Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Kuingia Katika Uzima | Dondoo 454

Yesu aliweza kukamilisha agizo la Mungu—kazi ya ukombozi wa wanadamu wote—kwa sababu alikabidhi kila tatizo kwa mapenzi ya Mungu, bila kufuata mipango na fikira Zake binafsi. Basi pia, Yeye Alikuwa rafiki mwema wa Mungu—Mungu Mwenyewe, jambo ambalo nyote mnalielewa vizuri sana. (Kwa kweli, alikuwa Mungu Mwenyewe aliyetolewa ushahidi na Mungu; Ninataja jambo hili hapa kwa kuutumia ukweli wa Yesu ili kuonyesha mfano wa suala hili.) Aliweza kuuweka mpango wa usimamizi wa Mungu katika kiini cha mambo yote, na kila mara alimwomba Baba wa mbinguni na kuyatafuta mapenzi ya Baba wa mbinguni. Aliomba, na kusema: “Mungu Baba! Timiza kile ambacho ni mapenzi Yako, na usitende kulingana na nia Zangu; ingekwa heri ukitenda kulingana na mpango Wako. Mwanadamu anaweza kuwa dhaifu, lakini kwa nini unapaswa kumshughulikia? Ni vipi ambavyo mwanadamu aliweza kuwa mhusika wa shughuli Zako, mwanadamu ambaye ni kama chungu mkononi Mwako? Ndani ya moyo Wangu, Ninatamani tu kutimiza mapenzi Yako, na Ninatamani Utende Unachotaka kutenda ndani Yangu kulingana na makusudio Yako mwenyewe.” Alipokuwa njiani kuelekea Yerusalemu, Yesu alihisi maumivu makali, kama kwamba kisu kilikuwa kimedungwa ndani ya moyo Wake, ilhali hakuwa na nia yoyote ya kwenda kinyume cha Neno lake; kila mara kulikuwa na nguvu zenye uwezo mkuu zilizomvutia Yeye kuelekea mahali ambapo Angesulubiwa. Mwishowe, alipigiliwa misumari juu ya msalaba na akawa mfano wa mwili wenye dhambi, akiikamilisha kazi hiyo ya ukombozi wa wanadamu, na kufufuka kutoka kwa pingu za kifo na Kuzimu. Mbele Yake, kifo, jehanamu, na Kuzimu vilipoteza nguvu zao, na vilishindwa Naye. Aliishi miaka thelathini na tatu, na katika miaka hiyo yote daima Alifanya kila Alichoweza kutimiza mapenzi ya Mungu kulingana na kazi ya Mungu wakati huo, bila kuzingatia atakachofaidi au kupoteza Yeye binafsi, na kila mara akiwaza kuhusu mapenzi ya Mungu Baba. Hivyo, baada ya Yeye kubatizwa, Mungu alisema: “Huyu ni Mwana wangu Mpendwa, ambaye Ninapendezwa naye.” Kwa sababu ya huduma Yake mbele ya Mungu, iliyokuwa na upatanifu na mapenzi ya Mungu, Mungu aliuweka mzigo mzito wa kuwakomboa wanadamu wote juu ya mabega yake na akamfanya ajitolee kuutimiza, na Alikuwa na ujuzi na ustahiki wa kuikamilisha kazi hii muhimu. Katika maisha Yake yote, alivumilia mateso yasiyokuwa na kipimo kwa ajili ya Mungu, na alijaribiwa na Shetani mara nyingi, lakini hakufa moyo. Mungu alimpa kazi ya aina hiyo kwa sababu Alimwamini Yeye, na kumpenda Yeye, na hivyo basi Mungu mwenyewe alisema: “Huyu ni Mwana wangu Mpendwa, ambaye Ninapendezwa naye.” Wakati huo, ni Yesu pekee ambaye angeweza kutimiza agizo hili, na hii ilikuwa sehemu moja ya Mungu kutimiza kazi Yake ya kuwakomboa wanadamu wote katika Enzi ya Neema.

Ikiwa, kama Yesu, unaweza kuushughulikia kwa makini mzigo wa Mungu, na kuyakataa mambo ya mwili wako, Mungu atakuaminia kazi Zake muhimu, ili uweze kufikia masharti ya kumhudumia Mungu. Ni katika hali hizo pekee ndipo utakapothubutu kusema kwamba unafanya mapenzi ya Mungu na kukamilisha agizo Lake, hapo ndipo utakapothubuthu kusema unamhudumia Mungu kweli. Ukilinganishwa na mfano wa Yesu, unaweza kuthubutu kusema kwamba wewe ni mwandani wa Mungu? Je, unaweza kuthubutu kusema kwamba unafanya mapenzi ya Mungu? Je, unaweza kuthubutu kusema kwamba kweli unamhudumia Mungu? Iwapo, leo, hufahamu aina hii ya huduma kwa Mungu, unaweza kuthubutu kusema kwamba wewe ni rafiki mwema wa Mungu? Ukisema kwamba unamhudumia Mungu, humkufuru Yeye? Fikiria kuhusu hilo: Je, unamhudumia Mungu, au unajihudumia wewe mwenyewe? Unamhudumia Shetani, ilhali kwa ukaidi unasema kwamba unamhudumia Mungu—katika jambo hili humkufuru Mungu? Watu wengi walio nyuma Yangu wanatamani baraka ya cheo, wana ulafi wa chakula, wanapenda kulala na kuushughulikia mwili kwa makini, kila mara wakiogopa kwamba hakuna njia ya kuondoka ndani ya mwili. Hawaifanyi kazi yao ya kawaida kanisani, na kula chakula cha bure, au wanawaonya ndugu zao kwa maneno Yangu, wanasimama juu na kuwatawala wengine. Watu hawa huendelea kusema kwamba wanafanya mapenzi ya Mungu, wao husema kila mara kwamba ni marafiki wema wa Mungu—huu si upuuzi? Ikiwa una motisha iliyo sahihi, lakini huwezi kutumikia mapenzi ya Mungu, basi wewe unakuwa mpumbavu; lakini ikiwa motisha yako si sahihi, na bado unasema kwamba unamhudumia Mungu, basi wewe ni mtu anayempinga Mungu, na unastahili kuadhibiwa na Mungu! Sina huruma kwa watu wa aina hiyo! Wao hula chakula cha bure katika nyumba ya Mungu, na kila mara wao hutamani raha za mwili, na hawazingatii mambo ambayo Mungu anayapenda; kila mara wao hutafuta mambo yaliyo mazuri kwao, wala hawatilii maanani mapenzi ya Mungu, mambo yote wanayoyafanya hayaongozwi na Roho wa Mungu, kila mara wao hufanya hila na njama dhidi ya ndugu zao, na kuwa ndumakuwili, kama mbweha ndani ya shamba la mizabibu, akiiba mizabibu kila mara na kulikanyaga na kuliharibu shamba la mizabibu. Je, watu wa aina hiyo wanaweza kuwa marafiki wema wa Mungu? Je, unastahili kupokea baraka za Mungu? Wewe huwajibiki kuhusu maisha yako na kanisa, unastahili kupokea agizo la Mungu? Ni nani anayeweza kuthubutu kumwamini mtu kama wewe? Unapohudumu kwa njia hii, je, Mungu anaweza kuthubutu kukuaminia kazi kubwa zaidi? Je, si wewe unachelewesha mambo?

Nasema hivi ili uweze kujua masharti yanayohitajika kutimizwa ili kuhudumu kwa upatanifu na mapenzi ya Mungu. Usipoutoa moyo wako kwa Mungu, usipoyashugulikia kwa makini mapenzi ya Mungu kama alivyofanya Yesu, basi huwezi kuaminiwa na Mungu, na mwishowe utahukumiwa na Mungu. Labda leo, katika huduma yako kwa Mungu, kila mara wewe huficha kusudi la kumdanganya Mungu—lakini bado Mungu atakugundua. Kwa kifupi, bila kujali mambo yote mengine, ukimdanganya Mungu hukumu isiyo na huruma itakujia. Unapaswa kutumia vizuri nafasi ya kuwa umeingia katika njia sahihi ya kumhudumia Mungu kwa kumpa Mungu moyo wako kwanza, bila kugawanya uaminifu wako. Bila kujali iwapo uko mbele za Mungu, au mbele ya watu wengine, moyo wako unapaswa kuelekezwa kwa Mungu kila wakati, na unapaswa kufanya uamuzi wa kumpenda Mungu kama Yesu. Kwa kufanya hivi, Mungu atakufanya uwe mkamilifu, ili uwe mtumishi wa Mungu anayempendeza Mungu. Ikiwa ungependa kweli kufanywa mkamilifu na Mungu, na huduma yako iwe katika upatanifu na mapenzi Yake, basi unapaswa kubadilisha maoni yako ya awali kuhusu imani kwa Mungu, na kubadilisha jinsi ulivyokuwa ukimhudumia Mungu, ili nafsi yako yote iweze kufanywa kuwa kamilifu na Mungu; kwa kufanya hivi, Mungu hatakuacha, na, kama Petro, utakuwa katika kikosi cha mbele cha wale wanaompenda Mungu. Ukibaki kuwa mtu asiyetubu, basi utakutana na mwisho kama wa Yuda. Hii inapaswa kufahamika na watu wote wanaomwamini Mungu.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Jinsi ya Kuhudumu kwa Upatanifu na Mapenzi ya Mungu

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp