizi, na ambaye Amebakia sirini kwa maelfu ya miaka. Anaihitimisha enzi ya Mungu asiye yakini, Anaihitimisha enzi ambayo kwayo wanadamu wote wanatamani kuutafuta uso wa Mungu lakini wanashindwa, Anahitimisha enzi ambayo kwayo wanadamu wote wanamtumikia Shetani, na Anawaongoza wanadamu wote katika enzi mpya kabisa. Haya yote ni matokeo ya kazi ya Mungu mwenye mwili kwa niaba ya Roho wa Mungu. Wakati Mungu anapofanya kazi katika mwili Wake, wale wanaomfuata wanakuwa hawatafuti tena na kupapasa vitu hivyo vinavyoonekana kuwa vipo na ambavyo havipo, na wanaacha kukisia mapenzi ya Mungu asiyeonekana. Mungu anapoeneza kazi Yake katika mwili, wale wanaomfuata wataieneza kazi ambayo Ameifanya katika mwili kwa dini na madhehebu yote, na watazungumza maneno Yake yote katika masikio ya wanadamu wote. Yote yanayosikiwa na wale wanaoipokea injili Yake yatakuwa ni ukweli wa kazi Yake, yatakuwa ni mambo ambayo mwanadamu ameyashuhudia na kuyaona binafsi, na utakuwa ukweli na sio uvumi. Ukweli huu ni ushahidi ambao kupitia huo Anaeneza kazi, na pia ni zana ambazo Anazitumia katika kueneza kazi. Bila uwepo wa ukweli, injili Yake isingeweza kuenea katika nchi zote na maeneo yote; bila ukweli bali tu kwa fikira za mwanadamu, Asingeweza kufanya kazi ya kuushinda ulimwengu wote. Roho hagusiki na mwanadamu, na wala Hawezi kuonekana na mwanadamu, na kazi ya Roho haiwezi kuacha ushahidi au ukweli wowote zaidi wa kazi ya Mungu kwa ajili ya mwanadamu. Mwanadamu kamwe hataweza kuuona uso halisi wa Mungu, na siku zote ataamini katika Mungu asiye yakini ambaye hayupo. Mwanadamu hataweza kuutazama uso wa Mungu, hataweza kusikia maneno yaliyozungumzwa na Mungu moja kwa moja. Mawazo ya mwanadamu, hata hivyo, ni matupu, na hayawezi kuchukua nafasi ya uso halisi wa Mungu; tabia ya asili ya Mungu, na kazi ya Mungu Mwenyewe haiwezi kuigwa na mwanadamu. Mungu wa mbinguni asiyeonekana na kazi Yake inaweza kuletwa tu duniani na Mungu mwenye mwili ambaye binafsi Anafanya kazi Yake miongoni mwa wanadamu. Hii ndiyo njia bora zaidi ya Mungu kuonekana kwa mwanadamu, ambayo kwayo mwanadamu anamwona Mungu na kuujua uso wa kweli wa Mungu, na haiwezi kufanikishwa na Mungu asiyekuwa katika mwili. Baada ya Mungu kufanya kazi Yake hadi hatua hii, kazi Yake tayari imeshafanikiwa kuwa na matokeo mazuri, na imekuwa na mafanikio kamili. Kazi binafsi ya Mungu mwenye mwili tayari imekwishakamilisha asilimia tisini ya kazi ya usimamizi Wake wote. Mwili huu umetoa mwanzo mzuri kwa kazi Yake yote, na muhtasari wa kazi Yake yote, na umetangaza kazi Yake yote, na umefanya ujazo kamili wa mwisho kwa kazi hii yote. Kuanzia sasa, hakutakuwa na Mungu mwingine mwenye mwili kwa ajili ya kufanya hatua ya nne ya kazi ya Mungu, na kamwe hakutakuwa na kazi yoyote ya ajabu ya Mungu mwenye mwili wa tatu.
Kila hatua ya kazi ya Mungu katika mwili inawakilisha kazi Yake ya enzi nzima, na haiwakilishi kipindi fulani kama kazi ya mwanadamu. Na kwa hivyo mwisho wa kazi ya kupata mwili Kwake kwa mara ya mwisho haimaanishi kwamba kazi Yake itakuwa imefikia mwisho kamili, kwa maana kazi Yake katika mwili inawakilisha enzi nzima, na haiwakilishi tu kipindi ambacho Anafanya kazi Yake katika mwili. Ni kwamba tu Anakamilisha kazi Yake ya enzi nzima wakati ambao Yupo katika mwili, na kisha itaenea sehemu zote. Baada ya Mungu mwenye mwili kutimiza huduma Yake, Atakabidhi kazi Yake ya baadaye kwa wale wanaomfuata. Kwa njia hii kazi Yake ya enzi nzima itaendelezwa bila kusitishwa. Kazi ya enzi nzima ya kupata mwili itachukuliwa tu kuwa imekamilika baada ya kuenea ulimwenguni kote. Kazi ya Mungu mwenye mwili huanzisha enzi mpya, na wale wanaoiendeleza kazi Yake ni watu wanaotumiwa na Yeye. Kazi inayofanywa na mwanadamu yote ipo ndani ya huduma ya Mungu mwenye mwili, na haina uwezo wa kwenda zaidi ya mawanda haya. Ikiwa Mungu mwenye mwili haji kufanya kazi Yake, mwanadamu hana uwezo wa kuhitimisha enzi ya zamani, na hana uwezo wa kuikaribisha enzi mpya. Kazi inayofanywa na mwanadamu ipo tu ndani ya wajibu wake ambao unawezekana kibinadamu, na haiwakilishi kazi ya Mungu. Ni Mungu mwenye mwili pekee ndiye anayeweza kuja na kukamilisha kazi ambayo Anapaswa kuifanya, na mbali na Yeye, hakuna anayeweza kuifanya kazi hii badala Yake. Bila shaka, kile Ninachozungumzia ni kuhusiana na kazi ya kufanyika mwili. Huyu Mungu mwenye mwili, kwanza Anatekeleza hatua ya kazi ambayo hailingani na dhana za mwanadamu, na kisha Anafanya kazi zaidi ambayo hailingani na dhana za mwanadamu. Lengo la kazi hii ni kumshinda mwanadamu. Kwa upande mmoja, kupata mwili kwa Mungu hakupatani na dhana za mwanadamu, aidha, Anafanya kazi zaidi ambayo haipatani na dhana za mwanadamu, na kwa hivyo mwanadamu anakuza mawazo zaidi ya kukosoa kumhusu. Anafanya kazi ya ushindi miongoni mwa wanadamu ambao wana dhana nyingi sana kumhusu. Bila kujali jinsi wanavyomchukulia, Atakapokuwa amekamilisha huduma Yake, wanadamu wote watakuwa chini ya utawala Wake. Ukweli wa kazi hii hauonekani tu miongoni mwa Wachina, bali unawakilisha pia jinsi ambavyo wanadamu wote watakavyoshindwa. Matokeo yanayoonekana kwa watu hawa ni utangulizi wa matokeo yatakayoonekana kwa wanadamu wote, na matokeo ya kazi Anayofanya wakati ujao yatazidi sana matokeo kwa watu hawa. Kazi ya Mungu katika mwili haihusishi matangazo mengi ya hadharani, wala haijafunikwa gizani. Ni halisi na ya kivitendo, na ni kazi ambayo ni sawa na moja kujumlisha na moja ni sawa sawa na mbili. Haijafichwa kwa mtu yeyote, na wala haimdanganyi mtu yeyote. Kile ambacho watu wanaona ni vitu halisi, na kile ambacho mwanadamu anapata ni ukweli halisi na maarifa. Kazi itakapokamilika, mwanadamu atakuwa na maarifa mapya juu Yake, na wale ambao kweli wanamtafuta Mungu hawatakuwa na dhana zozote juu Yake. Haya siyo tu matokeo ya kazi Yake kwa Wachina, lakini pia inawakilisha matokeo ya kazi Yake katika kuwashinda wanadamu wote, kwa maana hakuna kitu ambacho ni cha manufaa zaidi katika kazi ya kuwashinda watu kuliko mwili huu, na kazi ya mwili huu, na kila kitu cha mwili huu. Vina manufaa katika kazi Yake leo, na vina manufaa katika kazi Yake hapo baadaye. Mwili huu utawashinda wanadamu wote na utawapata wanadamu wote. Hakuna kazi bora zaidi ambayo kwayo wanadamu wote watamwona Mungu, na kumtii Mungu, na kumfahamu Mungu. Kazi inayofanywa na mwanadamu inawakilisha tu mawanda finyu, na Mungu anapofanya kazi Yake hazungumzi na watu fulani, bali Anazungumza na wanadamu wote, na wale wote wanaoikubali kazi Yake. Mwisho Anaoutangaza ni mwisho wa wanadamu wote, na sio mwisho wa mtu fulani tu. Hamtendei mtu yeyote kwa upendeleo maalum, wala Hamwonei mtu yeyote, na Anafanya kazi kwa ajili ya, na Anazungumza na wanadamu wote. Na kwa hiyo huyu Mungu katika mwili Ameshawaainisha wanadamu wote kulingana na aina zao, tayari Ameshawahukumu wanadamu wote, na Ameshapangilia hatima inayofaa kwa wanadamu wote. Ingawa Mungu anafanya kazi Yake Uchina tu, kwa hakika Ameshaamua kazi ya ulimwengu mzima. Hawezi kusubiri hadi kazi Yake itakapoenea miongoni mwa wanadamu wote kabla ya kutoa matamko Yake na kuweka mipango hatua kwa hatua. Je, hio haingekuwa kuchelewa sana? Sasa Anaweza kabisa kukamilisha kazi ya wakati ujao kabla ya wakati huo. Kwa sababu Yule anayefanya kazi ni Mungu mwenye mwili, Anafanya kazi isiyokuwa na mipaka ndani ya mawanda yenye mipaka, na baadaye Atamfanya mwanadamu atekeleze jukumu ambalo mwanadamu anapaswa kulitekeleza; hii ni kanuni ya kazi Yake. Anaweza kuishi tu na mwanadamu kwa muda, na Hawezi kuambatana na mwanadamu hadi kazi ya enzi nzima itakapokamilika. Ni kwa sababu Yeye ni Mungu kwamba Yeye hutabiri kazi Yake ya wakati ujao mapema. Baada ya hapo, Atawaainisha wanadamu wote kulingana na aina kwa maneno Yake, na mwanadamu ataingia katika kazi Yake ya hatua kwa hatua kulingana na maneno Yake. Hakuna atakayekwepa, na wote wanapaswa kutenda kulingana na hili. Hivyo, katika wakati ujao, enzi itaongozwa na maneno Yake, na sio kuongozwa na Roho.
Kazi ya Mungu katika mwili ni lazima ifanywe katika mwili. Kama ingefanywa moja kwa moja na Roho wa Mungu isingeweza kutoa matokeo yoyote. Hata kama ingefanywa na Roho, kazi hii isingekuwa na maana kubwa, na hatimaye isingekuwa na ushawishi. Viumbe vyote vilivyoumbwa vinatamani kujua kama kazi ya Muumba ina maana, na inawakilisha kitu gani, na ni kwa ajili ya nini, na iwapo kazi ya Mungu ina mamlaka kamili na hekima, na endapo ina thamani na maana ya kina. Kazi Anayofanya ni kwa ajili ya wokovu wa wanadamu wote, kwa ajili ya kumshinda Shetani, na kwa ajili ya kutoa ushuhuda kwa Mungu miongoni mwa vitu vyote. Hivyo, kazi Anayoifanya ni lazima iwe na umuhimu mkubwa. Mwili wa mwanadamu umepotoshwa na Shetani, na umepofushwa kwa kina sana, na kujeruhiwa kwa kiasi kikubwa. Sababu muhimu sana ambayo inamfanya Mungu kufanya kazi katika mwili ni kwa sababu mlengwa wa wokovu Wake ni mwanadamu, ambaye ni wa mwili, na kwa sababu Shetani pia anatumia mwili wa mwanadamu kusumbua kazi ya Mungu. Vita na Shetani kwa hakika ni kazi ya kumshinda mwanadamu, na wakati uo huo mwanadamu pia ni mlengwa wa wokovu wa Mungu. Kwa njia hii, kazi ya Mungu mwenye mwili ni muhimu. Shetani aliupotosha mwili wa mwanadamu, na mwanadamu akawa mfano halisi wa Shetani, na akawa mlengwa wa kushindwa na Mungu. Kwa njia hii, kazi ya kupambana na Shetani na kumwokoa mwanadamu inatokea duniani, na Mungu ni lazima awe mwanadamu ili Afanye vita na Shetani. Hii ni kazi ya kivitendo kabisa. Mungu anapofanya kazi katika mwili, kwa hakika Anapambana na Shetani katika mwili. Anapofanya kazi katika mwili, Anafanya kazi Yake katika ulimwengu wa kiroho, na Anafanya kazi Yake yote katika ulimwengu wa kiroho iwe halisi duniani. Anayeshindaniwa ni mwanadamu, asiye mtiifu Kwake, yule anayeshindwa ni mfano halisi wa Shetani (bila shaka, huyu pia ni mwanadamu), ambaye ana uadui na Yeye, na ambaye ataokolewa hatimaye ni mwanadamu. Kwa njia hii, ni muhimu hata zaidi kwa Mungu kuwa mwanadamu ambaye Ana ganda la nje la kiumbe, ili kwamba Aweze kufanya vita halisi na Shetani, Aweze kumshinda mwanadamu, ambaye si mtiifu Kwake, na ambaye ana ganda la nje sawa na Yeye, na kumwokoa mwanadamu, ambaye ana umbo la nje kama Lake na aliyeumizwa na Shetani. Adui Wake ni mwanadamu, mlengwa wa ushindi Wake ni mwanadamu, na mlengwa wa wokovu Wake ni mwanadamu, aliyeumbwa na Yeye. Hivyo ni lazima Awe mwanadamu, na kwa njia hii, kazi Yake inakuwa rahisi zaidi. Ana uwezo wa kumshinda Shetani na kumshinda mwanadamu, na, zaidi ya hayo, Anaweza kuwaokoa wanadamu. Ingawa mwili huu ni wa kawaida na halisi, Yeye si mwili wa kawaida. Yeye si mwili ambao ni mwanadamu tu, bali mwili ambao una ubinadamu na uungu. Hii ndiyo tofauti Yake na mwanadamu, na ni alama ya utambulisho wa Mungu. Ni mwili tu kama huu ndio unaweza kufanya kazi Anayokusudia kufanya, na kutimiza huduma ya Mungu katika mwili, na kukamilisha kazi Yake miongoni mwa wanadamu. Isingekuwa hivyo, kazi Yake miongoni mwa wanadamu ingekuwa tupu na yenye dosari. Ingawa Mungu anaweza kupambana na roho ya Shetani na kuibuka mshindi, asili ya zamani ya mwanadamu aliyepotoka haiwezi kuondolewa, na wale ambao sio watiifu Kwake na wanaompinga hawawezi kamwe kuwa chini ya utawala Wake, ambayo ni kusema, Hataweza kamwe kuwashinda wanadamu, na Hataweza kamwe kuwapata wanadamu wote. Kama kazi Yake duniani haiwezi kutatuliwa, basi usimamizi Wake hautafika mwisho, na wanadamu wote hawataweza kuingia katika pumziko. Kama Mungu hawezi kuingia katika pumziko pamoja na viumbe Wake wote, basi hakutakuwa na matokeo ya usimamizi huo, na utukufu wa Mungu kwa sababu hiyo utatoweka. Ingawa mwili Wake hauna mamlaka, kazi Anayofanya itapata matokeo yake. Huu ndio mwelekeo usioepukika wa kazi Yake. Haijalishi kama mwili Wake una mamlaka au la, maadamu Ana uwezo wa kufanya kazi ya Mungu Mwenyewe, basi Yeye ni Mungu Mwenyewe. Haijalishi mwili huu ni wa kawaida kiasi gani, Anaweza kufanya kazi Anayopaswa kufanya, maana mwili huu ni Mungu na wala si mwanadamu tu. Sababu ambayo mwili huu unaweza kufanya kazi ambayo mwanadamu hawezi kufanya ni kwamba kiini Chake cha ndani si kama cha mwanadamu yeyote yule, na sababu kuwa Anaweza kumwokoa mwanadamu ni kwa sababu utambulisho Wake ni tofauti na wa mwanadamu yeyote yule. Mwili huu ni muhimu sana kwa mwanadamu kwa sababu Yeye ni mwanadamu na, hata zaidi, Yeye ni Mungu, kwa sababu Anaweza kufanya kazi ambayo hakuna mwanadamu wa kawaida anayeweza kuifanya, na kwa sababu Anaweza kumwokoa mwanadamu aliyepotoka, ambaye anaishi pamoja na Yeye duniani. Ingawa Anafanana na mwanadamu, Mungu mwenye mwili ni wa muhimu sana kwa mwanadamu kuliko mtu yeyote wa thamani, kwa maana Anaweza kufanya kazi ambayo haiwezi kufanywa na Roho wa Mungu, Ana uwezo zaidi kuliko Roho wa Mungu kwa kutoa ushuhuda kwa Mungu Mwenyewe, na Ana uwezo zaidi kuliko Roho wa Mungu kwa kuweza kumpata mwanadamu kikamilifu. Kwa sababu hii, ingawa mwili huu ni wa kawaida, mchango Wake kwa wanadamu na umuhimu Wake katika uwepo wa wanadamu unamfanya Awe wa thamani zaidi, na thamani halisi na umuhimu wa mwili huu hauwezi kupimwa na mwanadamu yeyote. Ingawa mwili huu hauwezi kumwangamiza Shetani moja kwa moja, Anaweza kutumia kazi Yake kumshinda mwanadamu na kumshinda Shetani, na kumfanya Shetani atii kikamilifu chini ya utawala Wake. Ni kwa sababu Mungu amepata mwili ndio maana Anaweza kumshinda Shetani na Anaweza kumwokoa binadamu. Hamwangamizi Shetani moja kwa moja, bali Anakuwa mwili ili kuweza kufanya kazi ya kumshinda binadamu, ambaye amepotoshwa na Shetani. Kwa njia hii, Anakuwa na uwezo zaidi wa kutoa ushuhuda Kwake Mwenyewe miongoni mwa viumbe, na Anakuwa na uwezo zaidi wa kumwokoa mwanadamu aliyepotea. Ushindi wa Mungu mwenye mwili dhidi ya Shetani unatoa ushuhuda mkubwa, na una ushawishi mkubwa, kuliko uangamizaji wa Shetani wa moja kwa moja na Roho wa Mungu. Mungu katika mwili Ana uwezo zaidi wa kumsaidia mwanadamu kumjua Muumba, na Ana uwezo zaidi wa kutoa ushuhuda Kwake Mwenyewe miongoni mwa viumbe Vyake vilivyoumbwa.