45. Kurejea Kutoka Ukingoni

Na Zhao Guangming, China

Mwanzoni mwa miaka ya 1980, nilikuwa katika miaka yangu 30 nami nilikuwa nikifanyia kazi kampuni ya ujenzi. Nilijifikira kuwa mchanga na mwenye afya nzuri, niliwatendea watu kwa uaminifu na heshima, nami nilifanya kazi yangu kwa uaminifu. Ujuzi wangu wa ujenzi pia ulikuwa bora sana, nami nilikuwa na hakika kuwa nitafanikiwa zaidi na zaidi kwenye kampuni na kwamba, mara tu kazi yangu itakapoanza, nitakuwa nikiishi kama mwana mfalme. Hili lilikuwa lengo langu na kwa hivyo niliendelea kufanya kazi kwenye kampuni hiyo na kufanya kazi kwa bidii kwa miaka mingi. Lakini licha ya tabia yangu maasumu na ustadi wa kitaalamu, juhudi zangu zilionekana kutotambuliwa na kampuni hiyo, jambo ambalo sikuwahi kulielewa. Daraja la mshahara wa juu katika kampuni yetu lilikuwa daraja la 6, lakini mshahara wangu haukuwahi kupita daraja la 3. Niliwaona wafanyakazi kadhaa, ambao hawakuwa na ujuzi wowote kama wangu wala hawakuwa wamefanya kazi katika kampuni hiyo kwa muda mrefu kama nilivyokuwa nimefanya, wakipata nyongeza za misharaha, lakini haikuwahi kutokea kwangu. Nilikanganyikiwa na kuwa mwenye chuki kuhusu sababu ya wao kupata nyongeza lakini mimi sikupata. Mwishowe, mmoja wa wenzangu ambaye nilielewana naye alinipa shauri: “Katika kampuni hii, jambo la muhimu zaidi ni kumpaka msimamizi mafuta kwa mgongo wa chupa na angalau kumtakia Mwaka Mpya wa Kichina wenye heri, na kufanya vivyo hivyo katika sherehe nyingine.” Baada ya kusikia haya, mwishowe nilielewa sababu halisi ya kupuuzwa na kampuni, na ukosefu wa haki wa jambo hilo ulinikasirisha. Lakini ingawa niliwachukia wale watu waliojipendekeza katika kampuni, na sikuwa na muda wa kupoteza kwa wale ambao walifanya kazi kidogo lakini bado walipata nyongeza ya ujira na kupandishwa vyeo kwa kutumia njia za hila, nilihitaji kufanya msimamo wangu uwe thabiti katika kampuni na kwa hivyo nililazimika kubadilika kufuatana na sheria hizi za mila na desturi. Kwa hivyo Mwaka Mpya wa Kichina uliofuata ulipofika “nilimtakia heri ya dhati” meneja nami nikapandishwa cheo na kuwa kiongozi wa timu mara moja.

Kama kiongozi wa timu, nilianza kuwa mwangalifu sana na mwaminifu hata zaidi katika kazi yangu. Nilienda kwenye maeneo ya ujenzi kusimamia na kudhibiti kazi kwa akali ili kuhakikisha kuwa ilikuwa ikifanywa kufikia kiwango kilichowekwa na kwamba malengo ya mradi yalifikiwa. Pia nilikumbuka usalama wa wafanyakazi wakati wote, na mtazamo wangu wa kazi na mwongozo wa kitaalamu ulisifiwa mahali kote na wafanyakazi katika timu yangu. Lakini hakuna lolote kati ya haya lililokuwa muhimu sana wakati wa kuwahifadhi au kuwapiga kalamu viongozi wa timu—kile kilichokuwa cha muhimu zaidi ni thamani ya zawadi ambazo kila kiongozi wa timu alimpa meneja. Ili kulinda kazi yangu katika kampuni, sikuwa na budi kufuata sheria hii ya kuendelea kudumu, jambo ambalo lilinisababisha nipitie kwa kina ukatili na kutojiweza kulikojumuishwa katika msemo usemao “kuendelea kuishi kwa wenye nguvu.”

Katika miaka iliyofuata, marekebisho ya kiuchumi na kulegezwa kwa vizuio na serikali vilisababisha miradi mikubwa ya maendeleo na ujenzi kuanza kote nchini China. Kwa hivyo kampuni yangu ilianza kutengea watu binafsi miradi, jambo ambalo lilimaanisha kwamba viongozi wa timu walipaswa kushindania kandarasi. Hii ilisababisha kula na kunywa mvinyo na kupeana zawadi hata zaidi, huku kila kiongozi wa timu akijaribu kuwashinda wengine. Wakati wowote ambapo sisi viongozi wa timu tulisikia kwamba kitengo fulani cha kazi kilikuwa na mradi wa zabuni, tulishindania kurahisisha mambo kwa kuwapa wahusika katika kitengo hicho zawadi zetu haraka iwezekanavyo. Ili kuepuka kukosea walichopenda viongozi wa vitengo hivi, tulipiga bongo zetu ili kufikiria zawadi bora na njia bora za kuwapa: Watu wengine waliweka dhahabu ndani ya matumbo ya samaki au kuku; wengine walitoa pesa; wengine walitoa vito vya dhahabu au pete za almasi. Pia mimi nilinaswa katika utamaduni huu wa kutoa hongo na nilitumia saa nyingi nikifikiria zawadi za kuwapa ili kujipendekeza kwa rairai kwa watu hawa. Mwishowe, nilishinda kandarasi kwa ugumu mwingi sana, lakini mara tu tulipoanza kufanya kazi, maofisa kutoka Ofisi ya Ujenzi, Taasisi ya Usanifu wa Ujenzi, na Ofisi za Ubora na Usimamizi wa Ufundi—pamoja na makada wa mtaa—wote walikuja “kusimamia na kudhibiti kazi hiyo.” Walisema kulikuwa na tatizo hili au lile kwenye eneo, kwamba kitu hiki au kile hakikufikia kiwango kilichofaa, na baada ya ukaguzi uliofanyika asubuhi nzima bado hatukuweza kuanza kazi. Niliwaalika wote mara moja kwenye chakula cha mchana cha kilevi kwenye hoteli ya daraja la juu, ​​mlo ambao ulinigharimu maelfu ya yuani. Na mwishoni mwa mlo, bado nililazimika kumpa rushwa kila mmoja wao, iliyoanzia yuani 2000 hadi yuani 10,000. Ilikuwa njia pekee ya kupata idhini na kibali chao ili kazi ianze. Lakini hata baada ya kazi kuanza mawakala hawa wa usimamizi bado walituma wakaguzi wakague mradi huo kila wakati. Waliita ukaguzi huu “utaratibu” lakini kwa kweli ulikuwa kisingizio kingine cha kuminya pesa zaidi kutoka kwetu. Kila walipotufanyia heshima ya kuwepo kwao kwenye eneo la kazi, niliharakisha potepote nikishughulika, nikitayarisha chakula na vinywaji ili kuwaburudisha, na wakurugenzi hawa wa usimamizi wa uajenti hata walitafuta sababu za kunifanya niende nao kwenye maduka makubwa ambapo walinunua nguo za bei ghali na kutarajia nilipie gharama. Wakati mwingine walikuwa hata na ujasiri wa kutosha wa kusema kuwa hawakuwa na fedha na kuniomba pesa za kutumia moja kwa moja. Ili kuendeleza mradi, nilisaga tu meno yangu, kumezea hasira yangu, kuwa mzuri kwao, na kustahimili tu dhihaka. Jambo baya hata zaidi ni kwamba nililazimika kuandamana na wakurugenzi wa uajenti kule nje ya mji kwa muda mrefu. Kwa sababu ya kunywa pombe kupita kiasi kwa muda mrefu na kuwa na mpangilio wa kulala usio wa kawaida, niliishia kupata matatizo ya tumbo na shinikizo la damu, nami nilihisi kuchoka kabisa. Na kwa hivyo, hatimaye mradi ulipokamilika na nikawa nimelipwa, niligundua kuwa nilikuwa nimechuma pesa kidogo sana. Kwa kweli ningeweza kulia. Nikiwa nimekabiliwa na hali ngumu ya maisha, niliwaza moyoni: “Kwa nini ni vigumu sana kwangu kupata pesa kwa kutegemea ujuzi na bidii yangu? Kwa nini viongozi wa kila idara katika mfumo wa kitaifa ni wafisadi sana?” Nilihisi kutojiweza kabisa, lakini sikuwa na chaguo lingine ila kuweka matumaini yangu yote ya kupata pesa kwa maofisa hawa. Hapo awali nilikuwa nimefikiria kwamba kuanzisha na kuendeleza uhusiano mzuri nao kungemaanisha pia kujenga misingi ya kukuza kazi yangu, na haikuwahi kunijia akilini kwamba yote niliyokuwa nikifanya ilikuwa ni kuzama zaidi ndani ya shimo la kinamasi la dhambi na kupitia kwa shida katika hali ya kutokuwa na tumaini.

Mnamo mwaka wa 1992, baada ya mchakato changamani na mgumu, nilishinda kandarasi ya mradi wa ujenzi jijini, nami nilikadiria kuwa mradi huo ungenipatia pesa kiasi fulani. Nilipokuwa tu nikitia bidii kwa shauku katika maandalizi ya kuanza kazi, meneja wangu aliniambia kuwa kwanza nilihitajika kumjengea kila mmoja wa maafisa 4 wa jiji nyumba ya shamba ya kibinafsi yenye bustani kubwa. Alisema kuwa hii ilikuwa fursa nzuri kuhusiana na kukua kwa kazi yangu, na kwamba kuwatendea wema maafisa wa jiji kungenihakikishia kuwa kamwe singekuwa na wasiwasi kuhusu pesa katika siku zijazo na hivi karibuni ningeishi maisha mazuri. Huku nikiwa na moyo uliojaa matumaini, nilichukua mkopo kutoka kwa benki na pia nikakopa pesa kutoka kwa marafiki na familia, nikikusanya pesa hizo kwa njia zozote zilizowezekana, ili kupata mtaji wa kutosha wa kujenga nyumba 4 zenye bustani kubwa. Lakini wakati tu ambapo kazi ya ujenzi ilikuwa ikikaribia kukamilika, maofisa kadhaa wakuu kutoka Tume ya Ukaguzi wa Nidhamu walikuja, nami nililazimika kutumia pesa nyingi zaidi ili kurahisisha mambo na kuwalinda maofisa wale wanne wa jiji. Lakini mwishowe, juhudi zangu zote hazikuweza kuwalinda kutokana na mkono mrefu wa sheria: Kwa sababu maafisa hao wanne walishukiwa kupokea rushwa na kuhusika na ufisadi, walishughulikiwa na viongozi wa ukaguzi. Mipango yangu iliyopangwa vizuri na kwa uangalifu iliambulia patupu, na zile nyumba 4 za shamba zenye bustani ambazo hazikuwa zimekamilika zilichukuliwa ngawira na serikali. Nilikuwa na deni kiasi cha yuani elfu mia kadhaa ambacho sikuwa na njia ya kulipa, na uchungu usioweza kuelezeka ulikaa tumboni mwangu kama mwamba mzito.

Katika hali yangu ya kutojiweza, niliweza tu kuweka matumaini yangu kwenye mradi mwingine wa ujenzi. Ili kulipa madeni yangu nilianza kufanya jambo ambalo sikuwahi kufanya katika kazi yangu yote, jambo ambalo sikutaka kabisa kufanya—kutumia njia za mkato na kutumia vifaa duni. Badala ya kutumia chuma cha kiwango cha kitaifa nilianza kutumia vitu vya daraja la 2, na badala ya vifungu vya fito 6 kwenye saruji nilianza kutumia vifungu vya fito 4, na hivyo kupunguza gharama yangu ya chuma kwa theluthi moja. Pia nilichanganya saruji duni ili kupunguza zaidi gharama zangu za jumla. Kusema ukweli, kila wakati nilipofanya hivi niliogopa sana kwa sababu nilihofu kwamba ubora wa ujenzi uliomalizika ungeathirika sana. Nami niliposikia ripoti za majengo yaliyojengwa shaghalabaghala kote Uchina ambayo yalikuwa yameanguka na kuwaua, kuwajeruhi na kuwafilisisha raia wengi wa kawaida, nilikuwa na wasiwasi zaidi na mara nyingi nilikuwa na majinamizi. Ilifikia hata kiwango ambacho sauti ya ngurumo ilikuwa kama tangazo la maangamizi yangu yaliyokaribia, labda kwa kupigwa na umeme au tukio lingine. Hofu ilininyemelea kila siku. Hali hii ilinifanya niugue mwishowe, na nilisumbuliwa na kizunguzungu, maumivu ya kichwa, na kukosa usingizi mara kwa mara, yote yakisababishwa na shinikizo la damu. Nilikuwa nimetambarika kimwili na kiroho, na maisha yakawa yenye mateso. Hivi ndivyo nilivyojizamisha katika mienendo ya kidunia na kuzama zaidi kabisa ndani ya shimo la dhambi la kinamasi. Jambo la kushangaza ni kwamba, mradi huo ulipokuwa umekamilika nusu, kitengo nilichokuwa nikikijengea kilikataa kunilipa kama tulivyokuwa tumeafikiana kwenye kandarasi. Mkopo niliokuwa nimepewa kutoka kwenye benki haukutosha kutosheleza ujira wa wafanyikazi, kwa hivyo sikuwa na budi kuchukua mkopo wa riba ya juu kutoka kwa mla riba. Baada ya vipingamizi vingi zaidi, mwishowe niligundua kuwa kitengo kilichokuwa kimenipa kandarasi kilikuwa na deni kwa muda mrefu na hakikuwa na namna ya kugharamia mradi wa ujenzi. Mradi wangu mwingine kati ya miradi yangu ilikuwa imefeli, nami nikafikiria sana mbinu ya kurekebisha hali hiyo. Nilikuwa nimechoka kabisa nami nilikuwa nikiishi katika hali ya kukata tamaa. Kisha nilisikia habari kuwa kiongozi wa timu katika kampuni nyingine ambaye alikuwa ameshinda mradi wa ujenzi alikuwa amechukua mkopo mkubwa sana na hakuweza kuulipa, na kwa hivyo alikuwa ameishia kujitia kitanzi. Nilihisi kana kwamba nilikuwa pia nimesimama kwenye lango la kuzimu na kwamba nilikuwa nikizama katika hali ya kukata tamaa. Baada ya hapo, wakopeshaji walianza kuja nyumbani kwangu ili warudishiwe pesa zao: Wengine wao walilala kitandani mwangu na wakakataa kuondoka, huku wengine wakileta fujo na kunitishia. Nilikuwa mpole na mnyenyekevu kadiri nilivyoweza, nami nilihisi kufedheheshwa kabisa. Hata marafiki na jamaa zangu wa karibu sana walidhani kwamba sikuweza kuwalipa na wakaanza kunichukia. Ilikuwa katika siku hizo ndipo nilipata kufahamu kwa kweli jinsi uhusiano wa binadamu unavyoweza kubadilika badilika. Nilikumbuka miaka hiyo yote ya kuwa na shughuli nyingi ambazo hazikuniacha tu nikiwa hohehahe lakini pia ilikuwa imeniacha nikiwa mchovu sana kimwili na kiakili, na nikiwa na madeni ya yuani elfu mia kadhaa ya kulipa. Niliangalia angani na kushusha pumzi ndefu na kusema, “Mbingu, hali hii ni ngumu sana. Kwa kweli sitaki kuishi tena!”

Nilipokuwa tu nikiyumbayumba kwenye lango la kuzimu, injili ya ufalme ya Mwenyezi Mungu ilifika masikioni mwangu. Niliona maneno haya ya Mwenyezi Mungu: “Leo, sababu Nimewaongoza hadi hapa, Nimefanya mipango ya kufaa, na Nina malengo Yangu Mwenyewe. Ningewaeleza kuyahusu leo, mngeweza kweli kuyajua? Nayajua vizuri mawazo ya akili ya mwanadamu na matakwa ya moyo wa mwanadamu: Nani hajawahi kutafuta njia ya kujitoa mwenyewe? Nani hajawahi fikiria matarajio yake mwenyewe? Lakini hata kama mwanadamu ana akili tajiri na wa mche nani aliweza kutabiri kwamba, kufuatia enzi, sasa kungekuwa kulivyo? Hili kweli ni tunda la juhudi zako binafsi? Haya ni malipo ya kazi yako ya bidii? Hii ndiyo picha nzuri iliyoonwa na akili yako? Nisingewaongoza wanadamu wote, nani angeweza kujitenga na mipango Yangu na kupata njia nyingine ya kutoka? Ni fikira akilini mwa mwanadamu na tamaa yake ambayo yamemleta hadi leo? Watu wengi wanaishi maisha yao yote bila kutimiziwa kwa matakwa yao. Kweli hili ni kwa sababu ya kosa katika fikira zao? Maisha ya watu wengi yamejawa na furaha na ridhaa isiyotarajiwa. Kweli ni kwa sababu wanatarajia kidogo sana? Je, nani kati ya wanadamu wote hatunzwi mbele ya macho ya Mwenyezi? Nani haishi maisha kati ya majaaliwa ya Mwenyezi? Je, kuishi kwa mwanadamu kifo chake kinatokana na uchaguzi wake mwenyewe? Je, mwanadamu anadhibiti hatima yake?(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Maneno ya Mungu kwa Ulimwengu Mzima, Sura ya 11). Nilipoyasoma maneno haya, nilisadiki kabisa. Nilihisi kwa kweli kwamba kudura zetu hazimo mikononi mwetu. Nilikumbuka miaka iliyopita, kuhusu jinsi nilivyokuwa nimepanga na kuazimia maisha yangu mwenyewe ya baadaye, lakini hakuna kitu ambacho kilikuwa kimefanikiwa. Nilikuwa nimefanya juu chini ili kuchuma pesa nyingi na kuishi maisha bora, lakini sikuwa nimekosa tu kuchuma pesa zozote, lakini pia nilikuwa nimepoteza pesa nyingi sana. Sikuwahi kufikiri hata mara moja kuwa mimi—ambaye hapo zamani nilikuwa mtu anayejulikana—ningeishia katika hali ya kusikitisha ya umasikini. Kwa nini nilikuwa nimefanya kazi kwa bidii sana kwa ajili ya maisha yangu ya baadaye na bado nilikuwa nimekabiliwa na hali moja ya kutofaulu baada ya nyingine? Ilikuwa kwa sababu hatima ya kila mtu haimo mikononi mwake bali imo mikononi mwa Mungu. Kila kitu kimetawaliwa na kuamuliwa kabla na Mungu; bahati nzuri au bahati mbaya zote husimamiwa na Mungu. Niliweza kuhisi kwa dhati kuwa haya yalikuwa maneno ya Mungu, nami sikuweza kujizuia kumlilia Mwenyezi Mungu: “Ee Mungu! Hapo zamani sikukujua. Nilijaribu kujitegemea na kutegemea nguvu za mwanadamu lakini niliishia katika hali isiyo na matumaini. Leo, nimeelewa hatimaye kuwa kudura, na maisha na kifo, cha kila mtu kiko mikononi Mwako. Hali hii isingenifika, nisingekuja mbele Yako. Ee Mungu! Nakushukuru kwa kuniokoa kutokana na kuwa karibu kabisa na kufa na kwa kunipa ujasiri wa kukabili maisha upya. Kuanzia sasa na kuendelea, nitaitii mipango Yako inayohusu njia ya maisha ninayopaswa kufuata.”

Baada ya hapo, nilianza kuishi maisha ya kanisa. Mazingira katika Kanisa la Mwenyezi Mungu yalikuwa tofauti kabisa na yale ya ulimwengu wa nje: Ndugu walikuwa na uhusiano rahisi na wa wazi baina yao, na walitendeana kwa uaminifu bila ishara yoyote ya kujifanya, mashindao makali au kupanga njama. Kila mtu alisoma maneno ya Mungu na kuimba nyimbo za kumsifu Mungu pamoja; kwenye mikusanyiko, ndugu walikuwa waaminifu na wazi mmoja kwa mwenzake, walifanya ushirika juu ya uzoefu, kasoro na shida zao wenyewe, pamoja na kuhusu ufahamu wao na maarifa kuhusu maneno ya Mungu. Nilihisi kuwa kila mkutano ambao nilihudhuria ulikuwa safi, mpya, na uliojaa uchangamfu. Hakukuwa na utengano au shaka kati ya ndugu; kila mtu alimwelewa mwingine na walijuana vizuri. Nilihisi hali ya faraja na uhuru usio na kifani huko nami nilihisi burudani na furaha zaidi kuliko nilivyowahi kuhisi hapo awali. Wakati huo huo, Mungu alinielekeza kuelewa kwa nini nilikuwa nimeishi katika mateso kama hayo katika miongo michache iliyopita. Nilisoma maneno haya ya Mwenyezi Mungu: “Kunayo siri kubwa moyoni mwako, ambayo hujawahi kuifahamu kamwe, kwa sababu umekuwa ukiishi katika ulimwengu bila mwanga. Moyo wako na roho yako vimepokonywa na yule mwovu. Macho yako yamezuiwa kwa giza yasione, na huwezi kuliona jua angani wala nyota ikimetameta wakati wa usiku. Masikio yako yamezibwa na maneno ya udanganyifu, na husikii sauti ya Yehova ingurumayo kama radi, wala sauti ya maji yakitiririka kutoka katika kiti cha enzi. Umepoteza kila kitu ambacho kilipaswa kuwa chako kwa haki, kila kitu ambacho Mwenye uweza alikupa. Umeingia katika bahari ya mateso isiyokuwa na mwisho, bila nguvu ya kukuokoa, bila matumaini ya kurudi ukiwa hai, na yote unayofanya ni kupambana na kusonga kila siku.… Tokea wakati huo, hungeweza kuepuka kuteswa na yule mwovu, uliwekwa mbali na baraka za mwenye Uweza, mbali na kukimu kwa mwenye Uweza, unatembea katika njia ambayo huwezi kurejea nyuma tena. Kuitwa mara milioni hakuwezi kusisimua moyo wako na roho yako. Unalala fofofo mikononi mwa yule mwovu, ambaye amekushawishi katika ulimwengu usio na mipaka, bila mwelekeo na bila alama za barabarani. Tokea hapo, umepoteza hali yako ya asili ya kutokuwa na hatia na utakatifu wako, na kuanza kujificha kutokana na utunzaji wa mwenye Uweza. Ndani ya moyo wako, yule mwovu anakuelekeza katika kila jambo na anakuwa uhai wako. Humwogopi tena, kumwepuka, au kumshuku; badala yake, unamchukulia kama Mungu aliye moyoni mwako. Unaanza kumtukuza na kumwabudu, na nyinyi wawili mnakuwa msiotengana kama mwili na kivuli chake, kila akitoa nafsi yake kwa mwingine katika uzima na mauti. Hujui lolote kabisa kuhusu mahali ulikotoka, kwa nini ulizaliwa, au kwa nini utakufa(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kutanafusi kwa Mwenye Uweza). “Shetani huwapotosha watu kwa kupitia masomo na ushawishi wa serikali za kitaifa na walio mashuhuri na wakuu. Upuuzi wao umekuwa uzima wa mwanadamu na asili. ‘Kila mtu kivyake na ibilisi achukue ya nyuma kabisa’ ni msemo wa kishetani unaojulikana sana ambao umeingizwa ndani ya kila mtu na umekuwa maisha ya watu. Kuna maneno mengine ya falsafa ya kuishi ambayo pia ni kama haya. Shetani hutumia utamaduni mzuri wa kila taifa kuwaelimisha watu, akisababisha wanadamu kuanguka ndani na kumezwa na lindi kuu lisilo na mipaka la uharibifu, na mwishowe watu wanaangamizwa na Mungu kwa sababu wanamtumikia Shetani na kumpinga Mungu(“Jinsi ya Kujua Asili ya Mwanadamu” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Kwa hivyo sababuya mimi kujichosha na kujitaabisha sana kwa kujipa shughuli nyingi katika ulimwengu huu kwa miongo michache iliyopita ni kuwa nilikuwa nikiishi kulingana na sheria za Shetani za maisha, kama vile, “Kudura ya mtu imo mkononi mwake mwenyewe,” “Pesa ni muhimu sana ulimwenguni,” “Mbingu huwaangamiza wale ambao hawajiwakilishi,” “Mtu hafanikishi chochote bila kubembeleza na kujipendekeza,” na kadhalika. Kwa kuishi kulingana na falsafa hizi za kishetani, sikujua kuhusu kuweko kwa Mungu, na sikuwa nimejua kuwa Mungu hutawala na kupanga kudura ya kila mtu. Nilikuwa nimefuata mkondo wa ulimwengu huu wa giza, bila mwelekeo wowote maishani mwangu au kanuni za maadili mema. Bila shaka sikuweza kuona kwamba ulimwengu huu wa giza unatawaliwa na Shetani, na kwamba jamii ya binadamu imejaa majaribu, mitego na udanganyifu wa Shetani. Ili kupata pesa katika ulimwengu huu wenye giza na ulio mbaya, nilijifunza jinsi ya kuwafurahisha na kujipendekeza kwa rairai kwa wale waliokuwa na madaraka na hata nilikuwa nimetumia vifaa duni kwa siri kwenye miradi yangu ya ujenzi. Dhamiri yangu ilikuwa imepotea polepole, na niliachwa bila uadilifu au hadhi hata kidogo. Kadiri nilivyozidi kuzama ndani kabisa katika dhambi ndivyo nilivyozidi kutohisi kama mwanadamu. Mwishowe, sikupata pesa zozote nami nilisalia na rundo la deni, na nilihisi kukata tamaa sana kiasi kwamba karibu nijitie kitanzi. Nilifikiri kuhusu yule kiongozi wa timu ambaye alikuwa amejiua kwa sababu ya madeni yake makubwa—si alikuwa sadaka ya tambiko kwa Shetani? Na ni nani ajuaye ni misiba mingapi kama hiyo hutokea kila siku ya kila mwaka? Wakati huo niligundua kuwa sababu ya watu kuingia katika hali kama hii ni kwa sababu ya madhara yanayosababishwa na sumu za Shetani, na kwa sababu ya mienendo wa ulimwengu ambayo huelekezwa na utawala wa Shetani. Nilipofikiria kuhusu haya yote, nilijawa na shukrani nyingi sana kwa Mungu nami nilishukuru sana kwa ajili ya rehema na wokovu wa Mungu. Mungu alikuwa Ameniokoa kutoka kwenye ulimwengu wenye giza na kunirudisha nyumbani kwa Mungu ambapo ningeweza kufurahia utunzaji na ulinzi Wake.

Baada ya kipindi cha muda, nililazimika tena kukabiliana na wakopeshaji wangu, na moyo wangu ulikuwa katika msukosuko mkubwa. Nilipofikiria kuhusu madeni yote ambayo bado nilihitajika kuyalipa, nilitaka tena kuchukua miradi ya ujenzi. Hata hivyo, nilijua kwamba uwezo wangu haukulingana na malengo yangu. Tatizo langu la shinikizo la damu liliibuka tena, nami sikujua la kufanya hata kidogo. Katika mojawapo ya mikutano, mmoja wa ndugu alinisomea baadhi ya maneno ya Mungu: “Imani ya kweli katika Mungu ina maana kupitia maneno na kazi ya Mungu kwa msingi wa imani kuwa Mungu ndiye mkuu juu ya vitu vyote. Kwa hivyo mtawekwa huru kutokana na tabia yenu ya upotovu, mtatimiza hamu ya Mungu, na mtapata kumjua Mungu. Ni kwa kupitia safari ya aina hii tu ndio mnaweza kusemekana kuwa mnaamini katika Mungu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Dibaji). Kisha ndugu huyoakatoa ushirika, akisema, “Kwa kuwa tunamwamini Mungu basi tunapaswa kuwa na imani ya kweli katika Mungu. Lazima tuamini kwa dhati katika mamlaka na uwezo wa Mungu ili tuwe na mamlaka juu ya vitu vyote, nasi tunapaswa kumkabidhi Mungu kila kitu maishani mwetu. Jambo la muhimu zaidi, tunapaswa kujifunza kumtegemea Mungu, kumtumainia Mungu, kupitia kazi ya Mungu, kutafuta uongozi wa Mungu, na tusiharakishe tena tukijishughulisha huku tukifikiri kwamba tunaweza kufanya yote sisi wenyewe. Kulipa madeni ni kitu ambacho watu wote wenye busara na waangalifu hufanya, kwa hiyo lazima tuwe na ujasiri na kukabili madeni yetu. Lazima tuamini kuwa kila kitu kiko mikononi mwa Mungu, na kwamba hakuna mlima wowote ambao hatuwezi kuupanda. Kuhusiana na madeni yako, unapaswa kumwomba Mungu zaidi na kutafuta mapenzi Yake.”

Kupitia msaada wa ndugu huyo, sasa nilikuwa na njia ya kutenda. Nilipata kazi kwenye eneo la ujenzi lililokuwa karibu ambayo haikuzuia kuhudhuria kwangu mikutano au kutimiza wajibu wangu, nami nilianza kupata kiasi fulani cha pesa za kulipa madeni yangu. Sikujitegemea tu tena ili kufanikiwa. Wakopeshaji wangu waliponijia kwa ajili ya pesa, nilijizoeza kuwa mwaminifu kwao na kuwapa chochote nilichokuwa nacho. Pia niliweza kulipa pesa kidogo kutoka kwa kile nilichokuwa nikichuma kwa kuuza mazao niliyovuna kutoka kwa shamba langu. Nilitoa ahadi ya dhati kwa wakopeshaji wangu wote kwamba nitalipa madeni yangu yote, na baada ya hapo hawakufanya maisha yawe magumu kwangu tena. Benki ilipowatuma watu wanishawishi nilipe mkopo, nilimwomba Mungu na nikamwaminia yote. “Ikiwa nitalazimika kutumikia kifungo gerezani kwa sababu siwezi kulipa mkopo huo mkubwa,” nilifikiri, “nitatii mipango yote na utaratibu wa Mungu.” Ni wakati ambapo nilimtii Mungu huku nikipitia kazi Yake ndipo nilipoona jinsi matendo Yake yanavyoweza kuwa ya kustaajabisha, kwani nilimuona Akinifungulia njia ya kuelekea mbele. Serikali ilitangaza kuwa mikopo yote ya benki iliyochukuliwa kabla ya mwaka wa 1993 haikuhitajika kulipwa, kwa sababu hakuna yoyote kati ya mikopo hiyo iliyowekwa kwenye mifumo ya tarakilishi ya benki na kuwepo kwa taarifa pungufu kulimaanisha kuwa baadhi ya mikopo haingeweza kuwahi kulipwa. Shukrani ziwe kwa Mungu! Mikopo yangu yote ilichukuliwa kabla ya mwaka wa 1993 na kwa hiyo deni langu la yuani elfu mia kadhaa lilifutwa. Huku nikiwa nimesisimuka, nilitoa shukrani na sifa zangu kwa Mungu. Nilifikiri: “Kama ningelazimika kuchuma kiasi hicho labda ningekufa kwa uchovu kabla ya kuchuma pesa zote.” Jambo hili lilinisababisha nione binafsi kuwa kwa kweli hatima ya kila mtu iko mikononi mwa Mungu, kama inavyoelezwa katika maneno haya ya Mungu: “Majaliwa ya mwanadamu yanadhibitiwa na mikono ya Mungu. Wewe huna uwezo wa kujidhibiti mwenyewe: Licha ya mwanadamu yeye mwenyewe daima kukimbilia na kujishughulisha, anabakia bila uwezo wa kujidhibiti. Kama ungejua matarajio yako mwenyewe, kama ungeweza kudhibiti majaliwa yako mwenyewe, ingekuwa wewe bado ni kiumbe? Kwa kifupi, bila kujali jinsi Mungu hufanya kazi, kazi yote yake ni kwa ajili ya mwanadamu. Chukua, kwa mfano, mbingu na nchi na vitu vyote ambavyo Mungu aliviumba ili kumhudumia mwanadamu: mwezi, jua, na nyota ambazo Yeye alimuumbia mwanadamu, wanyama na mimea, majira ya machipuko, majira ya joto, vuli na baridi, na kadhalika—yote yametengenezwa kwa ajili ya kuwepo kwa mwanadamu. Na kwa hivyo, bila kujali ni jinsi gani anavyoadibu na kuhukumu mwanadamu, yote ni kwa ajili ya wokovu wa mwanadamu. Japokuwa yeye humnyang’anya mwanadamu matumaini yake ya kimwili, ni kwa ajili ya kumtakasa mwanadamu, na utakaso wa mwanadamu ni kwa ajili ya kuishi kwake. Hatima ya mwanadamu iko mikononi mwa Muumba, hivyo ni jinsi gani mwanadamu anaweza kujidhibiti mwenyewe?(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kurejesha Maisha ya Kawaida ya Mwanadamu na Kumpeleka Kwenye Hatima ya Ajabu).

Wakati wa matukio yangu, nilikuwa na hakika hata zaidi kuhusu kazi ya Mwenyezi Mungu na imani yangu ikaimarishwa. Katika miaka iliyofuata, niliendelea kwenda mikutanoni na kutimiza wajibu wangu huku pia nikifanya kazi katika timu za mtaa za ujenzi ili kuchuma pesa za kulipa madeni yangu yaliyosalia. Kila nilipokutana na mtu mwenye tabia nzuri ambaye alikuwa mgombea mzuri wa kusikia injili, nilimhubiria, nami niliwaleta baadhi ya watu niliokuwa na uhusiano mzuri nao mbele za Mungu. Ingawa bado nilikuwa na shughuli nyingi kila siku, maisha yalikuwa tofauti kwa sababu sikuishi tena kulingana na falsafa na sheria za Shetani, nami sikufuata tena mienendo mibaya ya dunia na nilitafuta kuifanya iwe bora na kuishi mtindo bora wa maisha. Badala yake, niliishi chini kwa kutii utawala wa Mungu na kulingana na matakwa Yake, nikienenda kulingana na ukweli, kuwa mwaminifu na mwema, nikimcha Mungu na kuepuka uovu. Njia hii ya kutenda ilionekana kuwa wazi na nyofu, nami nilianza kuhisi raha na kujazwa na mwanga kwa ndani. Polepole, nilianza kupata dhamiri na mantiki yangu tena, na maradhi mbalimbali ambayo nilikuwa nikiugua yakaanza kutoweka. Mwaka huu nilitimia umri wa miaka 75, lakini mimi ni mzima kiafya, niko tayari kung’amua na kutenda, na nimelipa madeni yangu yote. Watu wote ambao wananijua vizuri husema kuwa wananistahi na kwamba nina bahati. Lakini najua bila shaka kuwa yote haya ni kwa sababu ya wokovu na wema wa Mwenyezi Mungu. Ni Mwenyezi Mungu aliyeniokoa nilipokuwa karibu kabisa na kufa, Aliyenirudishia maisha yangu katika wakati wangu wa uhitaji, na Aliyenionyesha mwelekeo sahihi kwa ajili ya maisha yangu. Wakati wa matukio haya yote, nilihisi kwa kweli kuwa bila uongozi wa Mungu sisi wanadamu tutadhuriwa na kumezwa na Shetani pasipo kuepuka. Ni Mwenyezi Mungu tu ndiye Anayeweza kuwaokoa watu; ni maneno yaliyoonyeshwa na Mwenyezi Mungu pekee ndiyo yanayoweza kuwaongoza watu kuondokana na utumwa wa dhambi na kutuonyesha jinsi ya kuishi kama wanadamu wa kweli. Ni kwa kuukubali tu ukweli ambao Mwenyezi Mungu ameonyesha na kumtii na kumwabudu Mwenyezi Mungu ndio wanadamu wanaweza kuishi katika furaha ya kweli na kuwa na mustakabali na hatima nzuri ya mwisho!

Iliyotangulia: 44. Nimerudi Nyumbani

Inayofuata: 46. Kurudi Uzimani Kutoka Ukingoni mwa Mauti

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

14. Bwana Ameonekana Mashariki

Na Qiu Zhen, ChinaSiku moja, dadangu mdogo alinipigia simu akisema kwamba alikuwa amerudi kutoka kaskazini na kwamba alikuwa na jambo...

2. Njia ya Utakaso

Na Christopher, UfilipinoJina langu ni Christopher, na mimi ni mchungaji wa kanisa la nyumbani huko Ufilipino. Mnamo mwaka wa 1987,...

12. Fumbo la Utatu Linafichuliwa

Na Jingmo, MalaysiaNilikuwa na bahati katika mwaka wa 1997 kukubali injili ya Bwana Yesu na nilipobatizwa, mchungaji aliomba na kunibatiza...

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp