II. Maneno Juu ya Kazi ya Mungu ya Hukumu katika Siku za Mwisho
51. Katika kazi Yake ya mwisho ya kuhitimisha enzi, tabia ya Mungu ni ya kuadibu na hukumu, ambapo Anafichua yote yasiyo ya haki, ili kuhukumu hadharani watu wote, na kuwakamilisha wale wanaompenda kwa moyo wa kweli. Ni tabia tu kama hii ndiyo ambayo inaweza kufikisha enzi hii mwisho. Siku za mwisho tayari zimewadia. Vitu vyote katika uumbaji vitatenganishwa kulingana na aina yao, na kugawanywa katika makundi tofauti kulingana na asili yao. Huu ni wakati ambapo Mungu Atafichua matokeo na hatima ya binadamu. Ikiwa watu hawatapitia kuadibu na hukumu, basi hakutakuwa na njia ya kufichua uasi wao na udhalimu wao. Ni kwa njia ya kuadibu na hukumu ndipo mwisho wa mambo yote yatafunuliwa. Mwanadamu huonyesha tu ukweli ulio ndani yake anapoadibiwa na kuhukumiwa. Mabaya yataekwa na mabaya, mema na mema, na wanadamu watatenganishwa kulingana na aina. Kupitia kuadibu na hukumu, mwisho wa mambo yote utafichuliwa, ili mabaya yaadhibiwe na mazuri yatunukiwe thawabu, na watu wote watakuwa wakunyenyekea chini ya utawala wa Mungu. Kazi hii yote lazima itimizwe kupitia kuadibu kwa haki na hukumu. Kwa sababu upotovu wa mwanadamu umefikia kilele chake na kutotii kwake kuwa kubaya kupita kiasi, ni tabia ya Mungu tu ya haki, ambayo kimsingi imechangiwa na kuadibu na hukumu na kufichuliwa wakati wa siku za mwisho, inayoweza kumbadilisha na kukamilisha mwanadamu kikamilifu. Ni tabia hii pekee ambayo itafichua maovu na hivyo kuwaadhibu watu wote dhalimu. Kwa hivyo, tabia kama hii imejazwa umuhimu wa enzi, na ufunuo na maonyesho ya tabia yake ni kwa ajili ya kazi ya kila enzi mpya. Mungu hafichui tabia yake kiholela na bila umuhimu. Kwa kudhania kwamba, katika kufichua matokeo ya mwanadamu katika siku za mwisho, Mungu bado angempa mwanadamu huruma na upendo usio na kikomo na kuendelea kuwa na upendo kwake, bila kumweka mwanadamu chini ya hukumu ya haki lakini badala yake kumwonyesha uvumilivu, subira, na msamaha; na kumsamehe mwanadamu haijalishi dhambi zake ni kubwa kiasi gani, bila hukumu yoyote ya haki: ni lini basi usimamizi wote wa Mungu ungefikishwa mwisho? Je, ni wakati gani tabia kama hii ingeweza kuwaongoza watu kwenye hatima inayofaa ya wanadamu? Chukua, kwa mfano, hakimu ambaye daima ni mwenye upendo, mwenye roho safi na mpole. Anawapenda watu bila kujali dhambi wanazozifanya, na ni mwenye upendo na stahamala kwa watu bila kujali hao ni nani. Kisha ni lini ambapo ataweza kufikia uamuzi wa haki? Katika siku za mwisho, ni hukumu ya haki tu inaweza kumtenganisha mwanadamu kulingana na aina yake na kumleta mwanadamu katika ufalme mpya. Kwa njia hii, enzi nzima inafikishwa mwisho kupitia kwa tabia ya Mungu iliyo ya haki ya hukumu na kuadibu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Maono ya Kazi ya Mungu (3)
52. Kabla ya mwanadamu kukombolewa, sumu nyingi za Shetani zilikuwa tayari zimepandwa ndani yake na, baada ya maelfu ya miaka ya kupotoshwa na Shetani, ndani yake ana asili inayompinga Mungu. Kwa hiyo, mwanadamu alipokombolewa, haikuwa chochote zaidi ya kisa cha ukombozi. Yaani, mwanadamu ananunuliwa tena kwa gharama ya juu, lakini asili ya sumu ndani yake haikuwa imeondolewa. Mwanadamu ambaye ni mchafu sana lazima apitie mabadiliko kabla ya kuwa mwenye kustahili kumtumikia Mungu. Kupitia kazi hii ya kuadibu na hukumu, mwanadamu atakuja kujua kikamlifu kiini cha uchafu na upotovu kilicho ndani yake, na ataweza kubadilika kabisa na kutakasika. Ni kwa namna hii tu ndivyo mwanadamu ataweza kustahili kurudi mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Kazi yote ifanywayo siku hii ya leo ni ili mwanadamu afanywe msafi na kubadilika; kupitia hukumu na kuadibiwa na neno, na pia kutakaswa, mwanadamu anaweza kuacha nje upotovu wake na kufanywa safi. Badala ya kuichukua hatua hii ya kazi kuwa ile ya wokovu, itafaa zaidi kusema kuwa ni kazi ya utakaso. Kwa kweli hatua hii ni ile ya ushindi na pia hatua ya pili ya wokovu. Mwanadamu anatwaliwa na Mungu kupitia hukumu na kuadibu na neno; kwa kutumia neno kusafisha, hukumu na kufichua, uchafu wote, fikira, nia, na matumaini ya mtu mwenyewe katika moyo wa mwanadamu zinafuliwa. Ingawa mwanadamu amekombolewa na kusamehewa dhambi zake, hili linachukuliwa kuwa Mungu kutokumbuka makosa ya mwanadamu na kutomtendea mwanadamu kulingana na makosa yake. Hata hivyo, mwanadamu anaishi katika mwili bila kuachiliwa huru kutoka kwa dhambi, na anaweza tu kuendelea kutenda dhambi, akifunua tabia yake potovu ya kishetani bila kukoma. Haya ndiyo maisha ambayo mwanadamu anaishi, mzunguko usiokoma wa dhambi na msamaha. Watu wengi hutenda dhambi mchana kisha wanakiri jioni. Na hivyo, hata ingawa sadaka ya dhambi ni yenye matokeo yanayotarajiwa kwa binadamu milele, haiwezi kumwokoa mwanadamu kutoka dhambini. Ni nusu tu ya kazi ya wokovu ndiyo ambayo imemalizika, kwa kuwa mwanadamu bado anazo tabia potovu. Kwa mfano, wakati ambapo watu walijua kwamba walitoka kwa Moabu, walitoa maneno ya malalamiko, hawakutafuta tena uzima, na wakawa hasi kabisa. Je, hili halionyeshi kwamba bado hawawezi kutii kwa ukamilifu kutawaliwa na Mungu? Je, hii siyo tabia ya kishetani ya upotovu kabisa? Ulipokuwa hupitii kuadibu, mikono yako iliinuliwa juu zaidi ya wengine wote, hata ile ya Yesu. Na ulilia kwa sauti kubwa: “Kuwa mwana mpendwa wa Mungu! Kuwa mwandani wa Mungu! Ni heri tufe kuliko kumtii Shetani! Muasi Shetani wa zamani! Liasi joka kuu jekundu! Acha joka kuu jekundu lianguke kabisa kutoka mamlakani! Acha Mungu atufanye kamili!” Vilio vyako vilikuwa vikubwa zaidi ya wengine. Lakini kisha ukaja wakati wa kuadibu na, mara tena, tabia ya upotovu ya watu ilifichuliwa. Kisha, vilio vyao vikakoma, na hawakuwa tena na azimio. Huu ni upotovu wa mwanadamu; unaingia ndani zaidi kuliko dhambi, ulipandwa na Shetani na umekita mizizi ndani zaidi ya mwanadamu. Sio rahisi kwa mwanadamu kuzifahamu dhambi zake; mwanadamu hawezi kufahamu asili yake iliyokita mizizi. Ni kupitia tu katika hukumu na neno ndipo mabadiliko haya yatatokea. Hapo tu ndipo mwanadamu ataendelea kubadilika kutoka hatua hiyo kuendelea.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (4)
53. Leo Mungu anawahukumu, na kuwaadibu, na kuwashutumu, lakini jueni kwamba shutuma yako ni ili kukufanya kuweza kujijua. Shutuma, laana, hukumu, kuadibu—haya yote ni ili kwamba uweze kujijua, ili tabia yako iweze kubadilika, na, zaidi ya hayo, ili uweze kujua thamani yako, na kutambua kwamba vitendo vyote vya Mungu ni vyenye haki, na kulingana na tabia Yake na mahitaji ya kazi Yake, kwamba Anafanya kazi kulingana na mpango Wake kwa wokovu wa mwanadamu, na kwamba Yeye ndiye Mungu mwenye haki anayempenda mwanadamu, na kumwokoa mwanadamu, na Anayemhukumu na kumwadibu mwanadamu. Kama utajua tu kwamba wewe ni mwenye hadhi ya chini, kwamba umepotoka na hutii, lakini hujui kwamba Mungu angependa kuweka wazi wokovu Wake kupitia kwa hukumu na kuadibu ambako Anafanya ndani yako leo, basi huna njia yoyote ya kupitia haya, isitoshe huwezi kuendelea mbele. Mungu hajaja kuua, au kuangamiza, lakini kuhukumu, kulaani, kuadibu, na kuokoa. Kabla ya kuhitimishwa kwa mpango Wake wa usimamizi wa miaka 6,000—kabla Hajaweka wazi mwisho wa kila aina ya mwanadamu—kazi ya Mungu duniani ni kwa ajili ya wokovu, yote ni ili kuwafanya wale wanaompenda kuwa kamili kabisa, na kuwarejesha katika utawala Wake. Bila kujali jinsi ambavyo Mungu huwaokoa watu, yote hufanywa kwa kuwafanya wajitenge na asili yao ya zamani ya kishetani; yaani, Yeye huwaokoa kwa kuwafanya watafute uzima. Wasipotafuta uzima basi hawatakuwa na njia yoyote ya kukubali wokovu wa Mungu. Wokovu ni kazi ya Mungu Mwenyewe na kutafuta uzima ni kitu ambacho mwanadamu anapaswa kumiliki ili kupokea wokovu. Machoni pa mwanadamu, wokovu ni upendo wa Mungu, na upendo wa Mungu hauwezi kuwa kuadibu, kuhukumu, na kulaani; wokovu lazima uwe na upendo, huruma, na, zaidi ya hayo, maneno ya faraja, na lazima wokovu uwe na baraka zisizo na mipaka kutoka kwa Mungu. Watu husadiki kwamba wakati Mungu anapomwokoa mwanadamu Anafanya hivyo kwa kumgusa kwa baraka na neema Zake, ili kwamba waweze kumpa Mungu mioyo yao. Hivyo ni kusema, Yeye kumgusa mwanadamu ni kumwokoa. Aina hii ya wokovu inafanywa kwa kufanya makubaliano. Pale tu ambapo Mungu atampa yeye mara mia ndipo mwanadamu atatii mbele ya jina la Mungu, na kulenga kuwa na mienendo mizuri mbele ya Mungu na kumletea Yeye utukufu. Haya si mapenzi ya Mungu kwa mwanadamu. Mungu amekuja kufanya kazi duniani ili kuwaokoa wanadamu wapotovu—hakuna uwongo katika hili; la sivyo, kwa hakika Hangekuja kufanya kazi Yake yeye Mwenyewe. Kitambo, mbinu Zake za wokovu zilikuwa kuonyesha upendo na huruma mkuu, kiasi cha kwamba Alijitolea Yake yote kwa Shetani ili naye aweze kuwapata wanadamu wote. Leo haifanani kamwe na kitambo: Wokovu uliopewa leo unatokea wakati wa siku za mwisho, wakati wa uainishaji wa kila mmoja kulingana na aina yake; mbinu za wokovu wako si upendo wala huruma, lakini kuadibu na hukumu ili mwanadamu aweze kuokolewa kabisa. Hivyo basi, kila kitu unachopokea ni kuadibu, hukumu, na kupigwa bila huruma, lakini jua kwamba katika kupigwa huku kusiko na huruma hakuna hata adhabu ndogo zaidi, jua kwamba licha ya namna ambavyo maneno haya yanavyoweza kuwa makali, kile kinachokupata ni maneno machache yanayoonekana kutokuwa na huruma kabisa kwako, na jua kwamba, licha ya namna ambavyo hasira Yangu itakavyokuwa, kile kitakachokujia bado ni maneno ya mafunzo, na sinuii kukudhuru, au kukuua. Je, haya yote ni ukweli, sivyo? Jua kwamba leo, iwe hukumu ya haki au usafishaji na kuadibu kusiko na huruma, yote haya ni kwa ajili ya wokovu. Haijalishi kama leo kila anaainishwa kulingana na aina yake, ama makundi ya wanadamu yanafichuliwa, matamko yote ya Mungu na kazi ni kwa ajili ya kuwaokoa wale wanaompenda Mungu kwa dhati. Kuhukumu kwa haki ni kwa ajili ya kumtakasa mwanadamu, utakasaji usio na huruma ni kwa ajili ya kumsafisha mwanadamu, maneno makali au kuadibu yote ni kwa ajili ya kutakasa, na kwa minajili ya wokovu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mnapaswa Kuweka Pembeni Baraka za Hadhi na Kuelewa Mapenzi ya Mungu ya Kumletea Mwanadamu Wokovu
54. Mungu anafanya kazi ya hukumu na kuadibu ili kwamba mwanadamu amjue, na kwa ajili ya ushuhuda Wake. Bila hukumu Yake juu jya tabia potovu ya mwanadamu, basi mwanadamu hangeweza kujua tabia Yake ya haki isiyoruhusu kosa lolote, na hangeweza kubadili ufahamu Wake wa Mungu kuwa mpya. Kwa ajili ya ushuhuda Wake, na kwa ajili ya usimamizi Wake, Anafanya ukamilifu Wake kuwa wazi kwa kila mtu, hivyo kumwezesha mwanadamu kupata ufahamu wa Mungu, na kubadili tabia yake, na kuwa na ushuhuda mkuu kwa Mungu kupitia kuonekana kwa Mungu hadharani. Mabadiliko ya tabia ya mwanadamu yanafanikishwa kupitia kazi nyingi tofauti za Mungu; bila mabadiliko ya aina hii katika tabia ya mwanadamu, mwanadamu hangeweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu, na hangeweza kuambatana na nia za Mungu. Mabadiliko ya tabia ya mwanadamu yanaashiria kwamba mwanadamu amewekwa huru kutoka kwa utumwa wa Shetani na kutoka kwa ushawishi wa giza, na kwa kweli amekuwa mfano na kielelezo cha kazi ya Mungu, shahidi wa Mungu, na mtu ambaye anaambatana na nia za Mungu. Leo hii, Mungu mwenye mwili Amekuja duniani kufanya kazi Yake, na Anahitaji kwamba mwanadamu apate ufahamu kumhusu, apate kumtii Yeye, na awe na ushuhuda Kwake—mwanadamu anapaswa kujua kazi Yake ya vitendo na ya kawaida, anapaswa kutii maneno Yake yote na kazi ambayo haiambatani na mawazo ya mwanadamu, na anapaswa kuwa na ushuhuda kwa kazi Yake yote anayofanya kumwokoa mwanadamu, na vilevile matendo Yake yote ya kumshinda mwanadamu. Wale walio na ushuhuda kwa Mungu lazima wawe na ufahamu wa Mungu; ni ushuhuda wa aina hii tu ndio ulio sahihi, na wa vitendo, na ni ushuhuda wa aina hii tu ndio unaoweza kumwaibisha Shetani. Mungu anawatumia wale ambao wamepata kumjua kupitia hukumu Yake, kuadibu, na upogoaji, kuwa na ushuhuda Kwake. Yeye huwatumia wale waliopotoshwa na Shetani kumtolea Yeye ushuhuda. Yeye huwatumia wale ambao tabia yao imebadilika, na wale ambao wamepokea baraka Zake, kumtolea ushuhuda. Yeye hamhitaji mwanadamu amsifu kwa kinywa chake, wala hana hitaji lolote la sifa na ushuhuda kutoka kwa aina ya Shetani, ambao hawajaokolewa na Yeye. Ni wale tu wanaomjua Mungu ndio wanaostahili kumtolea Mungu ushuhuda, na ni wale tu ambao tabia zao zimebadilika ndio wanastahili kumshuhudia Mungu, na Mungu hatamruhusu mwanadamu aliletee jina Lake aibu kwa makusudi.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wale Wanaomjua Mungu Pekee Ndio Wanaoweza Kuwa na Ushuhuda Kwa Mungu
55. Kristo wa siku za mwisho hutumia aina mbalimbali za ukweli kumfundisha mwanadamu, kufichua kiini cha mwanadamu, na kuchanganua maneno na matendo ya mwanadamu. Maneno haya yanajumuisha ukweli mbalimbali, kama vile wajibu wa mwanadamu, jinsi mwanadamu anavyopaswa kumtii Mungu, jinsi mwanadamu anavyopaswa kuwa mwaminifu kwa Mungu, jinsi mwanadamu anavyopaswa kuishi kwa kudhihirisha ubinadamu wa kawaida, na vilevile hekima na tabia ya Mungu. Maneno haya yote yanaelekezwa kwa kiini cha mwanadamu na tabia zake potovu. Hasa, maneno yanayofichua jinsi mwanadamu humkataa Mungu yanaelekezwa hata zaidi kwa jinsi mwanadamu alivyo mfano halisi wa Shetani, na nguvu ya adui dhidi ya Mungu. Katika kufanya kazi Yake ya hukumu, Mungu haelezi kwa ukamilifu asili ya mwanadamu kwa maneno machache tu; Anafichua na kupogoa kwa muda mrefu. Mbinu hizi zote tofauti za kufichua, na kupogoa haziwezi kubadilishwa na maneno ya kawaida; badala yake, ukweli ambao mwanadamu hana kabisa hutumiwa kutekeleza kazi hii ya ufichuzi na upogoaji. Ni mbinu kama hizi pekee ndizo zinaweza kuitwa hukumu; ni kupitia kwa hukumu ya aina hii pekee ndiyo mwanadamu anaweza kutiishwa na kushawishiwa kuhusu Mungu, na zaidi ya hayo kupata ufahamu halisi wa Mungu. Kile ambacho kazi ya hukumu humletea mwanadamu ni ufahamu wa uso halisi wa Mungu na ukweli kuhusu uasi wake mwenyewe. Kazi ya hukumu imemwezesha mwanadamu kupata ufahamu zaidi wa nia za Mungu, wa makusudi ya kazi ya Mungu, na wa mafumbo yasiyoweza kueleweka kwa mwanadamu. Pia imemwezesha mwanadamu kuelewa na kujua kiini chake potovu na asili ya upotovu wake, na vilevile kugundua sura yake mbaya. Matokeo haya yote huletwa na kazi ya hukumu, kwa kweli kiini cha kazi hii hasa ni kazi ya kuweka wazi ukweli wa Mungu, njia, na uzima wa Mungu kwa wale wote walio na imani Kwake. Kazi hii ndiyo kazi ya hukumu inayofanywa na Mungu. Usipouchukulia ukweli huu kuwa muhimu na kila mara kufikiria kuuepuka au kutafuta njia nyingine isipokuwa ukweli, basi ninasema kuwa wewe ni mtenda dhambi mkubwa. Iwapo una imani kwa Mungu, lakini hutafuti ukweli au mapenzi ya Mungu, wala hupendi njia inayokuleta karibu na Mungu, basi nakwambia kuwa wewe ni yule anayejaribu kuepuka hukumu, na kwamba wewe ni kibaraka na msaliti anayekikimbia kiti kikuu cheupe cha enzi. Mungu hatawasamehe waasi wowote wanaotoroka machoni Pake. Wanadamu wa aina hii watapokea adhabu kali zaidi. Wale wanaokuja mbele za Mungu ili wahukumiwe, na zaidi ya hayo wametakaswa, wataishi milele katika ufalme wa Mungu. Bila shaka, hili ni jambo ambalo liko katika siku za usoni.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kristo Hufanya Kazi ya Hukumu kwa Ukweli
56. Kazi ya hukumu ni kazi ya Mungu Mwenyewe, kwa hivyo lazima ifanywe na Mungu Mwenyewe kwa kawaida; haiwezi kufanywa na mwanadamu kwa niaba Yake. Kwa sababu hukumu ni kumshinda mwanadamu kupitia ukweli, ni jambo lisilo na shaka kwamba Mungu bado anaonekana kama sura ya mwili kufanya kazi hii miongoni mwa wanadamu. Hiyo ni kumaanisha, wakati wa siku za mwisho, Kristo atautumia ukweli kuwafunza wanadamu duniani kote na kufanya ukweli wote ujulikane kwao. Hii ni kazi ya hukumu ya Mungu. Wengi wana hisia mbaya kuhusu kupata mwili kwa Mungu kwa mara ya pili, kwa maana mwanadamu huona vigumu kuamini ya kwamba Mungu angefanya kazi ya hukumu akiwa na mwili. Hata hivyo, lazima Nikueleze kwamba mara nyingi kazi ya Mungu huzidi sana matarajio ya mwanadamu na ni vigumu kwa mawazo yao kukubali. Kwa maana wanadamu ni mabuu tu kwenye ardhi, ilhali Mungu ni mkuu Anayejaza ulimwengu mzima; mawazo ya mwanadamu ni kama shimo la maji machafu ambayo yanazalisha mabuu peke yake, ilhali kila hatua ya kazi inayoelekezwa na mawazo ya Mungu ni utoneshaji wa hekima ya Mungu. Mwanadamu hutaka kila wakati kushindana na Mungu, ambalo kwalo Nasema ni wazi nani atapata hasara mwishowe. Nawasihi nyote msijichukulie kuwa wa maana zaidi kushinda dhahabu. Ikiwa wengine wanaweza kukubali hukumu ya Mungu, ni kwa nini wewe usiikubali? Ni vipi ambavyo ninyi ni bora zaidi kuliko wengine? Iwapo wengine wanaweza kuinamisha vichwa vyao mbele ya ukweli, ni kwa nini usifanye hivyo pia? Mwelekeo mkuu wa kazi ya Mungu hauwezi kukomeshwa. Hatarudia kazi ya hukumu tena kwa sababu tu ya “mchango” ambao umetoa, na utajawa na majuto mengi kwa kupoteza nafasi nzuri kama hiyo. Usipoyaamini maneno Yangu, basi kingoje tu kiti cheupe kikuu cha enzi kilicho angani kipitishe hukumu juu yako! Lazima ujue kwamba Waisraeli wote walimkataa kwa dharau na kumkana Yesu, ilhali uhakika wa ukombozi wa Yesu kwa wanadamu ulizidi kusambazwa kote ulimwenguni hadi miisho ya dunia. Je, hili silo jambo ambalo Mungu tayari Amelitimiza? Iwapo bado unangoja Yesu aje kukupeleka mbinguni, basi Nasema kuwa wewe ni kipande sugu cha mti mkavu[a]. Yesu hatamkubali mfuasi bandia kama wewe asiye mwaminifu kwa ukweli na anayetafuta baraka pekee. Kinyume chake, Hataonyesha huruma Anapokutupa kwenye ziwa la moto uungue kwa makumi ya maelfu ya miaka.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kristo Hufanya Kazi ya Hukumu kwa Ukweli
Tanbihi:
a. Kipande cha mti mkavu: nahau ya Kichina inayomaanisha “hali isiyo na matumaini.”
57. Mungu hamhukumu mwanadamu mmoja baada ya mwingine, na hamjaribu mwanadamu mmoja baada ya mwingine; kufanya hivyo hakungekuwa kazi ya hukumu. Je, upotovu wa wanadamu wote si ni sawa? Je, kiini cha wanadamu wote hakifanani? Kinachohukumiwa ni kiini cha mwanadamu kilichopotoka, kiini cha mwanadamu kilichopotoshwa na Shetani, na dhambi zote za mwanadamu. Mungu hahukumu makosa madogo madogo ya mwanadamu na yasiyokuwa na umuhimu. Kazi ya hukumu ni ya uwakilishi, na haifanywi mahususi kwa ajili ya mtu fulani. Badala yake, ni kazi ambayo kwayo kundi la watu wanahukumiwa ili kuiwakilisha hukumu ya wanadamu wote. Kwa Yeye mwenyewe kufanya kazi Yake katika kundi la watu, Mungu mwenye mwili anatumia kazi Yake ili kuwakilisha kazi ya wanadamu wote, ambayo inaenea taratibu. Kazi ya hukumu pia iko hivyo. Mungu hahukumu aina fulani ya mtu au kundi fulani la watu, bali Anawahukumu wasio na haki wote miongoni mwa wanadamu—kwa mfano, upinzani wa mwanadamu kwa Mungu, au mwanadamu kutomcha Yeye, au kusababisha usumbufu katika kazi ya Mungu, na kadhalika. Kile kinachohukumiwa ni kiini cha mwanadamu cha kumpinga Mungu, na kazi hii ni kazi ya ushindi ya siku za mwisho. Kazi na neno la Mungu mwenye mwili lililoshuhudiwa na mwanadamu ni kazi ya hukumu mbele ya kiti kikuu cheupe cha enzi wakati wa siku za mwisho, ambacho kilibuniwa na mwanadamu katika kipindi cha siku za nyuma. Kazi ambayo sasa inafanywa na Mungu mwenye mwili ni hukumu yenyewe mbele ya kiti kikuu cheupe cha enzi. Mungu mwenye mwili wa leo ni Yule Mungu anayewahukumu wanadamu wote wakati wa siku za mwisho. Mwili huu na kazi, neno, na tabia yote ya nwili hii ni ukamilifu Wake. Ingawa mawanda ya kazi Yake ni finyu, na hayahusishi moja kwa moja ulimwengu wote, kiini cha kazi ya hukumu ni hukumu ya moja kwa moja kwa wanadamu wote; si kazi inayofanywa kwa ajili ya watu weteule wa Uchina tu, au kwa ajili ya idadi ndogo ya watu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mwanadamu Aliyepotoka Anahitaji Zaidi Wokovu wa Mungu Mwenye Mwili
58. Maneno Ninayonena leo ni kwa ajili ya kuzihukumu dhambi za mwanadamu, kuhukumu udhalimu wa mwanadamu, kulaani uasi wa mwanadamu. Upotovu na udanganyifu wa mwanadamu, maneno na vitendo vya mwanadamu—yote ambayo hayapatani na mapenzi ya Mungu lazima yatapitia hukumu, na uasi wote wa mwanadamu kushutumiwa kama dhambi. Maneno Yake yanahusu kanuni za hukumu; Yeye hutumia hukumu ya udhalimu wa mwanadamu, laana ya uasi wa mwanadamu, na mfichuo wa asili mbaya za mwanadamu ili kudhihirisha tabia Yake mwenyewe yenye haki. Utakatifu ni kielelezo cha tabia Yake yenye haki, na kwa kweli utakatifu wa Mungu ni tabia Yake yenye haki. Tabia zenu potovu ni muktadha wa maneno ya leo—Ninazitumia kunena na kuhukumu, na kutekeleza kazi ya ushindi. Hii pekee ndiyo kazi halisi, na hii pekee inadhihirisha kabisa utakatifu wa Mungu. Ikiwa hakuna dalili ya tabia potovu ndani yako, basi Mungu hatakuhukumu, wala hatakuonyesha tabia Yake yenye haki. Kwa kuwa unayo tabia potovu, Mungu hatakusamehe, na ni kwa njia hii ndiyo utakatifu Wake unaonyeshwa. Mungu angaliona kuwa uchafu na uasi wa mwanadamu vilikuwa vikubwa sana lakini Asinene au kukuhukumu, wala kukuadibu kwa ajili ya udhalimu wako, basi hii ingethibitisha kwamba Yeye si Mungu, kwa maana Asingeichukia dhambi; Angelikuwa mchafu sawasawa na mwanadamu. Leo, ni kwa sababu ya uchafu wako ndiyo Ninakuhukumu, na ni kwa sababu ya upotovu na uasi wako ndiyo Ninakuadibu. Mimi sijivunii nguvu Zangu kwenu au kuwadhulumu kwa makusudi; Ninafanya mambo haya kwa sababu ninyi, ambao mmezaliwa katika nchi hii ya uchafu, mmenajisiwa vikali kwa uchafu. Mmepoteza uadilifu na ubinadamu wenu kabisa na mmekuwa kama nguruwe waliozaliwa katika pembe chafu zaidi za ulimwengu, na kwa hiyo ni kwa sababu ya jambo hili ndiyo mnahukumiwa na kwamba Ninaaachilia ghadhabu Yangu juu yenu. Ni kwa sababu hasa ya hukumu hii ndiyo mmeweza kuona kuwa Mungu ndiye Mungu mwenye haki, na kwamba Mungu ndiye Mungu mtakatifu; ni kwa sababu hasa ya utakatifu Wake na haki Yake ndiyo Anawahukumu na kuachia huru hasira Yake juu yenu. Kwa sababu Anaweza kufichua tabia Yake yenye haki Aonapo uasi wa mwanadamu, na kwa sababu Anaweza kufichua utakatifu Wake anapoona uchafu wa mwanadamu, hii inatosha kuonyesha kuwa Yeye ndiye Mungu Mwenyewe ambaye ni mtakatifu na wa asili, na bado Anaishi katika nchi ya uchafu. Mungu angelikuwa mtu na kufuata mfano wa mwanadamu na kugaagaa na wanadamu katika matope machafu, basi kusingelikuwa na chochote kitakatifu kumhusu, na Asingelikuwa na tabia yenye haki, na kwa hiyo Asingelikuwa na haki ya kuhukumu uovu wa mwanadamu, wala Asingelikuwa na haki ya kutekeleza hukumu ya mwanadamu. Mtu angelimhukumu mtu mwingine, haingekuwa kana kwamba anajipiga kofi usoni? Watu ambao wote ni wachafu kwa kiwango sawa wanastahili vipi kuwahukumu wale ambao ni sawa na wao? Ni Mungu mtakatifu Mwenyewe pekee ndiye Anayeweza kuwahukumu wanadamu wote wachafu. Mwanadamu angewezaje kuhukumu dhambi za mwanadamu? Mwanadamu angewezaje kuona dhambi za mwanadamu, na mwanadamu angewezaje kuwa na sifa za kulaani dhambi hizi? Mungu Asingelikuwa na sifa ya kuzihukumu dhambi za mwanadamu, basi Angewezaje kuwa Mungu mwenye haki Mwenyewe? Tabia potovu za watu zinapofichuliwa, Mungu hunena ili Awahukumu watu, na ni hapo tu ndipo watu wanapoona kuwa Yeye ni mtakatifu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Jinsi Athari za Hatua ya Pili ya Kazi ya Ushindi Zinavyotimizwa
59. Ni kupitia nini ndiyo ukamilishaji wa Mungu kwa mwanadamu hutimizwa? Kupitia tabia Yake yenye haki. Tabia ya Mungu hasa huwa na haki, ghadhabu, uadhama, hukumu, na laana, na ukamilishaji Wake wa mwanadamu hasa ni kupitia hukumu. Watu wengine hawaelewi, na huuliza ni kwa nini Mungu anaweza tu kumfanya mwanadamu kuwa mkamilifu kupitia hukumu na laana. Wao husema, “Kama Mungu angemlaani mwanadamu, si mwanadamu angekufa? Kama Mungu angemhukumu mwanadamu, si mwanadamu angelaaniwa? Basi anawezaje hata hivyo kufanywa mkamilifu?” Hayo ndiyo maneno ya watu wasioijua kazi ya Mungu. Kile ambacho Mungu hulaani ni uasi wa mwanadamu, na kile Anachohukumu ni dhambi za mwanadamu. Ingawa Yeye hunena kwa ukali, na bila kiwango cha hisia hata kidogo, Yeye hufichua yote yaliyo ndani ya mwanadamu, na kupitia maneno haya makali Yeye hufichua kile kilicho muhimu ndani ya mwanadamu, lakini kupitia hukumu kama hiyo, Yeye humpa mwanadamu ufahamu mkubwa wa kiini cha mwili, na hivyo mwanadamu hujitiisha chini ya utii mbele za Mungu. Mwili wa mwanadamu ni wa dhambi, na wa Shetani, ni wa kutotii, na chombo cha kuadibu kwa Mungu—na kwa hiyo, ili kumruhusu mwanadamu kujijua, maneno ya hukumu ya Mungu lazima yamfike na lazima kila aina ya usafishaji itumike; ni wakati huo tu ndiyo kazi ya Mungu inaweza kuwa ya kufaa.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu
60. Mungu hutumia hukumu Yake kumfanya mwanadamu awe mkamilifu, Amekuwa Akimpenda mwanadamu, na kumwokoa mwanadamu—lakini ni kiasi gani kiko ndani ya upendo Wake? Kuna hukumu, uadhama, ghadhabu, na laana. Ingawa Mungu alimlaani mwanadamu katika wakati uliopita, Hakumtupa mwanadamu kabisa ndani ya shimo la kuzimu, lakini Alitumia njia hiyo kuisafisha imani ya mwanadamu; Hakumuua mwanadamu, lakini alitenda ili kumfanya mwanadamu awe mkamilifu. Kiini cha mwili ni kile ambacho ni cha Shetani—Mungu alikisema sahihi kabisa—lakini ukweli unaotekelezwa na Mungu haukamilishwi kufuatana na maneno Yake. Yeye hukulaani ili uweze kumpenda, na ili uweze kujua kiini cha mwili; Yeye hukuadibu ili uweze kuamshwa, kukuruhusu wewe ujue kasoro zilizo ndani yako, na kujua kutostahili kabisa kwa mwanadamu. Hivyo, laana za Mungu, hukumu Yake, na uadhama na ghadhabu Yake—yote ni kwa ajili ya kumfanya mwanadamu awe mkamilifu. Yote ambayo Mungu anafanya leo, na tabia yenye haki ambayo Yeye huifanya kuwa wazi ndani yenu—yote ni kwa ajili ya kumfanya mwanadamu awe mkamilifu, na huo ndio upendo wa Mungu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu
61. Kama Mungu atamhukumu mwanadamu au kumlaani, yote mawili humfanya mwanadamu kuwa mkamilifu: Yote mawili yanafanywa ili kukifanya kamili kile ambacho ni kichafu ndani ya mwanadamu. Kupitia njia hii mwanadamu anasafishwa, na kile ambacho kinakosekana ndani ya mwanadamu kinafanywa kamilifu kupitia maneno na kazi Yake. Kila hatua ya kazi ya Mungu—kama ni maneno makali, au hukumu, au kuadibu—humfanya mwanadamu kuwa mkamilifu, na inafaa kwa uhalisi. Kotekote katika enzi zote Mungu hajawahi kufanya kazi kama hii; leo, Yeye hufanya kazi ndani yenu ili muweze kufahamu hekima Yake. Ingawa mmepitia maumivu fulani ndani yenu, mioyo yenu inajisikia thabiti na kwa amani; ni baraka yenu kuweza kufurahia hatua hii ya kazi ya Mungu. Haijalishi kile mnachoweza kupata katika siku za baadaye, yote mnayoona kuhusu kazi ya Mungu ndani yenu leo ni upendo. Kama mwanadamu hapitii hukumu na kuadibu kwa Mungu, matendo yake na ari daima yatakuwa nje, na tabia yake daima itaendelea kutobadilika. Je, hii inahesabika kama kupatwa na Mungu? Leo, ingawa bado kuna mengi ndani ya mwanadamu ambayo ni yenye kiburi na yenye majivuno, tabia ya mwanadamu ni imara zaidi kuliko awali. Mungu kukushughulikia wewe ni ili kukuokoa, na ingawa unaweza kuhisi maumivu kidogo wakati huo, siku itafika ambapo kutatokea mabadiliko katika tabia yako. Wakati huo, utakumbuka ya nyuma na kuona vile kazi ya Mungu ni ya hekima, na huo utakuwa wakati ambao utaweza kufahamu kwa kweli mapenzi ya Mungu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu
62. Kazi inayofanywa sasa ni kuwafanya watu kumtoroka Shetani, kutoroka babu zao wa kale. Hukumu zote kwa neno zinalenga kufichua tabia potovu ya binadamu na kuwawezesha watu kuelewa kiini cha maisha. Hukumu hizi zinazorudiwa mara kwa mara zote huchoma mioyo ya watu. Kila hukumu inaathiri moja kwa moja hatima yao na inakusudiwa kuumiza mioyo yao ili waweze kuachana na mambo hayo yote na hivyo basi kuja kujua maisha, kuujua ulimwengu huu mchafu, na pia kujua hekima ya Mungu na uweza Wake na kujua mwanadamu huyu aliyepotoshwa na Shetani. Kadiri aina hii ya kuadibu na hukumu inavyozidi, ndivyo moyo wa mwanadamu unavyoweza kujeruhiwa na ndivyo roho yake inavyoweza kuamshwa. Kuziamsha roho za watu hawa waliopotoshwa sana na waliodanganyika sana ndilo lengo la aina hii ya hukumu. Mwanadamu hana roho, yaani, roho yake ilikufa zamani na hajui kwamba kuna Mbingu, hajui kwamba kuna Mungu, na kwa hakika hajui kwamba anahangaika katika shimo la kifo; anaweza kujuaje kwamba anaishi katika kuzimu hii yenye maovu hapa ulimwenguni? Angewezaje kujua kwamba maiti hii yake ambayo imeoza, kwa kupotoshwa na shetani, imeanguka Kuzimuni kwenye kifo? Angewezaje kujua kwamba kila kitu hapa ulimwenguni kimeharibiwa kitambo kiasi cha kutokarabatika na mwanadamu? Na angewezaje kujua kwamba Muumba amekuja duniani leo na anatafuta kikundi cha watu wapotovu ambao Anaweza kuwaokoa? Hata baada ya mwanadamu kupitia kila usafishaji na hukumu inayowezekana, ufahamu wake wa chini unashtuka kwa shida na kwa kweli hauitikii chochote. Binadamu wamezoroteka kweli! Ingawa aina hii ya hukumu ni kama mvua katili ya mawe inyeshayo kutoka mbinguni, ni yenye manufaa makubwa zaidi kwa binadamu. Lau si kwa kuwahukumu watu namna hii, kusingekuwa na matokeo na isingewezekana kabisa kuwaokoa watu kutoka kwenye dimbwi la taabu. Kama isingekuwa kwa kazi hii, ingekuwa vigumu sana kwa watu kutoka Kuzimuni kwa sababu mioyo yao imekufa kitambo na roho zao kukanyagiwa kitambo na Shetani. Kuwaokoa nyinyi ambao mmeanguka kwenye kina kirefu cha uozo kunahitaji kuwaita kwa bidii sana, kuwahukumu kwa bidii sana, na kwa kufanya hivi tu ndipo mioyo hiyo yenu migumu itakapozinduka.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Wale Waliokamilishwa Pekee Ndio Wanaoweza Kuishi Maisha Yenye Maana
63. Unapaswa kujua kwamba Mungu kuwakamilisha, kuwatimiza, na kuwapata wanadamu hakuleti kitu chochote ila panga na maangamizi juu ya miili yao, na na vile vile mateso yasiyokoma, moto mkali, hukumu zisizokuwa na huruma, kuadibu, laana, na majaribu yasiyokuwa na mipaka. Hicho ni kisa cha ndani na ukweli wa kazi ya kumsimamia binadamu. Hata hivyo, vitu hivi vyote vinalengwa kwa mwili wa mwanadamu, na mishale yote ya uhasama bila huruma inaelekezwa kwenye mwili wa mwanadamu (kwa maana mwanadamu hana hatia). Haya yote ni kwa ajili ya utukufu na ushuhuda Wake, na kwa ajili ya usimamizi Wake. Hii ni kwa sababu kazi Yake si kwa ajili ya binadamu tu, bali pia kwa ajili ya mpango wote, na vile vile kutimiza mapenzi Yake ya asili Alipomuumba binadamu. Kwa hiyo, pengine asilimia tisini ya kile ambacho mwanadamu hupitia kinajumuisha mateso na majaribu ya moto, na kuna siku chache sana ambazo ni tamu na zenye furaha au hata hakuna kabisa, ambazo mwili wa mwanadamu umekuwa ukitamani sana. Sembuse mwanadamu kuweza kufurahia nyakati za furaha katika mwili, akishinda nyakati nzuri pamoja na Mungu. Mwili ni mchafu, hivyo kile ambacho mwili wa mwanadamu unakiona au unakifurahia ni kuadibu kwa Mungu tu ambako mwanadamu huona kukiwa kusiko kuzuri, na ni kana kwamba hakuna mantiki ya kawaida. Hii ni kwa sababu Mungu atadhihirisha tabia Yake ya haki, ambayo haipendwi na mwanadamu, haivumilii makosa ya mwanadamu, na huchukia kabisa maadui. Mungu hufichua waziwazi tabia Yake yote kwa njia yoyote inayolazimu, na hivyo Akihitimisha kazi ya vita Vyake na Shetani vya miaka elfu sita—kazi ya wokovu wa binadamu wote na maangamizo ya Shetani wa zamani!
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kusudi la Kuwasimamia Binadamu
64. Je, sasa unaelewa hukumu ni nini na ukweli ni nini? Ikiwa umeelewa, basi Nakusihi ujisalimishe kwa hukumu kwa utii, la sivyo hutapata kamwe fursa ya kusifiwa na Mungu au kupelekwa na Mungu katika ufalme Wake. Wale wanaokubali hukumu pekee yake lakini hawawezi kamwe kutakaswa, yaani, wale wanaotoroka wakati kazi ya hukumu inapoendelea, watachukiwa na kukataliwa na Mungu milele. Dhambi zao ni nyingi zaidi, na za kusikitisha zaidi, kuliko zile za Mafarisayo, kwa maana wamemsaliti Mungu na ni waasi dhidi ya Mungu. Wanadamu wa aina hii wasiostahili hata kufanya huduma watapokea adhabu kali zaidi, aidha adhabu inayodumu milele. Mungu hatamsamehe msaliti yeyote ambaye kwa wakati mmoja alidhihirisha uaminifu kwa Mungu kwa maneno tu ilhali alimsaliti Mungu. Wanadamu kama hao watapata adhabu ya malipo kupitia adhabu ya roho, nafsi, na mwili. Je, huu si ufichuzi wa tabia yenye haki ya Mungu? Je, hili silo kusudi la Mungu katika kumhukumu mwanadamu na kumfichua mwanadamu? Wakati wa hukumu, Mungu huwapeleka wote wanaofanya aina zote za uovu mahali palipojaa roho waovu, Akiacha miili yao ya nyama iharibiwe vile wapendavyo roho hao waovu. Miili yao inatoa harufu mbaya ya maiti, na adhabu kama hiyo ndiyo inayowafaa. Mungu huandika kwenye vitabu vyao vya kumbukumbu kila mojawapo ya dhambi za waumini hawa wanafiki wasio waaminifu, mitume wanafiki, na wafanyakazi bandia; kisha, wakati unapowadia, Anawatupa katikati ya roho wachafu, Akiacha miili yao ichafuliwe na roho hao wachafu wanavyopenda, na matokeo yake ni kwamba hawatawahi kamwe kuzaliwa upya katika miili mipya na hawatauona mwanga kamwe. Wale wanafiki waliotoa huduma wakati mmoja lakini hawawezi kuwa waaminifu mpaka mwisho wanahesabiwa na Mungu miongoni mwa waovu, ili watembee katika baraza la waovu, na kuungana na halaiki ya wasio na mpangilio; mwishowe, Mungu atawaangamiza. Mungu huwatenga na Hawatambui wote ambao hawajawahi kuwa waaminifu kwa Kristo au kuweka juhudi yoyote, na Atawaangamiza wote wakati wa mabadiliko ya enzi. Hawatakuwepo tena duniani, sembuse kupata njia ya kuingia katika ufalme wa Mungu. Wale ambao hawajawahi kuwa wa kweli kwa Mungu lakini wamelazimishwa na hali kumshughulikia Mungu kwa uzembe wanahesabiwa miongoni mwa wale wanaotoa huduma kwa watu wa Mungu. Ni idadi ndogo tu ya wanadamu wa aina hii ndio wanaweza kuendelea kuishi, huku wengi wao wataangamia pamoja na wasiohitimu hata kufanya huduma. Hatimaye, Mungu ataleta kwenye ufalme Wake wale wote walio na mawazo kama Yake, watu na wana wa Mungu na vilevile waliojaaliwa na Mungu kuwa makuhani. Hili ndilo tone Analopata Mungu kutokana na kazi Yake. Na kwa wale wasio katika sehemu zozote zilizotengwa na Mungu, watahesabiwa miongoni mwa wasioamini. Na kwa hakika mnaweza kuwaza jinsi hatima yao itakavyokuwa. Tayari Nimewaambia yote Ninayopaswa kusema; njia mnayochagua itakuwa uamuzi wenu kufanya. Mnachopaswa kuelewa ni hiki: Kazi ya Mungu kamwe haimsubiri mtu yeyote asiyeweza kwenda sambamba na hatua za Mungu, na tabia ya Mungu ya haki haimwonyeshi mwanadamu yeyote huruma.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kristo Hufanya Kazi ya Hukumu kwa Ukweli