Ni Nini Maana ya Krismasi, na Je, Unamwabudu Bwana Yesu Kweli?

30/12/2018

Na Siyuan

Yaliyomo
Vyanzo vya Krismasi
Bwana Yesu Alizaliwa Kwa Sababu ya Upendo wa Mungu na Wokovu wa Mwanadamu
Yale Ambayo ni Mapenzi ya Bwana na Matakwa Yake Kwetu
Je, Tunamwabudu Bwana Kweli?
Jinsi ya Kupatana na Mapenzi ya Mungu na Kupata Sifa Zake

Ni Nini Maana ya Krismasi, na Je, Unamwabudu Bwana Yesu Kweli?

(Chanzo: Megapixl)

Vyanzo vya Krismasi

Kila mwaka, Krismasi inapokaribia, maduka kwenye mitaa hutayarisha maonyesho yang’aayo ya zawadi za Krismasi, pamoja na Baba Krismasi na miti ya Krismasi, na kadhalika. Kuna taa nyingi za rangi nyingi zilizoning’inizwa katika miti na kwenye majengo, na miji mizima hupambwa kwa fanusi na mapazia ya rangi nyingi, na kila mahali kuna furaha na msisimko. Kwa Ukristo, Krismasi ni likizo ya pekee sana, na miezi kadhaa kabla ya Krismasi, makanisa mengi yataanza kujishughulisha na kuandaa kila kitu kilicho muhimu kwa likizo ya Krismasi. Katika Siku ya Krismasi, makanisa hujaa, na ndugu hushiriki katika sherehe, wakila chakula rasmi cha Krismasi, kuigiza na kumwabudu Bwana Yesu, na kadhalika. Uso wa kila mtu hujawa na furaha. Hata hivyo, tunapokutana pamoja katika mikusanyiko yenye furaha ili kusherehekea kuzaliwa kwa Bwana Yesu, je, tunaelewa maana ya Krismasi? Pengine ndugu watasema, “Bwana Yesu alisulubiwa msalabani ili kuwakomboa watu wote, na kwa hivyo ili kukumbuka na kusherehekea kuzaliwa kwa Bwana Yesu, Wakristo walianzisha Krismasi. Ingawa siku maalum ambayo Bwana Yesu alizaliwa haijaandikwa katika Biblia, Krismasi hatua kwa hatua ilianza kuwa likizo ya watu wote baada ya upanuzi wa injili ya Yesu Kristo.” Huenda ikawa twalijua hili, lakini je, tunajua upendo wa Mungu na mapenzi Yake kwetu ambayo kwa kweli yalifichwa katika kuzaliwa kwa Bwana Yesu? Na tunapaswaje kukabili Krismasi kwa njia ambayo inaupendeza moyo wa Bwana?

Bwana Yesu Alizaliwa Kwa Sababu ya Upendo wa Mungu na Wokovu wa Mwanadamu

Bwana Yesu Alizaliwa Kwa Sababu ya Upendo wa Mungu na Wokovu wa Mwanadamu

Mwanzoni, Yehova alifanya kazi katika umbo la Roho miongoni mwa wanadamu, Alimtumia Musa kutangaza sheria na amri Zake, Aliwaongoza wanadamu kuhusu jinsi ya kuishi duniani, Aliwaruhusu watu kujua yaliyokuwa mema na yaliyokuwa maovu, namna ya kumwabudu Mungu, na kadhalika. Lakini Enzi ya Sheria ilipokuwa ikifika mwisho wake, kwa sababu wanadamu walikuwa wakipotoshwa na Shetani kwa undani zaidi kuliko wakati wowote mwingine, mwanadamu hakuweza kufuata sheria na hakukuwa tena na sadaka tosha za dhambi ambazo wangeweza kuzitoa ambazo zingelipia dhambi zao; watu walikabiliwa na hatari ya kulaaniwa na kuhukumiwa kifo na sheria wakati wowote. Mungu hakuweza kuvumilia kuwaona wanadamu, ambao Alikuwa amewaumba kwa mikono Yake Mwenyewe, waangamizwe kwa njia kama hiyo. Kwa hivyo, ili kuwaruhusu wanadamu waendelee kuishi, Mungu alishuka kutoka mbinguni na kupata mwili kama Bwana Yesu Kristo, Alionekana na kutekeleza kazi Zake, Alionyesha njia ya “Ninyi tubuni: kwa kuwa ufalme wa mbinguni uko karibu(Mathayo 4: 17), Aliwafundisha watu kuwa na uvumilivu, subira na kuwapenda maadui zao, na kuwasamehe watu mara sabini mara saba. Pia Aliwaponya wagonjwa na kuwatoa pepo, na kufanya ishara na maajabu mengi na, mwishoni, Alisulubiwa msalabani, hivyo kuwaokoa wanadamu kutoka kwa dhambi zao. Ilimradi tumkubali Bwana Yesu kama Mwokozi wetu na kumwomba Bwana kwa kweli, tukikiri dhambi zetu na kutubu, basi dhambi zetu zimesamehewa, na tunaweza kufurahia amani, furaha na wingi wa neema ambayo hutoka kwa Bwana. Inaweza kusemwa kwamba, ni kwa sababu tu Bwana Yesu alizaliwa na Mungu binafsi alipata mwili ili kutenda kazi ya ukombozi, ndiyo wanadamu waliweza kuepuka hukumu na pingu za sheria, na hivyo hawakuwa tena na uelekeo wa kulaaniwa au kuhukumiwa kifo. Kwa sababu tu Bwana Yesu alizaliwa, wale waliomfuata waliweza kufurahia amani na furaha halisi. Hata zaidi, ni kwa sababu tu Bwana Yesu alizaliwa, na Roho wa Mungu akapata mwili wa kawaida, Akitumia lugha ya wanadamu kuyanena maneno Yake, ndiyo tunajua wazi zaidi kutoka kwa maneno ya Bwana mapenzi ya Mungu na mahitaji Yake kwa mwanadamu, tunaweza kuwa na utendaji mpya na wa juu zaidi, na uhusiano wetu na Mungu unaweza kuwa wa karibu zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Lile ambalo lilisababisha kuja kwa Bwana Yesu duniani, kuonyesha Kwake ukweli na kukamilisha kazi ya kusulubiwa, lilijawa na jitihada za Mungu za kuokoa wanadamu—ulikuwa upendo na rehema ya Mungu kwetu sisi wanadamu wapotovu!

Yale Ambayo ni Mapenzi ya Bwana na Matakwa Yake Kwetu

Ingawa, Bwana Yesu alipomaliza kazi ya ukombozi, Alifufuka na kupaa mbinguni, ili kukumbuka kuzaliwa Kwake, watu wengi huandaa karamu za jioni wakati wa Krismasi, wao huigiza na kusherehekea kuzaliwa kwa Bwana Yesu. Lakini je, tumewahi kuwa na ufahamu wa maana ya Krismasi ni nini, na kujua mapenzi na mahitaji ya Bwana Yesu kwetu ni nini? Je, ni nini hasa tunachopaswa kufanya ili kumridhisha Mungu na kupata sifa Zake?

Bwana Yesu alisema, “Saa inakuja, ambayo hamtamwabudu baba katika mlima huu, wala huko Yerusalemu. … Lakini saa inakuja, nayo ni sasa, ambayo waabuduo wa kweli watamwabudu Baba katika roho na kweli: kwa kuwa Baba anawatafuta watu kama hao wamwabudu(Yohana 4:21, 23). Tunaelewa kutoka kwa maneno ya Bwana Yesu kwamba Bwana anatarajia tumwabudu Mungu kwa roho na kwa ukweli, na sio kushika kwa ugumu aina zote za utaratibu au kushiriki katika shughuli. Mafarisayo, wakuu wa makuhani na waandishi hekaluni katika siku za zamani walisisitiza tu kujihusisha katika sherehe mbalimbali za dini na kushikilia sheria. Kila siku, walitoa sadaka ili kumwabudu Mungu, lakini hawakutilia maanani sana kuweka maneno ya Mungu kwenye vitendo, wala hawakufuata amri za Yehova, sana kiasi kwamba hata walitelekeza amri za Mungu na kufuata tu desturi za mwanadamu. Mwishoni, hawakukosa tu kupata sifa ya Mungu, bali pia walichukiwa na kulaaniwa na Bwana Yesu. Makanisa sasa yakifanya maadhimisho makubwa ya Krismasi, ni usitawi wa msisimko wa mara moja tu; kila mtu hukusanyika pamoja kwa shangwe na furaha, lakini kweli hatumwabudu Bwana, au kutumia fursa hii kuelewa mapenzi Yake au kupata kumjua, na hivyo hatutapokea kibali cha Bwana Yesu. Kwa kweli, tangu Bwana Yesu alipoanza kazi Yake rasmi hadi alipomaliza kazi Yake ya ukombozi, Alionyesha ukweli mwingi na kutuwekea mahitaji mengi. Mapenzi ya Bwana ni kutumaini kwamba sote tutasisitiza kuyaweka maneno Yake katika vitendo, na kufuata mafundisho Yake wakati wote, katika maeneo yote, bila kujali masuala au watu ambao huenda tutakutana nao. Hili ndilo ambalo Bwana anataka kutoka kwetu, na ndio kanuni muhimu sana ya utendaji kwa wale wetu ambao tunaamini katika Mungu. Kama Bwana alivyosema: “Mkidumu katika neno langu, basi ninyi ni wanafunzi wangu kweli(Yohana 8:31), “Ninyi ni rafiki zangu, mkifanya chochote ninachowaamuru(Yohana 15:14). Kwa hivyo, inaweza kuonekana kwamba, katika maisha yetu ya kawaida na katika kuwashughulikia watu wengine, ni muhimu sana kusisitiza kutenda kulingana na maneno ya Bwana, kwa maana hiki ni kitu ambacho wale ambao wanaamini katika Mungu na kumwabudu Mungu kwa kweli lazima wakifikie zaidi ya yote.

Je, Tunamwabudu Bwana Kweli?

Je, Tunamwabudu Bwana Kweli?

Sasa, ndugu wengi huja kanisani wakati wa Krismasi kusherehekea kuzaliwa kwa Bwana Yesu, kuomba pamoja, kusoma Biblia pamoja, na kuimba sifa za Bwana pamoja. Lakini wakati mwingine wote, tunajishughulisha na kazi na amaili zetu wenyewe au na kuingiliana na watu wengine. Mara chache sana tunajituliza mbele za Bwana na kuomba na kusoma maneno Yake au kutafuta kuelewa mapenzi Yake. Ndugu wengine mara nyingi huhudhuria mikutano, lakini wao hutenda na kuyapitia maneno ya Bwana kwa nadra sana katika maisha yao, bado wanaishi katika dhambi, na dhambi zao zinakua kwa kasi. Kwa mfano, Bwana Yesu anataka tuwe wanyenyekevu na wapole, lakini tunapopatana na kufanya kazi pamoja na wafanyakazi wenza na pamoja na ndugu katika kanisa, tunatawaliwa na tabia zetu zenye kiburi, tunaona maoni yetu na mawazo yetu kama yaliyo sahihi na tunajitetea, na hatuwezi kuelewana na wengine kwa utulivu. Bwana Yesu anahitaji kwamba tujifunze kuwasamehe wengine na kuwapenda wengine kama tunavyojipenda. Lakini wengine wanapoingilia vitu tunavyovipenda, tunahisi kukerwa, sana hivi kwamba tunaishi ndani ya tabia mbovu za Shetani, na tunawahukumu na kuwalaani watu wengine. Bwana Yesu anataka kwamba tujitenge na watu wa kidunia, lakini katika ufuatiliaji wetu wa sifa ya kidunia, hadhi na anasa za mwili, tunafuata mienendo mibaya ya ulimwengu, tunaishi katika dhambi na tunazidi kuwa mbali zaidi na zaidi na Bwana. Hii ni mifano michache tu ya jinsi ambavyo sisi hushindwa kuishi kulingana na mahitaji ya Bwana. Ingawa sisi husisitiza sana kuendeleza sherehe za dini, na tunasisitiza kuwa na shukrani kwa ajili ya wokovu wa Bwana na tunamsifu Bwana katika siku mahsusi za likizo mbalimbali, lakini hatufuati njia ya Bwana na mara nyingi sisi huishi katika dhambi. Je, hivi ndivyo tunavyomwabudu Bwana Yesu? Je, Bwana anaweza kutusifu kwa ajili ya hili kweli? Chukua kwa mfano wakati ambapo wazazi wanamlea mtoto wao awe mtu mzima. Ikiwa mtoto huyo kwa kweli ni mwenye busara na mwenye kuwapenda wazazi, atatahadhari kujua kile ambacho wazazi wake wanakipenda na kile wasichokipenda, na wakati wowote anapowafanyia wazazi wake chochote, kila mara atajua cha kufanya ili kuwapendeza. Lakini kama chote anachofanya ni kufanya karamu kubwa ya siku za kuzaliwa kwa wazazi wake, na kusema tu, “Ninawapenda, mama na baba!” na wazazi wake wanapomhitaji kwa kweli, yeye hujishughulisha sana na maisha yake kiasi kwamba hawezi kutimiza majukumu yake kwa wazazi, je, anaweza kusemekana kuwa mwenye kuwapenda wazazi wake kweli?

Jinsi ya Kupatana na Mapenzi ya Mungu na Kupata Sifa Zake

Jinsi ya Kupatana na Mapenzi ya Mungu na Kupata Sifa Zake

Ikiwa tunataka kuwa watu ambao kweli wanamwabudu Mungu na kupata sifa Zake, jambo la muhimu ni kutenda kulingana na maneno ya Mungu, kumtukuza Mungu mioyoni mwetu, kusisitiza kufuata njia ya Bwana katika kila kitu, kutilia umuhimu maneno ya Bwana, na kutumia kile tunachoishi kwa kudhihirisha kwa kweli kuwa na ushuhuda kwa Mungu na kumtukuza Mungu. Bila shaka, baadhi ya ndugu hukusanyika pamoja wakati wa Krismasi kuimba nyimbo na kumsifu Bwana, kubadilishana uzoefu wetu na ufahamu wa kuyatenda maneno ya Bwana katika maisha yetu, kuauniana na kusaidiana kutatua masuala katika maisha yetu ya kiroho, na kufunga umbali kati yetu na Mungu, hii pia inapatana na mapenzi ya Mungu. Aidha, Krismasi inapokaribia, sasa kuna nchi nyingi za magharibi ambazo huandaa matukio ya usaidizi kwa ajili ya Wakristo walioteswa na watu wasiokuwa na makao, na ambazo huwakusanya pamoja watu wanaotafuta kimbilio na Wakristo wakimbizi walioteswa kutoka duniani kote ili waweze kubadilishana uzoefu, hivyo kuwawezesha kuhisi ukunjufu wa Mungu katika majira ya baridi kali. Hivi pia ni vitu ambavyo Mungu atavikumbuka. Kwa ufupi, likizo yenyewe si muhimu na sherehe zote mbalimbali si muhimu. Yale ambayo ni muhimu zaidi ni maneno ya Bwana Yesu na mambo anayohitaji kutoka kwetu. Kuweza kuwa na moyo wa kumcha Mungu na kuyatafuta mapenzi ya Bwana katika kila kitu, kutenda maneno ya Bwana na kumridhisha Bwana kwa kukidhi mahitaji Yake—hili ndilo jambo la muhimu zaidi. Ni kwa kutenda tu kwa njia hii ndiyo tunamwabudu Bwana Yesu kwa kweli na kupata sifa Zake.

Shukrani ziwe kwa nuru na mwongozo wa Mungu, na Awe na sisi sote!

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp