Kazi ya Mungu na Utendaji wa Mwanadamu (Sehemu ya Kwanza)

Kazi ya Mungu miongoni mwa mwanadamu haitengani na mwanadamu, kwa kuwa mwanadamu ni chombo cha kazi hii na kiumbe wa pekee aliyeumbwa na Mungu anayeweza kutoa ushuhuda kwa Mungu. Maisha ya mwanadamu na shughuli zake zote havitengani na Mungu, na vyote vinaongozwa na mkono wa Mungu, na inaweza kusemwa kuwa hakuna mtu anayeweza kuishi bila Mungu. Hakuna anayeweza kupinga hili, kwani ndio ukweli. Kila Akifanyacho Mungu ni kwa faida ya mwanadamu, na kinalenga hila za Shetani. Kila anachokihitaji mwanadamu kinatoka kwa Mungu, na Mungu ndiye chanzo cha maisha ya mwanadamu. Hivyo basi, mwanadamu hana uwezo wa kujitenga na Mungu. Vilevile, Mungu Hajawahi kuwa na nia ya kujitenga na mwanadamu. Kazi Aifanyayo Mungu ni kwa ajili ya wanadamu wote na mawazo Yake daima ni mema. Kwa mwanadamu, kwa hivyo, kazi ya Mungu na mawazo ya Mungu kwa mwanadamu (yaani mapenzi ya Mungu) ni “maono” ambayo yanafaa kutambuliwa na mwanadamu. Maono kama hayo pia ni usimamizi wa Mungu, na kazi ambayo haiwezi kufanywa na mwanadamu. Mahitaji ambayo Mungu anatarajia kutoka kwa mwanadamu wakati wa kazi Yake, wakati uo huo, yanaitwa “vitendo” vya mwanadamu. Maono ni kazi ya Mungu Mwenyewe au ni mapenzi Yake kwa mwanadamu au madhumuni na umuhimu wa kazi Yake. Maono pia yanaweza kusemekana kuwa sehemu ya usimamizi, kwani usimamizi huu ni kazi ya Mungu, iliyokusudiwa kwa mwanadamu, kwa maana kwamba ni kazi ambayo Mungu anaifanya miongoni mwa wanadamu. Kazi hii ni ushahidi na njia ambayo kwayo mwanadamu anamfahamu Mungu na ni ya umuhimu wa hali ya juu kwa mwanadamu. Iwapo wanadamu hawatatilia maanani kuijua kazi ya Mungu na badala yake kutilia maanani mafundisho ya dini kuhusu imani kwa Mungu au kutilia maanani vitu vidogo visivyo na maana, hawatamjua Mungu, na, aidha, hawatakuwa wanautafuta moyo wa Mungu. Kazi ya Mungu inamsaidia sana mwanadamu kumfahamu Mungu na inaitwa maono. Maono haya ni kazi ya Mungu, mapenzi, madhumuni na umuhimu wa kazi ya Mungu na yote ni kwa manufaa ya mwanadamu. Vitendo vinamaanisha yale ambayo yanafaa kufanywa na mwanadamu, yale ambayo yanafaa yafanywe na viumbe wanaomfuata Mungu. Ni wajibu wa mwanadamu pia. Kinachotakiwa kufanywa na mwanadamu si kile alichokielewa tangu awali bali ni yale matakwa ya Mungu wakati wa kuifanya kazi Yake. Matakwa haya taratibu yanakuwa ya kina na kuinuliwa kadri Mungu anavyofanya kazi. Kwa mfano, katika Enzi ya Sheria, mwanadamu alilazimika kuifuata sheria na katika Enzi ya Neema mwanadamu alitakiwa kuubeba msalaba. Enzi ya Ufalme ni tofauti: Matakwa kwa mwanadamu ni mazito kuliko yale ya Enzi ya Sheria na Enzi ya Neema. Kadiri maono yanavyoinuliwa zaidi ndivyo matakwa haya yanavyokuwa mazito, ya wazi zaidi na halisi. Vivyo hivyo, maono yanaendelea kuwa halisi. Maono haya mengi na halisi si fursa tu ya utiifu wa mwanadamu kwa Mungu, bali pia, zaidi ya hayo, yanamsaidia yeye kumfahamu Mungu.

Ikilinganishwa na enzi za awali, kazi ya Mungu katika Enzi ya Ufalme ni ya vitendo zaidi, imekusudiwa zaidi dutu ya mwanadamu na mabadiliko katika tabia yake na uwezo zaidi wa kuwa na ushuhuda wa Mungu Mwenyewe kwa wale wote wamfuatao Mungu. Kwa maneno mengine, katika Enzi ya Ufalme, Mungu anapofanya kazi hujionyesha zaidi kwa mwanadamu, kuliko kipindi kingine chochote kile cha awali, ikiwa inamaanisha kuwa maono ambayo yanafaa kujulikana na mwanadamu ni ya juu kuliko yale ya enzi yoyote ile ya awali. Kwa kuwa kazi ya Mungu miongoni mwa mwanadamu imeingia maeneo ambayo haikuwa imefika, maono yanayojulikana na mwanadamu katika Enzi ya Ufalme ni ya juu zaidi katika kazi nzima ya usimamizi. Kazi ya Mungu imeingia katika maeneo ambayo haikuwa imewahi kufika, na kwa hivyo maono yanayojulikana na mwanadamu yamekuwa ya juu zaidi katika maono yote, na matokeo ya vitendo vya mwanadamu ni ya juu zaidi kuliko enzi za awali kwani utendaji wa mwanadamu hubadilika kulingana na mabadiliko ya maono na ukamilifu wa maono vilevile huonyesha ukamilifu wa vitendo vya mwanadamu. Punde tu usimamizi wa Mungu usitapo, vitendo vya mwanadamu navyo husimama, na bila kazi ya Mungu mwanadamu hatakuwa na jingine ila tu kujikita katika mafundisho ya zamani, vinginevyo hatakuwa na pa kukimbilia. Bila maono mapya, hapatakuwa na utendaji mpya kutoka kwa mwanadamu; bila kuwepo na maono kamili hapatakuwa na utendaji kamili wa mwanadamu; na bila maono ya juu hapatakuwa na utendaji wa juu wa mwanadamu. Utendaji wa mwanadamu huandamana na nyayo za Mungu na vivyo hivyo ufahamu na tajriba ya mwanadamu hubadilika sawa na kazi ya Mungu. Bila kujali mwanadamu ana uwezo kiasi gani, hawezi kujitenga na Mungu, na iwapo Mungu angaliacha kufanya kazi hata kwa muda kidogo, mwanadamu angalikufa ghafla kutokana na ghadhabu ya Mungu. Mwanadamu hana lolote la kujivunia, kwani haijalishi ufahamu wa mwanadamu ulivyo wa juu leo, haijalishi jinsi uzoefu wake ulivyo wa kina, hawezi kujitenga na kazi ya Mungu—kwani vitendo vya mwanadamu na yale yote anayoyaandama katika imani yake kwa Mungu, hayatengani na maono haya. Katika kila aina ya kazi ya Mungu kuna maono yanayofahamika na mwanadamu; maono yanayofuatwa na matarajio mwafaka ya Mungu kwa mwanadamu. Bila haya maono kama msingi, mwanadamu hawezi kuwa na uwezo wa utendaji na pia hangeweza kumfuata Mungu bila kuyumbayumba. Ikiwa mwanadamu hamjui Mungu au hayaelewi mapenzi ya Mungu, basi yote ayafanyayo ni bure na yasiyoweza kukubalika na Mungu. Hata mwanadamu awe na vipawa vingi kiasi gani, bado hawezi kujitenga na kazi ya Mungu na uongozi wa Mungu. Bila kujali uzuri na wingi wa matendo ya mwanadamu, bado hayawezi kuchukua nafasi ya kazi ya Mungu. Kwa hivyo basi, utendaji wa mwanadamu hauwezi kutenganishwa na maono katika hali yoyote ile. Wale ambao hawakubali maono mapya hawana vitendo vipya. Vitendo vyao havina uhusiano na ukweli kwani wanajifunga katika mafundisho ya dini na kufuata sheria zilizokufa; hawana maono mapya kabisa na kwa sababu hiyo hawatendi kulingana na enzi mpya. Wamepoteza maono na kwa kufanya hivyo wamepoteza kazi ya Roho Mtakatifu, hivyo basi kupoteza ukweli pia. Wasio na ukweli ni wazawa wa upuuzi, ni mifano ya Shetani. Bila kujali mtu ni wa aina gani, hawezi kuwepo bila maono ya kazi ya Mungu, hawezi kuishi pasipo na uwepo wa Roho Mtakatifu; punde tu mtu apotezapo maono, anaingia Kuzimu na kuishi gizani. Watu wasio na maono ni wale wamfuatao Mungu kipumbavu, ni wale wasio na kazi ya Roho Mtakatifu, na wanaishi kuzimu. Watu kama hawa huwa hawafuatilii ukweli, na hulitundika jina la Mungu kama bango. Wale ambao hawafahamu kazi ya Roho Mtakatifu, ambao hawamjui Mungu katika mwili, ambao hawajui hatua tatu za kazi katika uzima wa usimamizi wa Mungu—hawajui maono na hivyo wanaishi bila ukweli. Je, si wale wote wasiokuwa na ukweli ni watenda maovu? Wale wanaotaka kuweka ukweli katika vitendo, ambao wako tayari kuutafuta ufahamu wa Mungu, na ambao kwa kweli wanashirikiana na Mungu ni watu ambao maono yanakuwa msingi wao. Wanakubaliwa na Mungu kwa sababu wanashirikiana na Mungu na ushirika huu ndio ambao unafaa kuwekwa katika vitendo na mwanadamu.

Katika maono kuna njia nyingi zinazoelekea kwa vitendo. Matakwa ya utendaji yaliyopo kwa mwanadamu yamo pia ndani ya maono sawa tu na kazi ya Mungu inayopaswa kufahamika na mwanadamu. Katika mikutano maalum ya zamani au mikutano mikuu iliyokuwa katika sehemu mbalimbali, ni kipengele kimoja tu cha vitendo kilichozungumziwa. Vitendo kama hivyo ni vile vilivyotiwa katika vitendo katika Enzi ya Neema na hapakuwa na mfanano wowote na ufahamu wa Mungu kwani maono ya Enzi ya Neema yalikuwa tu maono ya kusulubiwa kwa Yesu, na hapakuwa na maono ya juu zaidi. Mwanadamu hakuhitajika kujua zaidi ya kazi Yake ya ukombozi wa mwanadamu kupitia kusulubiwa, na kwa hivyo katika Enzi ya Neema hapakuwa na maono mengine ya kufahamiwa na mwanadamu. Kwa njia hii, mwanadamu alikuwa na ufahamu mdogo sana wa Mungu na mbali na upendo na huruma za Yesu, kulikuwa na vitu vichache tu vya mwanadamu kuweka katika vitendo, vitu ambavyo vilikuwa tofauti na hali ya leo. Zamani, haikujalisha ni aina gani ya mkutano, mwanadamu hakuwa na uwezo wa kuzungumzia ufahamu wa vitendo wa kazi ya Mungu, aidha hapakuwa na yeyote aliyeweza kusema kwa dhahiri njia iliyokuwa sawa ya utendaji kwa mwanadamu kuiingilia. Aliongeza tu mambo kidogo katika msingi wa stahamala na uvumilivu; hapakuwa na mabadiliko yoyote katika kiini cha vitendo vyake kwani katika enzi hiyo Mungu hakufanya kazi yoyote mpya na matakwa ya pekee Aliyomwekea mwanadamu yalikuwa stahamala na uvumilivu, au kuubeba msalaba. Mbali na vitendo kama hivyo, hapakuwa na maono ya juu zaidi kuliko yale ya kusulubishwa kwa Yesu. Zamani hapakutajwa maono mengine kwa sababu Mungu hakufanya kazi kubwa na kwa sababu Alimwekea mwanadamu matakwa machache. Kwa njia hii, haikujalisha mwanadamu alifanya nini, hakuweza kuivuka mipaka ya viwango hivi, viwango ambavyo vilikuwa rahisi na vya juu juu vya mwanadamu kuweka katika vitendo. Leo Nazungumzia maono mengine kwa kuwa leo kazi nyingi zaidi imefanywa, kazi ambayo ni mara kadha zaidi ya ile ya Enzi ya Sheria na Enzi ya Neema. Yanayohitajika kwa mwanadamu, aidha, ni mara kadhaa juu zaidi kuliko enzi zilizopita. Iwapo mwanadamu hana uwezo wa kuijua kikamilifu kazi kama hiyo, basi haitakuwa na umuhimu mkubwa; inaweza kuchukuliwa kuwa mwanadamu atakuwa na ugumu kuifahamu kazi yenyewe kikamilifu ikiwa hawezi kuitengea maisha yake yote. Katika kazi ya ushindi, kuzungumzia tu njia ya vitendo kutaufanya ushindi wa mwanadamu kuwa jambo lisilowezekana. Mazungumzo ya maono tu bila matakwa yoyote kwa mwanadamu vilevile kutaufanya ushindi wa mwanadamu kuwa jambo lisilowezekana. Iwapo hapana kitu kingine kitakachoweza kuzungumziwa ila tu njia ya vitendo, basi ingekuwa vigumu kuuweza udhaifu wa mwanadamu, au kuondoa dhana za mwanadamu, na vilevile itakuwa vigumu kumshinda mwanadamu. Maono ni zana muhimu ya ushindi wa mwanadamu, na bado pasingelikuwepo na njia tofauti na maono basi mwanadamu asingelikuwa na njia ya kufuata wala jinsi ya kuingia. Hii imekuwa kanuni ya kazi ya Mungu toka mwanzo hadi mwisho: Katika maono kuna kile ambacho chaweza kuwekwa katika vitendo, na vivyo hivyo kuna maono kuongezea kwa kutenda. Kiwango cha mabadiliko katika maisha na tabia za mwanadamu huambatana na mabadiliko katika maono. Kama mwanadamu angetegemea tu juhudi zake, basi ingekuwa vigumu kwake kufikia kiwango cha juu cha mabadiliko. Maono huzungumzia kazi ya Mungu Mwenyewe na usimamizi wa Mungu. Utendaji hurejelea njia ya vitendo vya mwanadamu na kwa namna ya maisha ya mwanadamu; katika usimamizi wote wa Mungu, uhusiano baina ya maono na vitendo ni uhusiano kati ya Mungu na mwanadamu. Maono yangetolewa au yangezungumziwa bila kuhusishwa na vitendo, ama kungekuwa tu na maono na vitendo vya mwanaadamu viondolewe, basi vitu kama hivyo visingechukuliwa kama usimamizi wa Mungu, wala isingesemwa kwamba kazi ya Mungu ni kwa ajili ya wanadamu; kwa namna hii, si tu kwamba wajibu wa mwanadamu ungeondolewa, bali pia kazi ya Mungu ingekosa kusudi. Iwapo tangu mwanzo hadi mwisho, mwanadamu angetarajiwa tu kutenda, bila kujihusisha na kazi ya Mungu, na, zaidi ya hayo, kama mwanadamu asingetarajiwa kuifahamu kazi ya Mungu, basi kazi hiyo isingeitwa usimamizi wa Mungu. Kama mwanadamu hangemjua Mungu, na hangejua mapenzi ya Mungu, na huendelea kufanya vitendo kidhahania bila kuwa na uwazi, basi asingekuwa kiumbe kilichohitimu. Hivyo basi, hivi vitu viwili ni vya lazima. Kama kungekuwepo kazi ya Mungu tu, ambayo ni kusema, kungekuwepo maono pekee na hakungekuwepo na ushirikiano au vitendo kutoka kwa mwanadamu, basi hivyo vitu visingeitwa usimamizi wa Mungu. Iwapo kungekuwa tu na vitendo na kuingia kwa mwanadamu, basi bila kujali kuingia kwa mtu kungekuwa kwa juu kiasi gani, haya, pia, hayangekubalika. Kuingia kwa mwanadamu kunafaa kubadilika taratibu kulingana na kazi na maono; hakuwezi kubadilika ghafla. Kanuni za vitendo vya mwanadamu haziko huru na bila vizuizi, lakini ziko ndani ya mipaka fulani. Kanuni hizo hubadilika kwa hatua sawa na maono ya kazi. Hivyo basi usimamizi wa Mungu hatimaye huishia katika kazi ya Mungu na vitendo vya mwanadamu.

Kazi ya usimamizi ilikuja tu kwa ajili ya wanadamu, yaani ilitolewa kwa ajili ya uwepo wa wanadamu. Usimamizi haukuwepo kabla ya uwepo wa wanadamu au mwanzo wakati mbingu na nchi na vilivyomo vilipoumbwa. Iwapo, katika kazi nzima ya Mungu, hakungekuwa na vitendo vinavyomfaidi mwanadamu, yaani kama Mungu asingeweka matakwa maalum kwa mwanadamu aliyepotoka (ikiwa kazi ifanywayo na Mungu haikuwa na njia nzuri ya vitendo vya mwanaadamu), basi kazi hii isingeitwa usimamizi wa Mungu. Iwapo kazi nzima ya Mungu ingehusisha tu kuwaambia wanadamu waliopotoka jinsi ya kuendeleza vitendo vyao, na Mungu hakuendeleza kazi yoyote ya mipango Yake, na Hakuonyesha uwepo wake wa daima au busara, basi bila kujali ni jinsi gani matakwa ya Mungu kwa mwanadamu yangewekwa juu, bila kujali Mungu aliishi muda mrefu kiasi gani miongoni mwa wanadamu, mwanadamu asingejua chochote juu ya tabia ya Mungu; kama ingekuwa hivyo, basi kazi hii isingeweza kukaribia kuitwa usimamizi wa Mungu. Kwa ufupi, kazi ya usimamizi wa Mungu ni kazi iliyofanywa na Mungu na kazi zote zilizofanywa chini ya uongozi wa Mungu na wale ambao wamepatikana na Mungu. Kazi kama hiyo inaweza kuchukuliwa kwa ufupisho kama usimamizi, na inaelezea kazi ya Mungu miongoni mwa wanadamu na vilevile ni ushirikiano Wake na wale wanaomfuata; kwa ujumla, hayo yote yanaweza kuitwa usimamizi. Hapa kazi ya Mungu inaitwa maono na ushirikianao wa mwanadamu unaitwa vitendo. Kadiri kazi ya Mungu ilivyo juu (yaani kadiri maono yalivyo juu), ndivyo tabia za Mungu zinakuwa wazi kwa mwanadamu, na kutoafikiana na mawazo ya mwanadamu, na ndivyo vitendo na ushirikiano wa mwanadamu huwa vya juu. Kadiri matakwa kwa mwanadamu yanavyokuwa ya juu, ndivyo kazi ya Mungu inavyotofautiana mawazo ya mwanadamu, matokeo yake yakiwa majaribu ya mwanadamu, na viwango anavyotarajiwa kuwa navyo, vilevile vinakuwa vya juu. Katika hatima ya kazi hii, maono yote yatakuwa yametimizwa, na yale yote mwanadamu anapaswa kuweka katika vitendo yatakuwa yamefikia kilele cha ukamilifu. Huu ndio wakati pia ambapo kila kitu kitawekwa katika kundi lake kwani kile kinachopaswa kufahamika na mwanadamu kitakuwa kimebainishwa kwake. Kwa hivyo maono yatakapofikia upeo wa juu, vivyo hivyo kazi nayo itakaribia hatima yake na vitendo vya mwanadamu vitakuwa vimefikia ufanisi wake. Vitendo vya mwanadamu vimekitwa katika kazi ya Mungu, na usimamizi wa Mungu unadhihirika tu kupitia vitendo na ushirikiano wa mwanadamu. Mwanadamu ni mfano wa kazi ya Mungu, na mlengwa wa kazi ya usimamizi mzima wa Mungu, na pia mazao ya kazi ya usimamizi wote wa Mungu. Iwapo Mungu angefanya kazi peke yake bila ushirika wa mwanadamu, basi pasingekuwepo na kitu cha kudhihirisha kazi Yake nzima na kwa hali hiyo kusingekuwa na umuhimu hata kidogo wa usimamizi wa Mungu. Ni kwa kuchagua tu chombo kifaacho kilicho nje ya kazi ya Mungu, na kinachoweza kudhihirisha kazi hii, na kuthibitisha kudura na busara zake, je, inawezekana kufikia dhumuni la usimamizi wa Mungu na kufikia dhumuni la kutumia kazi hii yote ili kumshinda kabisa Shetani. Na kwa hivyo mwanadamu ni sehemu muhimu katika kazi ya usimamizi ya Mungu, na mwanadamu ndiye pekee anayeweza kuifanya kazi ya usimamizi ya Mungu izae matunda na kufikia lengo Lake kuu; mbali na mwanadamu, hakuna kiumbe kingine chenye uhai kinachoweza kuchukua nafasi hiyo. Ikiwa mwanadamu atakuwa dhihirisho kamili la kazi ya usimamizi, basi uasi wa wanadamu wenye maovu lazima utokomezwe. Hii inahitaji kuwa mwanadamu apewe utendaji ufaao kwa kila muktadha, na kwamba Mungu afanye kazi inayotangamana miongoni mwa wanadamu. Ni kwa njia hii tu ndipo kutakuwa na kundi la watu waliokubaliwa ambao ni dhihirisho la kazi ya usimamizi. Kazi ya Mungu miongoni mwa wanadamu haiwezi kuwa ushuhuda kwa Mungu Mwenyewe kupitia kazi ya Mungu peke yake; ushuhuda huo vilevile unahitaji wanadamu ambao wanafaa ili kazi yake iafikiwe. Mwanzo Mungu atawatayarisha watu hawa ambao kupitia kwao kazi Yake itadhihirika na ushuhuda Wake utachukuliwa miongoni mwa viumbe. Kwa hili, Mungu atakuwa ameafiki lengo la kazi Yake. Mungu hafanyi kazi peke Yake kumshinda Shetani kwa sababu Mungu hawezi kujishuhudia Mwenyewe moja kwa moja miongoni mwa viumbe wote. Angefanya hivyo, ingekuwa vigumu kumshawishi mwanadamu, kwa hivyo Mungu lazima Afanye kazi kwa mwanadamu ili kumshinda na ndipo Atakapoweza kupata ushuhuda miongoni mwa viumbe vyote. Mungu angefanya kazi peke Yake bila kushirikiana na mwanadamu, au kama mwanadamu asingetakiwa kushirikiana, basi mwanadamu asingeitambua tabia ya Mungu na daima asingefahamu nia ya Mungu; na kwa hali hii haiwezi kuitwa usimamizi wa Mungu. Mwanadamu mwenyewe angejizatiti, na kutafuta, na kufanya bidii, bila kuifahamu kazi ya Mungu, basi mwanadamu angekuwa anafanya mizaha. Bila kazi ya Roho Mtakatifu, akifanyacho mwanadamu ni cha Shetani, ni muasi na mtenda maovu; Shetani anadhihirika katika yote yafanywayo na mwanadamu mwenye maovu na hamna kinachoafikiana na Mungu, na yote ni dalili ya Shetani. Hakuna kati ya vilivyozungumziwa kisichokuwa na maono na vitendo. Katika msingi wa maono, mwanadamu hupata vitendo, anapata njia ya utiifu, ili kwamba aweze kuweka kando mawazo yake ili apate vile ambavyo hajawahi kuwa navyo hapo awali. Mungu huhitaji mwanadamu ashirikiane naye, kwamba mwanadamu asikilize matakwa Yake, na mwanadamu ashikilie kazi ifanywayo na Mungu Mwenyewe na kuupitia uwezo mkubwa wa Mungu na kuifahamu tabia ya Mungu. Kwa kifupi, haya ndiyo usimamizi wa Mungu. Ushirika wa Mungu na mwanadamu ndio usimamizi, na ni usimamizi mkuu zaidi.

Kile kinachohusisha maono kimsingi hurejelea kazi ya Mungu Mwenyewe, na kile kinachohusisha vitendo ni sharti kifanywe na mwanadamu, na hakina uhusiano na Mungu. Kazi ya Mungu hukamilishwa na Mungu Mwenyewe, na vitendo vya mwanadamu hufikiwa na mwanadamu mwenyewe. Kile ambacho ni sharti kifanywe na Mungu Mwenyewe hakihitajiki kufanywa na mwanadamu, na kile kitendwacho na mwanadamu hakihusiani na Mungu. Kazi ya Mungu ni huduma Yake Mwenyewe na haina uhusiano na mwanadamu. Hii kazi haihitaji kufanywa na mwanadamu, na hata zaidi, mwanadamu hatakuwa na uwezo wa kufanya kazi ambayo ni ya kufanywa na Mungu. Kile ambacho kinafaa kutendwa na mwanadamu ni sharti kitimizwe na mwanadamu, iwe ni kujitoa kafara au kuwasilishwa kwake kwa Shetani ili kushuhudia—haya ni lazima yatimizwe na mwanadamu. Mungu Mwenyewe anatimiza kazi Yake yote, na kile ambacho ni wajibu wa mwanadamu, mwanadamu hufunuliwa na kazi iliyobaki huachiwa mwanadamu. Mungu hafanyi kazi ya ziada. Anafanya ile kazi iliyo katika huduma Yake na kumuonyesha mwanadamu na kumfunulia njia tu bali hampambanulii njia; hili lazima lieleweke kwa mwanadamu. Kuweka ukweli katika vitendo kunamaanisha kuweka neno la Mungu katika vitendo, na haya yote ni wajibu wa mwanadamu, ni kile kinachofaa kufanywa na mwanadamu, na wala halihusiani na Mungu. Iwapo mwanadamu atataka Mungu apitie masaibu na utakaso katika ukweli sawa na mwanadamu, basi mwanadamu atakuwa hatii. Kazi ya Mungu ni kuendeleza huduma Yake, na wajibu wa mwanadamu ni kutii uongozi wote wa Mungu, bila pingamizi yoyote. Kinachotakiwa kufikiwa na mwanadamu anawajibika kutimiza, bila kujali ni namna gani Mungu hufanya kazi au kuishi. Ni Mungu Mwenyewe tu ndiye anayeweza kumwekea mwanadamu matakwa, ambayo ni kusema, ni Mungu Mwenyewe tu ndiye anayestahili kumwekea mwanadamu matakwa. Mwanadamu hastahili kuwa na jingine, hastahili kufanya chochote ila tu kutii kikamilifu na kutenda; hii ndiyo busara ambayo mwanadamu anapaswa kuwa nayo. Punde kazi ifaayo kufanywa na Mungu Mwenyewe itakapokamilika, mwanadamu anatakiwa kuipitia, hatua kwa hatua. Iwapo mwishowe, baada ya usimamizi wote wa Mungu kukamilika, mwanadamu atakuwa hajafanya anachotakiwa na Mungu kufanya, basi mwanadamu anafaa aadhibiwe. Ikiwa mwanadamu hatimizi matakwa ya Mungu, basi hili ni kwa sababu ya uasi wa mwanadamu; haimaanishi kuwa Mungu hajakuwa makini vya kutosha katika kazi Yake. Wale wote wasioweka neno la Mungu katika vitendo, ambao hawatimizi matakwa ya Mungu na wale wote wasiokuwa na uaminifu na kutimiza wajibu wao—wataadhibiwa wote. Leo hii mnachohitajika kufikia si madai ya ziada, ila ni wajibu wa mwanadamu, na kile kinachofaa kufanywa na kila mtu. Kama hamuwezi hata kufanya wajibu wenu, au kuufanya vizuri, hamuoni mnajiletea masaibu nyinyi wenyewe? Hamwuoni mnajitakia kifo? Mtatarajiaje maisha ya baadaye na matarajio? Kazi ya Mungu ni kwa ajili ya wanadamu, na ushirika wa mwanadamu ni kwa minajili ya usimamizi wa Mungu. Baada ya Mungu kufanya yale yote Anayopaswa kufanya, mwanadamu anapaswa kufanya vitendo bila kukoma, na kushirikiana na Mungu. Mwanadamu hapaswi kulegeza kamba katika kazi ya Mungu, lazima aonyeshe uaminifu na asijitie katika mawazo mengi au kukaa akisubiri kifo bila kufanya kitu. Mungu Mwenyewe anaweza kujitolea kwa mwanadamu, basi ni kwa nini mwanadamu asiweze kuwa mwaminifu kwa Mungu? Mawazo na moyo wa Mungu vipo kwa mwanadamu, basi ni kwa nini mwanadamu asijitolee katika ushirika? Mungu huwafanyia wanadamu kazi, basi ni kwa nini mwanadamu asifanye wajibu wake kwa minajili ya usimamizi wa Mungu? Kazi ya Mungu imefika umbali huu, bado mnaona ila hutendi, mnasikia ila hamsogei. Je, si watu kama hawa wanafaa kuangamizwa kabisa? Tayari Mungu amejitolea kikamilifu kwa ajili ya mwanadamu, basi ni kwa nini siku hizi mwanadamu hafanyi wajibu wake kwa dhati? Kwa Mungu, kazi Yake ni ya kipaumbele Kwake, na kazi ya usimamizi Wake ni ya umuhimu wa hali ya juu. Kwa mwanadamu, kuweka maneno ya Mungu katika vitendo na kutimiza mahitaji ya Mungu ndiyo kipaumbele kwake. Ni lazima nyote myafahamu haya. Maneno mliyoambiwa yamefika kiini halisi cha nafsi yenu, na kazi ya Mungu imefika katika maeneo ambayo hayakuwa yamefikiwa awali. Watu wengi bado hawafahamu ukweli na uongo wa njia hii; bado wanasubiri na kutazama na hawafanyi wajibu wao. Badala yake huchunguza kila neno na tendo la Mungu, wanalenga juu ya Anachokula na Anachokivaa na mawazo yao huwa hata ya kuhuzunisha zaidi. Si watu wa aina hii wanafanya msukosuko bure? Hawa wanawezaje kuwa watu wamtafutao Mungu? Wanawezaje kuwa watu wa kumnyenyekea Mungu kwa kudhamiria? Wanasahau uaminifu na wajibu wao na badala yake kujishughulisha na mahali alipo Mungu. Wanaghadhabisha! Ikiwa mwanadamu amefahamu yale yote anayopaswa kufahamu na kuweka katika vitendo yale yote anayopaswa, basi Mungu atampa mwanadamu baraka Zake, kwa sababu kile ambacho Yeye huhitaji kutoka kwa mwanadamu ni wajibu wa mwanadamu, na kile ambacho mwanadamu anastahili kufanya. Ikiwa mwanadamu hawezi kufahamu yale yote anayopaswa kufahamu na hawezi kutia katika vitendo yale anayopasa kuweka katika vitendo, basi mwanadamu ataadhibiwa. Wasioshirikiana na Mungu wana uhasama Naye, wasioikubali kazi mpya wanaipinga, hata kama watu kama hao hawafanyi chochote ambacho ni cha pingamizi dhahiri. Wale wote wasioweka ukweli unaohitajika na Mungu katika vitendo ni watu wanaopinga kwa makusudi na ni waasi wa maneno ya Mungu hata kama watu kama hawa hutilia maanani maalum kwa kazi ya Roho Mtakatifu. Watu wasiotii maneno ya Mungu na kumnyenyekea Mungu ni waasi, na wapinzani wa Mungu. Watu wasiofanya wajibu wao ni wale wasioshirikiana na Mungu, na watu wasioshirikiana na Mungu ni wale wasioikubali kazi ya Roho Mtakatifu.

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp