Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Kupata Mwili | Dondoo 100

Maisha Aliyoishi Yesu duniani yalikuwa maisha ya kimwili ya kawaida. Aliishi katika ubinadamu wa kawaida wa mwili Wake. Mamlaka Yake—kufanya kazi ya Mungu na kuzungumza neno la Mungu, au kuwaponya wagonjwa au kufukuza mapepo, kufanya hiyo kazi isiyo ya kawaida—hayakujitokeza, kwa kiasi kikubwa, hadi Alipoanza huduma Yake. Maisha Yake kabla ya umri wa miaka ishirini na tisa, kabla ya Yeye kuanza kutekeleza huduma Yake, yalikuwa uthibitisho tosha kuwa Alikuwa mwili wa kawaida. Kwa sababu ya hili, na kwa kuwa Alikuwa bado Hajaanza kutekeleza huduma Yake, watu hawakuona chochote cha uungu ndani Yake, hawakuona chochote zaidi ya ubinadamu wa kawaida, mwanadamu wa kawaida—sawa tu na mwanzoni ambapo baadhi ya watu walimwamini kuwa mwana wa Yosefu. Watu walidhani kuwa Alikuwa mwana wa mwanadamu wa kawaida, hawakuwa na njia ya kugundua kuwa Alikuwa mwili wa Mungu; hata wakati Alipotenda miujiza mingi katika harakati za kutekeleza huduma Yake, watu wengi bado walisema Alikuwa mwana wa Yosefu, kwani Alikuwa Kristo mwenye umbo la nje la ubinadamu wa kawaida. Ubinadamu Wake wa kawaida pamoja na kazi yake vyote vilikuwepo ili kutimiza umuhimu wa kupata mwili kwa mara ya kwanza, kuthibitisha kuwa Mungu Alikuwa Amekuja katika mwili kwa ukamilifu, kuwa mwanadamu wa kawaida kabisa. Kuwa na ubinadamu wa kawaida kabla ya kuanza kazi Yake ulikuwa uthibitisho kuwa Alikuwa mwili wa kawaida; na kwa kuwa Alifanya kazi baadaye lilithibitisha pia kuwa Alikuwa mwili wa kawaida, kwa kuwa Alifanya ishara na miujiza, kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo katika mwili na ubinadamu wa kawaida. Sababu za kufanya miujiza ilikuwa kwamba mwili Wake ulikuwa umebeba mamlaka ya Mungu, ulikuwa mwili ambamo Roho wa Mungu Alikuwa Amesetiriwa. Alikuwa na mamlaka haya kwa sababu ya Roho wa Mungu, na haikumaanishi kuwa Hakuwa Mwili. Kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo ilikuwa kazi Aliyopaswa kutekeleza katika huduma Yake, onyesho la uungu Wake uliojificha ndani ya ubinadamu Wake, na haijalishi ni ishara za aina gani Alionyesha au Alidhihirisha vipi mamlaka Yake, bado Aliishi katika ubinadamu wa kawaida na bado Alikuwa mwili wa kawaida. Aliishi katika mwili wa kawaida mpaka wakati Alipofufuliwa baada ya kufa msalabani. Aliishi katika mwili wa kawaida. Akitoa neema, Akiwaponya wagonjwa, na kufukuza mapepo hayo yote yalikuwa sehemu ya huduma Yake, hiyo yote ilikuwa kazi Aliyotekeleza katika mwili Wake wa kawaida. Kabla ya kwenda msalabani, Hakuuacha mwili Wake wa kawaida, haijalishi Alikuwa Anafanya nini. Alikuwa Mungu Mwenyewe, Akifanya kazi ya Mungu, lakini kwa sababu Alikuwa Mwili wa Mungu, Alikula chakula na kuvaa nguo, Alikuwa na mahitaji ya kawaida ya binadamu, Alikuwa na fikira za kawaida za binadamu na akili za kawaida. Haya yote yalikuwa uthibitisho kwamba Alikuwa mwanadamu wa kawaida, ambayo yalithibitisha kuwa mwili wa Mungu ulikuwa mwili wenye ubinadamu wa kawaida, haukuwa wa rohoni. Kazi Yake ilikuwa kukamilisha kazi ya Mungu kupata mwili mara ya kwanza, kutimiza huduma ya kupata mwili mara ya kwanza. Umuhimu wa kupata mwili ni kwamba mtu wa kawaida Anatekeleza kazi ya Mungu Mwenyewe; yaani, kwamba Mungu Anatekeleza kazi Yake ya uungu katika ubinadamu na hivyo kumshinda Shetani. Kupata mwili kunamaanisha kwamba Roho wa Mungu Anakuwa Mwili, yaani, Mungu Anakuwa mwili; kazi Anayoifanya katika mwili ni kazi ya Roho, inayothibitika katika mwili, na kuonyeshwa kwa mwili. Hakuna mwingine ila tu mwili wa Mungu Anayeweza kutimiza huduma ya Mungu mwenye mwili; yaani, mwili wa Mungu kuwa mwili pekee, ubinadamu huu wa kawaida—na hakuna mwingine yeyote—anayeweza kuonyesha kazi ya uungu. Ikiwa, wakati wa kuja Kwake wa kwanza, Mungu Asingekuwa Amekuwa na ubinadamu wa kawaida kabla ya umri wa miaka ishirini na tisa—ikiwa mara tu Alipozaliwa Angeweza kufanya miujiza, ikiwa mara tu Alipojifunza kuongea Angeweza kuongea lugha ya mbinguni, ikiwa mara tu Alipokanyaga duniani Angeweza kuyaelewa mambo yote ya kidunia, kung’amua fikira za kila mtu na nia zao—basi kamwe Asingeitwa mwanadamu wa kawaida, na mwili Wake usingeitwa mwili wa mwanadamu. Iwapo mambo yangekuwa hivi kwa Kristo, basi maana na kiini cha kuwa mwili kwa Mungu ingepotea. Kuwa Kwake na ubinadamu wa kawaida kunathibitisha kuwa Alikuwa Mungu Aliyejidhihirisha katika mwili; ukweli kwamba Alipitia ukuaji wa kawaida wa binadamu unaonyesha zaidi kuwa Alikuwa mwili wa kawaida; na zaidi, kazi Yake ni uthibitisho tosha kuwa Alikuwa Neno la Mungu, Roho wa Mungu, kuwa mwili. Mungu Anakuwa mwili kwa sababu ya mahitaji ya kazi; kwa maneno mengine, hii hatua ya kazi inapaswa kufanywa kwa mwili, kufanywa katika ubinadamu wa kawaida. Hili ndilo sharti la “Neno kuwa mwili,” la “Neno kuonekana katika mwili,” na ndio ukweli wa Mungu kupata mwili mara Mbili. Watu huenda wakaamini kuwa maisha yote ya Yesu yaliambatana na miujiza, kwamba hadi mwisho wa kazi Yake duniani Hakudhihirisha ubinadamu wa kawaida, kwamba Hakuwa na mahitaji ya kawaida ya mwanadamu au udhaifu au hisia za binadamu, kwamba Hakuhitaji vitu vya kimsingi vya maisha au kuwa na fikira za kawaida za binadamu. Wanadhani kuwa Alikuwa mwanadamu asiyekuwa na akili ya kawaida, aliyevuka mipaka ya ubinadamu. Wanaamini kuwa kwa sababu Yeye ni Mungu, Hapaswi kufikiri na kuishi jinsi wanadamu wa kawaida hufanya, kwamba ni mtu wa kawaida tu, mwanadamu halisi, anayeweza kufikiri fikira za mwanadamu wa kawaida na kuishi maisha ya mwanadamu wa kawaida. Haya yote ni mawazo ya wanadamu na maoni ya wanadamu, ambayo yanakinzana na madhumuni asilia ya kazi ya Mungu. Kufikiri kwa mwanadamu wa kawaida kunadumisha mawazo ya kawaida ya mwanadamu na ubinadamu wa kawaida; ubinadamu wa kawaida unadumisha kazi za kawaida za mwili; na kazi za kawaida za mwili zinawezesha maisha ya kawaida ya mwili katika ukamilifu wake. Ni kwa kufanya kazi tu katika mwili kama huo ndipo Mungu Anaweza kutimiza kusudi la kupata mwili Kwake. Kama Mungu mwenye mwili angekuwa na umbo la nje tu la mwili, bila kufikiri fikira za kawaida za binadamu, basi mwili huu usingekuwa na mawazo ya binadamu, sembuse ubinadamu halisi. Ni vipi ambavyo mwili kama huu, usio na ubinadamu, ungeweza kutimiza huduma ambayo Mungu mwenye mwili Anapaswa kutekeleza? Akili za kawaida huwezesha vipengele vyote vya maisha ya binadamu; bila akili ya kawaida, mtu hawezi kuwa mwanadamu. Kwa maneno mengine, mtu asiyefikiria fikra za kawaida ni mgonjwa wa akili. Na Kristo ambaye Hana ubinadamu ila uungu pekee Hawezi kuitwa mwili wa Mungu. Basi, mwili wa Mungu unawezaje kukosa ubinadamu wa kawaida? Je, si kufuru kusema kwamba Kristo hana ubinadamu? Kila shughuli ambazo wanadamu wa kawaida hufanya hutegemea utendaji kazi wa akili ya kawaida ya mwanadamu. Bila hiyo, wanadamu wangekuwa na mienendo iliyopotoka; wangeshindwa hata kutofautisha kati ya nyeupe na nyeusi, wema na uovu; na hawangekuwa na maadili ya binadamu na kanuni za uadilifu. Vivyo hivyo, iwapo Mungu mwenye mwili Asingefikiri kama mwanadamu wa kawaida, basi Asingekuwa mwili halisi, mwili wa kawaida. Mwili usiofikiri kama huo haungeweza kuikabili kazi ya uungu. Haungeweza kushiriki katika shughuli za kawaida za kimwili, wala hata kuishi na wanadamu duniani. Hivyo basi, umuhimu wa Mungu kupata mwili, kiini kabisa cha Mungu kuja duniani, kingepotea. Ubinadamu wa Mungu kuwa mwili huwepo kudumisha kazi ya kawaida ya uungu katika mwili; fikira Zake za kawaida za binadamu zinadumisha ubinadamu Wake wa kawaida na shughuli Zake zote za kimwili. Mtu anaweza kusema kuwa fikira zake za kawaida za binadamu zipo ili kudumisha kazi yote ya Mungu katika mwili. Kama mwili huu usingekuwa na akili ya mwanadamu wa kawaida, basi Mungu Asingefanya kazi katika mwili, na Anachopaswa kufanya kimwili kisingetimilika. Japo Mungu mwenye mwili Ana akili ya mwanadamu wa kawaida, kazi Yake haijatiwa doa na mawazo ya binadamu; Anafanya kazi katika ubinadamu na akili ya kawaida chini ya masharti ya awali kuwa atakuwa na ubinadamu na akili ya kawaida, na si na mawazo ya kawaida ya binadamu. Haijalishi mawazo ya mwili Wake ni bora kiasi gani, kazi Yake haionyeshi alama ya mantiki au kufikiria. Kwa maneno mengine, kazi Yake haiwazwi na akili ya mwili Wake, ila ni onyesho la moja kwa moja la kazi ya uungu katika ubinadamu Wake. Kazi Yake yote ni huduma Anayostahili kutimiza, na haiwazwi hata chembe kwa akili Zake. Kwa mfano, kuponya wagonjwa, kufukuza mapepo na kusulubishwa hayakuwa mazao ya akili Zake za binadamu, yasingeweza kutimizwa na mwanadamu yeyote mwenye akili za binadamu. Vivyo hivyo, kazi ya ushindi ya leo ni huduma ambayo ni sharti itekelezwe na Mungu mwenye mwili, lakini si kazi ya mapenzi ya mwanadamu, ni kazi ambayo uungu Wake unapaswa kufanya, kazi ambayo hakuna mwanadamu wa mwili anaiweza. Kwa hivyo, Mungu mwenye mwili ni lazima Awe na akili za binadamu, ni lazima Awe na ubinadamu wa kawaida, kwa sababu ni lazima Atekeleze kazi Yake katika ubinadamu akiwa na akili za kawaida. Hiki ndicho kiini cha kazi ya Mungu mwenye Mwili, kiini chenyewe cha Mungu mwenye mwili.

Kimetoholewa kutoka katika Neno Laonekana katika Mwili

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp