Kupata Mwili Mara Mbili Kunakamilisha Umuhimu wa Kupata Mwili

Kila hatua ya kazi iliyofanywa na Mungu ina umuhimu mkubwa. Yesu alipokuja zamani, Alikuwa mwanaume, lakini Mungu anapokuja wakati huu Yeye ni mwanamke. Kutokana na hili, unaweza kuona kwamba Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamke kwa ajili ya kazi Yake na Kwake hakuna tofauti ya jinsia. Roho Wake anapowasili, Anaweza kuchukua umbo la mwili wowote kwa matakwa Yake na mwili unamwakilisha Yeye. Awe mwanamume au mwanamke, wote wanamwakilisha Mungu ili mradi tu ni Mungu mwenye mwili. Kama Yesu angekuja na Angeonekana kama mwanamke, kwa maneno mengine, iwapo mtoto wa kike, sio wa kiume, angezaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, hatua hiyo ya kazi ingeweza kukamilika pia. Kama hali ingekuwa hivyo, hatua hii ya kazi ingeweza kukamilishwa badala yake na mwanaume na kazi ingekuwa imekamilika pia. Kazi inayofanywa katika hatua zote ni muhimu sana; hakuna kazi inayojirudia au kupingana na nyingine. Wakati wa kazi Yake, Yesu alikuwa anaitwa Mwana wa pekee, ikiwa inaashiria jinsia ya kiume. Sasa kwa nini Mwana wa pekee hakutajwa katika hatua hii? Hii ni kwa sababu mahitaji ya kazi yamelazimisha badiliko la jinsia tofauti na ile ya Yesu. Kwa Mungu hakuna tofauti ya jinsia. Kazi Yake inafanywa kama Anavyotaka na haizuiliwi na kitu chochote kile, kimsingi ipo huru, lakini kila hatua ina umuhimu mkubwa. Mungu alifanyika mwili mara mbili, na ni dhahiri kwamba kupata mwili kwake katika siku za mwisho ni mara ya mwisho. Amekuja kufichua matendo Yake yote. Ikiwa katika hatua hii Hakufanyika mwili ili Yeye binafsi afanye kazi kwa ajili ya mwanadamu kushuhudia, mwanadamu milele angeshikilia fikra kwamba Mungu ni wa kuime tu, na sio wa kike. Kabla ya hili, wote waliamini kwamba Mungu anaweza kuwa tu mwanaume na kwamba mwanamke hawezi kuitwa Mungu, maana wote walichukulia kwamba mwanamume ana mamlaka juu ya mwanamke. Waliamini kwamba hakuna mwanamke anayeweza kuchukua mamlaka, bali ni mwanamume tu. Hata walisema kwamba mwanamume alikuwa ni kichwa cha mwanamke na kwamba mwanamke anapaswa kumheshimu mwanaume na asiweze kuwa juu yake. Iliposemwa hapo nyuma kwamba mwanamume alikuwa kichwa cha mwanamke, ilisemwa kwa kurejelea Adamu na Hawa ambao walidanganywa na yule nyoka, na wala sio mwanamume na mwanamke walioumbwa na Yehova hapo mwanzo. Kimsingi, mwanamke anapaswa kumtii na kumpenda mume wake, kama vile ambavyo mwanamume anapaswa kujifunza kuisaidia familia yake. Hizi ni sheria na kanuni zilizowekwa na Yehova ambazo kwazo mwanadamu anapaswa kuzifuata katika maisha yake ya hapa duniani. Yehova alimwambia mwanamke “tamaa yako itakuwa ni kwa mumeo, naye atatawala juu yako.” Hii ilisemwa tu ili kwamba mwanadamu (yaani, mwanamume na mwanamke) waweze kuishi maisha ya kawaida chini ya utawala wa Yehova, ili kwamba maisha ya mwanadamu yawe na mfumo na yasipoteze mwelekeo. Kwa hivyo, Yehova alitengeneza kanuni zinazofaa kwa ajili ya namna ambavyo mwanamume na mwanamke wanavyopaswa kutenda, lakini kanuni hizi zilirejelea tu viumbe wote wanaoishi duniani, na sio kwa Mungu kupata mwili. Inawezekanaje Mungu awe sawa na uumbaji Wake? Maneno Yake yalielekezwa tu kwa mwanadamu wa uumbaji Wake; zilikuwa kanuni zilizowekwa kwa ajili ya mwanamume na mwanamke ili kwamba mwanadamu huyo aweze kuishi maisha ya kawaida. Hapo mwanzo, ambapo Yehova alimuumba mwanadamu, aliwaumba mwanamume na mwanamke; kwa hiyo, kupata Kwake mwili pia kulitofautishwa kuwa ama mwanamume au mwanamke. Hakuamua kazi Yake kulingana na maneno aliyozungumza kwa Adamu na Hawa. Kufanyika mwili mara mbili kuliamuliwa kabisa kwa kuzingatia mawazo Yake alipomuumba mwanadamu kwa mara ya kwanza. Yaani, alikamilisha kazi ya kupata kwake mwili mara mbili, kwa msingi wa mwanamke na mwanamume ambao hawakuwa wameharibiwa na dhambi. Ikiwa mwanadamu atatumia maneno yaliyozungumzwa na Yehova kwa Adamu na Hawa ambao walidanganywa na yule nyoka katika kazi ya Mungu katika mwili, je, si kwamba Yesu pia anapaswa kumpenda mke Wake kama Alivyotakiwa? Je, Mungu bado ni Mungu wakati huo tena? Ikiwa ni hivyo, je, Anaweza kukamilisha kazi Yake? Ikiwa ni vibaya kwa Mungu aliyepata mwili kuwa mwanamke, je, lisingekuwa kosa kubwa Mungu alipomuumba mwanamke? Ikiwa mwanadamu bado anaamini kwamba Mungu kupata mwili kama mwanamke ni vibaya, je, Yesu, ambaye hakuoa na hivyo hakuweza kumpenda mke Wake, hangekuwa na makosa kama kupata mwili kwa sasa? Kwa kuwa unatumia maneno yaliyozungumzwa na Mungu kwa Hawa ili kupima ukweli wa Mungu kupata mwili leo, unapaswa kutumia maneno ya Mungu kwa Adamu kumhukumu Bwana Yesu ambaye alikuwa mwili katika Enzi ya Neema. Je, hawa wawili sio sawa? Kwa kuwa unamhukumu Bwana Yesu kwa kumtumia mwanamume ambaye hakudanganywa na yule nyoka, huwezi kuhukumu ukweli wa kupata mwili leo hii kwa mwanamke ambaye alidanganywa na yule nyoka. Hiyo sio sawa kabisa! Ikiwa unafanya hukumu ya namna hiyo, basi hii inathibitisha kukosa urazini kwako. Yehova alipopata mwili mara mbili, jinsia ya mwili Wake ilikuwa inahusiana na mwanamume na mwanamke ambaye hakudanganywa na yule nyoka. Alipata mwili mara mbili kulingana na mwanamume na mwanamke ambaye hakudanganywa na yule nyoka. Usifikiri kwamba uanaume wa Yesu ulikuwa sawa na uanaume wa Adamu ambaye alidanganywa na yule nyoka. Hahusiani naye kabisa, na ni wanaume wawili wa asili tofauti. Hakika haiwezi kuwa kwamba uanaume wa Yesu unathibitisha yeye ni kichwa cha wanawake wote na sio kichwa cha wanaume wote? Je, yeye si Mfalme wa Wayahudi wote (ikiwa ni pamoja na wanaume na wanawake)? Ni Mungu Mwenyewe, sio tu kichwa cha mwanamke bali ni kichwa cha mwanamume pia. Ni Bwana wa viumbe vyote, na kichwa cha viumbe vyote. Unawezaje kuamua uanaume wa Yesu kuwa ishara ya kichwa cha mwanamke? Hii si kufuru? Yesu ni mwanamume ambaye hajapotoshwa. Yeye ni Mungu; ni Kristo; ni Bwana. Anawezaje kuwa mwanamume kama Adamu ambaye ameharibiwa na dhambi? Yesu ni mwili uliovaliwa na Roho wa Mungu aliye mtakatifu sana. Unawezaje kusema kuwa Yeye ni Mungu katika uanaume wa Adamu? Je, haingekuwa kwamba kazi yote ya Mungu ingekuwa na makosa? Je, Yehova angeweza kuuweka ndani ya Yesu uanaume wa Adamu ambaye alidanganywa? Sio kwamba kupata mwili kwa wakati huu ni kazi nyingine ya Mungu katika mwili tofauti kijinsia na Yesu lakini wanafanana katika asili? Bado unathubutu kusema kwamba Mungu aliyepata mwili hakuweza kuwa mwanamke kwa kuwa mwanamke ndiye aliyedanganywa kwanza na yule nyoka? Bado unathubutu kusema kwamba mwanamke ni najisi sana na ni chanzo cha upotovu wa mwanadamu, Mungu hawezi kufanyika mwili kama mwanamke? Bado unathubutu kusema kwamba “mwanamke siku zote atamtii mwanamume na hawezi kamwe kudhihirisha au kumwakilisha Mungu moja kwa moja”? Hukuelewa hapo nyuma; sasa bado unaweza kukufuru kazi ya Mungu, hususan Mungu aliyepata mwili? Kama huwezi kuona hili wazi wazi, ni vizuri zaidi ukawa makini na ulimi wako, la sivyo upumbavu na ujinga wako vitawekwa wazi na ubaya wako utadhihirishwa. Usidhani kwamba unaelewa kila kitu. Nakueleza kwamba yote uliyokwishayaona na kuyapitia hayatoshelezi kuelewa hata milenia ya mpango Wangu wa usimamizi. Sasa kwa nini basi unakuwa na kiburi? Talanta ndogo hiyo uliyonayo na maarifa kidogo hayo uliyonayo hayatoshelezi kutumika hata katika sekunde moja ya kazi ya Yesu! Je, una uzoefu mkubwa kiasi gani hasa? Yote uliyoyaona na yote uliyoyasikia katika maisha yako na yote uliyowahi kuyafikiria ni kidogo sana kulinganisha na kazi Ninayoifanya kwa muda mfupi sana! Ni bora usichambue chambue na kutafuta kosa. Haijalishi una kiburi kiasi gani, wewe bado ni kuimbe tu mdogo kuliko sisimizi! Vyote hivyo vilivyomo katika tumbo lako ni vichache zaidi ya vile vilivyomo katika tumbo la sisimizi! Usifikiri kwamba kwa kuwa umepitia mengi na umekuwa mkubwa, unaweza kuzungumza na kutenda kwa majivuno na ujeuri. Je, uzoefu wako na ukuu wako sio matokeo ya maneno Niliyoyazungumza? Je, unaamini kwamba umekuwa hivyo kwa sababu ya kufanya kwako kazi kwa bidii na kutokwa jasho? Siku hii, unaona kupata Kwangu mwili, na matokeo yake ni kwamba unakuwa na dhana nyingi hizo, kutoka kwazo unakuwa na fikira nyingi isiyohesabika. Ikiwa sio kwa kupata mwili Kwangu, bila kujali talanta zako ni za ajabu kiasi gani, usingeweza kuwa na dhana hizi nyingi. Sio kutokana na hili ndipo imeibuka fikira yako? Kama si kupata mwili kwa Yesu kwa mara ya kwanza, je, ungejua nini kuhusu kupata mwili? Je, si kwa sababu ya maarifa yako ya kupata mwili kwa mara ya kwanza ndio maana unathubutu kuhukumu kupata mwili kwa mara ya pili? Kwa nini uchunguze kwa makini badala ya kuwa mfuasi mtiifu? Umeingia katika mkondo huu na umekuja mbele ya Mungu aliyepata mwili. Ungewezaje kuruhusiwa kujifunza? Ni sawa kwako kujifunza historia ya familia yako, lakini ukichunguza “historia ya familia” ya Mungu, inawezekanaje Mungu wa leo akuruhusu kufanya hivyo? Je, wewe sio kipofu? Je, hujiletei dharau kwako mwenyewe?

Ikiwa tu kazi ya Yesu ingefanywa bila kitimizo cha hatua hii katika siku za mwisho, basi mwanadamu milele angeshikilia fikira kwamba Yesu pekee ndiye Mwana wa Mungu, yaani, Mungu ana mwana mmoja tu, na kwamba yeyote anayekuja baada yake akiwa na jina jingine hawezi kuwa Mwana pekee wa Mungu, wala Mungu Mwenyewe. Mwanadamu ana fikira kwamba Yule ambaye anajitoa sadaka kwa ajili ya dhambi au yule ambaye anachukua mamlaka kwa ajili ya Mungu na anayewakomboa wanadamu wote ni Mwana wa Mungu tu. Kuna baadhi ambao wanaamini kwamba ili mradi Yeye ni mwanamume ambaye anakuja, Anaweza kuchukuliwa kuwa ni Mwana wa Mungu wa pekee na mwakilishi wa Mungu. Na hata kuna wale wanaosema kwamba Yesu ni Mwana wa Yehova, Mwanaye wa pekee. Je, hii siyo fikira tu ya mwanadamu? Ikiwa hatua hii ya kazi haingefanywa katika enzi ya mwisho, basi wanadamu wote wangekuwa wamegubikwa katika kivuli suala la Mungu linapohusika. Ikiwa ni hivyo, mwanamume angejidhania kuwa ni mwenye hadhi ya juu kuliko mwanamke, na wanawake hawangeweza kuwa na uwezo wa kuinua vichwa vyao juu. Katika wakati kama huo, hakuna mwanamke angeweza kupokea wokovu. Watu siku zote wanaamini kwamba Mungu ni mwanamume, na siku zote Anawachukia wanawake na asingeweza kumpa mwanamke wokovu. Ikiwa ni hivyo, basi si kweli kwamba wanawake wote walioumbwa na Yehova na pia waovu wasingeweza kuwa na fursa ya kuokolewa? Je, ingekuwa na maana gani Yehova kumuumba mwanamke, yaani, kumuumba Hawa? Na je, mwanamke asingeangamia milele? Kwa hiyo, hatua hii ya kazi katika siku za mwisho ni kuwaokoa wanadamu wote, sio mwanamke tu bali wanadamu wote. Kazi hii ni kwa ajili ya wanadamu wote, na sio tu kwa ajili ya mwanamke. Ikiwa kuna watu wanaofikiria vinginevyo, basi ni wapumbavu kabisa!

Kazi inayofanywa kwa sasa imesukuma mbele kazi ya Enzi ya Neema; yaani, kazi katika mpango mzima wa usimamizi wa miaka elfu sita imesonga mbele. Ingawa Enzi ya Neema imekoma, kazi ya Mungu imeendelea sana. Kwa nini Ninazungumza mara kwa mara kwamba hatua hii ya kazi inajenga juu ya Enzi ya Neema na Enzi ya Sheria? Hii ina maana kwamba kazi ya wakati huu ni mwendelezo wa kazi iliyofanyika katika Enzi ya Neema na kuinua kazi ile iliyofanyika katika Enzi ya Sheria. Hatua hizi tatu zinaingiliana kwa karibu na kuunganika moja kwa inayofuata. Kwa nini pia Ninasema kwamba hatua hii ya kazi inajenga juu ya kile kilichofanywa na Yesu? Tuseme kwamba hatua hii haingejengwa juu ya kazi iliyofanywa na Yesu, ingebidi kusulubiwa kwingine kufanyike katika hatua hii, na kazi ya ukombozi ya hatua iliyopita ingelazimika kufanywa upya tena. Hii isingekuwa na maana yoyote. Kwa hiyo, sio kwamba kazi imekamilika kabisa, bali ni kwamba enzi imesonga mbele, na kazi imekuwa ya juu kabisa kuliko ilivyokuwa kabla. Inaweza kusemwa kwamba hatua hii ya kazi imejengwa juu ya msingi wa Enzi ya Sheria na katika mwamba wa kazi ya Yesu. Kazi hii imejengwa hatua kwa hatua, na hatua hii sio mwanzo mpya. Ni muungano tu wa hatua tatu za kazi ndio unaweza kuchukuliwa kuwa mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita. Hatua hii inafanywa katika msingi wa kazi ya Enzi ya Neema. Ikiwa hatua hizi mbili za kazi hazihusiani, kwa nini hakuna msalaba katika hatua hii? Kwa nini Sibebi dhambi za wanadamu? Siji kupitia kuzaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu na wala Sitosulubiwa ili kubeba dhambi za wanadamu; badala yake, Nipo hapa moja kwa moja kumwadibu mwanadamu. Ikiwa Mimi kumwadibu mwanadamu na kuja Kwangu si kwa njia ya Roho Mtakatifu na hakukufuata usulubisho, basi Nisingekuwa na sifa zinazostahili kumwadibu mwanadamu. Ni hasa kwa sababu Mimi ni mmoja na Yesu ndiyo Nimekuja moja kwa moja kumwadibu na kumhukumu mwanadamu. Hatua hii ya kazi inajenga kwa ujumla juu ya hatua iliyotangulia. Hii ndiyo maana ni kazi kama hiyo tu inaweza ikamletea mwanadamu wokovu hatua kwa hatua. Yesu pamoja na Mimi tunatoka katika Roho Mmoja. Ingawa miili Yetu haina uhusiano, Roho Zetu ni moja; ingawa kile Tunachofanya na kazi Tulizonazo hazifanani, kwa asili Tunafanana; miili Yetu ina maumbo tofauti, na hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya enzi na mahitaji ya kazi Yetu; huduma Zetu hazifanani, hivyo kazi Tunayoileta na tabia Tunayoifichua kwa mwanadamu pia ni tofauti. Ndio maana kile ambacho mwanadamu anakiona na kukipokea leo hii si kama kile cha wakati uliopita; hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya enzi. Ingawa jinsia na maumbo ya miili Yao ni tofauti, na ingawa hawakuzaliwa kutoka katika familia moja, achilia mbali katika kipindi kimoja, Roho Zao ni moja. Ingawa miili Yao haina uhusiano wa damu au kimwili kwa namna yoyote ile, hii haipingi kwamba Wao ni Mungu kupata mwili katika vipindi viwili tofauti vya nyakati. Ni ukweli usiopingika kwamba Wao ni Mungu katika miili, ingawa hawatoki katika ukoo mmoja au hawatumii lugha moja ya binadamu (mmoja alikuwa mwanamume aliyezungumza lugha ya Kiyahudi na mwingine ni mwanamke anayezungumza Kichina pekee). Ni kwa sababu hizi ndiyo maana Wameishi katika nchi tofauti kufanya kazi ambayo inampasa kila mmoja kufanya, na katika nyakati tofauti vilevile. Licha ya ukweli kwamba ni Roho moja, wakiwa na asili inayofanana, hakuna mfanano wa wazi kabisa kati ya ngozi ya nje ya miili Yao. Wanashiriki tu ubinadamu sawa, lakini umbo na kuzaliwa kwa miili Yao hakufanani. Haya hayana athari katika kazi Zao au maarifa aliyonayo mwanadamu juu yao, maana, hata hivyo, ni Roho moja na hakuna anayeweza kuwatenganisha. Ingawa Hawana uhusiano wa damu, nafsi zao zinaongozwa na Roho Zao, ili kwamba waweze kufanya kazi tofauti katika nyakati tofauti, wakiwa na miili Yao isiyokuwa na undugu wa damu. Kwa namna ile ile, Roho wa Yehova sio baba wa Roho ya Yesu na Roho wa Yesu sio mwana wa Roho wa Yehova. Ni wa Roho moja. Kama tu Mungu katika mwili wa leo na Yesu. Ingawa Hawahusiani kwa damu, ni Wamoja; hii ni kwa sababu Roho Zao ni moja. Anaweza kufanya kazi ya rehema na wema, vilevile na ile kazi ya hukumu ya haki na kumwadibu mwanadamu, na ile ya kuleta laana kwa mwanadamu. Hatimaye, Anaweza kufanya kazi ya kuuharibu ulimwengu na kuwaadhibu waovu. Je, hafanyi haya yote Mwenyewe? Je, huu si ukuu wa Mungu? Angeweza kutangaza sheria kwa ajili ya mwanadamu na kutoa amri, na angeweza pia kuwaongoza Waisraeli wa awali katika maisha yao duniani na kuwaongoza kujenga hekalu na madhabahu, kutawala Israeli yote. Kwa sababu ya mamlaka Yake, Aliishi pamoja nao duniani kwa miaka elfu mbili. Waisraeli hawakuthubutu kuasi; wote walimheshimu sana Yehova na walifuata amri Zake. Kazi hii ilifanywa kwa sababu ya mamlaka Yake na ukuu Wake. Katika Enzi ya Neema, Yesu alikuja kuwakomboa wanadamu wote walioanguka (sio Waisraeli pekee). Alionyesha rehema na wema kwa mwanadamu. Yesu ambaye mwanadamu alimwona katika Enzi ya Neema Alikuwa amejazwa na wema na siku zote Alikuwa mwenye upendo, maana Alikuja kumkomboa mwanadamu kutoka dhambini. Angeweza kuwasamehe wanadamu dhambi zao hadi pale ambapo msalaba Wake ungeweza kumkomboa mwanadamu kutoka dhambini. Wakati huo, Mungu alionekana kwa mwanadamu katika rehema na wema; yaani, Alijitoa sadaka kwa ajili ya mwanadamu na Alisulubiwa kwa ajili ya dhambi za mwanadamu ili kwamba waweze kusamehewa milele. Alikuwa mwenye rehema, mwenye huruma, mwenye upendo na mstahimilivu. Na wale wote waliomfuata Yesu katika Enzi ya Neema nao pia walionekana kuwa wastahimilivu na wenye upendo katika mambo yote. Walistahimili mateso yote, na hawakuweza kulipiza kisasi hata walipopigwa, kulaaniwa au kupigwa mawe. Lakini haipo hivyo tena katika hatua hii ya mwisho, kama vile kazi ya Yesu na Yehova hazikufanana ingawa Roho Zao zilikuwa moja. Kazi ya Yehova haikuwa kwa ajili ya kukamilisha enzi bali kuiongoza na kuipeleka katika maisha ya mwanadamu duniani. Hata hivyo, kazi sasa ni kuwashinda wale wanadamu walioharibiwa sana katika nchi za Wamataifa na kuongoza sio tu familia ya China bali ulimwengu mzima. Unaona kazi hii ikifanywa sasa China pekee, lakini kwa kweli imekwishaanza kusambaa katika nchi za ughaibuni. Ni kwa nini wageni mara kwa mara wanatafuta njia ya kweli? Hiyo ni kwa sababu Roho tayari amekwishaanza kazi Yake, na maneno sasa yameelekezwa kwa watu wa ulimwengu mzima. Hii tayari ni nusu ya kazi. Roho wa Mungu amefanya kazi kubwa hiyo tangu dunia ilipoumbwa; Amefanya kazi tofauti katika enzi tofautitofauti, na katika mataifa tofauti. Watu wa kila enzi wanaiona tabia Yake tofauti, ambayo kwa asili inafichuliwa kupitia kazi tofauti Anazozifanya. Yeye ni Mungu, mwingi wa rehema na wema; Yeye ni sadaka ya dhambi kwa ajili ya mwanadamu na mchungaji wa mwanadamu, pia Yeye ni hukumu, kuadibu, na laana kwa mwanadamu. Angeweza kumwongoza mwanadamu kuishi duniani kwa miaka elfu mbili na pia kumwokoa mwanadamu aliyepotoka. Na siku hii, pia Anaweza kumshinda mwanadamu ambaye hamjui na kumfanya awe chini ya utawala Wake, ili kwamba wote wajinyenyekeze kwake kikamilifu. Mwishoni, Atachoma yote ambayo si safi na ambayo si ya haki ndani ya wanadamu katika ulimwengu mzima, kuwaonyesha kwamba Yeye si Mungu wa Rehema, wema, hekima, maajabu na utakatifu pekee, bali pia ni Mungu anayemhukumu mwanadamu. Kwa waovu miongoni mwa wanadamu wote, Yeye ni moto, hukumu na adhabu; kwa wale ambao wanapaswa kukamilishwa, Yeye ni mateso, usafishaji, na majaribu, vilevile faraja, ustahimilivu, kutoa maneno, kushughulika na kupogoa. Na kwa wale ambao wameondolewa, Yeye ni adhabu, vilevile mapatilizo. Niambie, je, Mungu si Mkuu? Anaweza kufanya kazi yote, sio tu kazi ya msalaba kama ulivyokuwa ukifikiri. Unamfikiria Mungu kuwa ni wa chini sana! Je, unaamini kwamba kila kitu kingefikia kikomo baada ya wokovu wa mwanadamu kupitia msalaba Wake? Na hivyo, kufuatia hii, ungeweza kumfuata mbinguni na kisha kula matunda kutoka katika mti wa uzima na kunywa kutoka katika mto wa uzima? … Je, inaweza kuwa rahisi hivyo? Niambie, umekamilisha nini? Je, una maisha ya Yesu? Ni kweli umekombolewa Naye, lakini msalaba ulikuwa ni kazi ya Yesu Mwenyewe. Ni wajibu gani umeukamilisha kama mwanadamu? Una utauwa wa nje lakini huielewi njia Yake. Hivyo ndivyo unavyomdhihirisha? Ikiwa hujapokea maisha ya Mungu au kuona ujumla wa tabia Yake ya haki, basi huwezi kudai kuwa mmoja wa wale wenye maisha, na hufai kupitia katika lango la ufalme wa mbinguni.

Sio tu kwamba Mungu ni Roho bali Anaweza pia kuwa mwili; aidha, ni mwili wa utukufu. Yesu, ingawa hamjamwona, alishuhudiwa na Waisraeli, yaani, Wayahudi wa wakati huo. Mwanzoni alikuwa mwili, lakini baada ya kusulubiwa, alikuwa mwili wa utukufu. Yeye ni Roho anayezunguka mambo yote na Anaweza kufanya kazi katika maeneo yote. Anaweza kuwa Yehova, Yesu na Masihi; hatimaye, Anaweza kuwa Mwenyezi Mungu. Yeye ni haki, hukumu, na kuadibu, ni laana na ghadhabu, lakini pia mwenye rehema na wema. Kazi zote zinazofanywa Naye zinaweza kumwakilisha. Unasema Yeye ni Mungu ni wa namna gani? Wala huwezi kuelezea na unaweza kusema tu, “Siwezi elezea Mungu ni wa namna gani.” Usihitimishe kwamba Mungu milele ni Mungu wa rehema na wema, kwa sababu tu Mungu alifanya kazi ya ukombozi katika hatua moja. Je, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yeye ni Mungu wa namna hiyo tu? Ikiwa Yeye ni Mungu wa rehema na mwenye upendo, kwa nini Ataikomesha enzi hii katika siku za mwisho? Kwa nini Ataleta chini majanga mengi? Ikiwa ni kama unavyofikiri, kwamba Yeye ni Mungu wa rehema na mwema kwa mwanadamu hadi mwisho, hata hadi katika hatua ya mwisho, sasa kwa nini atatuma chini majanga kutoka mbinguni? Ikiwa Anampenda mwanadamu kama Yeye Mwenyewe na kama Anavyompenda Mwanawe wa pekee, kwa nini Atatuma chini mapigo na mvua ya mawe kutoka mbinguni? Kwa nini Anaruhusu mwanadamu kuteseka na njaa na ndwele ya kufisha? Kwa nini anaruhusu mwanadamu kuteseka na majanga haya? Hakuna mmoja wenu anayethubutu kusema Yeye ni Mungu wa namna gani, na hakuna anayeweza kuelezea. Je, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yeye ni Roho? Je, unathubutu kusema kuwa Yeye ni mwili wa Yesu? Na unathubutu kusema kuwa Yeye ni Mungu ambaye milele atasulubiwa kwa ajili ya mwanadamu?

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp