Sura ya 43
Labda ni kwa sababu tu ya amri Zangu za utawala ndio watu “wamevutiwa sana” na maneno Yangu. Ikiwa hawangetawaliwa na amri Zangu za utawala, wote wangekuwa wakilia kama simbamarara ambao wametatizwa tu. Kila siku Mimi Huzurura juu ya mawingu, Nikitazama ubinadamu unaoifunika dunia huku wakizungukazunguka, wakizuiliwa na Mimi kwa njia ya amri Zangu za utawala. Kwa njia hii jamii ya binadamu inawekwa kwa hali ya utaratibu, na hivyo Ninadumisha amri Zangu za utawala. Kuanzia wakati huu na kuendelea, wale walio duniani wanapokea kila aina za kuadibu kwa sababu ya amri Zangu za utawala, na kuadibu huku kunapowashukia wanadamu wote husababisha ghasia kubwa na kukimbia kila upande. Wakati huu, mataifa ya dunia yanaangamia mara moja, mipaka kati ya taifa na taifa inaacha kuwepo, mahali hapagawanyiki tena, na hakuna kitu cha kumtenganisha mwanadamu kutoka kwa mwanadamu. Ninaanza kufanya “kazi ya kiitikadi” katikati ya ubinadamu, ili watu waweze kuishi pamoja kwa amani, bila kupigana tena, na, Ninapojenga madaraja na kuanzisha miunganisho kati ya wanadamu, watu wanakuwa na umoja. Nitajaza mbingu na maonyesho ya kazi Yangu, ili kila kitu kilicho chini ya ardhi kisujudu chini ya nguvu Zangu, Nikitekeleza mpango Wangu wa “umoja wa ulimwengu” na kusababisha hili tamanio Langu moja kufaulu, na ili binadamu wasiweze “kuzurura kote” juu ya uso wa dunia lakini wapate hatima ya kufaa bila kuchelewa. Naifikiria jamii ya binadamu kwa kila njia, Nikifanya hilo ili kwamba wanadamu wote waje kuishi katika nchi ya amani na furaha hivi punde, ili siku za maisha yao zisiwe na huzuni na ukiwa tena, na ili mpango Wangu hautakuwa bure duniani. Kwa kuwa mwanadamu yupo pale, Nitalijenga taifa Langu duniani, kwani sehemu ya maonyesho ya utukufu Wangu iko duniani. Juu mbinguni, Nitaiweka miji Yangu kwenye haki na hivyo kufanya kila kitu kiwe kipya juu na chini. Nitaleta yote yaliyopo juu na chini ya mbingu kuwa katika umoja, ili vitu vyote duniani viungane na vyote vilivyo mbinguni. Huu ndio mpango Wangu, ndio Nitakaoutimiza katika enzi ya mwisho—mtu yeyote asiingilie sehemu hii ya kazi Yangu! Kupanua kazi yangu katika nchi za Mataifa ni sehemu ya mwisho ya kazi Yangu duniani. Hakuna anayeweza kuelewa kazi Nitakayoifanya, na hivyo watu wamepumbazwa kabisa. Na kwa sababu Nina shughuli nyingi za kazi Yangu duniani, watu huchukua fursa hiyo “kufanya mzaha.” Ili kuwazuia kuwa watundu sana, Nimewaweka chini ya kuadibu Kwangu kwanza ili wastahamili nidhamu ya ziwa la moto. Hii ni hatua moja katika kazi Yangu, nami Nitatumia uwezo wa ziwa la moto kutimiza kazi hii Yangu, la sivyo haitawezekana kutekeleza kazi Yangu. Nitawafanya wanadamu ulimwenguni kote kutii mbele ya kiti Changu cha enzi, Nikiwagawanya katika makundi mbalimbali kulingana na hukumu Yangu, Nikiwaainisha kulingana na makundi haya, na kuwaainisha zaidi katika jamii zao, ili binadamu wote wakome kuniasi, badala yake waingie katika mpango mzuri na wa taratibu kulingana na makundi ambayo Nimeyataja—mtu yeyote asitembee huku na huko bila kufikiria! Katika ulimwengu wote, Nimefanya kazi mpya; katika ulimwengu wote, binadamu wote hutunduwaa na kupigwa na bumbuwazi kwa kuonekana Kwangu kwa ghafla, upeo wao wa macho ulibubujika kwa namna ambayo haijawahi kutendeka awali kwa ajili ya kuonekana Kwangu wazi. Je, leo haiko hivi hasa?
Nimechukua hatua ya kwanza na kuanzisha sehemu ya kwanza ya kazi Yangu kati ya mataifa yote na watu wote. Sitavuruga mpango wangu wa kuanza upya: Utaratibu wa kazi miongoni mwa nchi za Mataifa umeanzishwa kwa mujibu wa taratibu za kazi Yangu mbinguni. Wakati wanadamu wote wanayainua macho yao ili kuangalia kila ishara na kitendo, huo ndio wakati ambapo Natupa ukungu duniani. Macho ya wanadamu yanafifilizwa mara moja, wasiweze kupata mwelekeo wowote, kama kondoo katika mbuga la jangwa, na, wakati dhoruba kali inapoanza kuvuma, vilio vyao huzamishwa na mvumo wa upepo mkali. Kati ya mawimbi ya upepo, umbo za binadamu zinaweza kuonekana kwa uhafifu, lakini hakuna sauti ya binadamu inaweza kusikika—ingawa wanadamu wanapiga kelele kwa sauti kubwa mno, jitihada hiyo ni bure. Wakati huu, binadamu hulia na kuomboleza kwa sauti kubwa, wakitumaini kwamba mwokozi atashuka ghafla kutoka angani ili kuwaongoza nje ya jangwa lisilo na mipaka. Lakini, haijalishi imani yao ni kubwa kiasi gani, mwokozi habanduki, na matumaini ya mwanadamu yanavunjika: Moto wa imani ambao umewashwa unazimwa kwa dhoruba kutoka jangwani, na mwanadamu analala kifudifudi katika eneo kame na lisilokaa watu, asiweze kamwe kuinua mwenge unaong’aa, na anazirai pasipo hisia…. Ninapotumia nafasi hiyo Nasababisha mahali penye raha kuonekana mbele ya macho ya mwanadamu. Lakini, ingawa moyo wake unaweza kuwa na furaha kupita kiasi, mwili wa mwanadamu ni dhaifu sana kuweza kuitikia, ukilala na kulegea katika kila ncha; hata ingawa anaona matunda mazuri yanayokua katika mahali penye raha, anakosa nguvu ya kuyachuma, kwa sababu “rasilimali za ndani” za mwanadamu zimemalizwa zote mpaka hakuna chochote kilichosalia ndani yake. Mimi Huchukua vitu ambavyo mwanadamu anahitaji na kumpatia, lakini yeye hutabasamu kwa muda mfupi tu, uso wake ukiwa hauna furaha kabisa: Kila sehemu ndogo ya nguvu za binadamu imetoweka isionekane tena, ikitoweka juu ya hewa inayosonga. Kwa sababu hii, uso wa mwanadamu hauonyeshi hisia kabisa, ni mwali mmoja tu wa upendo unaong’aa kutoka katika macho yake mekundu, na upole mkarimu kama ule wa mama akimwangalia mtoto wake. Mara kwa mara, midomo mikavu na iliyopasuka ya mwanadamu hufanya mwendo wa kutetemeka, kana kwamba inakaribia kusema lakini haina nguvu za kufanya hivyo. Nampa mwanadamu maji kidogo, lakini anatikisa kichwa chake tu. Kutokana na vitendo hivi visivyo vya kawaida na visivyotabirika, Ninajifunza kwamba mwanadamu tayari amepoteza matumaini yote katika nafsi yake mwenyewe, na Ananitazama tu kwa mtazamo wa maombi machoni pake, kana kwamba anasihi jambo fulani. Lakini, bila kujua desturi na maadili ya wanadamu, Nastaajabishwa na maonyesho ya uso na matendo ya binadamu. Ni katika wakati huu tu ambapo Ninagundua kwa ghafla kwamba siku za kuwepo kwa mwanadamu zinakaribia mwisho, na Mimi huelekeza macho ya huruma kwake. Na ni wakati huu tu ambapo mwanadamu huonyesha tabasamu la furaha, akinitikisa kichwa, kana kwamba ametimiza kila tamanio lake. Ubinadamu hauna huzuni tena; duniani, watu hawalalamiki tena juu ya utupu wa maisha, na wanaacha kushughulika na “maisha.” Kutoka hapo, hakutakuwa na kuomboleza tena duniani, na siku ambazo wanadamu wataishi zitajawa na furaha …
Nitaziondoa shughuli za binadamu kwa njia inayostahili kabla ya kujishughulisha na kazi Yangu Mwenyewe, binadamu wasije wakaendelea kuingilia kazi Yangu. Shughuli za mwanadamu sio dhamira Yangu kuu, shughuli za wanadamu hazina mpango kabisa. Kwa sababu mwanadamu ni mdogo sana wa roho—inaonekana kwamba ubinadamu hauko tayari kuonyesha huruma hata kwa chungu, au kwamba chungu ni maadui wa wanadamu—kila mara kuna fujo inayoendelea kati ya wanadamu. Nikisikiliza fujo zinazofanywa na wanadamu, Ninaondoka mara nyingine tena na kutozingatia zaidi hadithi zao. Katika macho ya binadamu, Mimi ni “kamati ya wakazi,” Nikiwa mtaalamu katika kusuluhisha “migogoro ya familia” kati ya “wakazi.” Watu wanapokuja mbele Yangu, wao siku zote huja na sababu za kibinafsi na, kwa shauku kubwa, hueleza “uzoefu wao wenyewe usio wa kawaida,” wakiongeza maoni yao wenyewe kadri wanavyoendelea. Naangalia mwenendo wa binadamu usio wa kawaida: Nyuso zao zimefunikwa kwa vumbi—vumbi ambalo, chini ya “umwagiliaji” wa jasho, linapoteza “uhuru” wake linapounda mchanganyiko na jasho kwa haraka, ili nyuso za wanadamu “zirutubishwe” zaidi, kama mchanga pwani kando ya bahari, ambapo nyayo zinaweza kuonekana mara chache. Nywele zao zinafanana na vivuli vya wafu, havina mng’aro, zinazosimama wima kama vipande vya majani yaliyosakama katika mviringo. Kwa sababu hasira yake ni kali sana, hadi amejiingiza katika hasira kali, uso wake hutoa “mvuke” hapa na pale, kama vile “kuvuja” kwa jasho. Nikimchunguza kwa karibu, Naona kwamba uso wa mwanadamu umefunikwa kwa “miale” kama jua kali, ndiyo sababu kuna mawingu ya gesi ya moto inayoinuka kutoka kwake, nami Nina wasiwasi sana kwamba hasira yake inaweza kuuchoma uso wake, ingawa yeye mwenyewe hajali. Kwa wakati huu, Ninamhimiza mwanadamu apunguze hasira yake kidogo, kwani hii ina faida gani? Kwa nini iwe hivi? Kwa sababu ya hasira, mabua ya majani juu ya uso wa “ulimwengu” huu yanateketezwa kivitendo na miale ya jua; katika hali kama hii, hata “mwezi” unageuka kuwa mwekundu. Namsihi mwanadamu apunguze hasira yake—ni muhimu kuilinda afya yake. Lakini mwanadamu hasikilizi ushauri Wangu; badala yake, anaendelea “kutoa malalamiko” Kwangu—ina maana gani? Hakika sio kwamba ukarimu Wangu hautoshi kwa raha ya binadamu? Au kwamba anakataa kile Ninachompa? Kwa hasira ya ghafla, Naigeuza meza, ambapo mwanadamu hathubutu kusimulia tena matukio yoyote ya kusisimua kutoka kwenye hadithi yake na, akiwa na hofu Nisije Nikamwelekeza kwenye “jela” ili kungojea kwa siku chache, anachukua fursa iliyosababishwa na hamaki Yangu ili kuponyoka. La sivyo, mwanadamu hangeweza kuwa tayari kuyaacha mambo kwa muda, lakini angeendelea kuchacharisha kwa kujipigia domo mwenyewe—Nimechoshwa Ninaposikia hivyo. Ni kwa nini binadamu ni wenye utata sana ndani ya mioyo yao? Yawezekana kuwa Nimeweka sehemu nyingi sana za “vipuri” katika umbo la mwanadamu? Kwa nini yeye daima hujifanya mbele Yangu? Hakika si kwamba mimi ni “mwelekezi” wa azimio la “migogoro ya kiraia”? Je, Nilimtaka mwanadamu aje Kwangu? Hakika Mimi si hakimu wa mkoa? Kwa nini mambo kati ya watu daima yanaripotiwa Kwangu? Tumaini Langu ni kwamba mwanadamu ataona haja ya kuchukua jukumu la nafsi yake mwenyewe na kutoniingilia, kwa sababu Nina kazi nyingi sana ya kufanya.
Mei 18, 1992